Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jilinde Usinaswe na Mtego Huu wa Shetani

Jilinde Usinaswe na Mtego Huu wa Shetani

WAISRAELI wa kale walipokuwa wakijitayarisha kuvuka Mto Yordani ili waingie katika nchi ambayo Mungu alikuwa amewaahidi, wageni fulani waliwatembelea. Wageni hao walikuwa wanawake wa kigeni waliowaalika wanaume Waisraeli kwa ajili ya sherehe. Ilionekana kuwa fursa ya pekee sana. Kupata marafiki wapya, kucheza dansi, kula chakula kizuri yalikuwa mambo yenye kuvutia sana. Ingawa desturi na maadili ya wanawake hao hayakupatana na Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli, huenda baadhi ya wanaume hao walifikiri hivi: ‘Hatuwezi kuathiriwa. Tutakuwa waangalifu.’

Ikawaje? Simulizi hilo lililoongozwa na roho takatifu linasema hivi: “Watu walianza kufanya uasherati na mabinti wa Moabu.” Ukweli wa mambo ni kwamba wanawake hao walitaka wanaume Waisraeli waabudu miungu ya uwongo. Na ndivyo walivyofanya! Na kwa sababu hiyo, “hasira ya Yehova ikawaka dhidi yao.”​—Hes. 25:1-3.

Waisraeli hao walivunja Sheria ya Mungu katika njia mbili: Waliinamia sanamu, na walifanya uasherati. Maelfu ya watu walikufa kwa sababu ya kutotii. (Kut. 20:4, 5, 14; Kum. 13:6-9) Ni nini kilichofanya msiba huo uwe wenye kuhuzunisha hata zaidi? Ni wakati ulipotokea. Ikiwa wanaume hao hawangevunja Sheria ya Mungu, baada ya muda mfupi maelfu ya Waisraeli hao wangevuka Mto Yordani na kuingia katika Nchi ya Ahadi.​—Hes. 25:5, 9.

Akizungumza kuhusu mambo hayo mtume Paulo aliandika hivi: “Mambo hayo yaliwapata ili kuwa vielelezo, nayo yaliandikwa ili kuwa onyo kwetu sisi ambao tumefikiwa na miisho ya mifumo ya mambo.” (1 Kor. 10:7-11) Bila shaka Shetani alifurahi sana kwamba baadhi ya Waisraeli walitumbukia katika dhambi nzito na kwa sababu hiyo hawakustahili kuingia katika Nchi ya Ahadi. Ni jambo la hekima sana kwetu kuzingatia moyoni onyo hilo, tukijua kwamba hakuna jambo linaloweza kumfurahisha Shetani zaidi kuliko kutuzuia kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu!

MTEGO HATARI

Shetani huwawinda Wakristo akitumia mbinu ambazo anazijua vizuri na ambazo ametumia kwa mafanikio kuwanasa watu wengi. Kama ilivyotajwa awali, alitumia mbinu ya uasherati kuwanasa Waisraeli. Katika siku zetu, bado uasherati ndio mtego hatari sana anaotumia. Njia moja yenye nguvu anayotumia kutunasa ni kupitia ponografia.

Leo, watu wanaweza kutazama ponografia bila kujulikana. Miaka mingi iliyopita, ikiwa mtu alitaka kutazama ponografia alilazimika kwenda kwenye kumbi za sinema ili kutazama sinema chafu au kutembelea duka lililouza vitabu vya ponografia. Inaelekea kwamba watu wengi hawakutembelea maeneo hayo kwa sababu waliaibika ikiwa wangeonekana humo au karibu na maeneo hayo. Lakini sasa, mtu yeyote anayeweza kupata Intaneti anaweza kutazama ponografia akiwa kazini au hata ndani ya gari lililoegeshwa. Na katika nchi nyingi, mwanamume au mwanamke anaweza kutazama ponografia hata akiwa nyumbani kwake.

