Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 11

Sikiliza Sauti ya Yehova

Sikiliza Sauti ya Yehova

“Huyu ni Mwanangu . . . Msikilizeni.”—MT. 17:5.

WIMBO 89 Sikiliza, Tii, Upate Baraka

MUHTASARI *

1-2. (a) Yehova ametumia njia zipi kuwasiliana na wanadamu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

YEHOVA anapenda kuwasiliana nasi. Zamani, aliwatumia manabii, malaika, na Mwana wake, Kristo Yesu, kutujulisha mawazo yake. (Amo. 3:7; Gal. 3:19; Ufu. 1:1) Leo, Yehova huwasiliana nasi kupitia Neno lake, Biblia. Alitupatia Neno hilo ili tujifunze mawazo yake na tuelewe njia zake.

2 Yesu alipokuwa duniani, Yehova alizungumza kutoka mbinguni mara tatu. Acheni tuchunguze mambo ambayo Yehova alisema, mambo tunayojifunza kutokana na maneno yake, na jinsi tunavyonufaika na mambo aliyosema.

“WEWE NI MWANANGU, MPENDWA”

3. Kama tulivyosoma kwenye andiko la Marko 1:9-11, Yehova alisema nini Yesu alipobatizwa, na maneno hayo yalithibitisha kweli gani muhimu?

3 Andiko la Marko 1:9-11 linasimulia pindi ya kwanza ambapo Yehova alizungumza kutoka mbinguni. (Soma.) Alisema hivi: “Wewe ni Mwanangu, mpendwa; nimekukubali.” Hapana shaka kwamba Yesu aliguswa moyo sana aliposikia sauti ya Baba yake akisema kwamba anampenda na ana kibali chake! Maneno ya Yehova yalithibitisha kweli tatu muhimu kumhusu Yesu. Kwanza, Yesu ni Mwana wake. Pili, Yehova anampenda Mwana wake. Na tatu, Yehova anamkubali Mwana wake. Acheni tuchunguze kwa undani mambo hayo.

4. Wakati wa ubatizo wake, Yesu aliingia katika uhusiano gani mpya pamoja na Mungu?

4 “Wewe ni Mwanangu.” Aliposema maneno hayo, Yehova alionyesha kwamba sasa Yesu, Mwana wake mpendwa, alikuwa ameingia katika uhusiano mpya pamoja Naye. Yesu alipokuwa mbinguni alikuwa Mwana wa kiroho wa Mungu. Hata hivyo, wakati wa ubatizo wake, Yesu alitiwa mafuta kwa roho takatifu. Wakati huo, Mungu alionyesha kwamba sasa, Yesu akiwa Mwana Wake mtiwa-mafuta, ana tumaini la kurudi mbinguni na kutumikia akiwa Mfalme na Kuhani Mkuu aliyewekwa rasmi. (Luka 1:31-33; Ebr. 1:8, 9; 2:17) Hivyo, wakati wa ubatizo wa Yesu, Baba yake alikuwa na sababu nzuri ya kusema hivi: “Wewe ni Mwanangu.”—Luka 3:22.

Sisi hunawiri tunapopongezwa na kutiwa moyo (Tazama fungu la 5) *

5. Tunaweza kuigaje mfano wa Yehova wa kuonyesha upendo na kuwatia moyo wengine?

5 “Wewe ni . . . mpendwa.” Mfano wa Yehova wa kumwonyesha Yesu upendo na kibali chake unatukumbusha kwamba tunapaswa kutafuta fursa za kuwatia moyo wengine. (Yoh. 5:20) Sisi hunawiri mtu fulani tunayempenda anapoonyesha kwamba anatupenda na kutupongeza kwa mambo mazuri tunayofanya. Vivyo hivyo, ndugu na dada zetu kutanikoni na watu wa familia yetu wanahitaji upendo wetu na kitia-moyo chetu. Tunapowapongeza wengine, tunafanya imani yao iimarike na kuwasaidia kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu. Wazazi hasa wanahitaji kuwatia moyo watoto wao. Wazazi wanapowapongeza watoto wao kwa unyoofu na kuwaonyesha upendo, wanawasaidia kunawiri.

6. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika katika Yesu Kristo?

