Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 7

Tafuta Upole ili Kumupendeza Yehova

Tafuta Upole ili Kumupendeza Yehova

“Mumutafute Yehova, ninyi wote wapole wa dunia . . . Mutafute upole.”​—SEF. 2:3.

WIMBO 80 “Onjeni Muone Kwamba Yehova Ni Mwema”

KIFUPI CHA HABARI *

1-2. (a) Biblia inaonyesha kama Musa alikuwa mutu wa namna gani, na alifanya nini? (b) Tuko na sababu gani yenye kutuchochea tujikaze kuwa na sifa ya upole?

BIBLIA inaonyesha kama Musa alikuwa “mupole sana kuliko watu wote juu ya uso wa dunia.” (Hes. 12:3) Je, ni kusema alikuwa muzaifu, mwenye kuogopa kukamata maamuzi, ao mwenye hakubakia imara wakati wengine walimupinga? Watu fulani wanaweza kusema kama ni vile mutu mupole anakuwaka. Lakini ile haiko kweli. Musa, mutumishi wa Mungu, alikuwa mwenye nguvu, hakuogopa kukamata maamuzi, na alikuwa hodari. Kwa musaada wa Yehova, alizungumuza bila woga na mufalme mwenye nguvu wa Misri, aliongoza pengine watu 3 000 000 katika jangwa, na alisaidia taifa la Israeli kushinda maadui wao.

2 Hatupatwe na magumu yenye Musa alishinda, lakini kila siku tunapaswa kushugulika na watu ao hali zenye zinafanya ikuwe nguvu kuonyesha upole. Hata hivyo, tuko na sababu kubwa yenye kutuchochea tujikaze kuwa na ile sifa. Yehova anaahidi kama “wapole watariti dunia.” (Zb. 37:11) Unajiona kuwa mupole? Wengine wanakuona vile? Mbele tujibu ile maulizo ya maana, tunapaswa kujua kwanza maana ya kuwa mupole.

UPOLE, MAANA YAKE NINI?

3-4. (a) Tunaweza kulinganisha upole na nini? (b) Tuko na lazima ya sifa gani ili tukuwe wapole, na juu ya nini?

3 Upole * uko kama muchoro ao picha ya muzuri. Namna gani? Kama vile tu mutu mwenye kuchora picha anachanga rangi mbalimbali zenye kupendeza ili kufanya picha fulani, tunapaswa kuwa na sifa mbalimbali zenye kupendeza ili kuwa wapole. Sifa kubwa kati ya sifa hizo ni unyenyekevu, kujitiisha, na uhodari. Juu ya nini tuko na lazima ya sifa hizo ikiwa tunataka kumupendeza Yehova?

4 Watu wanyenyekevu tu njo wanajitiisha ili kufanya mapenzi ya Mungu. Mapenzi ya Mungu inatia ndani kuwa wapole. (Mt. 5:5; Gal. 5:23) Wakati tunafanya mapenzi ya Mungu, tunamufanya Shetani akasirike. Kwa hiyo, hata kama tuko wanyenyekevu na wapole, watu wengi wenye kuwa sehemu ya ulimwengu wa Shetani wanatuchukia. (Yoh. 15:18, 19) Njo maana, tuko na lazima ya uhodari ili kumupinga Shetani.

5-6. (a) Juu ya nini Shetani anachukia watu wapole? (b) Tutajibu maulizo gani?

5 Mutu mwenye haiko mupole ni mwenye majivuno, hazuie kasirani yake, na hamutii Yehova. Njo vile Shetani iko kabisa. Njo maana anachukiaka watu wapole! Wanaonyesha kama iko muovu sana kwa sababu wako na sifa za muzuri zenye yeye hana. Na jambo lenye kumuchukiza Shetani zaidi ni hili: wanaonyesha kama yeye ni musema-uongo. Juu ya nini ni musema-uongo? Kwa sababu hata aseme ao kufanya nini, hawezi kuzuia watu wapole waache kumutumikia Yehova!​—Yob. 2:3-5.

6 Ni wakati gani tunaweza kuona kama ni nguvu kuwa wapole? Na juu ya nini tunapaswa kuendelea kutafuta upole? Ili kujibu ile maulizo, tutazungumuzia mufano wenye watu hawa walituachia: Musa, Waebrania tatu wenye walikuwa mu uhamisho katika Babiloni, na Yesu.

