Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 7

Tafuta Upole Umpendeze Yehova

Tafuta Upole Umpendeze Yehova

“Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia . . . Utafuteni upole.”—SEF. 2:3.

WIMBO 80 “Onjeni Mwone Kwamba Yehova Ni Mwema”

MUHTASARI *

1-2. (a) Musa anafafanuliwaje katika Biblia, naye alifanya nini? (b) Tuna sababu gani nzuri ya kusitawisha sifa ya upole?

BIBLIA inasema kwamba Musa “alikuwa mtu mpole zaidi kuliko watu wote duniani.” (Hes. 12:3) Je, hilo linamaanisha kwamba alikuwa mtu asiye thabiti, asiye na msimamo, na mwoga? Hivyo ndivyo baadhi ya watu humfafanua mtu mpole. Lakini hilo si kweli hata kidogo. Musa alikuwa mtu thabiti, mwenye msimamo, na mtumishi jasiri wa Mungu. Kwa msaada wa Yehova, alimkabili mtawala mwenye nguvu wa Misri, huenda aliwaongoza watu 3,000,000 hivi kupita jangwani, na akalisaidia taifa la Israeli kushinda adui zao.

2 Leo, hatukabili changamoto ambazo Musa alikabili, lakini kila siku tunalazimika kushughulika na watu au hali zinazofanya iwe vigumu kwetu kuwa wapole. Hata hivyo, tuna sababu nzuri ya kusitawisha sifa hiyo. Yehova anaahidi kwamba “wapole wataimiliki dunia.” (Zab. 37:11) Je, unaweza kusema kwamba wewe ni mpole? Je, wengine wanaweza kusema kwamba wewe ni mpole? Kabla ya kujibu maswali hayo muhimu, tunahitaji kujua maana hasa ya kuwa mpole.

UPOLE NI NINI?

3-4. (a) Sifa ya upole inaweza kulinganishwa na nini? (b) Tunahitaji kuwa na sifa gani ili tusitawishe upole, na kwa nini?

3 Tunaweza kulinganisha sifa ya upole * na mchoro maridadi. Jinsi gani? Kama tu ambavyo mchoraji huchanganya rangi mbalimbali zenye kuvutia ili kutokeza mchoro fulani, sisi pia tunapaswa kuwa na sifa mbalimbali zenye kuvutia ili kusitawisha sifa ya upole. Miongoni mwa sifa hizo ni unyenyekevu, utii, na ujasiri. Kwa nini tunahitaji kuwa na sifa hizo ili kumfurahisha Yehova?

4 Ni watu wanyenyekevu tu ambao hujitiisha ili wafanye mapenzi ya Mungu. Ni mapenzi ya Mungu kwamba tusitawishe sifa ya upole. (Mt. 5:5; Gal. 5:23) Tunapofanya mapenzi ya Mungu, tunamkasirisha sana Shetani. Hivyo, ingawa sisi ni wanyenyekevu na wapole, watu wengi katika ulimwengu wa Shetani hutuchukia. (Yoh. 15:18, 19) Kwa sababu hiyo, tunahitaji ujasiri ili kumpinga Shetani.

5-6. (a) Kwa nini Shetani anawachukia watu wapole? (b) Tutajibu maswali gani?

5 Mtu ambaye hana sifa ya upole ana kiburi, hawezi kudhibiti hasira yake, na hamtii Yehova. Hivyo ndivyo Shetani alivyo hasa. Haishangazi kwamba anawachukia wapole! Wanafunua sifa zake mbaya kwa kuwa wana sifa nzuri ambazo yeye hana. Na wanazidi kumkasirisha wanapothibitisha kwamba yeye ni mwongo. Jinsi gani? Kwa sababu hata aseme au afanye nini, Shetani hawezi kuwazuia wapole kumtumikia Yehova!—Ayu. 2:3-5.

6 Huenda ikawa vigumu kuonyesha sifa ya upole chini ya hali gani? Na kwa nini tunapaswa kuendelea kusitawisha sifa ya upole? Ili kujibu maswali hayo, tutazungumzia mfano wa Musa, wale Waebrania watatu waliokuwa mateka Babiloni, na Yesu.

