Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 9

Upendo na Haki Katika Taifa la Kale la Israeli

Upendo na Haki Katika Taifa la Kale la Israeli

“Anapenda uadilifu na haki. Dunia imejaa upendo mshikamanifu wa Yehova.”—ZAB. 33:5.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

MUHTASARI *

1-2. (a) Sisi sote tunatamani nini? (b) Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu nini?

SISI sote tunatamani kupendwa. Na sisi sote tunatamani kutendewa kwa haki. Tusipoonyeshwa upendo au tukitendewa isivyo haki tena na tena, huenda tukahisi hatufai na hata kukata tamaa.

2 Yehova anajua kwamba tunatamani sana kupendwa na kutendewa kwa haki. (Zab. 33:5) Tuna hakika kwamba Mungu wetu anatupenda sana na angependa tutendewe kwa haki. Tunajionea wazi jambo hilo tunapochunguza kwa makini Sheria ambayo Yehova aliwapa Waisraeli kupitia Musa. Ikiwa umevunjika moyo kwa sababu hujaonyeshwa upendo au umepondeka roho kwa sababu ya kutendewa isivyo haki, tafadhali chunguza Sheria ya Musa * uone jinsi Yehova anavyowajali watu wake.

3. (a) Kulingana na Waroma 13:8-10, tunajionea nini tunapochunguza Sheria ya Musa? (b) Tutajibu maswali gani katika makala hii?

3 Tunapojifunza Sheria ya Musa, tunajionea hisia nyororo za Yehova, Mungu wetu mwenye upendo. (Soma Waroma 13:8-10.) Katika makala hii, tutachunguza baadhi ya sheria ambazo Waisraeli walipewa na tutajibu maswali haya: Kwa nini tunaweza kusema kwamba upendo ndio uliokuwa msingi wa sheria hizo? Kwa nini tunaweza kusema kwamba Sheria ilitetea haki? Wale waliokuwa na mamlaka walipaswa kutekeleza Sheria jinsi gani? Na Sheria iliwalinda nani hasa? Majibu ya maswali hayo yanaweza kutufariji, kutupatia tumaini, na kutusaidia tumkaribie zaidi Baba yetu mwenye upendo.—Mdo. 17:27; Rom. 15:4.

MFUMO WA SHERIA ULIOTEGEMEA UPENDO

4. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba upendo ndio uliokuwa msingi wa Sheria ya Musa? (b) Kama inavyotajwa kwenye Mathayo 22:36-40, Yesu alikazia amri zipi?

4 Tunaweza kusema kwamba upendo ndio uliokuwa msingi wa Sheria ya Musa kwa sababu mambo yote ambayo Yehova hufanya huchochewa na upendo. (1 Yoh. 4:8) Mfumo wote wa Sheria ambao Yehova alianzisha unategemea amri mbili za msingi—kumpenda Mungu, na kumpenda jirani yako. (Law. 19:18; Kum. 6:5; soma Mathayo 22:36-40.) Hivyo, kila moja ya zile amri 600 na nyingine zinazofanyiza Sheria, zinatufundisha jambo fulani kuhusu upendo wa Yehova. Acheni tuchunguze mifano kadhaa.

5-6. Yehova anataka wenzi wa ndoa wafanye nini, naye anajua nini? Toa mfano.

5 Uwe mshikamanifu kwa mwenzi wako wa ndoa, na uwatunze watoto wako. Yehova anataka wenzi wa ndoa wawe na upendo wenye nguvu sana utakaodumu maisha yao yote. (Mwa. 2:24; Mt. 19:3-6) Uzinzi ni mojawapo ya matendo ya kikatili zaidi ambayo mtu anaweza kumtendea mwenzi wake. Haishangazi kwa nini amri ya saba kwenye zile Amri Kumi ilikataza uzinzi. (Kum. 5:18) Kufanya uzinzi ni ‘kumtendea Mungu’ dhambi na ni pigo kubwa sana kwa mwenzi mwaminifu. (Mwa. 39:7-9) Mwenzi aliyesalitiwa anaweza kuhisi maumivu makali ya kihisia kwa miaka mingi sana.

