Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 20

Faraja kwa Watu Waliotendewa Vibaya Kingono

Faraja kwa Watu Waliotendewa Vibaya Kingono

“Mungu wa faraja yote. . . hutufariji katika majaribu yetu yote.”​—2 KOR. 1:3, 4.

WIMBO 134 Watoto—Amana Kutoka kwa Mungu

MUHTASARI *

1-2. (a) Toa mfano unaoonyesha kwamba kiasili wanadamu wana uhitaji wa kufarijiwa na wana uwezo wa kuwafariji wengine. (b) Baadhi ya watoto huumizwa katika njia gani?

KIASILI, wanadamu wana uhitaji wa kufarijiwa, na wana uwezo wa pekee wa kuwafariji wengine. Kwa mfano, mtoto mdogo anapoanguka chini na kuchubua goti lake akicheza, huenda akamkimbilia Mama au Baba huku akilia. Wazazi hawawezi kuponya jeraha lake, lakini wanaweza kumfariji mtoto wao. Huenda wakamuuliza kilichompata, wakamfuta machozi, wakambembeleza na kumpakata kwa upendo, na huenda wakampaka dawa au kufunga jeraha lake. Muda si muda, mtoto huacha kulia na huenda hata akarudi kucheza. Baada ya kipindi fulani, kidonda chake hupona.

2 Hata hivyo, nyakati nyingine watoto huumizwa katika njia mbaya zaidi. Baadhi yao hutendewa vibaya kingono. Huenda wakatendewa vibaya kingono mara moja, au mara nyingi kwa kipindi cha miaka kadhaa. Katika hali zote hizo, jambo hilo linaweza kuwasababishia madhara makubwa sana ya kihisia. Katika visa fulani, mtu aliyetenda kosa hilo hukamatwa na kuadhibiwa. Katika visa vingine, huenda ikaonekana ni kana kwamba mkosaji amekwepa mkono wa sheria. Na hata ikiwa haki inatendeka upesi, madhara ya kutendewa vibaya kingono yanaweza kudumu hadi utu uzima.

3. Kama inavyotajwa kwenye 2 Wakorintho 1:3, 4, mapenzi ya Yehova ni nini, na tutazungumzia maswali gani?

3 Ikiwa Mkristo alitendewa vibaya kingono akiwa mtoto na angali anapambana na maumivu ya kihisia, anaweza kupata msaada gani? (Soma 2 Wakorintho 1:3, 4.) Ni wazi kuwa mapenzi ya Yehova ni kwamba kondoo wake waonyeshwe upendo na wapokee faraja wanayohitaji. Hivyo, acheni tuzungumzie maswali matatu: (1) Kwa nini wale waliotendewa vibaya kingono wakiwa watoto wanahitaji faraja? (2) Ni nani wanaoweza kuwapa faraja wanayohitaji? (3) Tunaweza kuwafariji jinsi gani?

KWA NINI WANAHITAJI FARAJA?

4-5. (a) Kwa nini ni muhimu kutambua kwamba watoto ni tofauti na watu wazima? (b) Kumtendea mtoto vibaya kingono kunaweza kuathirije uwezo wake wa kuwaamini wengine?

4 Baadhi ya watu wazima waliotendewa vibaya kingono wakiwa watoto wanahitaji faraja hata baada ya miaka mingi kupita. Kwa nini? Ili kuelewa hilo, tunapaswa kwanza kuelewa kuwa watoto ni tofauti sana na watu wazima. Kwa kawaida, madhara ambayo mtoto hupata anapotendewa vibaya ni tofauti kabisa na madhara ambayo huenda mtu mzima akapata. Fikiria mifano hii.

5 Watoto wanahitaji kuwaamini wale wanaowalea na kuwatunza na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja nao. Uhusiano wa aina hiyo huwafanya watoto wahisi wakiwa salama na wanajifunza kuwaamini wanaowapenda. (Zab. 22:9) Inasikitisha kwamba mara nyingi watoto hutendewa vibaya kingono nyumbani, na kwa kawaida watu wa karibu wa familia na marafiki wa familia ndio wanaofanya hivyo. Mtoto aliyetendewa vibaya kingono na mtu anayemwamini, anaweza kushindwa kuwaamini wengine, hata baada ya miaka mingi kupita.

