Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 12

Onyesha Kwamba Unajali Hisia za Wengine

Onyesha Kwamba Unajali Hisia za Wengine

“Ninyi nyote . . . muwe na hisia-mwenzi.”—1 PET. 3:8.

WIMBO 90 Tianeni Moyo

MUHTASARI *

1. Kulingana na 1 Petro 3:8, kwa nini sisi hufurahia kushirikiana na watu wanaojali hisia zetu na hali yetu njema?

SISI hufurahia kushirikiana na watu wanaojali hisia zetu na hali yetu njema. Wao hujitahidi kujiweka katika hali zetu, yaani, wanajitahidi kutambua mawazo na hisia zetu. Wanajitahidi kutambua kimbele mahitaji yetu na kutupatia msaada, na nyakati nyingine wanafanya hivyo hata kabla hatujawaomba msaada. Tunawathamini watu wanaotuonyesha “hisia-mwenzi.” *Soma 1 Petro 3:8.

2. Kwa nini huenda ikawa vigumu kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi?

2 Tukiwa Wakristo, sisi sote tungependa kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi. Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba si rahisi kufanya hivyo. Kwa nini? Kwanza, sisi si wakamilifu. (Rom. 3:23) Hivyo, ni lazima tushinde mwelekeo tuliozaliwa nao wa kujifikiria wenyewe. Pili, huenda ikawa vigumu kwa baadhi yetu kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi kwa sababu ya malezi au mambo tuliyopitia maishani. Na tatu, huenda tumeathiriwa na mtazamo wa watu wanaotuzunguka. Katika siku hizi za mwisho, watu wengi hawajali hisia za wengine. Badala yake, ‘wanajipenda wenyewe.’ (2 Tim. 3:1, 2) Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda mambo yanayofanya iwe vigumu kwetu kujali hisia za wengine?

3. (a) Tunaweza kuboreshaje jinsi tunavyowaonyesha wengine hisia-mwenzi? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Tunaweza kuboresha jinsi tunavyowaonyesha wengine hisia-mwenzi kwa kumwiga Yehova Mungu na Yesu Kristo, Mwana wake. Yehova ni Mungu mwenye upendo, naye ameweka mfano bora kabisa wa kuwajali wengine. (1 Yoh. 4:8) Yesu aliiga kikamilifu utu wa Baba yake. (Yoh. 14:9) Alipokuwa duniani, alionyesha jinsi mwanadamu anavyoweza kuonyesha huruma. Jambo la kwanza tutakalojifunza katika makala hii, ni jinsi ambavyo Yehova na Yesu wameonyesha kwamba wanajali hisia za wengine. Kisha tutajifunza jinsi tunavyoweza kuiga mfano wao.

MFANO WA YEHOVA WA KUWAJALI WENGINE

4. Andiko la Isaya 63:7-9 linaonyeshaje kwamba Yehova anajali hisia za watumishi wake?

4 Biblia hufundisha kwamba Yehova anajali hisia za watumishi wake. Kwa mfano, fikiria jinsi Yehova alivyohisi taifa la kale la Israeli lilipopitia majaribu mbalimbali. Neno la Mungu linasema hivi: “Katika taabu zao zote, yeye alitaabika.” (Soma Isaya 63:7-9.) Baadaye, kupitia nabii Zekaria, Yehova alitangaza kwamba watu wake wanapoteswa anahisi ni kana kwamba yeye ndiye anayeteswa. Yehova aliwaambia hivi watumishi wake: “Yeyote anayewagusa ninyi anaigusa mboni ya jicho langu.” (Zek. 2:8) Huo ni ulinganisho mzuri sana unaoonyesha jinsi Yehova anavyowajali watu wake!

Kwa huruma, Yehova aliwakomboa Waisraeli kutoka utumwani Misri (Tazama fungu la 5)

5. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yehova alivyochukua hatua ya kuwasaidia watumishi wake waliokuwa wakiteseka.