6 Yehova anajua vizuri sana jinsi wenzi wa ndoa wanavyotendeana. Na hususan alitaka wanawake walioolewa katika Israeli watendewe vizuri. Mwanamume aliyeiheshimu Sheria, alimpenda mke wake na hangemtaliki kwa sababu ndogo-ndogo. (Kum. 24:1-4; Mt. 19:3, 8) Lakini ikiwa tatizo zito lingetokea naye alazimike kumtaliki, alipaswa kumpa cheti cha talaka. Cheti hicho kilimlinda mwanamke huyo asishtakiwe isivyo haki kwamba amefanya uasherati. Isitoshe, inaonekana kwamba kabla ya mwanamume kumpa mke wake cheti cha talaka, alipaswa kuzungumza na wazee wa jiji. Kwa njia hiyo, wazee wa jiji wangepata fursa ya kuwasaidia wenzi hao kuokoa ndoa yao. Mwanamume Mwisraeli alipomtaliki mke wake kwa sababu ya ubinafsi, Yehova hakuingilia kati jambo hilo nyakati zote. Ingawa hivyo, aliona machozi ya mwanamke huyo, na alihisi maumivu yake.—Mal. 2:13-16.

(Tazama fungu la 7 na 8) *

7-8. (a) Yehova aliwaamuru wazazi wafanye nini? (Tazama picha kwenye jalada.) (b) Tunajifunza mambo gani?

7 Sheria inafunua pia kwamba Yehova anawajali sana watoto. Yehova hakuwaamuru wazazi wawaandalie watoto wao mahitaji ya kimwili tu, bali pia mahitaji ya kiroho. Wazazi walipaswa kutumia kila fursa kuwafundisha watoto wao kumpenda Yehova na kuwasaidia kuelewa na kuithamini Sheria yake. (Kum. 6:6-9; 7:13) Sababu moja iliyofanya Waisraeli waadhibiwe na Yehova ni kwamba waliwatesa watoto wao kwa njia yenye kushtua. (Yer. 7:31, 33) Wazazi hawakupaswa kuwaona watoto wao kama vitu vinavyoweza kupuuzwa au kutelekezwa, bali kama urithi, zawadi kutoka kwa Yehova iliyopaswa kutunzwa vizuri.—Zab. 127:3.

8 Somo: Yehova anaona vizuri jinsi wenzi wa ndoa wanavyotendeana. Anataka wazazi wawapende watoto wao, na atawahukumu kulingana na wanavyowatendea watoto wao.

9-11. Kwa nini Yehova alitoa sheria iliyokataza kutamani?

9 Usitamani. Amri ya mwisho kwenye zile Amri Kumi ilikataza kutamani, au kuwa na tamaa isiyofaa kuelekea mali ya mtu mwingine. (Kum. 5:21; Rom. 7:7) Yehova alitoa sheria hiyo ili kufundisha jambo fulani muhimu—ni lazima watu wake walinde mioyo yao, yaani, mawazo, hisia, na njia yao ya kufikiri. Anajua kwamba hisia na mawazo maovu huongoza kwenye matendo maovu. (Met. 4:23) Ikiwa Mwisraeli angeruhusu tamaa mbaya isitawi moyoni mwake, ingekuwa rahisi kwake kuwatendea wengine kwa njia isiyo na upendo. Mfalme Daudi alinaswa na mtego huo. Kwa ujumla, alikuwa mtu mzuri. Lakini pindi moja, alimtamani mke wa mwanamume mwingine. Tamaa hiyo ilimfanya atende dhambi. (Yak. 1:14, 15) Daudi alifanya uzinzi, akajaribu kumdanganya mume wa mwanamke huyo, na kisha akapanga auawe.—2 Sam. 11:2-4; 12:7-11.

10 Yehova alijua wakati ambapo Mwisraeli alivunja sheria iliyokataza kutamani—Anaweza kusoma moyo. (1 Nya. 28:9) Sheria iliyokataza kutamani iliwasaidia watu wake kufahamu kwamba walipaswa kuepuka mawazo yaliyoongoza kwenye matendo mabaya. Kwa kweli Yehova ni Baba mwenye hekima na upendo sana!

