Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 18

Upendo na Haki Katika Kutaniko la Kikristo

Upendo na Haki Katika Kutaniko la Kikristo

“Endeleeni kubebeana mizigo mizito, na hivyo mtaitimiza sheria ya Kristo.”​—GAL. 6:2.

WIMBO 12 Mungu Mkuu, Yehova

MUHTASARI *

1. Tunaweza kuwa na uhakika kuhusu mambo gani mawili?

YEHOVA MUNGU anawapenda waabudu wake. Amekuwa akiwapenda, na ataendelea kuwapenda. Pia, anapenda haki. (Zab. 33:5) Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kuhusu mambo haya mawili: (1) Yehova huumia anapoona watumishi wake wakitendewa isivyo haki. (2) Atahakikisha kwamba haki inatendeka. Kwenye makala ya kwanza katika mfululizo huu, * tulijifunza kwamba upendo ndio uliokuwa msingi wa Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kupitia Musa. Sheria ilitetea haki—haki kwa wote, hata wanyonge. (Kum. 10:18) Sheria hiyo inafunua jinsi Yehova anavyowajali sana waabudu wake.

2. Tutajibu maswali gani?

2 Sheria ya Musa ilikoma mwaka wa 33 W.K., kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa. Je, sasa Wakristo wangekosa ulinzi kwa sababu hawana sheria iliyotetea haki na ambayo msingi wake ulikuwa upendo? Sivyo hata kidogo! Wakristo walikuwa na sheria mpya. Jambo la kwanza tutakalozungumzia katika makala hii ni: Sheria hiyo ni nini? Kisha tutajibu maswali haya: Kwa nini tunaweza kusema kwamba upendo ndio msingi wa sheria hiyo? Kwa nini tunaweza kusema kwamba inatetea haki? Chini ya sheria hiyo, wale walio na mamlaka wanapaswa kuwatendeaje wengine?

“SHERIA YA KRISTO” NI NINI?

3. “Sheria ya Kristo” inayotajwa kwenye Wagalatia 6:2 inatia ndani mambo gani?

3 Soma Wagalatia 6:2. Wakristo wako chini ya “sheria ya Kristo.” Yesu hakuwaandikia wafuasi wake orodha ya sheria, bali aliwapa maagizo, amri, na kanuni ambazo zingewaongoza maishani. “Sheria ya Kristo” inatia ndani mambo yote ambayo Yesu alifundisha. Ili kuelewa sheria hiyo vizuri zaidi, fikiria mambo yafuatayo.

4-5. Yesu alifundisha katika njia zipi, na alifundisha lini?

4 Yesu alifundisha katika njia zipi? Kwanza, kupitia mambo aliyosema. Maneno yake yalikuwa na nguvu kwa sababu alifundisha kweli kumhusu Mungu, kuhusu kusudi halisi la maisha, na kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho pekee la mateso yote ya wanadamu. (Luka 24:19) Pia, Yesu alifundisha kupitia mfano wake. Kupitia jinsi alivyoishi, aliwaonyesha wafuasi wake jinsi wanavyopaswa kuishi.—Yoh. 13:15.

5 Yesu alifundisha lini? Alifundisha wakati wa huduma yake alipokuwa duniani. (Mt. 4:23) Pia, aliwafundisha wafuasi wake muda mfupi baada ya kufufuliwa. Kwa mfano, aliwatokea wanafunzi wake 500 hivi wakiwa kikundi na kuwapa amri ya ‘kufanya wanafunzi.’ (Mt. 28:19, 20; 1 Kor. 15:6) Akiwa kichwa cha kutaniko, Yesu aliendelea kuwapa maagizo wanafunzi wake baada ya kurudi mbinguni. Kwa mfano, mwaka wa 96 W.K. hivi, Kristo alimpa maagizo mtume Yohana awatie moyo na kuwashauri Wakristo watiwa-mafuta.—Kol. 1:18; Ufu. 1:1.

6-7. (a) Mafundisho ya Yesu yanapatikana wapi? (b) Tunatii sheria ya Kristo jinsi gani?