5 Yehova anafanya mengi zaidi ya kuhisi tu kwamba anawahurumia watumishi wake wanaoteseka. Anachukua hatua ya kuwasaidia. Kwa mfano, Waisraeli walipokuwa wakiteseka wakiwa watumwa nchini Misri, Yehova alielewa maumivu yao na alichochewa kuwapa kitulizo. Yehova alimwambia Musa hivi: “Hakika nimeyaona mateso ya watu wangu . . . , nami nimesikia kilio chao . . . ninajua vema maumivu yao. Nitashuka huko ili niwaokoe kutoka mikononi mwa Wamisri.” (Kut. 3:7, 8) Kwa kuwa Yehova aliwahurumia watu wake, aliwakomboa kutoka utumwani. Karne nyingi baadaye, Waisraeli walipokuwa katika Nchi ya Ahadi, walishambuliwa na maadui. Yehova alitendaje? “Aliwahurumia kwa sababu ya kilio chao cha uchungu kilichosababishwa na wale waliowakandamiza na wale waliowatesa.” Kwa mara nyingine tena, sifa ya hisia-mwenzi ilimchochea Yehova kuwasaidia watu wake. Aliwatuma waamuzi ili kuwaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa maadui wao.—Amu. 2:16, 18.

6. Toa mfano unaoonyesha jinsi Yehova alivyojali hisia za mtu ambaye njia yake ya kufikiri haikuwa sahihi.

6 Yehova hujali hisia za watu wake—hata wakati ambapo njia yao ya kufikiri si sahihi. Mfikirie Yona. Mungu alimtuma nabii huyo akatangaze ujumbe wa hukumu dhidi ya Waninawi. Walipotubu, Mungu aliamua kwamba hatawaangamiza. Hata hivyo, Yona hakufurahishwa na uamuzi huo. ‘Alikasirika sana’ kwa sababu unabii wake wa maangamizi haukutimia. Lakini Yehova alikuwa na subira kumwelekea Yona na akamsaidia kurekebisha njia yake ya kufikiri. (Yona 3:10–4:11) Baada ya muda, Yona alipata somo, na hata alitumiwa na Yehova kuandika simulizi hilo kwa faida yetu.—Rom. 15:4. *

7. Masimulizi ya jinsi Yehova alivyoshughulika na watumishi wake yanatuhakikishia nini?

7 Masimulizi ya jinsi Yehova alivyoshughulika na watu wake yanatuhakikishia kwamba anajali hisia za watumishi wake. Anajua maumivu na mateso ya kila mmoja wetu. Yehova ‘anaujua vizuri moyo wa mwanadamu.’ (2 Nya. 6:30) Anaelewa mawazo yetu yote, hisia zetu za ndani kabisa, na uwezo wetu. Na ‘hatatuacha tujaribiwe kupita tunavyoweza kuhimili.’ (1 Kor. 10:13) Huo ni uhakikisho wenye kufariji sana!

MFANO WA YESU WA KUWAJALI WENGINE

8-10. Ni mambo gani ambayo yalimchochea Yesu kuwajali wengine?

8 Alipokuwa mwanadamu hapa duniani, Yesu aliwajali sana wengine. Kuna mambo matatu hivi yaliyomchochea Yesu kuwajali wengine. Kwanza, kama ilivyotajwa awali, Yesu aliiga kikamilifu utu wa Baba yake. Kama Baba yake, Yesu pia aliwapenda watu. Ingawa alishangilia kwa sababu ya kila kitu ambacho alimsaidia Yehova kufanya, Yesu ‘aliwapenda sana wanadamu.’ (Met. 8:31) Upendo ulimchochea Yesu kujali hisia za wengine.

9 Pili, kama Yehova, Yesu alikuwa na uwezo wa kusoma moyo. Alikuwa na uwezo wa kujua nia na hisia za watu. (Mt. 9:4; Yoh. 13:10, 11) Hivyo, Yesu alipotambua kwamba watu walikuwa wamevunjika moyo, sifa ya hisia-mwenzi ilimchochea kuwafariji.—Isa. 61:1, 2; Luka 4:17-21.

10 Tatu, Yesu mwenyewe alikabili baadhi ya changamoto ambazo ziliwapata watu. Kwa mfano, inaonekana kwamba Yesu alizaliwa na kulelewa katika familia maskini. Kwa kufanya kazi na Yosefu, baba yake mlezi, Yesu alijifunza jinsi ya kufanya kazi ngumu za mikono. (Mt. 13:55; Marko 6:3) Inaonekana kwamba Yosefu alikufa wakati fulani kabla ya Yesu kumaliza huduma yake. Hivyo, inaelekea kwamba Yesu alihisi maumivu ambayo mtu hupata anapopoteza mpendwa wake katika kifo. Na Yesu alijua jinsi mtu anavyohisi anapokuwa katika familia yenye watu wenye maoni yanayotofautiana kuhusu dini. (Yoh. 7:5) Hali hizo pamoja na nyingine zingeweza kumsaidia Yesu kuelewa changamoto na hisia za watu wa kawaida.

Yesu anamchukua mwanamume fulani kiziwi mbali na umati na anachochewa na huruma kumponya (Tazama fungu la 11)

11. Hisia za Yesu za kuwajali watu zilionekana waziwazi hasa wakati gani? Eleza. (Tazama picha kwenye jalada.)

11 Hisia za Yesu za kuwajali watu zilionekana waziwazi hasa kupitia miujiza aliyofanya. Yesu hakufanya miujiza ili tu kutimiza wajibu. ‘Aliwasikitikia’ wale waliokuwa wakiteseka. (Mt. 20:29-34; Marko 1:40-42) Kwa mfano, wazia hisia ambazo Yesu alikuwa nazo alipompeleka mwanamume fulani kiziwi mbali na umati na kumponya au alipokuwa akimfufua mwana pekee wa mjane fulani. (Marko 7:32-35; Luka 7:12-15) Yesu aliwahurumia watu hao na alitaka kuwasaidia.

12. Andiko la Yohana 11:32-35 linatusaidiaje kujua kwamba Yesu aliwaonyesha hisia-mwenzi Martha na Maria?

12 Yesu aliwaonyesha hisia-mwenzi Martha na Maria. Alipoona huzuni waliyokuwa nayo kwa sababu ya kufiwa na Lazaro, ndugu yao, “Yesu akatokwa na machozi.” (Soma Yohana 11:32-35.) Hakutokwa na machozi kwa sababu tu alikuwa amempoteza rafiki yake wa karibu. Bila shaka alijua kwamba angemfufua Lazaro. Yesu alitokwa na machozi kwa sababu alielewa na aliguswa na maumivu ya moyoni ambayo rafiki zake wapendwa walikuwa nayo.

13. Kwa nini tunatiwa moyo tunapojifunza jinsi Yesu alivyowaonyesha wengine hisia-mwenzi?

13 Tunanufaika sana tunapojifunza jinsi Yesu alivyowaonyesha watu hisia-mwenzi. Ni kweli kwamba, tofauti na Yesu, sisi si wakamilifu. Ingawa hivyo, tunampenda kwa sababu ya jinsi alivyowatendea watu kwa huruma. (1 Pet. 1:8) Tunatiwa moyo kujua kwamba sasa anatawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Hivi karibuni atakomesha mateso yote. Kwa kuwa Yesu aliwahi kuwa mwanadamu, yeye ndiye anayefaa zaidi kuwasaidia wanadamu wapone kutokana na madhara yaliyosababishwa na utawala wa Shetani. Kwa kweli, tumebarikiwa sana kuwa na Mtawala ambaye anaweza “kuusikitikia udhaifu wetu.”—Ebr. 2:17, 18; 4:15, 16.

MWIGE YEHOVA NA YESU

14. Kwa msingi wa andiko la Waefeso 5:1, 2, tunachochewa kufanya nini?

14 Tunapochunguza mfano ambao Yehova na Yesu wametuwekea, sisi pia tunachochewa kujitahidi kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi kwa kadiri kubwa zaidi. (Soma Waefeso 5:1, 2.) Tofauti nao, sisi hatuwezi kusoma moyo. Ingawa hivyo, tunaweza kujitahidi kuelewa hisia na mahitaji ya wengine. (2 Kor. 11:29) Tofauti na ulimwengu huu wenye ubinafsi, sisi hujitahidi ‘kuangalia, si faida zetu wenyewe, bali pia faida za wengine.’—Flp. 2:4.

(Tazama fungu la 15 hadi 19) *

15. Ni nani hasa wanaohitaji kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi?

15 Wazee wa kutaniko hasa wanahitaji kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi. Wanajua kwamba wanawajibika kwa Yehova kwa jinsi wanavyowatunza kondoo wake. (Ebr. 13:17) Ili wawasaidie waabudu wenzao, wazee wanapaswa kujali hisia za wengine. Wazee wanaweza kuwaonyeshaje wengine hisia-mwenzi?

16. Mzee wa kutaniko anayejali hisia za wengine hufanya nini, na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo?

16 Mzee wa kutaniko anayejali hisia za wengine, hutumia wakati pamoja na ndugu na dada zake Wakristo. Yeye huwauliza maswali na kuwasikiliza kwa makini na kwa subira. Jambo hilo ni muhimu hasa wakati ambapo mmoja wa kondoo mpendwa wa Yehova anataka kumimina moyo wake lakini anashindwa kujieleza vizuri. (Met. 20:5) Mzee wa kutaniko anapokuwa tayari kutumia muda wake pamoja na ndugu zake, yeye hujenga urafiki, upendo, na uhusiano wenye nguvu wa kutumainiana pamoja na ndugu zake.—Mdo. 20:37.