Na si hivyo tu. Vifaa vya mkononi vimefanya iwe rahisi hata zaidi kutazama ponografia. Watu wanapotembea barabarani au wakiwa ndani ya mabasi au treni, wanaweza kutazama picha chafu kwenye vifaa vyao vya mkononi.

Kwa kuwa ni rahisi zaidi kutazama ponografia na kuficha jambo hilo, ponografia husababisha madhara makubwa zaidi leo kuliko ilivyokuwa zamani. Watu wengi sana wanaotazama ponografia wameharibu ndoa zao, wamekosa kujiheshimu, na wameharibu dhamiri zao. Na jambo baya hata zaidi, wanahatarisha urafiki wao pamoja na Mungu. Ukweli wa mambo ni kwamba ponografia huwadhuru wale wanaoitazama. Katika visa vingi, ponografia husababisha majeraha makubwa ya kihisia. Huenda majeraha hayo yakapona taratibu lakini huacha makovu yanayoweza kudumu kwa muda mrefu sana.

Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba Yehova anaandaa ulinzi dhidi ya mtego huo wa Shetani. Ikiwa tunataka kupata ulinzi wa Yehova, ni lazima tufanye jambo ambalo wanaume wa kale wa Israeli walishindwa kufanya​—ni lazima ‘tumtii Yehova kabisa.’ (Kut. 19:5) Tunahitaji kutambua kwamba Yehova anachukizwa sana na ponografia. Kwa nini tunasema hivyo?

ICHUKIE KAMA YEHOVA ANAVYOICHUKIA

Fikiria jambo hili: Sheria za Mungu kwa taifa la Israeli zilitofautiana kabisa na sheria za mataifa mengine ya wakati huo. Kama ukuta, sheria hizo ziliwasaidia Waisraeli wajitenge na mataifa yaliyowazunguka na mazoea yao machafu. (Kum. 4:6-8) Sheria hizo zilifunua wazi ukweli huu muhimu: Yehova anachukizwa na uasherati.

Alipokuwa akiorodhesha mambo yaliyopotoka ambayo mataifa jirani yalifanya, Yehova aliwaambia hivi Waisraeli: “Msifanye kama wanavyofanya katika nchi ya Kanaani ambako nawapeleka. . . . Nchi si safi, nami nitaiadhibu kwa sababu ya dhambi yake.” Machoni pa Mungu mtakatifu wa Israeli, mtindo wa maisha wa Wakanaani ulikuwa wenye kuchukiza sana hivi kwamba nchi waliyoishi ilikuwa si safi, yaani, ilikuwa imechafuliwa.​—Law. 18:3, 25.

Ingawa Yehova aliwaadhibu Wakanaani, mataifa mengine yaliendelea kufanya uasherati. Zaidi ya miaka 1,500 hivi baadaye, Paulo alisema kwamba watu wa mataifa walioishi miongoni mwa Wakristo walikuwa “wamepotoka kabisa kimaadili.” Ukweli ni kwamba walikuwa “wamejiingiza katika mwenendo mpotovu na kufanya mambo machafu ya kila namna kwa pupa.” (Efe. 4:17-19) Leo pia, watu wengi sana wamepotoka sana kimaadili na hawaoni aibu. Ni lazima waabudu wa kweli, wajitahidi kadiri wawezavyo kuepuka kutazama mambo machafu kiadili yanayofanywa na watu wa ulimwengu huu.

Ponografia ni jambo linalomvunjia Mungu heshima sana. Mungu aliwaumba wanadamu kwa mfano na sura yake na alitupatia uwezo wa kutambua mambo yanayofaa na yasiyofaa. Kwa hekima, Mungu aliweka mipaka inayofaa kuhusu ngono. Ngono ilikusudiwa kutimiza jukumu lenye kuheshimika na lenye kufurahisha ndani ya ndoa. (Mwa. 1:26-28; Met. 5:18, 19) Lakini wale wanaotengeneza au kueneza ponografia wanafanya nini? Wanapuuza na kudharau kabisa viwango vya Mungu vya maadili. Ndiyo, watu wanaoeneza ponografia wanamvunjia heshima Yehova. Mungu atawahukumu wale wanaopuuza viwango vyake kwa kutengeneza au kueneza mambo machafu kingono.​—Rom. 1:24-27.