6 Mafundisho ya Yesu yanapatikana wapi? Vitabu vinne vya Injili vina mambo mengi ambayo Yesu alisema na kutenda alipokuwa duniani. Vitabu vingine vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ambavyo viliandikwa na wanaume walioongozwa na roho takatifu na ambao walikuwa na “akili ya Kristo,” vinatusaidia kuelewa hata zaidi njia ya Yesu ya kuona mambo.—1 Kor. 2:16.

7 Somo: Mafundisho ya Yesu yanagusa nyanja zote za maisha. Hivyo, sheria ya Kristo inagusa mambo tunayofanya nyumbani, kazini au shuleni, na kutanikoni. Tunajifunza sheria hiyo kwa kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na kuyatafakari. Tunaitii kwa kupatanisha maisha yetu na mafundisho, amri, na kanuni zinazopatikana katika vitabu hivyo vya Biblia. Tunapotii sheria ya Kristo, tunamtii Yehova, Mungu wetu mwenye upendo, ambaye ndiye Chanzo cha mambo yote ambayo Yesu alifundisha.—Yoh. 8:28.

SHERIA INAYOTEGEMEA UPENDO

8. Msingi wa sheria ya Kristo ni nini?

8 Nyumba nzuri iliyojengwa juu ya msingi imara huwafanya wale wanaoishi ndani yake wahisi wakiwa salama na bila wasiwasi. Vivyo hivyo, sheria nzuri iliyo na msingi imara huwafanya wale wanaoishi kupatana nayo wahisi wakiwa salama na bila wasiwasi. Sheria ya Kristo imejengwa juu ya msingi bora zaidi, yaani, upendo. Kwa nini tunasema hivyo?

Tunatii “sheria ya Kristo” tunapowatendea wengine kwa upendo (Tazama fungu la 9 hadi 14) *

9-10. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba Yesu alichochewa na upendo, na tunaweza kumwigaje?

9 Kwanza, Yesu alichochewa na upendo katika mambo yote aliyofanya. Kuwasikitikia watu, au kuwaonyesha huruma nyororo ni njia ya kuwaonyesha upendo. Kwa kuwa Yesu aliusikitikia umati, alisukumwa kuwafundisha, kuponya wagonjwa, kulisha wenye njaa, na kuwafufua wafu. (Mt. 14:14; 15:32-38; Marko 6:34; Luka 7:11-15) Ingawa mambo hayo yalitumia muda na nguvu zake nyingi, kwa hiari, Yesu alitanguliza kwanza mahitaji ya wengine. Zaidi ya yote, alionyesha upendo mkubwa sana kwa kutoa uhai wake kwa ajili ya wengine.—Yoh. 15:13.

10 Somo: Tunaweza kumwiga Yesu kwa kutanguliza kwanza mahitaji ya wengine. Pia, tunaweza kumwiga kwa kujifunza jinsi ya kuwaonyesha huruma nyororo watu katika eneo letu. Tunaposukumwa na huruma kama hiyo kuhubiri na kufundisha habari njema, tunatii sheria ya Kristo.

11-12. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova anatujali sana? (b) Tunaweza kuiga upendo wa Yehova jinsi gani?

11 Pili, Yesu alionyesha jinsi Baba yake alivyo mwenye upendo. Wakati wa huduma yake, Yesu alionyesha jinsi Yehova anavyowajali sana waabudu wake. Miongoni mwa mambo mengine, Yesu alifundisha hivi: Kila mmoja wetu ni mwenye thamani sana machoni pa Baba yetu wa mbinguni. (Mt. 10:31) Yehova anatamani sana kumkaribisha kondoo aliyepotea ambaye anatubu na kurudi kutanikoni. (Luka 15:7, 10) Yehova alithibitisha kwamba anatupenda alipomtoa Mwana wake kuwa fidia kwa ajili yetu.—Yoh. 3:16.

