Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anathamini Unaposema “Amina”

Yehova Anathamini Unaposema “Amina”

YEHOVA anathamini ibada yetu. Yeye ‘huwakazia uangalifu na kuwasikiliza’ watumishi wake, na hakosi kamwe kuona tendo lolote la ibada wanalofanya, hata liwe dogo kadiri gani. (Mal. 3:16) Kwa mfano, fikiria neno ambalo huenda tumelitaja mara nyingi sana. Neno hilo ni “amina.” Je, Yehova anathamini hata tunapotamka neno hilo moja? Ndiyo! Ili tujue kwa nini anathamini, acheni tuchunguze maana ya neno hilo na jinsi linavyotumika katika Biblia.

“WATU WOTE WATASEMA, ‘AMINA!’”

Neno la Kiingereza linalotafsiriwa kuwa “amina” linamaanisha “na iwe hivyo,” au “bila shaka.” Linatokana na shina la neno la Kiebrania linalomaanisha “kuwa mwaminifu” au “mwenye kutegemeka.” Nyakati nyingine, neno hilo lilitumiwa katika mambo ya kisheria. Mtu alipokula kiapo, alisema “amina” ili kuthibitisha kwamba mambo aliyosema ni sahihi na kwamba anakubali matokeo ya mambo aliyosema. (Hes. 5:22) Alipotamka neno “amina” hadharani, alikuwa na sababu kubwa hata zaidi ya kutimiza ahadi yake.—Neh. 5:13.

Mfano wa pekee wa matumizi ya neno “amina” unapatikana kwenye kitabu cha Kumbukumbu la Torati sura ya 27. Waisraeli walipoingia katika Nchi ya Ahadi, walipaswa kukusanyika kati ya Mlima Ebali na Mlima Gerizimu ili kusikiliza Sheria ikisomwa. Hawakukusanyika huko ili kusikiliza tu Sheria ikisomwa, bali pia kutangaza kwamba wameikubali. Waliikubali kwa kusema “Amina!” waliposomewa matokeo mabaya ambayo wangepata ikiwa wangekosa kutii. (Kum. 27:15-26) Wazia mamia ya maelfu ya wanaume, wanawake, na watoto wakisema kwa sauti kubwa, “Amina”! (Yos. 8:30-35) Kwa hakika hawangesahau kamwe maneno waliyosema siku hiyo. Na Waisraeli hao walitenda kulingana na maneno yao, kwa kuwa simulizi hilo linasema: “Waisraeli waliendelea kumtumikia Yehova siku zote za Yoshua na sikuzote za wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua kufa ambao walikuwa wameona mambo yote makuu ambayo Yehova aliwatendea Waisraeli.”—Yos. 24:31.

Yesu pia alitumia neno “amina” kusisitiza ukweli wa mambo aliyosema, lakini alifanya hivyo kwa njia ya pekee. Badala ya kutamka neno hilo baada ya kusikia taarifa fulani, alitumia neno “amina” (linalotafsiriwa kwa Kiswahili kuwa “kwa kweli”) kabla ya kutamka ujumbe au taarifa fulani hakika. Nyakati nyingine alirudia neno hilo kwa kusema “amina amina.” (Mt. 5:18; Yoh. 1:51) Hivyo, aliwahakikishia wasikilizaji wake kwamba maneno yake yalikuwa ukweli mtupu. Yesu angeweza kuzungumza akiwa na uhakika huo kwa sababu yeye ndiye aliyepewa mamlaka ya kufanya ahadi zote za Mungu zitimie.—2 Kor. 1:20; Ufu. 3:14.