6. Kwa nini kuwatendea watoto vibaya kingono ni jambo la kikatili na linalodhuru?

6 Watoto hawawezi kujilinda, na kuwatendea vibaya kingono ni jambo la kikatili na linalowadhuru. Kuwalazimisha watoto wafanye vitendo vya kingono miaka mingi kabla hawajawa tayari kimwili, kihisia, au kiakili kunaweza kuwasababishia madhara makubwa. Kuwatendea vibaya kingono kunaweza kupotosha mtazamo wao kuelekea ngono, kujielekea, au kuelekea mtu yeyote anayejaribu kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja nao.

7. (a) Kwa nini huenda ikawa rahisi kwa mtu mwenye hila anayewatendea watoto vibaya kingono kumdanganya mtoto, na anaweza kufanya hivyo jinsi gani? (b) Uwongo huo unaweza kuwa na madhara gani kwa watoto?

7 Watoto hawana uwezo wa kutosha wa kufikiri, kuchanganua mambo, na wa kutambua na kuepuka hatari. (1 Kor. 13:11) Hivyo, ni rahisi sana kwa watu wenye hila wanaowatendea watoto vibaya kingono kuwadanganya watoto. Watu hao huwajaza watoto uwongo kwa kuwafanya waamini kwamba wao ndio wa kulaumiwa, kwamba matendo hayo yanapaswa kuwa siri, kwamba hakuna atakayewasikiliza au kuwajali iwapo wataripoti jambo hilo, na kwamba vitendo vya kingono kati ya mtu mzima na mtoto ni mambo ya kawaida yanayoonyesha kuwa wanapendana kikweli. Uwongo wa aina hiyo unaweza kupotosha njia ya mtoto ya kufikiri na kumfanya asielewe ukweli wa mambo kwa miaka mingi. Mtoto aliyetendewa hivyo hukua akiamini kwamba hafai, ni mchafu, na hastahili kupendwa au kufarijiwa na yeyote.

8. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anaweza kuwafariji wale walioumizwa?

8 Hivyo, haishangazi kwamba kumtendea mtoto vibaya kingono kunaweza kumsababishia madhara ya kudumu. Huo ni uovu na ukatili mkubwa sana! Kuenea kwa janga hilo ni uthibitisho ulio wazi kwamba tunaishi katika siku za mwisho, kipindi ambacho watu wengi hawana “upendo wa asili” na ambacho “watu waovu na wajanja [wanaendelea] kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.” (2 Tim. 3:1-5, 13) Mbinu za Shetani ni za kikatili sana, na inasikitisha wakati wanadamu wanapotenda kwa njia inayomfurahisha Ibilisi. Hata hivyo, Yehova ana nguvu nyingi kuliko Shetani na watumishi wake. Anajua vizuri mbinu za Shetani. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anajua vizuri sana maumivu tunayopitia, na anaweza kutupatia faraja tunayohitaji. Tumebarikiwa kumtumikia “Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika majaribu yetu yote, ili tuweze kuwafariji wengine walio katika majaribu ya namna yoyote, kwa faraja ambayo tunapokea kutoka kwa Mungu.” (2 Kor. 1:3, 4) Hata hivyo, Yehova huwatumia nani kuwafariji wengine?

NI NANI WANAOWEZA KUTOA FARAJA?

9. Kulingana na maneno ya Mfalme Daudi kwenye Zaburi 27:10, Yehova atawafanyia nini wale walioachwa na familia zao?

9 Wale walioachwa na wazazi wao au waliotendewa vibaya kingono na watu wao wa karibu, huenda ndio hasa wanaohitaji faraja. Mtunga zaburi Daudi alijua kwamba Yehova ndiye chanzo cha faraja tunachoweza kutegemea nyakati zote. (Soma Zaburi 27:10.) Daudi alikuwa na imani kwamba Yehova huwachukua wale waliokataliwa na wapendwa wao. Yehova hufanyaje hivyo? Yeye huwatumia watumishi wake waaminifu. Waabudu wenzetu ni familia yetu ya kiroho. Kwa mfano, Yesu aliwarejelea wale walioshirikiana naye kumwabudu Yehova kuwa ndugu, dada, na mama.—Mt. 12:48-50.