12 Somo: Tunaweza kuiga upendo wa Yehova jinsi gani? (Efe. 5:1, 2) Tunamwona kila ndugu na dada kuwa mwenye thamani sana, na tunamkaribisha kwa shangwe kila “kondoo aliyepotea” ambaye anamrudia Yehova. (Zab. 119:176) Tunathibitisha kwamba tunawapenda ndugu na dada zetu kwa kujitoa ili kuwasaidia, hasa nyakati za uhitaji. (1 Yoh. 3:17) Tunapowatendea wengine kwa upendo, tunatii sheria ya Kristo.

13-14. (a) Kama inavyotajwa kwenye Yohana 13:34, 35, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wafanye nini, na kwa nini amri hiyo ni mpya? (b) Tunatii amri hiyo mpya jinsi gani?

13 Tatu, Yesu aliwaamuru wafuasi wake waonyeshane upendo bila ubinafsi. (Soma Yohana 13:34, 35.) Amri ya Yesu ni mpya kwa sababu inataka tuwaonyeshe wengine aina ya upendo ambao haukuwa takwa chini ya Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli: Wapende waabudu wenzako kama Yesu alivyokupenda. Ili mtu afanye hivyo, anahitaji kuwa na upendo usio na ubinafsi. * Tunapaswa kuwapenda ndugu na dada zetu kuliko hata jinsi tunavyojipenda wenyewe. Ni lazima tuwapende kufikia hatua ya kuwa tayari kufa kwa ajili yao, kama Yesu alivyofanya kwa ajili yetu.

14 Somo: Tunatii amri hiyo mpya jinsi gani? Kwa ufupi, ni kwa kujidhabihu kwa ajili ya ndugu na dada zetu. Hatutakuwa tayari tu kufa kwa ajili yao, bali pia tutakuwa tayari kujidhabihu katika mambo madogo-madogo. Kwa mfano, tunatii amri ya Kristo tunapokuwa na kawaida ya kujidhabihu ili kumsaidia ndugu au dada aliyezeeka kufika mikutanoni, au tunapokuwa tayari kuacha mambo tunayopenda ili kumfurahisha mwabudu mwenzetu, au kuomba ruhusa kazini ili kujitolea kutoa msaada misiba inapotokea. Tunapofanya hivyo tunasaidia pia kufanya kutaniko kuwa mahali ambapo kila mtu anahisi akiwa salama na bila wasiwasi.

SHERIA INAYOTETEA HAKI

15-17. (a) Matendo ya Yesu yalifunuaje hisia zake kuhusu haki? (b) Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani?

15 Neno “haki” kama linavyotumika katika Biblia, linamaanisha kufanya mambo ambayo Yehova anaona kuwa sawa na kuyafanya bila ubaguzi. Kwa nini tunaweza kusema kwamba sheria ya Kristo inatetea haki?

Yesu aliwaheshimu na kuwatendea kwa fadhili wanawake, kutia ndani wale waliodharauliwa na watu wengine (Tazama fungu la 16) *

16 Kwanza, fikiria jinsi matendo ya Yesu yalivyofunua hisia zake kuhusu haki. Katika siku zake, viongozi wa dini ya Kiyahudi waliwachukia watu wasio Wayahudi, waliwadharau Wayahudi wa hali ya chini, na hawakuwaheshimu wanawake. Hata hivyo, Yesu hakuwa na upendeleo wala ubaguzi aliposhughulika na watu wote. Alikubali kuwasaidia watu wasio Wayahudi ambao walionyesha imani kwake. (Mt. 8:5-10, 13) Aliwahubiria wote bila ubaguzi, matajiri na maskini. (Mt. 11:5; Luka 19:2, 9) Hakuwahi kamwe kuwatendea wanawake kikatili au kwa ukali. Kinyume chake, aliwatendea wanawake kwa heshima na fadhili, kutia ndani wale waliodharauliwa na watu wengine.—Luka 7:37-39, 44-50.

17 Somo: Tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwatendea wengine bila ubaguzi na kuwahubiria wote walio tayari kusikiliza, hata iwe wana cheo gani katika jamii au wanashirikiana na dini gani. Wanaume Wakristo wanamwiga Yesu kwa kuwatendea wanawake kwa heshima. Tunapofanya mambo kama hayo, tunatii sheria ya Kristo.

