Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 25

Mtegemee Yehova Unapopatwa na Mkazo

Mtegemee Yehova Unapopatwa na Mkazo

“Mimi ni . . . mwenye mkazo mkubwa sana.”​—1 SAM. 1:15.

WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu

MUHTASARI *

1. Kwa nini ni lazima tutii onyo la Yesu?

KATIKA unabii wake kuhusu siku za mwisho Yesu alisema hivi: “Jiangalieni wenyewe ili mioyo yenu isilemewe kamwe . . . na mahangaiko ya maisha,” yaani, mahangaiko kuhusu kujiruzuku au wasiwasi kuhusu maisha ya kila siku. (Luka 21:34) Tunahitaji kutii onyo hilo. Kwa nini? Kwa sasa, ni lazima tukabiliane na matatizo yaleyale yanayosababisha mkazo ambayo kila mtu anakabili.

2. Ndugu na dada zetu wanakabili matatizo gani yanayowaletea mkazo?

2 Nyakati nyingine, tunalazimika kukabiliana kwa wakati mmoja na matatizo kadhaa yanayotuletea mkazo. Fikiria mifano ifuatayo. Shahidi mmoja anayeitwa John, * aliye na ugonjwa unaodhoofisha misuli na mfumo wa neva, alihuzunika sana mke wake aliyekuwa amefunga ndoa naye kwa miaka 19 alipomwacha. Kisha binti zake wawili wakaacha kumtumikia Yehova. Wenzi wa ndoa, Bob na Linda, walikabili matatizo tofauti na ya John. Wote wawili walipoteza kazi, na hawangeweza kuendelea kulipia nyumba waliyokuwa wakiishi, hivyo walihamia kwenye nyumba ndogo sana. Mbali na matatizo hayo, Linda aligunduliwa kwamba alikuwa na ugonjwa mbaya sana wa moyo unaoweza kusababisha kifo, na ugonjwa mwingine ulianza kushambulia mfumo wake wa kinga.

3. Kulingana na Wafilipi 4:6, 7, tuna uhakika gani?

3 Tuna uhakika kwamba Yehova, Muumba na Baba yetu mwenye upendo, anaelewa jinsi mikazo inavyotuathiri. Naye anataka kutusaidia tufaulu kukabiliana na matatizo yanayotupata. (Soma Wafilipi 4:6, 7.) Neno la Mungu lina masimulizi mengi yanayoeleza kuhusu matatizo ambayo watumishi wa Mungu walikabili. Pia, linaeleza jinsi Yehova alivyowasaidia wakabiliane na hali hizo zilizowasababishia mikazo. Acheni tuchunguze mifano michache.

ELIYA​—“MTU MWENYE HISIA KAMA ZETU”

4. Eliya alikabili matatizo gani, naye alihisije kumhusu Yehova?

4 Eliya alimtumikia Yehova katika kipindi kigumu sana na alikabili matatizo makubwa sana. Mfalme Ahabu, mmojawapo wa wafalme wasio waaminifu wa Israeli, alimwoa Yezebeli, mwanamke mwovu aliyeabudu Baali. Wote wawili walishirikiana kueneza ibada ya Baali katika taifa la Israeli na waliwaua manabii wengi wa Yehova. Eliya alifanikiwa kutoroka. Alifanikiwa pia kuokoka njaa kali sana iliyotokea kwa kumtegemea Yehova. (1 Fal. 17:2-4, 14-16) Zaidi ya hilo, Eliya alimtegemea Yehova alipokabiliana na manabii na waabudu wa Baali. Aliwahimiza Waisraeli wamtumikie Yehova. (1 Fal. 18:21-24, 36-38) Eliya alikuwa amejionea mambo mengi yaliyothibitisha kwamba Yehova alikuwa akimtegemeza katika nyakati hizo zenye mkazo.

Yehova alimtuma malaika ili amsaidie Eliya apate nguvu tena (Tazama fungu la 5 na 6) *

5-6. Kulingana na 1 Wafalme 19:1-4, Eliya alihisije, na Yehova alionyeshaje kwamba alimpenda Eliya?