11 Somo: Yehova haangalii tu sura ya nje. Anaona jinsi tulivyo hasa kwa ndani, yaani, jinsi tulivyo moyoni. (1 Sam. 16:7) Hakuna wazo, hisia, au tendo lolote tunaloweza kumficha. Yeye hutafuta mambo mazuri ndani yetu na kutusaidia kuyakuza. Lakini anataka tutambue na kudhibiti mawazo mabaya kabla hayajatuongoza kwenye matendo mabaya.—2 Nya. 16:9; Mt. 5:27-30.

MFUMO WA SHERIA ULIOTETEA HAKI

12. Sheria ya Musa inakazia nini?

12 Sheria ya Musa inakazia pia kwamba Yehova anapenda haki. (Zab. 37:28; Isa. 61:8) Ametuwekea kielelezo kikamilifu cha jinsi ya kuwatendea wengine bila upendeleo. Waisraeli walipotii sheria ambazo Yehova aliwapa, Yehova aliwabariki. Walipopuuza viwango vyake vya haki na uadilifu, walipatwa na matatizo. Fikiria sheria nyingine mbili kati ya zile Amri Kumi.

13-14. Sheria mbili za kwanza katika zile Amri Kumi ziliwataka Waisraeli wafanye nini, nao wangenufaikaje kwa kuzitii?

13 Mwabudu Yehova peke yake. Sheria mbili za kwanza katika zile Amri Kumi ziliwataka Waisraeli wamwabudu Yehova peke yake na ziliwaonya dhidi ya kuabudu sanamu. (Kut. 20:3-6) Yehova hakutoa amri hizo kwa faida yake. Badala yake, zilikusudiwa ziwanufaishe watu wake. Watu wake walipoendelea kuwa washikamanifu kwake, walipata ufanisi. Walipoabudu miungu ya mataifa mengine, walipatwa na matatizo.

14 Wafikirie Wakanaani. Waliabudu sanamu zisizo na uhai badala ya kumwabudu Mungu wa kweli aliye hai. Na kwa sababu hiyo, walijishushia heshima. (Zab. 115:4-8) Ibada yao ilihusisha matendo machafu sana ya kingono na zoea lenye kushtua la kuwateketeza motoni watoto wao kama dhabihu. Vivyo hivyo, Waisraeli walipompuuza Yehova na kuchagua kuabudu sanamu, walijishushia heshima na kuumiza familia zao. (2 Nya. 28:1-4) Wale waliokuwa na mamlaka waliacha kufuata viwango vya Yehova vya haki. Walitumia vibaya mamlaka yao kwa kuwakandamiza watu wa hali ya chini na wanyonge. (Eze. 34:1-4) Yehova aliwaonya Waisraeli kwamba angeleta hukumu dhidi ya wale waliowatesa wanawake na watoto ambao hawakuwa na mtetezi. (Kum. 10:17, 18; 27:19) Kinyume cha hilo, Yehova aliwabariki watu wake walipoendelea kuwa washikamanifu kwake na kuwatendea wengine kwa haki.—1 Fal. 10:4-9.

Yehova anatupenda na anajua tunapotendewa isivyo haki (Tazama fungu la 15)

15. Tunajifunza mambo gani kumhusu Yehova?

15 Somo: Yehova hapaswi kulaumiwa wakati ambapo wale wanaodai kuwa watumishi wake wanapuuza viwango vyake na kuwaumiza watu wake. Hata hivyo, Yehova anatupenda na anajua tunapotendewa isivyo haki. Anahisi kikamili maumivu yetu hata kuliko jinsi mama anavyohisi maumivu ya mtoto wake. (Isa. 49:15) Ingawa huenda asiingilie kati mara moja, kwa wakati unaofaa atawatoza hesabu watenda dhambi wasiotubu kulingana na jinsi walivyowatendea wengine.

SHERIA ILIPASWA KUTEKELEZWA JINSI GANI?

16-18. Sheria ya Musa iligusa nyanja gani mbalimbali, na tunajifunza mambo gani?

16 Sheria ya Musa iligusa nyanja mbalimbali za maisha ya Waisraeli, hivyo lilikuwa jambo muhimu kwa wanaume wazee waliowekwa rasmi kuwahukumu kwa haki watu wa Yehova. Mbali na kushughulikia kesi za madai na za uhalifu, wazee waliowekwa rasmi walikuwa na jukumu la kushughulikia mambo ya kiroho. Fikiria mifano ifuatayo.