10. Mtume Paulo alifafanuaje kazi yake akiwa mzee wa kutaniko?

10 Fikiria mfano mmoja wa uhusiano wa kifamilia ulio katika kutaniko la Kikristo. Mtume Paulo alikuwa mzee mwaminifu na mwenye bidii. Alikuwa mfano mzuri, na hata aliongozwa na roho takatifu kuwaambia wengine wamwige yeye kama anavyomwiga Kristo. (1 Kor. 11:1) Wakati fulani, Paulo alifafanua hivi kazi yake akiwa mzee wa kutaniko: “Tuliwatendea kwa upole, kama vile mama anayenyonyesha anavyowatunza watoto wake kwa wororo.” (1 The. 2:7) Vivyo hivyo, wazee washikamanifu leo hutumia maneno ya upole na ya wororo wanapowafariji kwa kutumia Maandiko wale wanaohitaji msaada.

Kwa kawaida, dada Wakristo waliokomaa kiroho wana uwezo mzuri sana wa kutoa faraja (Tazama fungu la 11) *

11. Ni nini kinachoonyesha kwamba si wazee tu wanaoweza kuwafariji wengine?

11 Je, ni wazee tu wanaoweza kuwafariji wale waliotendewa vibaya kingono? Hapana. Sisi sote tuna jukumu la ‘kuendelea kufarijiana.’ (1 The. 4:18) Dada Wakristo waliokomaa kiroho wanaweza kuwatia moyo sana hasa dada wenzao wanaohitaji faraja. Hivyo, haishangazi kwamba Yehova Mungu anajilinganisha na mama anayemfariji mwanawe. (Isa. 66:13) Biblia ina mifano ya wanawake waliowafariji wale waliokuwa wakiteseka. (Ayu. 42:11) Lazima Yehova anafurahi sana kuwaona wanawake Wakristo leo wakiwafariji dada wenzao wanaopambana na maumivu ya kihisia! Katika visa vingine, huenda mzee mmoja au wawili wakamwomba kwa busara dada aliyekomaa kiroho amsaidie dada anayekabili maumivu ya kihisia, ikiwa anaweza. *

TUNAWEZA KUWAFARIJI WENGINE JINSI GANI?

12. Tutajihadhari tusifanye nini?

12 Bila shaka tunajihadhari tusiingilie mambo ambayo Mkristo mwenzetu hangependa kuyazungumzia. (1 The. 4:11) Hata hivyo, tunaweza kuwasaidiaje wale wanaohitaji na wanaotaka msaada na faraja? Acheni tuzungumzie njia tano za Kimaandiko tunazoweza kutumia kuwafariji wengine.

13. Kama simulizi la 1 Wafalme 19:5-8 linavyoonyesha, malaika wa Yehova alimfanyia nini Eliya, na tunaweza kumwigaje malaika huyo?

13 Toa msaada hususa. Nabii Eliya alipokuwa akikimbia ili aokoe maisha yake, alikuwa amevunjika moyo sana hivi kwamba alitamani kufa. Yehova alimtuma malaika mwenye nguvu amtembelee mwanamume huyo aliyevunjika moyo. Malaika huyo alitoa msaada hususa aliohitaji. Alimpa Eliya chakula cha moto na akamtia moyo ale. (Soma 1 Wafalme 19:5-8.) Simulizi hilo linafunua ukweli fulani muhimu: Nyakati nyingine tendo fulani dogo la fadhili linaweza kuwa msaada mkubwa. Huenda mlo, zawadi ndogo, au kadi yenye maneno yanayogusa moyo ikamfariji na kumhakikishia ndugu au dada kwamba tunampenda na kumjali. Tunaweza kutoa msaada wa aina hiyo ikiwa si rahisi kwetu kuzungumza nao kuhusu mambo yao ya kibinafsi au mambo yanayowaumiza hisia.