5 Soma 1 Wafalme 19:1-4. Hata hivyo, Eliya aliogopa Malkia Yezebeli alipotishia kumuua. Hivyo alikimbilia eneo la Beer-sheba. Alivunjika moyo sana hivi kwamba “akaomba afe.” Ni nini kilichomfanya ahisi hivyo? Eliya alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu, “mtu mwenye hisia kama zetu.” (Yak. 5:17) Huenda alikuwa amelemewa na mkazo na uchovu mwingi. Inaonekana Eliya alifikiri kwamba jitihada zake za kuendeleza ibada safi zilikuwa za bure, na kwamba hali nchini Israeli haikuwa imebadilika, na kwamba yeye pekee ndiye aliyekuwa akimtumikia Yehova. (1 Fal. 18:3, 4, 13; 19:10, 14) Huenda tukashangazwa na jinsi nabii huyo mwaminifu alivyotenda. Lakini Yehova alielewa hisia za Eliya.

6 Yehova hakumkaripia Eliya kwa kueleza hisia zake. Badala yake, alimsaidia Eliya apate nguvu tena. (1 Fal. 19:5-7) Baadaye, Yehova alirekebisha fikira za Eliya kwa upole kwa kumwonyesha nguvu zake zenye kustaajabisha. Kisha Yehova akataja kwamba bado kulikuwa na watu 7,000 nchini Israeli ambao walikataa kuabudu Baali. (1 Fal. 19:11-18) Kupitia mambo halisi, Yehova alimwonyesha Eliya kwamba anampenda.

JINSI YEHOVA ATAKAVYOTUSAIDIA

7. Tunapata uhakika gani kutokana na jinsi Yehova alivyomsaidia Eliya?

7 Je, unapitia hali fulani yenye mkazo? Tunafarijika sana kujua kwamba Yehova alielewa hisia za Eliya! Jambo hilo linatuhakikishia kwamba anaelewa pia matatizo ya kihisia tunayopambana nayo. Anajua uwezo wetu, na hata anajua fikira na hisia zetu. (Zab. 103:14; 139:3, 4) Tukimwiga Eliya kwa kumtegemea Yehova, Yehova atatusaidia kukabiliana na matatizo yanayoweza kutusababishia mikazo.​—Zab. 55:22.

8. Yehova atakusaidiaje kukabiliana na mikazo?

8 Mkazo unaweza kukufanya ufikiri kwamba hali unayopitia haitawahi kubadilika, na jambo hilo linaweza kukufanya uvunjike moyo. Ukikumbwa na hali kama hiyo, kumbuka kwamba Yehova atakusaidia ukabiliane na mkazo. Atakusaidiaje? Anakualika umweleze matatizo yako na jinsi unavyohisi. Naye atajibu vilio vyako vya kuomba msaada. (Zab. 5:3; 1 Pet. 5:7) Hivyo, sali kwa Yehova mara nyingi kuhusu matatizo yako. Hatazungumza nawe moja kwa moja kama alivyofanya kwa Eliya, lakini atazungumza nawe kupitia Neno lake Biblia, na kupitia tengenezo lake. Masimulizi unayosoma katika Biblia yanaweza kukufariji na kukupa tumaini. Pia, ndugu na dada zako wanaweza kukutia moyo.​—Rom. 15:4; Ebr. 10:24, 25.

9. Rafiki wa karibu anaweza kukusaidiaje?

9 Yehova alipomwambia Eliya amgawie Elisha baadhi ya majukumu yake, alimsaidia Eliya kupata rafiki aliyethibitika kuwa msaada mkubwa sana kwake, ambaye bila shaka alimsaidia alipokuwa amevunjika moyo sana. Vivyo hivyo, tunapomweleza rafiki wa karibu kuhusu mahangaiko yetu anaweza kutusaidia kuyabeba. (2 Fal. 2:2; Met. 17:17) Ukihisi ni kana kwamba huna yeyote unayeweza kumweleza mahangaiko yako, mwombe Yehova akusaidie kupata Mkristo aliyekomaa kiroho anayeweza kukutia moyo.