HALI ZINAZOFANYA IWE VIGUMU KUONYESHA UPOLE

7-8. Musa alitendaje alipovunjiwa heshima?

7 Tunapokuwa na mamlaka juu ya wengine: Inaweza kuwa vigumu kwa mtu aliye na mamlaka kuendelea kuwa mpole, hasa mtu fulani aliye chini ya mamlaka yake anapomvunjia heshima au kutilia shaka uamuzi fulani aliofanya. Je, jambo hilo limewahi kukupata? Vipi ikiwa aliyefanya hivyo ni mtu wa familia yako? Ungetendaje? Fikiria jinsi Musa alivyoshughulika na hali kama hiyo.

8 Yehova alimchagua Musa awe kiongozi wa Waisraeli na akampa pendeleo la kuandika sheria zilizoongoza taifa hilo. Hakukuwa na shaka yoyote kwamba Yehova alikuwa akimtumia Musa. Ingawa hivyo, Miriamu, dada ya Musa mwenyewe, na Haruni ndugu yake, walimchambua na kutilia shaka uamuzi wake kuhusu mke aliyechagua. Huenda wanaume wengine wenye mamlaka kama ya Musa wangekasirika na kujaribu kulipiza kisasi, lakini Musa hakufanya hivyo. Hakukasirika upesi. Hata alimsihi Yehova asiendelee kumwadhibu Miriamu. (Hes. 12:1-13) Kwa nini Musa alifanya hivyo?

Musa alimsihi Yehova asiendelee kumwadhibu Miriamu (Tazama fungu la 8)

9-10. (a) Yehova alimsaidia Musa kuelewa nini? (b) Vichwa vya familia na wazee wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Musa?

9 Musa alikuwa amekubali Yehova amzoeze. Miaka 40 hivi mapema, alipokuwa mshiriki wa familia ya kifalme nchini Misri, Musa hakuwa mpole. Kwa kweli, alikuwa mwepesi wa hasira hivi kwamba alimuua mtu fulani ambaye, kulingana na maoni yake, alihisi kwamba hakutenda kwa haki. Musa alifikiri kwamba Yehova angeunga mkono matendo yake. Yehova alitumia miaka 40 kumsaidia Musa kuelewa kwamba alihitaji sifa nyingine zaidi ya ujasiri ili awaongoze Waisraeli; alihitaji kuwa na sifa ya upole. Na ili awe mpole, alihitaji kuwa mnyenyekevu na mtiifu. Alifaulu kusitawisha sifa ya upole na akawa mwangalizi mzuri sana. —Kut. 2:11, 12; Mdo. 7:21-30, 36.

10 Leo, vichwa vya familia na wazee wa kutaniko wanapaswa kumwiga Musa. Unapovunjiwa heshima, usiwe mwepesi wa kukasirika. Kubali kwa unyenyekevu makosa yoyote uliyofanya. (Mhu. 7:9, 20) Kwa unyenyekevu, tii na ufuate mwongozo wa Yehova kuhusu jinsi ya kushughulikia matatizo. Na sikuzote wajibu wengine kwa upole. (Met. 15:1) Vichwa vya familia na waangalizi wanaofanya hivyo humfurahisha Yehova, huendeleza amani, na kuweka kielelezo kizuri cha jinsi ya kuwa wapole.

11-13. Wale vijana watatu Waebrania walituwekea mfano gani?

11 Tunapoteswa: Katika historia yote ya wanadamu, watawala wamekuwa wakiwatesa watu wa Yehova. Huenda wakatushtaki kwamba “tumevunja sheria,” lakini sababu hasa inayowakasirisha ni kwamba tunachagua ‘kumtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.’ (Mdo. 5:29) Huenda tukadhihakiwa, tukafungwa gerezani, au hata kupigwa. Hata hivyo, kwa msaada wa Yehova hatutalipiza kisasi, badala yake tutaendelea kuwa wapole tunapojaribiwa.