14. Simulizi la Eliya linatufundisha nini?

14 Wafanye wale waliovunjika moyo wahisi wakiwa salama na bila wasiwasi. Simulizi la Eliya linatufundisha somo lingine. Kwa njia ya kimuujiza, Yehova alimpa nabii huyo msaada aliohitaji ambao ulimwezesha kusafiri kwa kilomita nyingi mpaka Mlima Horebu. Huenda Eliya alihisi akiwa salama kwenye eneo hilo la mbali, ambako Yehova alikuwa amefanya agano pamoja na watu wake karne kadhaa mapema. Inaelekea sasa alihisi akiwa mbali sana na watu waliotaka kumuua. Tunajifunza nini? Ikiwa tunataka kuwafariji watu waliotendewa vibaya kingono, tunahitaji kwanza kuwafanya wahisi wakiwa salama. Kwa mfano, wazee wanahitaji kukumbuka kwamba huenda dada aliyevunjika moyo akahisi akiwa salama zaidi na huru kujieleza akiwa nyumbani katika mazingira matulivu kuliko Jumba la Ufalme. Huenda dada mwingine akahisi tofauti.

Tunaweza kumponya mtu kwa kumsikiliza kwa subira, kusali naye kwa unyoofu, na kwa kuchagua maneno yenye kufariji (Tazama fungu la 15 hadi 20) *

15-16. Kuwa msikilizaji mzuri kunahusisha nini?

15 Uwe msikilizaji mzuri. Biblia hutoa ushauri huu ulio wazi: “Kila mtu lazima awe mwepesi wa kusikia, si mwepesi wa kusema.” (Yak. 1:19) Je, sisi ni wasikilizaji wazuri? Huenda tukafikiri kwamba msikilizaji mzuri ni yule anayenyamaza tu na kumtazama anayezungumza, bila kusema chochote. Lakini ili tuwe wasikilizaji wazuri tunahitaji kufanya mengi zaidi. Kwa mfano, Eliya alimmiminia Yehova hisia zilizomfadhaisha, na Yehova alimsikiliza kwa makini. Yehova alitambua kwamba Eliya aliogopa, alihisi upweke, na alihisi kwamba kazi yote aliyokuwa amefanya ilikuwa ya bure. Yehova alishughulikia kwa upendo kila jambo lililomhangaisha. Alionyesha kwamba alikuwa amemsikiliza Eliya kwa makini.—1 Fal. 19:9-11, 15-18.

16 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunamhurumia kwa wororo na kumsikitikia ndugu au dada tunayemsikiliza, mambo yanayoonyesha kwamba tunampenda? Nyakati nyingine, maneno machache ya busara na yenye kutia moyo huonyesha jinsi tunavyohisi. Unaweza kusema hivi: “Nasikitika sana kwamba ulipatwa na jambo hilo! Hakuna mtoto yeyote anayepaswa kutendewa hivyo!” Unaweza kumuuliza rafiki yako anayefadhaika maswali machache ili kuhakikisha kwamba unaelewa jambo analosema. Labda unaweza kumuuliza, “Tafadhali unaweza kunisaidia kuelewa unachomaanisha?” au “Uliposema hivi, nilielewa kwamba . . . Niko sahihi?” Kufanya hivyo kunaweza kumhakikishia rafiki yako kwamba unamsikiliza kwa makini, na unajitahidi kumwelewa.—1 Kor. 13:4, 7.

17. Kwa nini tunapaswa kuwa na subira na ‘tusiwe wepesi wa kusema’?

17 Hata hivyo, uwe mwangalifu ‘usiwe mwepesi wa kusema.’ Usimkatize mtu ili kumpa ushauri au kurekebisha njia yake ya kufikiri. Na uwe na subira! Eliya alipommiminia Yehova moyo wake, alizungumza kwa uchungu mwingi na maumivu makali. Baadaye, baada ya Yehova kuimarisha imani yake, Eliya alijieleza tena kwa uchungu mwingi na maumivu makali, akitumia maneno yaleyale. (1 Fal. 19:9, 10, 13, 14) Tunajifunza nini? Nyakati nyingine, huenda watu waliovunjika moyo wakahitaji kumimina moyo wao zaidi ya mara moja. Kama Yehova, tungependa kuwasikiliza kwa subira. Badala ya kuwaeleza jinsi wanavyoweza kusuluhisha matatizo yao, tutajitahidi kuwaonyesha huruma nyororo na kuwasikitikia.—1 Pet. 3:8.