6 “Nimekukubali.” Maneno hayo yanaonyesha kwamba Yehova alikuwa na uhakika kwamba Yesu angetimiza mapenzi ya Baba yake kwa uaminifu. Yehova ana uhakika huo kumwelekea Mwana wake, hivyo sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kamili kwamba Yesu atatimiza kwa uaminifu ahadi zote za Yehova. (2 Kor. 1:20) Tunapofikiria kuhusu mfano wa Yesu, azimio letu la kujifunza kutoka kwake na kufuata hatua zake huzidi kuimarika. Yehova ana uhakika huohuo pia kuelekea watumishi wake kwamba wakiwa kikundi wataendelea kujifunza kutokana na mfano wa Mwana wake.—1 Pet. 2:21.

“MSIKILIZENI”

7. Kulingana na Mathayo 17:1-5, Yehova alizungumza kutoka mbinguni wakati wa tukio gani, naye alisema nini?

7 Soma Mathayo 17:1-5. Mara ya pili ambayo Yehova alizungumza kutoka mbinguni ni wakati Yesu ‘alipogeuka sura.’ Yesu alikuwa amemwalika Petro, Yakobo, na Yohana waende pamoja naye kwenye mlima fulani mrefu. Huko, waliona maono yenye kustaajabisha. Uso wa Yesu uling’aa na mavazi yake yalimetameta. Watu wawili, waliowakilisha Musa na Eliya, walianza kuzungumza na Yesu kuhusu kifo chake kilichokuwa kikikaribia pamoja na ufufuo wake. Ingawa mitume hao watatu walikuwa “wamelemewa na usingizi,” waliona maono hayo ya ajabu walipoamka kabisa. (Luka 9:29-32) Kisha, wingu jangavu likawafunika, nao wakasikia sauti ikitoka kwenye wingu hilo—sauti ya Mungu! Na kama ilivyokuwa wakati Yesu alipobatizwa, Yehova alionyesha kwamba Yesu ana kibali chake na anampenda, aliposema hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” Lakini pindi hii Yehova aliongeza hivi: “Msikilizeni.”

8. Maono ya kugeuka sura yalimwimarishaje Yesu na wanafunzi wake?

8 Maono hayo yalionyesha utukufu na mamlaka ambayo Yesu atakuwa nayo akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Hapana shaka kwamba Kristo alitiwa moyo na kuimarishwa kuvumilia mateso na kifo chenye maumivu makali ambacho angekabili. Maono hayo pia yaliimarisha imani ya wanafunzi wake na kuwatia nguvu ili waweze kuvumilia majaribu ya utimilifu na kazi ngumu iliyokuwa mbele yao ambayo ingechukua miaka mingi. Miaka 30 hivi baadaye, mtume Petro aliyarejelea maono hayo, kuonyesha kwamba bado alikuwa akiyakumbuka vizuri.—2 Pet. 1:16-18.

9. Yesu aliwapa wanafunzi wake ushauri gani unaofaa?

9 “Msikilizeni.” Yehova alitaja waziwazi kwamba anataka tumsikilize Mwanaye na tumtii. Yesu alisema nini alipokuwa duniani? Alisema mambo mengi muhimu tunayopaswa kusikiliza! Kwa mfano, upendo ulimchochea kuwafundisha wafuasi wake jinsi ya kuhubiri habari njema, na aliwakumbusha tena na tena kwamba wanapaswa kuendelea kukesha. (Mt. 24:42; 28:19, 20) Pia, aliwahimiza wajitahidi sana, na akawatia moyo wasikate tamaa. (Luka 13:24) Yesu aliwasisitizia wafuasi wake umuhimu wa kupendana, kuendelea kuwa na umoja, na kushika amri zake. (Yoh. 15:10, 12, 13) Ushauri huo wa Yesu uliwafaa kabisa wanafunzi wake! Ushauri huo ni muhimu leo pia kama tu ulivyokuwa Yesu alipoutoa.

10-11. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamsikiliza Yesu?

10 Yesu alisema hivi: “Kila mtu aliye upande wa kweli huisikiliza sauti yangu.” (Yoh. 18:37) Tunaonyesha kwamba tunasikiliza sauti yake tunapoendelea “kuvumiliana na kusameheana kwa hiari.” (Kol. 3:13; Luka 17:3, 4) Pia, tunaonyesha kwamba tunasikiliza sauti yake kwa kuhubiri habari njema kwa bidii “katika nyakati zinazofaa na nyakati ngumu.”—2 Tim. 4:2.

