Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 10

Ni Nini Kinachonizuia Kubatizwa?

Ni Nini Kinachonizuia Kubatizwa?

“Filipo na towashi wakaingia ndani ya maji, naye akambatiza.”—MDO. 8:38.

WIMBO 52 Wakfu wa Kikristo

MUHTASARI *

1. Adamu na Hawa walipoteza nini, na matokeo yalikuwa nini?

UNAFIKIRI ni nani anayepaswa kuweka viwango vya mema na mabaya? Adamu na Hawa walipokula matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya walionyesha wazi jambo fulani: Hawakumtumaini Yehova na viwango vyake. Walichagua kujiwekea viwango vyao wenyewe vya mema na mabaya. (Mwa. 3:22) Lakini fikiria kuhusu mambo waliyopoteza. Walipoteza urafiki wao pamoja na Yehova. Pia, walipoteza fursa ya kuishi milele, na wakawapitishia watoto wao dhambi na kifo. (Rom. 5:12) Uamuzi wa Adamu na Hawa ulileta majonzi.

Baada ya kumkubali Yesu, towashi Mwethiopia alitaka kubatizwa haraka iwezekanavyo (Tazama fungu la 2 na 3)

2-3. (a) Towashi Mwethiopia aliitikiaje Filipo alipomhubiria? (b) Tunapata baraka gani tunapobatizwa, na tutazungumzia maswali gani?

2 Sasa, linganisha jinsi Adamu na Hawa walivyotenda na jinsi towashi Mwethiopia alivyoitikia Filipo alipomhubiria. Towashi huyo alithamini sana mambo ambayo Yehova na Yesu walikuwa wamemtendea hivi kwamba akaamua kubatizwa bila kukawia. (Mdo. 8:34-38) Tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa kama alivyofanya towashi huyo, tunaonyesha wazi jambo fulani. Tunaonyesha kwamba tunathamini mambo ambayo Yehova na Yesu wametufanyia. Pia, tunaonyesha kwamba tunamtumaini Yehova na tunatambua kwamba yeye ndiye anayepaswa kuweka viwango vya mema na mabaya.

3 Fikiria kuhusu baraka tunazopata tunapomtumikia Yehova! Kwanza, tuna tumaini kwamba hatimaye tutapata baraka zote ambazo Adamu na Hawa walipoteza, kutia ndani fursa ya kuishi milele. Kwa sababu tuna imani katika Yesu Kristo, Yehova hutusamehe makosa yetu na kutupatia dhamiri safi. (Mt. 20:28; Mdo. 10:43) Pia, tunakuwa sehemu ya familia ya Yehova ya watumishi wake aliowakubali na walio na tumaini zuri la wakati ujao. (Yoh. 10:14-16; Rom. 8:20, 21) Hata hivyo, licha ya faida hizo zilizo wazi, baadhi ya watu ambao wamejifunza kumhusu Yehova husita kuiga mfano wa towashi Mwethiopia. Ni mambo gani ambayo huenda yanawazuia kubatizwa? Na wanaweza kushinda changamoto hizo jinsi gani?

CHANGAMOTO ZINAZOWAZUIA WENGINE KUBATIZWA

Changamoto ambazo baadhi ya watu hukabili kabla ya kuamua kubatizwa

Kutojiamini (Tazama fungu la 4 na 5) *

4-5. Kijana anayeitwa Avery na msichana anayeitwa Hannah walikabili changamoto gani?

4 Kutojiamini. Wazazi wa kijana anayeitwa Avery ni Mashahidi wa Yehova. Baba yake anajulikana kuwa baba mwenye upendo na mzee wa kutaniko mwenye bidii. Licha ya hilo, Avery alisita kuchukua hatua ya kubatizwa. Kwa nini? Anasema hivi: “Nilihisi kwamba siwezi kuwa kama baba yangu.” Pia, Avery alihisi kwamba hangeweza kushughulikia majukumu ambayo huenda angepewa wakati ujao. Anaeleza hivi: “Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kusali hadharani, kutoa hotuba, au kuongoza kikundi cha utumishi ikiwa ningeombwa kufanya hivyo.”