18-19. Yesu alifundisha nini kuhusu haki, na mafundisho yake yanatufundisha mambo gani?

18 Pili, fikiria mambo ambayo Yesu alifundisha kuhusu haki. Aliwafundisha wafuasi wake kanuni ambazo zingewasaidia kuwatendea wengine bila upendeleo. Kwa mfano, fikiria kuhusu ile Kanuni Bora. (Mt. 7:12) Sisi sote tunapenda kutendewa kwa haki. Hivyo, tunapaswa kuwatendea wengine kwa haki. Tukifanya hivyo, huenda wao pia wakachochewa kututendea kwa haki. Lakini vipi ikiwa tumetendewa isivyo haki? Yesu aliwafundisha wafuasi wake wawe na imani kwamba Yehova ‘atawatendea haki wale wanaomlilia mchana na usiku.’ (Luka 18:6, 7) Kihalisi, taarifa hiyo ni ahadi: Mungu wetu mwenye haki anajua majaribu tunayokabili katika siku hizi za mwisho, na kwa wakati wake atahakikisha kwamba tunatendewa haki.—2 The. 1:6.

19 Somo: Tunapofuata kanuni ambazo Yesu alifundisha, tutawatendea wengine kwa haki. Na ikiwa tumetendewa isivyo haki katika ulimwengu huu wa Shetani, tunaweza kufarijika kwa kujua kwamba Yehova atahakikisha kuwa tumetendewa haki.

WALE WALIO NA MAMLAKA WANAPASWA KUWATENDEAJE WENGINE?

20-21. (a) Wale walio na mamlaka wanapaswa kuwatendeaje wengine? (b) Mume anaweza kuonyeshaje upendo usio na ubinafsi, na baba anapaswa kuwatendeaje watoto wake?

20 Chini ya sheria ya Kristo, wale walio na mamlaka wanapaswa kuwatendeaje wengine? Kwa kuwa upendo ndio msingi wa sheria hiyo, wale walio na mamlaka wanapaswa kuwaheshimu wale walio chini ya utunzaji wao na kuwatendea kwa upendo. Wanapaswa kukumbuka kwamba njia ya Kristo ndiyo njia ya upendo.

21 Katika familia. Mume anapaswa kumpenda mke wake ‘kama vile Kristo anavyolipenda kutaniko.’ (Efe. 5:25, 28, 29) Mume anapaswa kuiga upendo wa Kristo usio na ubinafsi kwa kutanguliza kwanza mahitaji na masilahi ya mke wake. Huenda ikawa vigumu kwa baadhi ya wanaume kuonyesha upendo kama huo, labda kwa sababu hawakulelewa katika mazingira ambayo watu walizoea kuwatendea wengine kwa haki na upendo. Huenda ikawa vigumu kwao kuacha mazoea hayo mabaya, lakini ni lazima wafanye mabadiliko ili kutii sheria ya Kristo. Mume anayeonyesha upendo usio na ubinafsi humchochea mke wake kumheshimu. Baba anayewapenda kikweli watoto wake hawezi kamwe kuwatendea kikatili kupitia maneno au matendo yake. (Efe. 4:31) Badala yake, yeye huwathamini watoto wake na kuwaonyesha upendo ili wahisi wakiwa salama na bila wasiwasi. Baba kama huyo hupendwa na kutumainiwa na watoto wake.

22. Kama inavyotajwa kwenye 1 Petro 5:1-3, “kondoo” ni mali ya nani, nao wanapaswa kutendewaje?

22 Kutanikoni. Wazee wanapaswa kukumbuka kwamba “kondoo” si mali yao. (Yoh. 10:16; soma 1 Petro 5:1-3.) Maneno “kundi la Mungu,” “mbele za Mungu,” na “urithi wa Mungu,” huwakumbusha wazee kwamba kondoo ni mali ya Yehova. Anataka kondoo wake watendewe kwa upendo na wororo. (1 The. 2:7, 8) Wazee wanaotimiza kwa upendo jukumu lao wakiwa wachungaji hupata kibali cha Yehova. Pia, wazee kama hao hupendwa na kuheshimiwa na ndugu na dada zao.