12 Fikiria mfano ambao Hanania, Mishaeli, na Azaria—Waebrania watatu waliokuwa uhamishoni—walituwekea. * Mfalme wa Babiloni aliwaamuru wainamie sanamu kubwa ya dhahabu. Walimweleza mfalme kwa upole kwa nini hawangeiabudu sanamu hiyo. Waliendelea kujitiisha kwa Mungu licha ya kwamba mfalme aliwaambia kuwa angewachoma kwenye tanuru lenye moto mkali. Yehova aliamua kuwaokoa wanaume hao papo hapo, ingawa hawakutazamia kwamba angewaokoa. Badala yake, walikuwa tayari kwa lolote ambalo Yehova angeruhusu. (Dan. 3:1, 8-28) Walithibitisha kwamba kwa kweli watu wapole ni jasiri—hakuna mfalme, kitisho, au adhabu yoyote inayoweza kuvunja azimio letu la ‘kumwabudu Yehova peke yake.’—Kut. 20:4, 5.

13 Ushikamanifu wetu kwa Mungu unapojaribiwa tunaweza kuwaigaje Waebrania hao watatu? Kwa unyenyekevu, tunatumaini kwamba Yehova atatutunza. (Zab. 118:6, 7) Tunawajibu kwa upole na kwa heshima wale wanaotushtaki kwamba tumefanya mambo mabaya. (1 Pet. 3:15) Na tunakataa katakata kufanya jambo lolote linaloweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Baba yetu mwenye upendo.

Watu wanapotupinga tunawajibu kwa heshima (Tazama fungu la 13)

14-15. (a) Ni nini kinachoweza kutokea tunapokuwa chini ya mkazo? (b) Kulingana na Isaya 53:7, 10, kwa nini tunaweza kusema kwamba Yesu ndiye mfano bora kabisa wa mtu aliyeonyesha upole chini ya mkazo?

14 Tunapokuwa chini ya mkazo: Sisi sote hupatwa na mkazo kwa sababu mbalimbali. Huenda umewahi kupatwa na mkazo shuleni kabla ya kufanya mtihani au kabla ya kufanya kazi fulani ukiwa kazini, au unapofikiria kuhusu matibabu fulani unayohitaji kupata. Si rahisi kuonyesha sifa ya upole unapokuwa chini ya mkazo. Huenda mambo ambayo kwa kawaida hayangetusumbua yakaanza kutuudhi. Huenda tukazungumza kwa ukali na kuwatendea wengine bila fadhili. Ikiwa umewahi kupatwa na mkazo, fikiria mfano wa Yesu.

15 Katika miezi ya mwisho ya maisha yake hapa duniani, Yesu alikuwa chini ya mkazo mkubwa sana. Alijua kwamba angeuawa na angeteswa vikali. (Yoh. 3:14, 15; Gal. 3:13) Miezi michache kabla ya kifo chake, Yesu alisema kwamba alikuwa anataabika. (Luka 12:50) Na siku chache tu kabla ya kifo chake, Yesu alisema: “Ninataabika.” Tunaweza kuona unyenyekevu wake na jinsi alivyojitiisha kwa Mungu alipommiminia hisia zake katika sala: “Baba, niokoe kutoka katika saa hii. Hata hivyo, ndiyo sababu nimekuja kwenye saa hii. Baba, litukuze jina lako.” (Yoh. 12:27, 28) Wakati ulipofika, kwa ujasiri Yesu alikubali kukamatwa na maadui wa Mungu, ambao walimuua kwa njia yenye maumivu makali na yenye kuaibisha. Licha ya mkazo, licha ya mateso, kwa upole Yesu alifanya mapenzi ya Mungu. Bila shaka, tunaweza kusema kwamba Yesu ndiye mfano bora kabisa wa mtu aliyeonyesha sifa ya upole chini ya mkazo!—Soma Isaya 53:7, 10.

Yesu ndiye mfano bora kabisa wa mtu aliyeonyesha upole (Tazama fungu la 16-17) *

16-17. (a) Marafiki wa Yesu walitahini upole wake jinsi gani? (b) Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani?