NI WAKATI GANI HAIKO MWEPESI KUWA WAPOLE?

7-8. Musa alitenda namna gani wakati wengine walimukosea heshima?

7 Wakati tunapewa mamlaka: Inaweza kuwa nguvu kwa wenye kuwa na mamlaka kuendelea kuwa wapole, zaidi sana wakati mutu fulani mwenye wanaongoza anawakosea heshima ao hakubaliane na maamuzi yao. Jambo hilo limekwisha kukufikia? Tuseme nini ikiwa mutu mumoja katika familia anafanya vile? Unaweza kutenda namna gani? Fikiria namna Musa alitenda mu hali kama hiyo.

8 Yehova alimuweka Musa kuwa kiongozi wa taifa la Israeli na alimuruhusu aandike sheria zenye ziliongoza taifa hilo. Ilionekana wazi kuwa Yehova alikuwa anamutegemeza Musa. Lakini, Miriamu dada ya Musa na Haruni ndugu yake, walisema mambo ya mubaya juu yake na kusema kama hakupaswa kuoa mwanamuke mwenye alikuwa ameoa. Wanaume fulani wangekuwa na mamlaka yenye Musa alikuwa nayo, wangekasirika na kujilipizia kisasi, lakini Musa hakufanya vile. Hakukasirika haraka. Hata alimuomba Yehova amuponyeshe Miriamu ugonjwa wa ukoma wenye alikuwa amepigwa. (Hes. 12:1-13) Juu ya nini Musa alitenda vile?

Musa alimuomba Yehova amuponyeshe Miriamu ugonjwa wa ukoma wenye alikuwa amepigwa (Picha hii inapatana na fungu la 8)

9-10. (a) Yehova alimusaidia Musa aelewe jambo gani? (b) Vichwa vya familia na wazee wa kutaniko wanaweza kujifunza nini kupitia mufano wa Musa?

9 Musa alikuwa ameacha Yehova amuzoeze. Miaka 40 hivi mbele ya pale, Musa hakukuwa mupole wakati alikuwa mu familia ya kifalme katika Misri. Kwa kweli, alikuwa mwenye kukasirika haraka mupaka akamuua mwanaume mwenye aliona kuwa alitendea mwingine bila haki. Musa aliwaza kama Yehova angekubali matendo yake. Kwa miaka 40, Yehova alimusaidia Musa aelewe kama, zaidi ya kuwa hodari, alipaswa kuwa mupole ili kuongoza Waisraeli. Na ili akuwe mupole, alipaswa pia kuwa munyenyekevu, na mwenye kujitiisha. Alijifunza muzuri somo hilo na akakuwa kiongozi muzuri zaidi.​—Kut. 2:11, 12; Mdo. 7:21-30, 36.

10 Leo, vichwa vya familia na wazee wa kutaniko wanapaswa kuiga mufano wa Musa. Wakati mutu anakukosea heshima, usikasirike haraka. Ukubali kwa unyenyekevu uzaifu wowote wenye uko nao. (Muh. 7:9, 20) Fuata kwa unyenyekevu muongozo wa Yehova juu ya namna ya kushugulikia matatizo. Na sikuzote ujibu kwa upole. (Mez. 15:1) Vichwa vya familia na wazee wa kutaniko wenye kufanya vile, wanamufurahisha Yehova, wanafanya kukuwe amani, na wanaonyesha mufano juu ya namna ya kuonyesha upole.

11-13. Waebrania tatu walituachia mufano gani?

11 Wakati tunateswa: Tangu zamani, watawala wanadamu wametesa watu wa Yehova. Wanaweza kutushitaki “makosa” mbalimbali, lakini sababu kubwa yenye kufanya watukasirikie ni hii: tunachagua “kumutii Mungu kuwa mutawala kuliko wanadamu.” (Mdo. 5:29) Tunaweza kuchekelewa, kufungwa, ao hata kutendewa mubaya kimwili. Hata hivyo, kwa musaada wa Yehova, hatutajilipizia kisasi lakini tutaendelea kuwa wapole wakati wote wa majaribu.