23-24. (a) Wazee wana jukumu gani inapohusu visa vya dhambi nzito? (b) Wanaposhughulikia visa kama hivyo, wazee hufikiria mambo gani?

23 Wazee wana jukumu gani inapohusu visa vya dhambi nzito? Jukumu lao ni tofauti na jukumu la waamuzi na wazee waliowekwa rasmi chini ya Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli. Chini ya Sheria hiyo, wanaume waliowekwa rasmi hawakushughulikia tu mambo ya kiroho, bali pia walishughulikia kesi za madai na za uhalifu. Lakini chini ya sheria ya Kristo, wazee wana jukumu la kushughulikia mambo ya kiroho tu inapohusu visa vya ukosaji. Wanatambua kwamba mamlaka za serikali zimekabidhiwa na Mungu wajibu wa kushughulikia kesi za madai na za uhalifu. Wajibu huo unatia ndani mamlaka ya kumtoza mhusika faini au kumfunga gerezani.—Rom. 13:1-4.

24 Wazee wa kutaniko hushughulikiaje visa vya dhambi nzito? Wao hutumia Maandiko kuchanganua mambo na kufanya maamuzi. Wanazingatia akilini kwamba upendo ndio msingi wa sheria ya Kristo. Upendo huwachochea wazee kufikiria maswali haya: Ni jambo gani linalohitaji kufanywa ili kumsaidia yeyote kutanikoni ambaye ametendewa isivyo haki? Upendo huwachochea wazee wa kutaniko wachunguze mambo yafuatayo kuhusu mkosaji: Je, mkosaji ametubu? Je, tunaweza kumsaidia awe tena na uhusiano mzuri pamoja na Yehova?

25. Makala inayofuata itazungumzia nini?

25 Tunashukuru sana kwamba tuko chini ya sheria ya Kristo! Sisi sote tunapojitahidi kuitii, tunasaidia kufanya kutaniko kuwa mahali ambapo kila mtu anahisi kwamba anapendwa, anathaminiwa, na yuko salama. Ingawa hivyo, tunaishi katika ulimwengu ambao “watu waovu” wanaendelea “kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.” (2 Tim. 3:13) Ni lazima tuendelee kuwa macho. Kutaniko la Kikristo linaweza kumwigaje Mungu katika kuonyesha haki linaposhughulika na visa vya kuwatendea watoto vibaya kingono? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

WIMBO 15 Msifuni Mzaliwa wa Kwanza wa Yehova!

^ fu. 5 Makala hii na makala nyingine mbili zitakazofuata, ni sehemu ya mfululizo unaozungumzia sababu zinazotusaidia kuwa na uhakika kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo na haki. Yehova anataka watu wake watendewe kwa haki, na anawafariji wale ambao wametendewa isivyo haki katika ulimwengu huu mwovu.

^ fu. 1 Tazama makala, “Upendo na Haki Katika Taifa la Kale la Israeli” kwenye toleo la Februari 2019 la gazeti Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 13 UFAFANUZI WA MANENO: Upendo usio na ubinafsi hutuchochea kutanguliza kwanza mahitaji na masilahi ya wengine badala ya masilahi yetu. Tutakuwa tayari kutoa au kujinyima kitu fulani ili kuwasaidia au kuwanufaisha wengine.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Yesu anamwona mjane ambaye amefiwa na mwana wake pekee. Akisukumwa na sikitiko, Yesu anamfufua kijana huyo.

^ fu. 63 MAELEZO YA PICHA: Yesu akila chakula katika nyumba ya Farisayo anayeitwa Simoni. Mwanamke fulani, labda ni kahaba, ametoka tu kuosha miguu ya Yesu kwa machozi yake na kuikausha kwa nywele zake na kisha kuimwagia mafuta. Simoni hafurahishwi na matendo ya mwanamke huyo, lakini Yesu anamtetea mwanamke huyo.