5 Hannah, msichana mwenye umri wa miaka 18, alikuwa na tatizo kubwa la kuhisi kuwa mtu asiyefaa hata kidogo. Alilelewa na wazazi waliomtumikia Yehova. Ingawa hivyo, alitilia shaka ikiwa angeweza kuishi kulingana na viwango vya Yehova. Kwa nini? Hannah alikuwa ameathiriwa na mtazamo wa kujiona kuwa mtu asiye na thamani. Nyakati nyingine alilemewa sana na hisia hizo hivi kwamba alijijeruhi kimakusudi, jambo lililofanya mambo yawe mabaya hata zaidi. Anaeleza hivi: “Sikumwambia yeyote mambo niliyofanya, kutia ndani wazazi wangu, na niliwaza kwamba Yehova hawezi kamwe kunikubali kuwa mtumishi wake kwa sababu ya mambo niliyokuwa nikijitendea.”

Marafiki (Tazama fungu la 6) *

6. Ni nini kilichomzuia Vanessa kubatizwa?

6 Marafiki. Vanessa, msichana mwenye umri wa miaka 22, anasema hivi: “Nilikuwa na rafiki wa karibu ambaye tulifahamiana kwa karibu miaka kumi.” Hata hivyo, rafiki ya Vanessa hakumtia moyo kufikia lengo la kubatizwa. Jambo hilo lilimuumiza Vanessa, na anasema hivi: “Si rahisi kwangu kuanzisha urafiki, na nilikuwa na wasiwasi kwamba ikiwa ningevunja urafiki wetu, nisingepata tena rafiki mwingine wa karibu.”

Woga wa kushindwa (Tazama fungu la 7) *

7. Mwanamke kijana anayeitwa Makayla aliogopa nini, na kwa nini?

7 Woga wa kushindwa. Makayla alikuwa na umri wa miaka mitano ndugu yake alipotengwa na ushirika. Alipokuwa akikua, alijionea jinsi wazazi wake walivyoathiriwa na matendo ya ndugu yake. Anasema hivi: “Niliogopa kwamba ikiwa ningebatizwa kisha nifanye kosa fulani, ningetengwa na ushirika, na jambo hilo lingewahuzunisha wazazi wangu hata zaidi.”

Upinzani (Tazama fungu la 8) *

8. Kijana anayeitwa Miles aliogopa nini?

8 Kuogopa upinzani. Baba ya Miles na mama yake wa kambo ni watumishi wa Yehova, lakini mama yake mzazi si Shahidi wa Yehova. Miles anasema hivi: “Niliishi na mama yangu kwa miaka 18, na niliogopa kumwambia kwamba nilitamani kubatizwa. Nilikuwa nimejionea jinsi alivyotenda baba yangu alipoamua kuwa Shahidi. Niliogopa kwamba angenipinga.”

JINSI YA KUSHINDA CHANGAMOTO HIZO

9. Ni nini kinachoweza kutokea unapojifunza jinsi Yehova alivyo mwenye upendo na subira?

9 Adamu na Hawa walichagua kutomtumikia Yehova kwa sababu hawakusitawisha upendo wenye nguvu kumwelekea. Ingawa hivyo, Yehova aliwaruhusu waishi muda mrefu vya kutosha kupata watoto na kujiwekea viwango vyao wenyewe vya kuwalea watoto hao. Punde si punde, matokeo ya uamuzi wa Adamu na Hawa wa kujitegemea badala ya kumtegemea Yehova, yalifunua wazi jinsi walivyotenda kipumbavu. Mwana wao wa kwanza alimuua ndugu yake asiye na hatia, na baada ya muda ukatili na ubinafsi ukaenea katika jamii ya wanadamu. (Mwa. 4:8; 6:11-13) Licha ya hayo, Yehova aliandaa njia ya kuwaokoa watoto wote wa Adamu na Hawa ambao walitaka kumtumikia. (Yoh. 6:38-40, 57, 58) Kadiri unavyoendelea kujifunza mengi zaidi kuhusu jinsi Yehova alivyo mwenye subira na upendo, inaelekea ndivyo upendo wako kwake utakavyozidi kuongezeka. Hutafuata njia ambayo Adamu na Hawa walichagua, badala yake utaamua kujiweka wakfu kwa Yehova.