Lakini vipi kuhusu watu wanaosoma au kutazama ponografia kimakusudi? Huenda wengine wakahisi kwamba ponografia ni burudani isiyo na madhara. Hata hivyo, uhalisi wa mambo ni kwamba wanawaunga mkono wale wanaopuuza viwango vya Yehova. Huenda hilo halikuwa kusudi lao walipoanza kutazama ponografia. Licha ya hilo, ni wazi kwamba waabudu wa Mungu wa kweli wanapaswa kuchukia vikali ponografia. Biblia inatuhimiza hivi: “Enyi mnaompenda Yehova, chukieni maovu.”​—Zab. 97:10.

Inaweza kuwa vigumu kuchukia maovu hata kwa wale ambao hawataki kutazama ponografia. Sisi si wakamilifu, na huenda tukalazimika kupambana ili tupinge tamaa chafu za kingono. Isitoshe moyo wetu usio mkamilifu unaweza kutafuta kisingizio cha kupuuza sheria ya Mungu. (Yer. 17:9) Lakini watu wengi ambao sasa ni Wakristo wameshinda pambano hilo. Kujua hilo kunaweza kukutia moyo ikiwa wewe pia unapambana na jambo hilo. Ona jinsi Neno la Mungu linavyoweza kukusaidia kuepuka mtego wa Shetani wa kutazama ponografia.

USIENDELEE KUFIKIRIA MAMBO MACHAFU

Kama tulivyoona awali, Waisraeli wengi waliruhusu tamaa zisizofaa ziwaongoze kwenye msiba. Jambo kama hilo linaweza kutupata leo. Yakobo, ndugu nusu ya Yesu anafafanua hivi hatari hiyo: “Kila mtu . . . [huvutwa] na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi.” (Yak. 1:14, 15) Mara tu tamaa iliyopotoka inapositawi moyoni mwa mtu na kufikia hatua fulani, kuna uwezekano mkubwa mtu huyo atafanya dhambi. Hivyo ni lazima tuondoe kabisa akilini mwetu mawazo machafu kingono, si kuendelea kuyafikiria.

Ikiwa unashawishiwa na mawazo machafu, chukua hatua mara moja. Yesu alisema hivi: “Basi, ikiwa mkono wako au mguu wako unakufanya ukwazike, ukate na kuutupa mbali nawe. . . . Pia, ikiwa jicho lako linakufanya ukwazike, ling’oe na kulitupa mbali nawe.” (Mt. 18:8, 9) Yesu hakumaanisha tukate sehemu fulani ya mwili wetu kihalisi. Alikuwa akitoa mfano unaoonyesha umuhimu wa kuondoa haraka na bila kukawia, chanzo kinachosababisha tukwazike. Tunaweza kutumiaje shauri hilo kuhusiana na ponografia?

Ukikumbana na ponografia, usijiambie, ‘Siwezi kuathiriwa.’ Tazama upande mwingine mara moja. Zima televisheni haraka. Zima kompyuta au kifaa cha mkononi papo hapo. Fikiria jambo lingine ambalo ni safi. Kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kudhibiti mawazo yako badala ya kuruhusu tamaa mbaya zikuongoze.

VIPI KUHUSU KUMBUKUMBU ZA BURUDANI CHAFU?