18. Sala zetu zinaweza kuwafariji jinsi gani wale walio na maumivu ya kihisia?

18 Sali kwa unyoofu pamoja na mtu aliye na maumivu ya kihisia. Huenda wale walioshuka moyo sana wakashindwa kusali. Mtu anaweza kuhisi kwamba hastahili kuzungumza na Yehova. Ikiwa tunatamani kumfariji mtu anayehisi hivyo, tunaweza kutoa sala pamoja naye na kumtaja kwa jina. Tunaweza kumweleza Yehova jinsi rafiki yetu mpendwa aliyeshuka moyo alivyo mwenye thamani kwetu na kutanikoni. Tunaweza kumwomba Yehova amliwaze na kumfariji kondoo wake mwenye thamani. Sala za aina hiyo zinaweza kumfariji sana rafiki yetu.—Yak. 5:16.

19. Ni nini kitakachotusaidia tuwe tayari kumfariji mtu?

19 Chagua maneno yanayoponya na kufariji. Tafakari kabla ya kuzungumza. Kuzungumza bila kufikiri kunaweza kumuumiza mtu. Maneno yenye fadhili yanaweza kuponya. (Met. 12:18) Hivyo, sali kwa Yehova akusaidie utumie maneno yenye fadhili, yenye kufariji, na yenye kuliwaza. Kumbuka kwamba hakuna maneno mengine yoyote yaliyo na nguvu kuliko maneno ya Yehova yaliyo katika Biblia.—Ebr. 4:12.

20. Huenda mambo mabaya ambayo baadhi ya ndugu na dada zetu wamepitia maishani yamefanya wasadiki nini, na tungependa kuwakumbusha nini?

20 Mtu aliyewahi kutendewa vibaya kingono anaweza kusadiki kwamba yeye ni mchafu, hafai, hapendwi, au hata hastahili kupendwa. Huo ni uwongo mbaya sana! Hivyo, tumia Maandiko kuwakumbusha kwamba wao ni wenye thamani sana machoni pa Yehova. (Tazama sanduku “ Faraja Kutoka Katika Maandiko.”) Kumbuka jinsi malaika alivyomtia nguvu nabii Danieli kwa wororo alipokuwa ameshuka moyo na kuhisi akiwa dhaifu. Yehova alitaka mwanamume huyo mpendwa ajue kwamba alikuwa mwenye thamani machoni pake. (Dan. 10:2, 11, 19) Vivyo hivyo, ndugu na dada zetu wenye maumivu moyoni ni wenye thamani machoni pa Yehova!

21. Watenda dhambi wasiotubu watapatwa na nini, lakini kwa sasa sisi sote tunapaswa kuazimia kufanya nini?

21 Tunapowafariji wengine, tunawakumbusha jinsi Yehova anavyowapenda. Na hatupaswi kamwe kusahau kwamba Yehova ni Mungu wa haki. Yehova anamjua kila mtu aliyetendewa vibaya kingono, hata ikiwa hakuna yeyote anayefahamu jambo hilo. Yehova huona mambo yote, naye atahakikisha kwamba watenda dhambi wote wasiotubu wameadhibiwa. (Hes. 14:18) Kwa sasa, acheni tufanye yote tuwezayo kuwaonyesha upendo wale waliotendewa vibaya kingono. Inafariji sana kujua kwamba Yehova atawaponya kwa umilele wale wote waliotendewa vibaya na Shetani na ulimwengu wake! Hivi karibuni, mambo hayo yenye kuumiza hayataingia tena kamwe akilini na moyoni.—Isa. 65:17.

WIMBO 109 Pendaneni Sana Kutoka Moyoni

^ fu. 5 Watu waliotendewa vibaya kingono wakiwa watoto huenda wakakabili changamoto nyingi hata baada ya miaka mingi kupita. Makala hii itatusaidia kujua kwa nini. Pia, tutazungumzia ni nani wanaoweza kuwafariji watu kama hao. Mwishowe, tutazungumzia baadhi ya njia nzuri tunazoweza kutumia ili kuwafariji.

^ fu. 11 Ni uamuzi wa kibinafsi wa mtu aliyetendewa vibaya kingono kuamua ikiwa anahitaji msaada wa wataalamu wa afya au la.

^ fu. 76 MAELEZO YA PICHA: Dada mkomavu akimfariji dada aliye na maumivu ya kihisia.

^ fu. 78 MAELEZO YA PICHA: Wazee wawili wamemtembelea dada huyo aliyefadhaika moyoni. Dada huyo amemwalika pia yule dada mkomavu.