10. Kisa cha Eliya kinatupatiaje tumaini, na ahadi iliyo kwenye Isaya 40:28, 29 inatusaidiaje?

10 Yehova alimsaidia Eliya kukabiliana na mkazo na aendelee kumtumikia kwa uaminifu kwa miaka mingi. Kisa cha Eliya kinatupatia tumaini. Nyakati nyingine huenda tukapitia vipindi vyenye mikazo mikali sana inayotufanya tuishiwe na nguvu kimwili na kihisia. Licha ya hilo, tukimtegemea Yehova, atatupatia nguvu tunazohitaji ili tuendelee kumtumikia.​—Soma Isaya 40:28, 29.

HANA, DAUDI, NA “ASAFU” WALIMTEGEMEA YEHOVA

11-13. Mikazo iliwaathirije watumishi watatu wa kale wa Mungu?

11 Watu wengine pia wanaotajwa katika Biblia walikabili mkazo mkubwa. Kwa mfano, Hana alivumilia aibu ya kutokuwa na watoto na dhihaka zenye kuumiza kutoka kwa mke-mwenza. (1 Sam. 1:2, 6) Hana alipatwa na mkazo mkubwa sana uliomtia uchungu mwingi sana hivi kwamba alilia na kupoteza hamu ya kula.​—1 Sam. 1:7, 10.

12 Kuna nyakati ambazo Mfalme Daudi pia alilemewa na mikazo. Fikiria kuhusu matatizo aliyokabili. Alilemewa sana na hisia za hatia kwa sababu ya makosa mengi aliyofanya. (Zab. 40:12) Mwana wake mpendwa Absalomu alimwasi, jambo lililofanya Absalomu afe. (2 Sam. 15:13, 14; 18:33) Na mmoja wa marafiki wa karibu zaidi wa Daudi alimsaliti. (2 Sam. 16:23–17:2; Zab. 55:12-14) Zaburi nyingi ambazo Daudi aliandika zinafunua hisia zake za kuvunjika moyo na vilevile jinsi alivyomtumaini Yehova bila kuyumbayumba.​—Zab. 38:5-10; 94:17-19.

Ni nini kilichomsaidia mtunga zaburi amtumikie Yehova tena akiwa na shangwe? (Tazama fungu la 13 hadi 15) *

13 Baadaye mtunga zaburi fulani alianza kuwaonea wivu watu waovu. Huenda alikuwa mmoja wa wazao wa Mlawi aliyeitwa Asafu, aliyetumikia katika “mahali patakatifu pa Mungu penye utukufu.” Mtunga zaburi huyo alipatwa na mkazo wa kihisia uliomfanya akose furaha na ashindwe kuridhika na hali yake. Hata alianza kutilia shaka baraka alizopata kwa kumtumikia Mungu.​—Zab. 73:2-5, 7, 12-14, 16, 17, 21.

14-15. Mifano mitatu ya watu wanaotajwa katika Biblia inatufundisha nini kuhusu kumtegemea Yehova ili tupate msaada?

14 Waabudu wote watatu wa kweli tuliotoka kuzungumzia walimtegemea Yehova ili awasaidie. Walisali kwake kwa bidii wakimweleza kuhusu mahangaiko yao. Walizungumza naye kwa uhuru wakimweleza sababu zilizowafanya wawe na mkazo mkubwa. Na waliendelea kwenda katika mahali pa Yehova pa ibada.​—1 Sam. 1:9, 10; Zab. 55:22; 73:17; 122:1.

15 Kwa huruma, Yehova alimjibu kila mmoja wao. Hana alipata amani ya akili. (1 Sam. 1:18) Daudi aliandika hivi: “Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.” (Zab. 34:19) Na baadaye mtunga zaburi alihisi kwamba Yehova alikuwa ‘ameushika mkono wake wa kulia,’ akimwongoza kwa kumpa ushauri wenye upendo. Aliimba hivi: “Kwa upande wangu, kumkaribia Mungu ni jambo jema kwangu. Nimemfanya Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova kuwa kimbilio langu.” (Zab. 73:23, 24, 28) Mifano hiyo inatufundisha nini? Kuna nyakati ambazo tutalemewa na matatizo yatakayotuletea mkazo. Lakini tunaweza kukabiliana na mkazo huo ikiwa tutatafakari jinsi Yehova alivyowasaidia wengine, ikiwa tutamtegemea katika sala, na kumtii kwa kufanya mambo anayotuambia tufanye.​—Zab. 143:1, 4-8.