12 Fikiria mufano wenye Waebrania tatu wenye walikuwa katika uhamisho walituachia. Waebrania hao ni Hanania, Mishaeli, na Azaria. * Mufalme wa Babiloni aliwaamuru wainame mbele ya sanamu kubwa ya zahabu. Kwa upole, walifasiria mufalme juu ya nini walikataa kuabudu ile sanamu. Waliendelea kujitiisha kwa Mungu hata kama mufalme aliwaogopesha kama atawaunguza mu tanuru yenye kuwaka moto. Yehova aliamua kuwaokoa palepale, lakini hawakufikiri kuwa Yehova alilazimika kufanya vile kwa ajili yao. Hata hivyo, walikuwa tayari kukubali jambo lolote lenye Yehova angeruhusu litokee. (Da. 3:1, 8-28) Walionyesha kama watu wapole ni wenye uhodari kabisa; hakuna mufalme, hakuna maneno yoyote yenye kuogopesha, na hakuna azabu ao malipizi yenye inaweza kuvunja azimio letu la kushikamana na Yehova tu.​—Kut. 20:4, 5.

13 Wakati ushikamanifu wetu kwa Yehova unajaribiwa, namna gani tunaweza kuiga wale Waebrania tatu? Tunatumainia kwa unyenyekevu kama Yehova atatuhangaikia. (Zb. 118:6, 7) Tunajibu kwa upole na heshima wale wenye kutushitaki mambo ya mubaya. (1 Pe. 3:15) Na tunakataa kabisa kufanya jambo lolote lenye linaweza kuharibu urafiki wetu pamoja na Baba yetu mwenye upendo.

Wakati wengine wanatupinga, tunajibu kwa heshima (Picha hii inapatana na fungu la 13)

14-15. (a) Ni nini inaweza kutokea wakati tuko na mahangaiko ya akili? (b) Kulingana na Isaya 53:7, 10, juu ya nini tunaweza kusema kama Yesu njo mutu mwenye alionyesha mufano muzuri zaidi wa upole wakati wa mahangaiko ya akili?

14 Wakati tuko na mahangaiko ya akili: Kuko sababu mbalimbali zenye zinafanya sisi wote tukuwe na mahangaiko ya akili. Pengine tulikuwa na mahangaiko ya akili mbele ya kufanya mashindano fulani ku masomo ao mbele ya kufanya mugao fulani ku kazi. Ao tunaweza kuwa na mahangaiko ya akili wakati tunafikiria matunzo fulani yenye tunapaswa kupata. Wakati tuko na mahangaiko ya akili, haiko mwepesi kuwa wapole. Hali zenye kwa kawaida hazitukwazake, zinaweza kuanza kutukasirisha. Tunaweza kusema kwa ukali na kutendea wengine bila fazili. Kama umekwisha kuwa na mahangaiko ya akili, fikiria mufano wa Yesu.

15 Katika miezi ya mwisho-mwisho ya maisha yake ku dunia, Yesu alikuwa na mahangaiko ya akili ya nguvu sana. Alijua kama angeteseka sana na kuuawa. (Yoh. 3:14, 15; Gal. 3:13) Miezi fulani mbele ya kifo chake, alisema kama alikuwa katika taabu sana. (Lu. 12:50) Na siku fulani tu mbele ya kifo chake, Yesu alisema hivi: “Ninavurugika.” Tunaweza kuona kama alikuwa munyenyekevu na mwenye kujitiisha kwa Mungu kupitia maneno yenye alisema mu sala ili kumuambia Mungu namna alikuwa anajisikia. Alisali hivi: “Baba, uniokoe kutoka katika saa hii. Hata hivyo, ndiyo sababu nimekuja kwenye saa hii. Baba, tukuza jina lako.” (Yoh. 12:27, 28) Wakati muda ulifika, kwa uhodari, Yesu alijitia mu mikono ya maadui wa Mungu, wenye walimuua katika njia yenye maumivu makali sana na yenye zarau kabisa. Hata kama alikuwa na mahangaiko ya akili, hata kama aliteseka, kwa upole, Yesu alifanya mapenzi ya Mungu. Kwa kweli, tunaweza kusema kama Yesu njo mutu mwenye alionyesha mufano muzuri zaidi wa upole wakati wa mahangaiko ya akili!​—Soma Isaya 53:7, 10.

Yesu njo alionyesha mufano muzuri zaidi wa upole (Picha hii inapatana na fungu la 16-17) *

16-17. (a) Namna gani marafiki wa Yesu walitia upole wake mu jaribu? (b) Namna gani tunaweza kumuiga Yesu?