11 Yesu alisema hivi: “Kondoo wangu husikiliza sauti yangu.” (Yoh. 10:27) Wafuasi wa Kristo huonyesha kwamba wanasikiliza maneno ya Yesu, si kwa kuyakazia fikira tu, bali pia kwa kutenda kulingana nayo. Hawakengeushwi na “mahangaiko ya maisha.” (Luka 21:34) Badala yake, jambo kuu maishani mwao ni kutii amri za Yesu, hata iwe wanakabili hali ngumu kadiri gani. Ndugu zetu wengi wanavumilia majaribu makali, kama vile kushambuliwa na wapinzani, umaskini uliokithiri, na misiba ya asili. Licha ya hayo yote, wanaendelea kuwa waaminifu kwa Yehova, hata wakumbwe na hali gani. Yesu anawahakikishia hivi: “Yeyote aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye anayenipenda. Na yeyote anayenipenda atapendwa na Baba yangu.”—Yoh. 14:21.

Huduma yetu hutusaidia kuendelea kusikiliza sauti ya Yesu (Tazama fungu la 12) *

12. Tunaweza kuonyesha kwamba tunamsikiliza Yesu katika njia gani nyingine?

12 Njia nyingine tunayoweza kuonyesha kwamba tunamsikiliza Yesu ni kwa kuwaunga mkono ndugu waliowekwa rasmi ili waongoze miongoni mwetu. (Ebr. 13:7, 17) Tengenezo la Mungu limefanya mabadiliko mengi katika miaka ya karibuni, kutia ndani matumizi ya vifaa na njia mpya za kuhubiri, mabadiliko katika mkutano unaofanywa katikati ya juma, na jinsi tunavyojenga, kukarabati, na kudumisha Majumba yetu ya Ufalme. Tunathamini sana miongozo hiyo yenye upendo na inayotufaa kabisa! Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kufuata mwongozo unaotolewa kwa wakati unaofaa na tengenezo lake.

13. Tunapata manufaa gani tunapomsikiliza Yesu?

13 Tunanufaika tunaposikiliza mambo yote ambayo Yesu alifundisha. Yesu aliwahakikishia wanafunzi wake kwamba mafundisho yake yangewaburudisha. Alisema hivi: “Nanyi mtapata burudisho kwa ajili yenu. Kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Neno la Mungu, linalotia ndani masimulizi manne ya Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu, hutuburudisha, hutupatia nguvu mpya za kiroho, na kutufanya tuwe na hekima. (Zab. 19:7; 23:3) Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:28.

‘NITALITUKUZA JINA LANGU’

14-15. (a) Ni pindi gani ya tatu inayosimuliwa kwenye Yohana 12:27, 28, ambapo Yehova alizungumza kutoka mbinguni? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba maneno ya Yehova yalimfariji na kumwimarisha Yesu?

14 Soma Yohana 12:27, 28. Injili ya Yohana inasimulia pindi ya tatu ambapo Yehova alizungumza kutoka mbinguni. Siku chache kabla ya kifo chake, Yesu alikuwa jijini Yerusalemu ili kusherehekea Pasaka kwa mara yake ya mwisho. Alisema hivi: “Ninataabika.” Halafu akasali hivi: “Baba, litukuze jina lako.” Kisha Baba yake akazungumza kutoka mbinguni na kusema: “Nimelitukuza nami nitalitukuza tena.”

15 Yesu alitaabika kwa sababu ya wajibu mkubwa aliokuwa nao wa kubaki akiwa mwaminifu kwa Yehova. Yesu alijua kwamba angepigwa vibaya na kuuawa kikatili. (Mt. 26:38) Lakini jambo muhimu zaidi kwa Yesu lilikuwa kulitukuza jina la Baba yake. Yesu alikuwa ameshtakiwa kwamba amekufuru, naye alihangaishwa na jinsi ambavyo kifo chake kingemletea Mungu suto. Bila shaka maneno hayo ya Yehova yalimtia moyo sana! Maneno hayo yalimhakikishia kwamba jina la Yehova lingetukuzwa. Hapana shaka kwamba yalimfariji sana na kumwimarisha akabili mambo ambayo yangempata. Ingawa huenda kwa wakati huo ni Yesu tu aliyeelewa maneno ya Baba yake, Yehova alihakikisha kwamba maneno hayo yaliandikwa kwa ajili yetu sote.—Yoh. 12:29, 30.

