Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Sinagogi la Karne ya Kwanza: Mchoro huu unaonyesha baadhi ya sehemu za sinagogi la karne ya kwanza lililoko Gamla, kilomita 10 kaskazini mashariki mwa Bahari ya Galilaya. Unatusaidia kuelewa jinsi masinagogi ya zamani yalivyokuwa

Masinagogi Yalitoka Wapi?

NENO “sinagogi” linatokana na neno la Kigiriki linalomaanisha “kusanyiko” au “kukusanyika pamoja.” Neno hilo linafaa kwa sababu tangu nyakati za zamani Wayahudi wamekuwa wakikusanyika pamoja kwenye masinagogi kwa ajili ya ibada na kufundishwa. Maandiko ya Kiebrania hayataji moja kwa moja neno sinagogi, lakini tunaona katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kwamba kufikia karne ya kwanza W.K., watu walikuwa wakikutanika kwa ukawaida katika masinagogi.

Wasomi wengi wanaamini kwamba Wayahudi walianza kutumia masinagogi walipokuwa utekwani Babiloni. Encyclopaedia Judaica inasema hivi: “Watu waliohamishwa walijipata katika nchi ya kigeni ambapo hakukuwa na hekalu, na walihitaji faraja kwa sababu ya taabu zao, hivyo wangekutanika mara kwa mara, huenda siku ya Sabato ili kusoma Maandiko.” Baada ya kuachiliwa huru kutoka uhamishoni, inaonekana kwamba Wayahudi waliendelea kukusanyika ili kusali na kusoma Maandiko, na walijenga masinagogi mahali popote walipohamia.

Hivyo, kufikia karne ya kwanza W.K., masinagogi yakawa kitovu cha dini ya Kiyahudi na sehemu ya maisha ya kila siku ya Wayahudi waliokuwa wakiishi katika eneo la Mediterania, Mashariki ya Kati, na eneo la Israeli. Profesa Lee Levine wa chuo fulani kikuu (The Hebrew University of Jerusalem) anaeleza hivi: “[Masinagogi] yalikuwa mahali ambapo watu walikuja ili kusoma, kula milo mitakatifu, kusikiliza kesi, kutoa michango ya jamii, na kufanyia mikutano ya kisiasa na ya kijamii.” Anaendelea kusema hivi: “Hata hivyo, jambo kuu lilikuwa kukutanika kwa ajili ya ibada.” Hivyo, haishangazi kwa nini Yesu alienda mara nyingi kwenye masinagogi. (Marko 1:21; 6:2; Luka 4:16) Aliwafundisha, aliwahimiza, na kuwatia moyo wale waliokusanyika kwenye masinagogi. Vivyo hivyo, baada ya kuanzishwa kwa kutaniko la Kikristo, mtume Paulo alihubiri mara nyingi katika masinagogi. Kwa kawaida watu waliopendezwa na mambo ya kiroho walienda katika masinagogi, hivyo Paulo alipoingia katika jiji fulani alikuwa na mazoea ya kwenda kwanza kwenye masinagogi ili kuhubiri huko.—Mdo. 17:1, 2; 18:4.