Vipi ikiwa umefanikiwa kuacha kutazama ponografia, lakini mara kwa mara unakumbuka mambo uliyotazama zamani? Picha au mawazo kuhusu ponografia yanaweza kubaki akilini mwa mtu kwa muda mrefu. Mambo hayo yanaweza kutujia akilini bila kutarajia. Hilo likitukia, huenda ukatamani kufanya jambo fulani lisilo safi, kama vile kupiga punyeto. Hivyo, tambua kwamba mawazo kama hayo yanaweza kuja akilini ghafla, na uwe tayari kupambana nayo ili uyashinde.

Imarisha azimio lako la kupatanisha mawazo na matendo yako na mapenzi ya Mungu. Uwe kama mtume Paulo ambaye alikuwa tayari ‘kuupigapiga mwili wake na kuuongoza kama mtumwa.’ (1 Kor. 9:27) Usiruhusu tamaa chafu zikufanye uwe mtumwa. ‘Geuzwa kwa kufanya upya akili yako, ili ujihakikishie mwenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.’ (Rom. 12:2) Kumbuka: Kufikiria na kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu ni mambo yatakayokuletea furaha kuliko kutii mielekeo yako yenye dhambi.

Kufikiria na kutenda kulingana na mapenzi ya Mungu ni mambo yatakayokuletea furaha kuliko kutii mielekeo yako yenye dhambi

Jitahidi kukariri mistari fulani ya Biblia. Kisha mawazo yasiyofaa yanapokujia akilini, jilazimishe kufikiria mistari hiyo. Maandiko kama vile Zaburi 119:37; Isaya 52:11; Mathayo 5:28; Waefeso 5:3; Wakolosai 3:5; na 1 Wathesalonike 4:4-8 yatakusaidia kupatanisha njia yako ya kufikiri na maoni ya Yehova kuhusu ponografia na mambo ambayo Yehova anatazamia kutoka kwako.

Vipi ikiwa pindi fulani unahisi kwamba umeshindwa kabisa kujizuia kutazama au kufikiria mambo machafu? Fuata kwa ukaribu hatua za Kielelezo chetu, Yesu. (1 Pet. 2:21) Baada ya Yesu kubatizwa, Shetani alimshawishi tena na tena. Yesu alifanya nini? Alimpinga tena na tena. Akitumia andiko moja baada ya lingine, Yesu alipinga vishawishi ambavyo Shetani alimletea. Alisema: “Nenda zako, Shetani!” na Shetani alimwacha. Kama tu ambavyo Yesu hakuchoka kupambana na Ibilisi, wewe pia hupaswi kuchoka. (Mt. 4:1-11) Shetani na ulimwengu wake utaendelea kujaribu kujaza akili yetu mawazo machafu, lakini usikubali kushindwa katika pambano hilo. Unaweza kushinda vita dhidi ya ponografia. Kwa msaada wa Yehova, unaweza kumshinda adui yako.

SALI KWA YEHOVA NA UMTII

Mtegemee Yehova kabisa kupitia sala. Paulo alisema hivi: “Mjulisheni Mungu maombi yenu; na amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kupitia Kristo Yesu.” (Flp. 4:6, 7) Amani ya Mungu hutuletea kitulizo tunapoendelea kupambana na dhambi. Ukimkaribia Yehova, ‘atakukaribia wewe.’​—Yak. 4:8.

Ulinzi bora zaidi unaoweza kupata dhidi ya hatari yoyote ile ni kumkaribia Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu. Yesu alisema: “Mtawala wa ulimwengu [Shetani] anakuja, naye hana uwezo juu yangu.” (Yoh. 14:30) Kwa nini Yesu alikuwa na uhakika huo? Alieleza hivi pindi fulani: “Yule aliyenituma yuko pamoja nami; naye hakuniacha peke yangu, kwa sababu sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza.” (Yoh. 8:29) Ukiendelea kufanya mambo yanayompendeza Yehova, uwe na hakika kwamba Yehova hatakuacha pia. Epuka mtego wa ponografia, na Shetani hatakuwa na uwezo wowote juu yako.