“WATU WOTE WAKASEMA, ‘AMINA!’ NAO WAKAMSIFU YEHOVA”

Waisraeli pia walitumia neno “amina” walipomsifu Yehova na kusali kwake. (Neh. 8:6; Zab. 41:13) Kwa kutamka neno hilo baada ya sala, wale waliokuwa wakisikiliza walionyesha kwamba walikubaliana na sala hiyo. Hivyo, wahudhuriaji wote walishiriki sala hiyo, na kufurahia pindi hiyo ya kiroho. Hivyo ndivyo ilivyokuwa Mfalme Daudi alipoleta Sanduku la Yehova jijini Yerusalemu. Wakati wa sherehe iliyofuata, Mfalme Daudi alitoa sala yenye kugusa moyo, iliyotolewa katika mtindo wa wimbo, nayo inapatikana kwenye 1 Mambo ya Nyakati 16:8-36. Wahudhuriaji walichochewa sana na maneno yake hivi kwamba “watu wote wakasema, ‘Amina!’ nao wakamsifu Yehova.” Naam, itikio lao la pamoja lilifanya siku hiyo iwe yenye shangwe kwelikweli.

Wakristo wa karne ya kwanza pia walitumia neno “amina” walipokuwa wakimsifu Yehova. Waandikaji wa Biblia walilitumia mara kwa mara walipoandika barua zao. (Rom. 1:25; 16:27; 1 Pet. 4:11) Kitabu cha Ufunuo hata kinawaonyesha viumbe wa roho mbinguni wakimtukuza Yehova kwa kusema: “Amina! Msifuni Yah!” (Ufu. 19:1, 4) Wakristo wa mapema walikuwa na kawaida ya kutamka neno “amina” baada ya sala zilizotolewa katika mikutano yao. (1 Kor. 14:16) Hata hivyo, hawakutamka neno hilo kidesturi tu.

KWA NINI KUSEMA “AMINA” NI JAMBO ZITO?

Baada ya kuchunguza historia na matumizi ya neno hilo, sasa tunaweza kuona kwa nini kusema “amina” ni njia inayofaa sana ya kuhitimisha sala. Tunapolitamka neno hilo mwishoni mwa sala zetu za kibinafsi, tunaonyesha kwamba kwa kweli tunamaanisha mambo tuliyosema. Na tunaposukumwa kutoka moyoni kusema neno “amina,” hata kimyakimya, baada ya sala kutolewa hadharani, tunaonyesha kwamba tunaunga mkono maneno yaliyosemwa. Fikiria sababu nyingine zinazofanya kusema “amina” kuwe jambo zito.

Tunakaza fikira na kuwa makini tunapokuwa katika ibada. Tunamwabudu Yehova wakati wa sala si kupitia mambo tunayosema tu, bali pia kupitia jinsi tunavyojiendesha. Kwa sababu tungependa kusema “amina” kutoka moyoni, tunachochewa kuwa na mtazamo unaofaa na kukaza fikira zetu kwenye sala inayotolewa.

Tunaunganishwa pamoja tukiwa waabudu. Sala ya watu wote inapotolewa, wote kutanikoni husikiliza ujumbe uleule. (Mdo. 1:14; 12:5) Tunapochochewa kutoka moyoni kusema “amina” pamoja na ndugu na dada zetu, umoja wetu huzidi kuimarika. Iwe tunasema “amina” kwa sauti au kimyakimya, itikio letu linampa Yehova sababu ya ziada ya kutenda kulingana na ombi letu la pamoja.

Tunaposema “amina” tunaungana na wengine katika kumsifu Yehova

Tunamsifu Yehova. Yehova anaona hata matendo madogo tunayofanya ya ibada. (Luka 21:2, 3) Anaona nia yetu na kilicho moyoni mwetu. Hata tukilazimika kusikiliza mkutano kupitia simu, tuna hakika kwamba Yehova anatambua tunaposema “amina” kwa unyenyekevu. Tunaposema “amina” tunaungana na wengine katika kumsifu Yehova.

Huenda kusema “amina” kukaonekana kuwa jambo dogo, lakini hilo ni jambo zito sana. Ensaiklopidia moja ya Biblia inaeleza kwamba “kupitia neno hilo moja” watumishi wa Mungu wanaweza kuonyesha kwamba “wana uhakika, wanakubaliana kabisa na yale yanayosemwa, na wanaonyesha tumaini lenye nguvu walilo nalo moyoni.” Acheni kila “amina” tunayosema impendeze Yehova.—Zab. 19:14.