16 Katika usiku wa mwisho wa maisha ya Yesu ku dunia, marafiki wake wa sana walitia upole wake mu jaribu. Wazia mahangaiko ya akili yenye Yesu alikuwa nayo usiku huo. Angeendelea kuwa muaminifu kabisa mupaka kifo? Kama hangeendelea kuwa muaminifu, hakuna mutu angekuwa na tumaini la kupata uzima wa milele. (Ro. 5:18, 19) Na jambo la maana zaidi, matendo yake ingeharibishia Baba yake sifa ao kumuletea sifa. (Yob. 2:4) Kisha, wakati wa chakula cha mwisho pamoja na marafiki wake wa sana, ni kusema, mitume wake, mazungumuzo ya mitume iligeuka na kuwa “bishano kali” juu ya kujua “ni nani kati yao alionwa kuwa mukubwa zaidi.” Yesu alikuwa amerekebisha marafiki wake mara mingi juu ya jambo hilo, hata katika mangaribi ileile! Jambo la kushangaza ni kwamba Yesu hakukasirika. Lakini, aliendelea kuwa mupole. Kwa upole, lakini waziwazi, Yesu aliwafasiria tena tabia yenye walipaswa kuwa nayo. Na kisha alipongeza marafiki wake kwa sababu walishikamana naye.​—Lu. 22:24-28; Yoh. 13:1-5, 12-15.

17 Ungetenda namna gani kama ungekuwa katika hali kama hiyo? Tunaweza kumuiga Yesu kwa kuendelea kuwa wenye tabia ya upole hata wakati tuko na mahangaiko ya akili. Ukuwe tayari kutii amri ya Yehova ya ‘kuendelea kuvumiliana.’ (Kol. 3:13) Tutatii amri hiyo ikiwa tunakumbuka kama sisi wote tunasemaka na kufanya mambo yenye kukwaza wengine. (Mez. 12:18; Yak. 3:2, 5) Na sikuzote, upongeze wengine juu ya sifa za muzuri zenye wako nazo.​—Efe. 4:29.

JUU YA NINI TUENDELEE KUTAFUTA UPOLE?

18. Yehova anafanya nini ili kusaidia watu wapole kukamata maamuzi ya muzuri, lakini wanapaswa kufanya nini?

18 Tutakamata maamuzi ya muzuri. Wakati tunapaswa kukamata maamuzi mazito katika maisha, Yehova atatusaidia kukamata maamuzi ya muzuri, kama tu tuko wapole. Anaahidi kama atasikia “ombi la wapole.” (Zb. 10:17) Na atafanya mengi zaidi kuliko tu kusikia maombi yetu. Biblia inaahidi hivi: “Ataongoza wapole katika mambo yenye kuwa sawa, na atafundisha wapole njia yake.” (Zb. 25:9) Yehova anatupatia muongozo huo kupitia Biblia na vichapo vyetu * na kupitia video na mikutano yenye kutayarishwa na “mutumwa muaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Tunapaswa kufanya sehemu yetu kwa kukubali kwa unyenyekevu musaada wa Yehova, kwa kujifunza vichapo vyenye Yehova anatutolea, na kuwa tayari kutumia mambo yenye tunajifunza.

19-21. Musa alifanya kosa gani katika Kadeshi, na hilo linaweza kutufundisha nini?

19 Tutaepuka kufanya makosa. Fikiria tena mufano wa Musa. Kwa miaka mingi aliendelea kuwa mupole na alimupendeza Yehova. Kisha, karibu na mwisho wa safari yenye magumu ya miaka 40 mu jangwa, Musa alishindwa kuonyesha upole. Dada yake, mwenye inawezekana kabisa kuwa alisaidia kuokoa uzima wake katika Misri, alitokea kufa na kuzikwa katika Kadeshi. Na mara ingine tena, Waisraeli walinungunika kama hawakuhangaikiwa muzuri. Wakati huo, ‘walibishana na Musa’ juu ya kukosa maji. Hata kama walikuwa wameona miujiza yote yenye Yehova alikuwa amefanya kupitia Musa, na hata kama Musa alikuwa amewaongoza kwa wakati murefu bila kutafuta faida zake mwenyewe, watu walinungunika. Hawakunungunika tu juu ya kukosa maji lakini pia walimunungunikia Musa; ni kama vile yeye njo alifanya wakose maji.​—Hes. 20:1-5, 9-11.

