Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 27

Jitayarishe Sasa kwa Ajili ya Mateso

Jitayarishe Sasa kwa Ajili ya Mateso

“Wote wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watateswa pia.”​—2 TIM. 3:12.

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

MUHTASARI *

1. Kwa nini tunahitaji kujitayarisha kwa ajili ya mateso?

KATIKA usiku ambao Bwana wetu Yesu aliuawa, alisema kwamba wote ambao wangechagua kuwa wanafunzi wake watachukiwa. (Yoh. 17:14) