Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 13

Onyesha Hisia-Mwenzi Katika Huduma

Onyesha Hisia-Mwenzi Katika Huduma

“Akawasikitikia . . . Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.”—MARKO 6:34.

WIMBO 70 Tafuteni Wanaostahili

MUHTASARI *

1. Ni sifa gani inayogusa moyo sana ya utu wa Yesu? Eleza.

MOJAWAPO ya sifa zenye kugusa moyo sana za utu wa Yesu ni uwezo wake wa kuelewa changamoto ambazo sisi wanadamu wasio wakamilifu tunapambana nazo. Alipokuwa duniani, Yesu ‘alishangilia na wale wanaoshangilia na kulia na wale wanaolia.’ (Rom. 12:15) Kwa mfano, wanafunzi wake 70 waliporudi wakiwa na shangwe baada ya kukamilisha kwa mafanikio mgawo wao wa kuhubiri, Yesu “akawa na shangwe kubwa kupitia roho takatifu.” (Luka 10:17-21) Kwa upande mwingine, alipoona jinsi kifo cha Lazaro kilivyowaathiri wapendwa wake, Yesu ‘aliugua moyoni na kutaabika.’—Yoh. 11:33.

2. Ni nini kilichomfanya Yesu awaonyeshe wanadamu hisia-mwenzi?

2 Ni nini kilichomfanya mwanamume huyo mkamilifu awe na rehema nyingi hivyo na huruma aliposhughulika na wanadamu wenye dhambi? Kwanza kabisa, Yesu aliwapenda watu. Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, Yesu ‘aliwapenda sana wanadamu.’ (Met. 8:31) Upendo wake kuelekea wanadamu ulimchochea kufahamu kwa undani jinsi ambavyo wanadamu hufikiri. Mtume Yohana anaeleza hivi: “Alijua kilicho ndani ya mwanadamu.” (Yoh. 2:25) Yesu alikuwa na hisia nyororo kuwaelekea wanadamu. Watu walihisi kwamba Yesu aliwapenda na kwa sababu hiyo, walisikiliza ujumbe wake wa Ufalme. Kadiri tunavyozidi kusitawisha hisia nyororo kama hizo kuelekea watu, ndivyo tutakavyopata matokeo mazuri zaidi tunapojitahidi kutimiza huduma yetu.—2 Tim. 4:5.

3-4. (a) Ikiwa tuna sifa ya hisia-mwenzi, tutahisije kuhusu huduma yetu? (b) Tutajifunza nini katika makala hii?

3 Mtume Paulo alijua kwamba alikuwa na wajibu wa kuhubiri, na ndivyo ilivyo kwetu pia. (1 Kor. 9:16) Hata hivyo, tukiwa na sifa ya hisia-mwenzi, hatutahisi kwamba huduma yetu ni wajibu tu tunaopaswa kutimiza. Tutakuwa na hamu ya kuonyesha kwamba tunawajali watu na tunatamani sana kuwasaidia. Tunajua kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Mdo. 20:35) Tunapotimiza huduma yetu tukiwa na maoni hayo akilini, ndivyo tutakavyofurahia zaidi kazi ya kuhubiri.

4 Katika makala hii, tutajifunza jinsi tunavyoweza kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi katika huduma. Kwanza, tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi Yesu alivyohisi kuhusu watu. Kisha tutachunguza njia nne za kumwiga.—1 Pet. 2:21.

YESU ALIONYESHA HISIA-MWENZI KATIKA HUDUMA

Sifa ya hisia-mwenzi ilimchochea Yesu kuhubiri ujumbe wa faraja (Tazama fungu la 5 na 6)

5-6. (a) Yesu aliwaonyesha nani hisia-mwenzi? (b) Kama ilivyotabiriwa kwenye Isaya 61:1, 2, kwa nini Yesu aliwasikitikia watu aliowahubiria?

5 Fikiria mfano huu unaoonyesha jinsi Yesu alivyoonyesha hisia-mwenzi. Pindi moja, Yesu na wanafunzi wake walikuwa wamechoka sana baada ya kuhubiri habari njema bila kupumzika. “Nao hawakuwa na wakati hata wa kula.” Hivyo, Yesu aliwapeleka wanafunzi wake “mahali pasipo na watu ili wawe peke yao” na ‘ili wapumzike kidogo.’ Hata hivyo, umati mkubwa wa watu ulikimbia na kutangulia kufika mahali ambapo Yesu na wanafunzi wake walikuwa wakielekea. Yesu alipofika mahali hapo na kuwaona watu, alitendaje? ‘Aliwasikitikia * kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.’—Marko 6:30-34.

6 Ona sababu iliyomfanya Yesu awasikitikie watu, yaani, awaonyeshe hisia-mwenzi. Alitambua kwamba watu “walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji.” Huenda Yesu aliona kwamba baadhi yao walikuwa maskini na walifanya kazi kwa saa nyingi ili kuandalia familia zao. Huenda wengine walikuwa na huzuni kwa sababu ya kufiwa na wapendwa wao. Ikiwa ndivyo ilivyokuwa, inawezekana kwamba Yesu alielewa hali zao. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, huenda Yesu mwenyewe alipambana na matatizo kama hayo. Yesu aliwajali wengine, na alichochewa kuwapa ujumbe wa faraja.—Soma Isaya 61:1, 2.

7. Tunaweza kumwigaje Yesu?

7 Mfano wa Yesu unatufunza nini? Kama Yesu, sisi pia tumezungukwa na watu walio “kama kondoo wasio na mchungaji.” Wanapambana na matatizo mengi. Nasi tuna kitu wanachohitaji—ujumbe wa Ufalme. (Ufu. 14:6) Hivyo, kwa kumwiga Bwana wetu, tunahubiri habari njema kwa sababu ‘tunawahurumia watu wa hali ya chini na maskini.’ (Zab. 72:13) Tunawahurumia watu, na tunatamani kuwasaidia.

TUNAWEZA KUONYESHAJE HISIA-MWENZI?

Zingatia mahitaji ya mtu mmoja-mmoja (Tazama fungu la 8 na 9)

8. Taja njia ya kwanza ya kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi katika huduma. Toa mfano.

8 Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwaonyesha hisia-mwenzi wale tunaowahubiria? Tungependa kujiweka katika hali za watu tunaowahubiria na kuwatendea kama ambavyo tungependa tutendewe. * (Mt. 7:12) Acheni tuchunguze njia nne hususa za kufanya hivyo. Kwanza, zingatia mahitaji ya mtu mmoja-mmoja. Tunapohubiri habari njema, kazi yetu inaweza kulinganishwa na kazi ya daktari. Daktari mzuri huzingatia mahitaji ya kila mgonjwa. Yeye huuliza maswali na kusikiliza kwa makini mgonjwa anapojieleza. Badala ya kumpendekezea mara moja matibabu yanayokuja akilini mwake, daktari anaweza kuamua kuruhusu muda upite ili amchunguze mgonjwa kisha ampe matibabu yatakayomfaa. Kwa njia hiyohiyo, hatupaswi kutumia mbinu ileile kuanzisha mazungumzo na kila mtu tunayekutana naye katika huduma. Badala yake, tunazingatia hali hususa na maoni ya mtu mmoja-mmoja.

9. Hatupaswi kufikiri tunajua nini? Eleza.

9 Unapokutana na mtu katika huduma, usifikiri kwamba unajua hali yake, mambo anayoamini, na kwa nini anayaamini. (Met. 18:13) Badala yake, muulize maswali kwa busara ili ujue mambo fulani kumhusu au mambo anayoamini. (Met. 20:5) Ikiwa ni sawa kulingana na tamaduni za kwenu, muulize kuhusu kazi yake, familia yake, malezi yake, na maoni yake kwa ujumla. Tunapowauliza watu maswali, tunawapa fursa ya kutueleza kwa nini wanahitaji habari njema. Baada ya kujua kwa nini wanahitaji habari njema, tunaweza kuwaonyesha hisia-mwenzi kwa kuwapa msaada wanaohitaji hasa kulingana na mahitaji yao, kama tu Yesu alivyofanya.—Linganisha 1 Wakorintho 9:19-23.

Jaribu kuwazia jinsi maisha ya mtu unayemhubiria yalivyo (Tazama fungu la 10 na 11)

10-11. Kulingana na 2 Wakorintho 4:7, 8, njia ya pili ya kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi ni ipi? Toa mfano.

10 Pili, jaribu kuwazia jinsi maisha yao yalivyo. Kwa kiasi fulani, tunaweza kuelewa hali wanazopitia. Bila shaka, sisi pia hupatwa na matatizo ambayo huwapata wanadamu wote wasio wakamilifu. (1 Kor. 10:13) Tunajua kwamba maisha katika mfumo huu wa mambo ni magumu sana. Ni kwa msaada wa Yehova pekee kwamba tunafanikiwa kuvumilia. (Soma 2 Wakorintho 4:7, 8.) Lakini fikiria kuhusu wale wanaopambana na maisha katika mfumo huu na hawana urafiki wa karibu na Yehova. Kama Yesu, tunawahurumia na kusukumwa kuwapa “habari njema za jambo bora.”—Isa. 52:7.

11 Fikiria mfano wa ndugu anayeitwa Sergey. Kabla ya kujifunza kweli, Sergey alikuwa mwenye haya na mkimya sana. Haikuwa rahisi kwake kuzungumza na watu. Baada ya muda, alikubali kujifunza Biblia. Sergey anaeleza hivi: “Nilipokuwa nikijifunza Biblia, nilitambua kwamba Wakristo wana wajibu wa kuwaeleza wengine kuhusu imani yao. Niliamini kabisa kwamba nisingeweza kufanya hivyo.” Lakini aliwafikiria wale ambao hawakuwa wamesikia kuhusu kweli, na aliwazia jinsi maisha yao yalivyo magumu kwa sababu hawamjui Yehova. Anasema hivi: “Mambo mapya niliyokuwa nikijifunza yalinifanya niwe na furaha nyingi na amani ya moyoni. Nilijua kwamba wengine walihitaji pia kujifunza kuhusu kweli hizi.” Kadiri Sergey alivyozidi kusitawisha sifa ya hisia-mwenzi, ndivyo ujasiri wake wa kuhubiri ulivyoongezeka. Anaongeza hivi: “Nilishangaa sana kuona kwamba ujasiri wangu uliongezeka nilipowaeleza wengine kuhusu Biblia. Pia, imani yangu ilizidi kuimarika.” *

Huenda baadhi ya watu wakachukua muda mrefu kufanya maendeleo ya kiroho (Tazama fungu la 12 na 13)

12-13. Kwa nini tunahitaji kuwa na subira kuelekea wale tunaowafundisha? Toa mfano.

12 Tatu, uwe na subira kuelekea watu unaowafundisha. Kumbuka kwamba huenda hawajawahi kukazia fikira kweli za Biblia ambazo sisi tunajua vizuri sana. Na wengi wao wanapenda mambo wanayoamini na wanayashikilia sana. Huenda wakahisi kwamba dini yao inawaunganisha na watu wa familia, utamaduni, na jamii yao. Tunaweza kuwasaidiaje?

13 Fikiria mfano huu: Ni hatua gani ambayo huchukuliwa wakati daraja lililozeeka linapohitaji kujengwa upya? Kwa kawaida, daraja jipya hujengwa huku lile la zamani likiendelea kutumiwa. Mara tu daraja jipya linapokamilika, daraja la zamani ambalo limekuwa likitumiwa kwa miaka mingi linaweza kubomolewa. Vivyo hivyo, kabla ya kuwaambia watu waache mambo wanayopenda ambayo wamekuwa wakiamini kwa “miaka mingi,” tunahitaji kwanza kuwasaidia wajenge uthamini wenye kina kuelekea kweli “mpya” wanazojifunza, yaani, mafundisho ya Biblia ambayo hawakuyajua awali. Hapo ndipo wanapoweza kuwa tayari kuachilia mambo waliyokuwa wakiamini. Inaweza kuchukua muda mrefu kuwasaidia watu kufanya mabadiliko kama hayo.—Rom. 12:2.

14-15. Tunaweza kuwasaidiaje watu wasiojua mengi au wasiojua chochote kuhusu tumaini la uzima wa milele katika Paradiso duniani? Toa mfano.

14 Ikiwa tuna subira kuelekea watu tunaowahubiria, hatutatarajia waelewe au kukubali kweli za Biblia wanapozisikia kwa mara ya kwanza. Badala yake, sifa ya hisia-mwenzi itatuchochea tuwasaidie pole kwa pole wafikirie kwa uzito kuhusu yale ambayo Biblia inafundisha. Kwa mfano, fikiria hoja tunazoweza kutumia tunapozungumza na mtu kuhusu tumaini la uzima wa milele katika Paradiso duniani. Watu wengi hawajui mengi au hawajui chochote kuhusu fundisho hilo. Huenda wanaamini kwamba kifo ndiyo mwisho wa mambo yote. Au huenda wanafikiri kwamba watu wote wazuri huenda mbinguni. Tunaweza kuwasaidiaje?

15 Ndugu mmoja anaeleza kuhusu njia fulani yenye matokeo ambayo yeye hutumia kuwasaidia watu waelewe fundisho hilo. Kwanza, yeye husoma andiko la Mwanzo 1:28. Kisha, yeye humuuliza mwenye nyumba, “Mungu alitaka wanadamu waishi wapi, na waishi katika hali gani?” Watu wengi hujibu, “Duniani, wakifurahia hali nzuri.” Halafu ndugu huyo husoma andiko la Isaya 55:11 na kuuliza, “Je, kusudi la Mungu limebadilika?” Kwa kawaida, mwenye nyumba hujibu hapana. Mwishowe, ndugu huyo husoma andiko la Zaburi 37:10, 11 na kumuuliza hivi: “Wakati ujao wa wanadamu utakuwaje?” Kwa kutumia hoja hizo za Kimaandiko, ndugu huyo amewasaidia watu kadhaa kuelewa kwamba bado Mungu anataka watu waishi milele katika Paradiso duniani.