Yehova atalitukuza jina lake na kuwakomboa watu wake (Tazama fungu la 16) *

16. Kwa nini huenda nyakati nyingine tukahangaishwa na jinsi jina la Yehova linavyochafuliwa?

16 Kama Yesu, sisi pia huenda tukahangaishwa na jinsi jina la Yehova linavyochafuliwa. Na kama ilivyokuwa kwa Yesu, huenda sisi pia tumetendewa isivyo haki. Au huenda tunahangaishwa na habari za uwongo zinazosambazwa na wapinzani wetu kutuhusu. Huenda tukafikiria jinsi ambavyo habari hizo zinachafua jina la Yehova na tengenezo lake. Katika pindi hizo, maneno ambayo Yehova alimwambia Yesu hutufariji sana. Hatuhitaji kuhangaika kupita kiasi. Tunaweza kuwa na hakika kwamba “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo [yetu] na nguvu [zetu] za akili kupitia Kristo Yesu.” (Flp. 4:6, 7) Yehova hatashindwa kamwe kulitukuza jina lake. Kupitia Ufalme wake, ataondoa madhara yote ambayo Shetani na ulimwengu huu umewasababishia watumishi Wake waaminifu.—Zab. 94:22, 23; Isa. 65:17.

NUFAIKA NA SAUTI YA YEHOVA LEO

17. Kwa msingi wa andiko la Isaya 30:21, Yehova anatumia njia zipi kuzungumza nasi leo?

17 Yehova angali anazungumza nasi leo. (Soma Isaya 30:21.) Ni kweli kwamba hatusikii kihalisi sauti ya Mungu ikizungumza nasi kutoka mbinguni. Hata hivyo, ametuandalia Biblia, Neno lake lililoandikwa, ambalo anatumia kutupatia mwongozo. Zaidi ya hilo, roho yake takatifu inamwongoza “msimamizi mwaminifu” aendelee kuwapa watumishi Wake chakula. (Luka 12:42) Tunapokea chakula kingi sana cha kiroho kinachoandaliwa kupitia machapisho, habari zinazopatikana kwenye mtandao, video, na rekodi za sauti.

18. Maneno ya Yehova yanaimarishaje imani yako na kukupa ujasiri?

18 Hivyo basi, acheni tuzingatie akilini maneno ambayo Yehova alisema Mwana wake alipokuwa duniani! Na acheni maneno ya Mungu yaliyoandikwa katika Biblia yatupatie uhakika kwamba Yehova anaongoza mambo, naye ataondoa madhara yote ambayo Shetani na ulimwengu wake mwovu unatusababishia. Na acheni tuazimie kusikiliza kwa makini sauti ya Yehova. Tukifanya hivyo, tutafanikiwa kuvumilia matatizo yoyote ambayo tunakabili sasa na changamoto zozote zitakazotupata wakati ujao. Biblia inatukumbusha hivi: “Mnahitaji uvumilivu, ili baada ya kufanya mapenzi ya Mungu, mpokee utimizo wa ile ahadi.”—Ebr. 10:36.

WIMBO 4 “Yehova Ni Mchungaji Wangu”

^ fu. 5 Yesu alipokuwa duniani, Yehova alizungumza mara tatu kutoka mbinguni. Katika mojawapo ya pindi hizo, Yehova aliwasihi wanafunzi wa Kristo wamsikilize Mwana wake. Leo, Yehova huzungumza nasi kupitia Neno lake lililoandikwa, linalotia ndani mafundisho ya Yesu, na anazungumza nasi pia kupitia tengenezo lake. Makala hii itazungumzia jinsi tunavyonufaika tunapomsikiliza Yehova na Yesu.

^ fu. 52 MAELEZO YA PICHA: Mzee wa kutaniko anamwona mtumishi wa huduma akifanya usafi kwenye Jumba la Ufalme na akishughulikia machapisho. Mzee huyo anampongeza kwa uchangamfu.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Wenzi wa ndoa nchini Sierra Leone wanampatia mvuvi mwaliko wa kuhudhuria mikutano.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Mashahidi wakifanya mkutano kwenye nyumba ya mtu binafsi katika nchi ambayo kazi yetu imewekewa vizuizi. Wamevalia isivyo rasmi ili kuepuka kuvuta fikira za watu.