17 Ikiwa Mwisraeli angemuua mtu mwingine, hilo halikumaanisha moja kwa moja kwamba alistahili kuuawa. Wazee wa jiji lake walichunguza hali zilizohusika kabla ya kuamua ikiwa alistahili kuhukumiwa kifo. (Kum. 19:2-7, 11-13) Pia, walisikiliza kesi mbalimbali zilizohusu maisha ya kila siku—iwe ni mizozo kuhusu mali au matatizo ya ndoa. (Kut. 21:35; Kum. 22:13-19) Wazee walipotenda kwa haki na Waisraeli walipotii Sheria, kila mtu alinufaika, na taifa zima lilimletea Yehova heshima.—Law. 20:7, 8; Isa. 48:17, 18.

18 Somo: Yehova anapendezwa na kila nyanja ya maisha yetu. Anataka tuwatendee wengine kwa haki na upendo. Naye anajua mambo tunayosema na kutenda, hata tunapokuwa nyumbani peke yetu.—Ebr. 4:13.

19-21. (a) Wanaume wazee na waamuzi walipaswa kuwatendeaje watu wa Mungu? (b) Sheria ambazo Yehova aliweka ziliwalinda watu wake jinsi gani, na tunajifunza mambo gani?

19 Yehova alitaka kuwalinda watu wake wasiathiriwe na mazoea mapotovu ya mataifa jirani. Hivyo, aliwataka wanaume wazee na waamuzi watekeleze Sheria bila upendeleo. Hata hivyo, wanaume hao hawakupaswa kuwatendea watu wake kwa ukali au bila huruma. Badala yake, walipaswa kupenda haki.—Kum. 1:13-17; 16:18-20.

20 Yehova ana huruma kuelekea watu wake, hivyo aliweka sheria mbalimbali zilizowalinda watu wake wasitendewe isivyo haki. Kwa mfano, Sheria ilipunguza uwezekano wa mtu kushtakiwa kwa uwongo kwa kosa ambalo hakufanya. Mshtakiwa alikuwa na haki ya kujua ni nani aliyemshtaki. (Kum. 19:16-19; 25:1) Na kabla ya kuhukumiwa kuwa na hatia, angalau mashahidi wawili walipaswa kutoa ushahidi. (Kum. 17:6; 19:15) Vipi kuhusu Mwisraeli aliyetenda kosa lililoshuhudiwa na mtu mmoja tu? Hakupaswa kuwazia kwamba hataadhibiwa kwa kosa hilo. Yehova aliona jambo alilofanya. Katika familia, akina baba walikuwa na mamlaka, lakini mamlaka hiyo ilikuwa na mipaka. Wazee wa jiji walikuwa na jukumu la kusikiliza baadhi ya migogoro ya kifamilia na kutoa uamuzi wa mwisho.—Kum. 21:18-21.

21 Somo: Yehova ameweka mfano mkamilifu; hana upendeleo hata kidogo. (Zab. 9:7) Yeye huwathawabisha wale wanaotii kwa ushikamanifu viwango vyake, lakini huwaadhibu wale wanaotumia vibaya mamlaka yao. (2 Sam. 22:21-23; Eze. 9:9, 10) Huenda baadhi ya watu wakatenda kwa uovu na ikaonekana ni kana kwamba hawataadhibiwa, lakini Yehova anapoamua kwamba wakati umefika wa kuwaadhibu, anahakikisha kwamba wanapokea hukumu yao. (Met. 28:13) Na ikiwa hawatubu, muda si muda wanatambua kwamba “ni jambo lenye kuogopesha kuanguka mikononi mwa Mungu aliye hai.”—Ebr. 10:30, 31.

SHERIA ILIWALINDA NANI HASA?

Walipokuwa wakisuluhisha mizozo, wazee walipaswa kumwiga Yehova kwa kuwapenda watu na kupenda haki (Tazama fungu la 22) *

22-24. (a) Sheria iliwalinda nani hasa, na tunajifunza mambo gani kumhusu Yehova? (b) Ni onyo gani linalopatikana kwenye Kutoka 22:22-24?