MTEGEMEE YEHOVA UFANIKIWE

Mwanzoni, dada mmoja alitaka kujitenga na watu, lakini hali ilibadilika alipotafuta njia za kuwasaidia wengine (Tazama fungu la 16 na 17)

16-17. (a) Kwa nini hatupaswi kujitenga na Yehova na watumishi wake? (b) Tunaweza kupataje nguvu tena?

16 Mifano hiyo mitatu inatufundisha somo lingine muhimu​—hatupaswi kujitenga na Yehova na watu wake. (Met. 18:1) Nancy, dada ambaye alikabili mkazo mkubwa sana mume wake alipomwacha, anasema hivi: “Kulikuwa na siku nyingi ambazo sikutaka kumwona mtu au kuzungumza na yeyote. Lakini kadiri nilivyojitenga na watu, ndivyo nilivyozidi kuhuzunika.” Hali ilibadilika Nancy alipotafuta njia za kuwasaidia wengine waliokuwa wakikabili matatizo. Anasema hivi: “Niliwasikiliza wengine walipoeleza mahangaiko yao. Niligundua kwamba kadiri nilivyozidi kuwaonyesha huruma, ndivyo nilivyoacha kujisikitikia.”

17 Tunaweza kupata nguvu tena kwa kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Tunapokuwa mikutanoni, tunampa Yehova fursa zaidi za kuwa ‘msaidizi na mfariji’ wetu. (Zab. 86:17) Katika mikutano, Yehova hutufariji kupitia roho yake takatifu, Neno lake, na watu wake. Mikutano hutupatia nafasi za kufurahia fursa za ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12) Dada anayeitwa Sophia alisema hivi: “Yehova pamoja na ushirika wa ndugu zetu ulinisaidia kuvumilia. Jambo muhimu kwangu lilikuwa mikutano yetu ya kutaniko. Nimetambua kwamba kadiri ninavyojihusisha kabisa na huduma na kutaniko langu, ndivyo ninavyofanikiwa kukabiliana na mikazo na mahangaiko.”

18. Tunapovunjika moyo, Yehova anaweza kutupatia nini?

18 Tunapovunjika moyo, acheni tukumbuke kwamba Yehova hajatuahidi tu kitulizo cha kudumu wakati ujao, bali pia yuko tayari kutusaidia kukabiliana na mikazo hata sasa. Yeye hutupatia “hamu na nguvu za kutenda” ili tushinde hisia za kuvunjika moyo na kukosa tumaini.​—Flp. 2:13.

19. Andiko la Waroma 8:37-39 linatupatia ahadi gani?

19 Soma Waroma 8:37-39. Mtume Paulo anatuhakikishia kwamba hakuna kitu chochote kinachoweza kututenganisha na upendo wa Mungu. Tunaweza kuwasaidiaje ndugu na dada zetu wanaokabiliana na mikazo? Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi tunavyoweza kumwiga Yehova kwa kuwaonyesha huruma ndugu na dada zetu na kuwategemeza wanapopatwa na mikazo.

WIMBO 44 Sala ya Mtu wa Hali ya Chini

^ fu. 5 Mkazo mwingi kupita kiasi au unaodumu kwa muda mrefu unaweza kutuletea madhara ya kimwili na ya kihisia. Yehova anaweza kutusaidiaje? Tutachunguza jinsi Yehova alivyomsaidia Eliya kukabiliana na mkazo. Vilevile tutaona mifano mingine ya Biblia itakayotusaidia kujua jinsi ya kumtegemea Yehova tunapopatwa na mkazo.

^ fu. 2 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 53 MAELEZO YA PICHA: Malaika wa Yehova anamwamsha Eliya kwa wororo kutoka usingizini na kumpa mkate na maji.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: Mtunga zaburi ambaye huenda alikuwa mzao wa Asafu anafurahia kuandika na kuimba zaburi akiwa pamoja na Walawi wenzake.