Unaweza kushinda changamoto hizi jinsi gani?

(Tazama fungu la 9 hadi 10) *

10. Kwa nini kutafakari Zaburi 19:7 kunaweza kukusaidia kumtumikia Yehova?

10 Endelea kujifunza kumhusu Yehova. Kadiri unavyojifunza mengi zaidi kumhusu Yehova, ndivyo utakavyokuwa na uhakika mwingi zaidi kwamba unaweza kumtumikia kwa mafanikio. Avery, kijana aliyetajwa awali anasema hivi: “Uhakika wangu uliongezeka niliposoma na kutafakari kuhusu ahadi inayopatikana kwenye Zaburi 19:7.” (Soma.) Avery alipojionea jinsi Yehova alivyotimiza ahadi ya kwamba atamfanya asiye na uzoefu awe na hekima, upendo wake kwa Mungu ulizidi kuimarika. Upendo haufanyi tu uhakika wetu uzidi kuongezeka, bali pia hutusaidia kumkazia fikira Yehova na mambo anayotaka tufanye. Hannah, msichana aliyetajwa awali, anasema hivi: “Kwa kusoma na kujifunza Biblia kibinafsi, niligundua kwamba ninapojiumiza, Yehova anaumia pia.” (1 Pet. 5:7) Hannah akawa ‘mtendaji wa neno.’ (Yak. 1:22) Ikawaje? Anaeleza hivi: “Nilipojionea manufaa ya kumtii Yehova, upendo wangu kwake uliongezeka. Sasa nina hakika kwamba sikuzote Yehova ataniongoza ninapohitaji msaada wake.” Hannah alifaulu kushinda zoea la kujijeruhi. Alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

(Tazama fungu la 11) *

11. Vanessa alifanya nini ili apate marafiki wazuri, na tunajifunza nini kutokana na mfano wake?

11 Chagua marafiki kwa hekima. Hatimaye, Vanessa, msichana aliyetajwa mapema, alitambua kwamba rafiki yake alikuwa akimzuia kumtumikia Yehova. Hivyo, alivunja urafiki huo. Lakini Vanessa hakuachia hapo. Alijitahidi kupata marafiki wapya ndani ya kutaniko. Anasema kwamba mfano wa Noa na familia yake ulimsaidia sana. Anaeleza hivi: “Noa na familia yake waliishi miongoni mwa watu ambao hawakumpenda Yehova, lakini walifurahia ushirika mzuri miongoni mwao wenyewe.” Baada ya kubatizwa, Vanessa alianza upainia. Sasa anasema hivi: “Mambo hayo yamenisaidia kupata marafiki wazuri kutanikoni na katika makutaniko mengine pia.” Wewe pia unaweza kupata marafiki wazuri unapokuwa na mengi ya kufanya katika kazi ambayo Yehova ametupatia.—Mt. 24:14.

(Tazama fungu 12 hadi 15) *

12. Adamu na Hawa hawakuogopa nini, na matokeo yalikuwa nini?

12 Uwe na maoni yanayofaa kuhusu woga. Ni vizuri kuwa na woga kuhusu mambo fulani. Kwa mfano, tunapaswa kuogopa kumkasirisha Yehova. (Zab. 111:10) Ikiwa Adamu na Hawa wangesitawisha woga huo, hawangemwasi Yehova. Lakini waliasi. Baada ya kuasi, macho yao yalifunguliwa katika maana ya kwamba walitambua kikamili kwamba walikuwa watenda dhambi. Sasa, urithi pekee ambao wangeweza kuwapitishia watoto wao ni dhambi na kifo. Na kwa kuwa wangeweza kuona au kuelewa kwamba wamevunja sheria ya Mungu, waliona aibu kwamba walikuwa uchi nao wakajifunika.—Mwa. 3:7, 21.