22 Sheria iliwalinda hasa wale ambao hawangeweza kujitetea, kama vile mayatima, wajane, na wakaaji wageni. Waamuzi wa Israeli waliambiwa hivi: “Usipotoshe hukumu ya mkaaji mgeni au ya yatima, nawe hupaswi kuchukua vazi la mjane kuwa dhamana ya mkopo.” (Kum. 24:17) Yehova alipendezwa kibinafsi na kuwajali kwa wororo maskini na wanyonge katika jamii. Naye aliwaadhibu wale waliowatesa.—Soma Kutoka 22:22-24.

23 Pia, Sheria iliwalinda washiriki wa familia kutokana na makosa mazito ya kingono kwa kukataza aina zote za ngono kati ya watu wa familia moja. (Law. 18:6-30) Tofauti na watu wa mataifa yaliyowazunguka Waisraeli, ambao hawakuona ubaya wa zoea hilo na hata waliliunga mkono, watu wa Yehova walipaswa kuwa na maoni kama ya Yehova kulihusu, kwamba ni tendo lenye kuchukiza.

24 Somo: Yehova anawataka wale anaowapa mamlaka miongoni mwa watu wake wawapende na kuwajali wale walio chini yao. Anachukia uhalifu wa kingono na anataka kuhakikisha kwamba watu wote, na hasa wanyonge, wanalindwa na kutendewa kwa haki.

SHERIA, “KIVULI CHA MAMBO MEMA YATAKAYOKUJA”

25-26. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba upendo na haki ni kama pumzi na uhai? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata kwenye mfululizo huu?

25 Upendo na haki ni kama pumzi na uhai; bila kimoja kingine hakiwezi kuwapo. Tunaposadiki kwamba Yehova hututendea kwa haki, upendo wetu kwake huongezeka. Na tunapompenda Mungu na kupenda viwango vyake vya uadilifu, tunachochewa kuwapenda wengine na kuwatendea kwa haki.

26 Agano la Sheria ya Musa liliwasaidia Waisraeli kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Hata hivyo, Sheria ilifutiliwa mbali baada ya Yesu kuitimiza, na mahali pake pakachukuliwa na kitu bora zaidi. (Rom. 10:4) Mtume Paulo aliifafanua Sheria kuwa “kivuli cha mambo mema yatakayokuja.” (Ebr. 10:1) Makala inayofuata katika mfululizo huu itazungumzia baadhi ya mambo hayo mema na umuhimu wa upendo na haki katika kutaniko la Kikristo.

WIMBO 109 Pendaneni Sana Kutoka Moyoni

^ fu. 5 Makala hii ni ya kwanza katika mfululizo wa makala nne utakaozungumzia kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anatujali. Makala tatu zilizosalia zitapatikana katika toleo la Mei 2019 la gazeti la Mnara wa Mlinzi. Vichwa vya makala hizo ni “Upendo na Haki Katika Kutaniko la Kikristo,” “Upendo na Haki Katika Ulimwengu Mwovu,” na “Faraja kwa Watu Waliotendewa Vibaya Kingono.”

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Sheria 600 na nyingine ambazo Yehova aliwapa Waisraeli kupitia Musa huitwa “Sheria,” “Sheria ya Musa,” na “zile amri.” Zaidi ya hilo, vitabu vya kwanza vya Biblia (Mwanzo hadi Kumbukumbu la Torati) kwa kawaida huitwa Sheria. Nyakati nyingine neno hilo hurejelea Maandiko yote ya Kiebrania yaliyoongozwa na roho ya Mungu.

^ fu. 60 PICHA KWENYE JALADA: Yehova alitaka watoto wajihisi wakiwa salama na walelewe na kufundishwa kwa upendo na wazazi wao

MAELEZO YA PICHA: Mama Mwisraeli akifurahia mazungumzo yenye kuchangamsha pamoja na binti zake huku wakitayarisha chakula. Nyuma yao, baba anamzoeza mwanaye kutunza kondoo.

^ fu. 64 MAELEZO YA PICHA: Wazee wakiwa kwenye lango la jiji wakimsaidia kwa upendo mjane na mtoto wake ambao wamedhulumiwa na mfanyabiashara.