20 Musa alikasirika sana; kwa hiyo, akakosa kuonyesha sifa yake ya upole. Hata kama Yehova alikuwa amemuamuru azungumuze na mwamba, Musa alisema na watu kwa kasirani na alisema kama yeye njo angefanya muujiza. Kisha, akapiga mwamba mara mbili na maji mingi ikatoka. Kwa sababu ya kiburi na kasirani, alifanya kosa nzito. (Zb. 106:32, 33) Juu Musa alikosa kuonyesha sifa ya upole kwa wakati fulani, hakuruhusiwa kuingia katika Inchi ya Ahadi.​—Hes. 20:12.

21 Mufano wa Musa unatufundisha mambo ya maana. Kwanza, tunapaswa kujikaza sikuzote ili tuendelee kuwa na tabia ya upole. Kama tunaacha kuonyesha upole kwa muda fulani, tunaweza kuwa na kiburi bila kukawia na kinaweza kutufanya tuseme na kutenda kwa upumbavu. Pili, wakati tuko na mahangaiko ya akili, inaweza kuwa nguvu kuendelea kuwa wapole. Kwa, hiyo tunapaswa kujikaza kuwa wapole hata wakati tuko na mikazo.

22-23. (a) Juu ya nini tunapaswa kuendelea kutafuta upole? (b) Maneno yenye kuwa mu andiko la Sefania 2:3 inaonyesha nini?

22 Tutapata ulinzi. Hivi karibuni, Yehova atatosha watu wabaya wote ku dunia, na wapole tu njo watabakia ku dunia. Wakati huo, amani itakuwa kabisa ku dunia. (Zb. 37:10, 11) Utakuwa kati ya wapole hao? Unaweza kuwa kati yao kama unatenda kulingana na mualiko wa upendo wenye Yehova anatutolea kupitia nabii Sefania.​—Soma Sefania 2:3.

23 Juu ya nini Sefania 2:3 inasema hivi: “Pengine mutafichwa”? Ile maneno haimaanishe kama Yehova hana uwezo wa kulinda wale wenye kutaka kumupendeza na wenye anapenda. Lakini, inaonyesha kama tunapaswa kufanya jambo fulani ili tupate ulinzi. Tunaweza kuokoka “siku ya kasirani ya Yehova” na kuishi milele kama tunajikaza sasa kutafuta upole na kumupendeza Yehova.

WIMBO 120 Igeni Upole wa Kristo

^ fu. 5 Hakuna mutu kati yetu mwenye anazaliwa na sifa ya upole. Tunapaswa kujikaza ili kuwa na ile sifa. Tunaweza kuona kama ni mwepesi kuwa wapole wakati tunashugulika na watu wenye kupenda amani, lakini tunaweza kuona kama ni nguvu kuendelea kuwa wapole wakati tunashugulika na watu wenye kiburi. Habari hii itazungumuzia magumu fulani yenye tunaweza kushinda ili tuonyeshe ile sifa ya muzuri sana ya upole.

^ fu. 3 MAFASIRIO YA MANENO FULANI: Upole. Watu wapole ni wenye fazili katika uhusiano wao pamoja na wengine na wanabakia wenye tabia ya upole hata wakati wanachokozwa. Unyenyekevu. Watu wanyenyekevu hawana kiburi ao majivuno; wanaona wengine kuwa wazuri zaidi kuwapita. Wakati neno unyenyekevu linatumiwa juu ya Yehova, linamaanisha kama anatendea watu wa hali ya chini kwa upendo na rehema.

^ fu. 12 Wababiloni walipatia Waebrania hao tatu majina Shadraki, Meshaki, na Abednego.​—Da. 1:7.

^ fu. 18 Kwa mufano, ona habari “Fanya Maamuzi Ambayo Yanamletea Mungu Heshima,” katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 4, 2011.

^ fu. 59 MAFASIRIO YA PICHA: Yesu anaendelea kuwa mwenye tabia ya upole na anarekebisha kwa utulivu wanafunzi wake, kisha wao kubishana juu ya kujua ni nani mwenye kuwa mukubwa kati yao.