16 Katika usiku wa mwisho wa maisha yake hapa duniani, marafiki wake wa karibu walitahini upole wake. Wazia mkazo ambao Yesu alikuwa nao usiku huo. Je, angeendelea kuwa mwaminifu kikamilifu hadi kifo? Fursa ya mabilioni ya watu kupata uzima ilimtegemea yeye. (Rom. 5:18, 19) Na jambo muhimu hata zaidi, sifa ya Baba yake ilihusika. (Ayu. 2:4) Kisha alipokuwa akila mlo wa mwisho pamoja na mitume—marafiki wake wa karibu—mazungumzo yao yalibadilika na kuwa ‘mabishano makali’ kuhusu “ni nani aliyekuwa mkuu zaidi kati yao.” Yesu alikuwa amewarekebisha marafiki wake kuhusu jambo hilo mara nyingi, kutia ndani mapema jioni hiyohiyo! Lakini jambo la kustaajabisha ni kwamba Yesu hakuudhika. Badala yake aliendelea kuonyesha sifa ya upole. Kwa fadhili, lakini kwa uthabiti, Yesu aliwaeleza—kwa mara nyingine tena—mtazamo waliopaswa kuwa nao. Kisha aliwapongeza marafiki wake kwa kushikamana naye.—Luka 22:24-28; Yoh. 13:1-5, 12-15.

17 Ungetendaje ikiwa ungejikuta katika hali kama hiyo? Tunaweza kumwiga Yesu na kuendelea kuwa wapole hata tunapokuwa chini ya mkazo. Kwa unyenyekevu, tii amri ya Yehova ya ‘kuendelea kuvumiliana.’ (Kol. 3:13) Tutatii amri hiyo ikiwa tutakumbuka kwamba sisi sote husema na kutenda mambo yanayowaudhi wengine. (Met. 12:18; Yak. 3:2, 5) Jitahidi pia kutaja mambo mazuri unayoona kwa wengine.—Efe. 4:29.

KWA NINI TUENDELEE KUTAFUTA UPOLE?

18. Yehova huwasaidiaje wapole kufanya maamuzi mazuri, lakini ni lazima wafanye nini?

18 Tutafanya maamuzi mazuri zaidi. Tunapohitaji kufanya maamuzi magumu maishani, Yehova atatusaidia kufanya maamuzi mazuri—lakini atafanya hivyo iwapo tu sisi ni wapole. Anaahidi kwamba atasikia “ombi la wapole.” (Zab. 10:17) Na atafanya mengi zaidi ya kusikiliza tu maombi yetu. Biblia inaahidi hivi: “Atawaongoza wapole katika yaliyo sawa, naye atawafundisha wapole njia yake.” (Zab. 25:9) Yehova anatoa mwongozo huo katika Biblia na kupitia machapisho * na programu zinazotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Ni lazima tutimize sehemu yetu kwa kukubali kwa unyenyekevu kwamba tunahitaji msaada, kwa kujifunza habari ambazo Yehova anatuandalia, na kutii kwa unyenyekevu mambo tunayojifunza.

19-21. Musa alifanya kosa gani huko Kadeshi, na kisa hicho kinatufunza mambo gani?

19 Tutaepuka kufanya makosa. Mfikirie Musa. Kwa miaka mingi aliendelea kuwa mpole na alimfurahisha Yehova. Kisha, karibu na mwisho wa safari ngumu ya miaka 40 nyikani, Musa alishindwa kuonyesha sifa ya upole. Dada yake, ambaye huenda ndiye aliyemwokoa Musa akiwa mchanga huko Misri, alikuwa ametoka tu kufa na kuzikwa huko Kadeshi. Na kwa mara nyingine tena Waisraeli walidai kwamba hawakuwa wakitunzwa vizuri. Pindi hii ‘waligombana na Musa’ kuhusu ukosefu wa maji. Licha ya miujiza yote ambayo Yehova alifanya kupitia Musa na licha ya rekodi yake ndefu ya kuwaongoza Waisraeli bila ubinafsi, bado walilalamika. Hawakulalamika tu kuhusu ukosefu wa maji bali pia kumhusu Musa, kana kwamba yeye ndiye aliyesababisha wawe na kiu.—Hes. 20:1-5, 9-11.