13-14. (a) Kulingana na 1 Petro 3:21, kwa nini hatupaswi kuwa na woga uliopita kiasi wa kifo? (b) Tuna sababu zipi za kumpenda Yehova?

13 Ingawa tunapaswa kuogopa kumkasirisha Yehova, hatupaswi kuwa na woga uliopita kiasi wa kifo. Yehova ametuandalia njia ya kupata uzima wa milele. Tukitenda dhambi na kutubu kutoka moyoni, Yehova atatusamehe makosa yetu. Atatusamehe kwa sababu tuna imani katika dhabihu ya fidia ya Mwana wake. Njia moja kuu tunayoonyesha kwamba tuna imani ni kwa kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.—Soma 1 Petro 3:21.

14 Tuna sababu nyingi za kumpenda Yehova. Yehova hatuandalii tu vitu vyema tunavyofurahia kila siku, bali pia anatufundisha ukweli kumhusu yeye na makusudi yake. (Yoh. 8:31, 32) Ametupatia kutaniko la Kikristo ili tupate mwongozo na utegemezo. Anatusaidia kubeba mizigo yetu sasa, na ametupatia tumaini la kuishi milele wakati ujao chini ya hali kamilifu. (Zab. 68:19; Ufu. 21:3, 4) Tunapotafakari kuhusu mambo ambayo tayari Yehova ametufanyia ili kuonyesha kwamba anatupenda, tunachochewa kumpenda. Na tunapompenda Yehova, tunajifunza kuwa na woga unaofaa. Tutaogopa kumuumiza kwa kuwa sasa tunampenda sana.

15. Makayla alishinda woga aliokuwa nao jinsi gani?

15 Makayla, msichana aliyetajwa awali, ambaye alikuwa na woga wa kushindwa, alifanikiwa kushinda hisia hizo alipoelewa jinsi Yehova alivyo mwenye kusamehe. Anasema hivi: “Nilitambua kwamba sisi sote si wakamilifu na hufanya makosa. Lakini pia, mwishowe nilielewa kwamba Yehova anatupenda na atatusamehe kwa msingi wa fidia.” Upendo wake kwa Yehova ulimchochea ajiweke wakfu kwake na kubatizwa.

(Tazama fungu la 16) *

16. Miles alipata msaada gani uliomsaidia kushinda woga wa kupingwa?

16 Miles, kijana aliyeogopa kwamba mama yake angepinga uamuzi wake wa kubatizwa, alitafuta msaada kutoka kwa mwangalizi wa mzunguko. Anasema hivi: “Mwangalizi huyo pia alikuwa amelelewa katika familia iliyogawanyika kidini. Alinisaidia nijue jinsi ambavyo ningeweza kumsadikisha mama yangu kwamba mimi ndiye niliyeamua kubatizwa na si kwamba Baba ndiye aliyekuwa akinishinikiza kufanya hivyo.” Mama ya Miles hakufurahishwa na uamuzi wa mwanawe. Hatimaye, Miles alilazimika kuondoka nyumbani kwa mama yake, lakini alishikamana na uamuzi wake. Anaeleza hivi: “Kujifunza kuhusu mambo mazuri ambayo Yehova amenifanyia kulinigusa moyo sana. Nilipotafakari kwa kina kuhusu dhabihu ya fidia ya Yesu, nilitambua kwamba kwa kweli Yehova ananipenda sana. Jambo hilo lilinichochea nijiweke wakfu kwa Yehova na kubatizwa.”