Tendo dogo la fadhili kama vile, kuandika barua yenye kutia moyo, linaweza kuwa na matokeo mazuri sana (Tazama fungu la 16 na 17)

16-17. Kwa kuzingatia andiko la Methali 3:27, tunaweza kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi katika njia zipi? Toa mfano.

16 Nne, tafuta njia za kuwaonyesha wengine kwamba unawajali. Kwa mfano, je, umemtembelea mwenye nyumba wakati usiomfaa? Unaweza kumwomba radhi na kumwahidi kwamba utarudi wakati mwingine unaomfaa zaidi. Vipi ikiwa mwenye nyumba anahitaji kusaidiwa kufanya kazi fulani ndogo? Au vipi ikiwa mtu ni mgonjwa au mzee na hawezi kutoka nyumbani lakini anahitaji kumtuma mtu mahali fulani? Katika hali kama hizo, tunaweza kumsaidia.—Soma Methali 3:27.

17 Dada mmoja alipata matokeo mazuri baada ya kufanya tendo fulani dogo la fadhili. Akichochewa na sifa ya hisia-mwenzi, aliiandikia barua familia fulani iliyokuwa imepoteza mtoto katika kifo. Barua hiyo ilikuwa na Maandiko fulani yenye kufariji. Familia hiyo iliitikiaje? Mama aliyefiwa aliandika hivi: “Jana nilikuwa nimelemewa sana na huzuni. Sidhani unaweza kuelewa jinsi barua yako ilivyotugusa moyo. Sina maneno ya kukushukuru au hata kueleza jinsi barua yako ilivyotufariji. Nafikiri niliisoma barua yako zaidi ya mara 20 jana. Sikuamini jinsi ilivyokuwa na maneno yenye fadhili, yenye kujali, na yenye kutia moyo. Tunakushukuru sana kutoka moyoni.” Hapana shaka yoyote kwamba sisi pia tunaweza kupata matokeo mazuri tunapojiweka katika hali za wale wanaoteseka na kisha kuchukua hatua fulani ili kuwasaidia.

UWE NA USAWAZIKO KUHUSU JUKUMU LAKO

18. Kulingana na 1 Wakorintho 3:6, 7, tungependa kuwa na maoni gani yenye usawaziko?

18 Bila shaka, tungependa kuwa na usawaziko kuhusu jukumu letu tunapokuwa katika huduma. Tunatimiza sehemu yetu tunapowasaidia wengine wajifunze kumhusu Mungu, lakini kuna yule anayetimiza sehemu muhimu zaidi. (Soma 1 Wakorintho 3:6, 7.) Yehova ndiye anayewavuta watu kwake. (Yoh. 6:44) Mwishowe, kila mtu atakubali au kukataa ujumbe wa habari njema ikitegemea hali ya moyo wake. (Mt. 13:4-8) Kumbuka kwamba watu wengi hawakuukubali ujumbe wa Yesu hata ingawa yeye ndiye Mwalimu mkuu zaidi aliyewahi kuishi! Hivyo, hatupaswi kuvunjika moyo ikiwa watu wengi tunaojitahidi kuwasaidia wanakataa kusikiliza ujumbe wetu.

19. Tunapata manufaa gani tunapowaonyesha wengine hisia-mwenzi katika huduma?

19 Tutapata matokeo mazuri tunapowaonyesha wengine hisia-mwenzi katika huduma. Tutafurahia zaidi kazi yetu ya kuhubiri. Tutapata furaha nyingi zaidi inayotokana na kutoa. Na tutafanya iwe rahisi zaidi kwa wale walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” kukubali habari njema. (Mdo. 13:48) Basi “tukiwa bado na nafasi, acheni tuwatendee watu wote mema.” (Gal. 6:10) Kisha tutakuwa na shangwe ya kumtukuza Baba yetu wa mbinguni.—Mt. 5:16.

WIMBO 64 Kuyashiriki Mavuno kwa Furaha

^ fu. 5 Tunapowaonyesha wengine hisia-mwenzi, tunaweza kuongeza shangwe yetu na vilevile matokeo tunayopata katika huduma. Kwa nini? Katika makala hii, tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kutoka kwa Yesu, na vilevile njia nne hususa za kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi tunapohubiri.

^ fu. 5 UFAFANUZI WA MANENO: Katika muktadha huu, kusikitikia kunamaanisha kuwa na hisia nyororo kuelekea mtu anayeteseka au aliyetendewa bila huruma. Hisia kama hizo zinaweza kumchochea mtu afanye yote awezayo kuwasaidia wengine.

^ fu. 8 Tazama makala “Tumia Ile Kanuni Bora Katika Huduma Yako” katika toleo la Mei 15, 2014, la gazeti la Mnara wa Mlinzi.