20 Musa alikasirika sana na hilo likamfanya ashindwe kuonyesha sifa ya upole. Badala ya kuonyesha imani na kuzungumza na mwamba kama Yehova alivyokuwa amemwamuru, Musa alizungumza na watu kwa uchungu na akajielekezea utukufu. Kisha aliupiga mwamba mara mbili na maji mengi sana yakabubujika. Kiburi na hasira zilisababisha afanye kosa zito sana. (Zab. 106:32, 33) Musa alipoteza upole wake kwa muda mfupi, na hilo lilisababisha asiingie katika Nchi ya Ahadi.—Hes. 20:12.

21 Tunajifunza masomo muhimu kutokana na kisa hicho. Kwanza, ni lazima sikuzote tuendelee kujitahidi kudumisha sifa ya upole. Tukiipuuza hata kwa muda mfupi, mara moja kiburi kinaweza kujitokeza na kufanya tuseme au kutenda kipumbavu. Pili, mkazo unaweza kufanya iwe vigumu kwetu kuonyesha sifa ya upole, hivyo ni lazima tujitahidi kuwa wapole hata tunapokuwa chini ya mkazo.

22-23. (a) Kwa nini tunapaswa kuendelea kutafuta upole? (b) Maneno yaliyo kwenye andiko la Sefania 2:3 yanaonyesha nini?

22 Tutalindwa. Hivi karibuni, Yehova atawaondoa watu wote waovu duniani, na ni wapole tu watakaobaki. Kisha, dunia itakuwa na amani kikweli. (Zab. 37:10, 11) Je, utakuwa miongoni mwa watu hao wapole? Unaweza kuwa mmoja wao ikiwa utatenda kulingana na mwaliko wenye upendo wa Yehova ulioandikwa na nabii Sefania.—Soma Sefania 2:3.

23 Kwa nini andiko la Sefania 2:3 linasema: “Huenda mtafichwa”? Maneno hayo hayamaanishi kwamba Yehova hana uwezo wa kuwalinda wale anaowapenda na wanaotaka kumfurahisha. Badala yake, yanaonyesha kwamba kuna jambo tunalopaswa kufanya ili tulindwe. Tunaweza kuokoka “siku ya hasira ya Yehova” na kuishi milele ikiwa tutajitahidi sasa kutafuta upole na kufanya mambo yanayomfurahisha Yehova.

WIMBO 120 Igeni Upole wa Kristo

^ fu. 5 Hakuna mtu yeyote anayezaliwa akiwa na sifa ya upole. Ni lazima tusitawishe sifa hiyo. Huenda ni rahisi kwetu kuonyesha sifa ya upole tunaposhughulika na watu wanaopenda amani, lakini huenda ikawa vigumu kwetu kuendelea kuwa wapole tunaposhughulika na watu wenye kiburi. Makala hii itazungumzia baadhi ya changamoto ambazo huenda tukahitaji kushinda ili tusitawishe sifa yenye kuvutia ya upole.

^ fu. 3 UFAFANUZI WA MANENO: Upole. Watu walio na sifa ya upole huwatendea wengine kwa fadhili na hubaki wakiwa watulivu hata wengine wanapowakasirisha. Unyenyekevu. Watu wanyenyekevu hawana kiburi au majivuno; wao huwaona wengine kuwa bora kuliko wao. Yehova anaposemwa kuwa mnyenyekevu, inamaanisha kwamba anawatendea kwa upendo na rehema wale walio chini ya mamlaka yake.

^ fu. 12 Wababiloni waliwapa Waebrania hao watatu majina Shadraki, Meshaki, na Abednego.—Dan. 1:7.

^ fu. 18 Kwa mfano, tazama makala “Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima,” iliyochapishwa kwenye toleo la Aprili 15, 2011, la gazeti la Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA Ukurasa wa 12: Yesu anaendelea kuwa mpole na anawarekebisha wanafunzi wake kwa utulivu baada ya wao kubishana kuhusu ni nani aliye mkuu kati yao.