17. Ni sifa gani ambayo ndugu na dada wengi huthamini zaidi wazee wa kutaniko wanapoionyesha? Toa mfano.

17 Ndugu na dada wengi husema kwamba sifa wanayothamini zaidi wazee wa kutaniko wanapoionyesha ni hisia-mwenzi au kujali hisia za wengine. Kwa nini? Adelaide anasema hivi: “Ni rahisi zaidi kuzungumza nao kwa sababu unajua kwamba watakuelewa.” Anaongeza hivi: “Unaweza kutambua kwamba wanaelewa hali yako kupitia jinsi wanavyoitikia unapozungumza nao.” Ndugu mmoja anaguswa moyo sana anapokumbuka hivi: “Niliona machozi yakimlengalenga mzee mmoja wa kutaniko nilipokuwa nikisimulia hali yangu. Taswira hiyo haitafutika kamwe akilini mwangu.”—Rom. 12:15.

18. Tunaweza kusitawishaje hisia-mwenzi kuwaelekea wengine?

18 Bila shaka, si wazee tu wanaohitaji kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi. Sisi sote tunaweza kusitawisha sifa hiyo. Jinsi gani? Jitahidi kuelewa hali ambazo watu wa familia yako au waabudu wenzako wanapitia. Pendezwa kibinafsi na vijana kutanikoni na vilevile wagonjwa, na ndugu na dada wenye umri mkubwa na wale ambao wamefiwa na wapendwa wao. Waulize wanaendeleaje. Wasikilize kwa makini wanapojieleza. Wafanye wahisi kwamba unaelewa vizuri mambo wanayokabiliana nayo. Waeleze kwamba uko tayari kuwasaidia kadiri uwezavyo. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwa matendo upendo wa kweli.—1 Yoh. 3:18.

19. Kwa nini tunahitaji kubadilikana kulingana na hali tunapojitahidi kuwasaidia wengine?

19 Tunahitaji kubadilikana kulingana na hali tunapojitahidi kuwasaidia wengine. Kwa nini? Kwa sababu watu hutenda kwa njia tofauti-tofauti wanapopatwa na hali ngumu. Wengine huwa tayari kujieleza, ilhali wengine hawapendi kuzungumzia matatizo yao. Tungependa kuwasaidia, lakini tunapaswa kuepuka kuwauliza maswali ambayo hawatajihisi huru kuyajibu. (1 The. 4:11) Hata wengine wanapojihisi huru kujieleza, huenda tukatambua kwamba nyakati nyingine hatukubaliani na maoni yao. Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba hivyo ndivyo wanavyohisi. Tungependa kuwa wepesi wa kusikia, si wepesi wa kusema.—Mt. 7:1; Yak. 1:19.

20. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Mbali na kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi kutanikoni, tungependa kuonyesha sifa hiyo yenye kuvutia tunapokuwa katika huduma. Tunaweza kuonyeshaje hisia-mwenzi tunapofanya wanafunzi? Tutachunguza jambo hilo katika makala inayofuata.

WIMBO 130 Uwe Mwenye Kusamehe

^ fu. 5 Yehova na Yesu wanajali hisia za wengine. Katika makala hii, tutazungumzia mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wao. Pia, tutazungumzia kwa nini tunahitaji kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi na jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

^ fu. 1 UFAFANUZI WA MANENO: Kuonyesha “hisia-mwenzi” kunamaanisha kujitahidi kuelewa jinsi wengine wanavyohisi na kuhisi kama wanavyohisi. (Rom. 12:15) Katika makala hii, maneno “hisia-mwenzi” na “kujali” yana maana ileile.

^ fu. 6 Pia, Yehova aliwatendea kwa huruma watumishi wake wengine waaminifu waliovunjika moyo au kuogopa. Fikiria simulizi la Hana (1 Sam. 1:10-20), Eliya (1 Fal. 19:1-18), na Ebed-meleki (Yer. 38:7-13; 39:15-18).

^ fu. 65 MAELEZO YA PICHA: Mikutano ya kutaniko katika Jumba la Ufalme hutupatia fursa nyingi za kufurahia ushirika mchangamfu. Tunamwona (1) mzee wa kutaniko akizungumza kwa fadhili na mhubiri mwenye umri mdogo pamoja na mama yake, (2) baba na binti yake wakimsaidia dada mwenye umri mkubwa kuingia kwenye gari, na (3) wazee wawili wa kutaniko wakimsikiliza kwa makini dada anayeomba ushauri.