SHIKAMANA NA UAMUZI WAKO

Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mambo ambayo Yehova ametutendea kwa kubatizwa (Tazama fungu la 17)

17. Sisi sote tuna fursa gani?

17 Hawa alipokula matunda ya mti uliokuwa katika bustani ya Edeni, alimwasi Baba yake. Adamu alipojiunga naye katika uasi huo, alionyesha ukosefu mkubwa sana wa shukrani kwa mambo yote mazuri ambayo Yehova alikuwa amemtendea. Sisi sote tuna fursa ya kuonyesha kwamba hatuungi mkono hata kidogo uamuzi ambao Adamu na Hawa walifanya. Tunapochukua hatua ya kubatizwa, tunamwonyesha Yehova kwamba tunaamini kuwa yeye ndiye aliye na mamlaka ya kutuwekea viwango vya mema na mabaya. Tunathibitisha kwamba tunampenda Baba yetu na kumtumaini.

18. Ni mambo gani yatakayokusaidia kufanikiwa kumtumikia Yehova?

18 Changamoto tunayokabili baada ya kubatizwa ni kuishi kila siku kulingana na viwango vya Yehova, si kulingana na viwango vyetu wenyewe. Mamilioni ya watu huishi kulingana na viwango hivyo mwaka baada ya mwaka. Unaweza kuwa kama wao ikiwa utaendelea kuongeza kina cha ujuzi ulio nao wa Neno la Mungu, Biblia; kushirikiana kwa ukawaida na ndugu na dada zako; na kushiriki kwa bidii pamoja na wengine mambo uliyojifunza kumhusu Baba yako mwenye upendo. (Ebr. 10:24, 25) Unapofanya maamuzi, sikiliza ushauri ambao Yehova anakupatia kupitia Neno lake na tengenezo lake. (Isa. 30:21) Kisha mambo yote unayofanya yatafanikiwa.—Met. 16:3, 20.

19. Unapaswa kuendelea kutambua nini, na kwa nini?

19 Kadiri unavyoendelea kutambua manufaa unayopata kwa kufuata mwongozo wa Yehova, ndivyo upendo ulio nao kwake na kwa viwango vyake utakavyozidi kuongezeka. Kisha hakuna kishawishi chochote cha Shetani kitakachokufanya uache kumtumikia Yehova. Jiwazie utakavyohisi miaka elfu moja kutoka sasa. Utakumbuka uamuzi uliofanya wa kubatizwa na kuuona kuwa uamuzi bora kabisa uliowahi kufanya!

WIMBO 28 Kuwa Rafiki ya Yehova

^ fu. 5 Kuamua ikiwa utabatizwa au la ndio uamuzi muhimu zaidi utakaofanya maishani. Kwa nini uamuzi huo ni muhimu sana? Makala hii itajibu swali hilo. Pia, itawasaidia wale wanaofikiria kubatizwa washinde changamoto ambazo huenda zinawazuia kuchukua hatua ya kubatizwa.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Kutojiamini: Kijana anaogopa kutoa maelezo mikutanoni.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Marafiki: Msichana Shahidi akiwa pamoja na rafiki mbaya anaaibika anapowaona Mashahidi wenzake.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Woga wa kushindwa: Ndugu yake anapotengwa na kuondoka nyumbani, msichana mdogo anaogopa kwamba huenda yeye pia akapatwa na hali hiyohiyo.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Upinzani: Mvulana anaogopa kusali huku mama yake ambaye si Shahidi akimtazama.

^ fu. 65 MAELEZO YA PICHA: Kutojiamini: Kijana anaboresha funzo lake la kibinafsi.

^ fu. 67 MAELEZO YA PICHA: Marafiki: Msichana Shahidi anajifunza kujivunia kuwa Shahidi.

^ fu. 69 MAELEZO YA PICHA: Woga wa kushindwa: Msichana anaifanya kweli iwe mali yake na kubatizwa.

^ fu. 71 MAELEZO YA PICHA: Upinzani: Kijana akimweleza kwa ujasiri mama yake asiye Shahidi kuhusu imani yake.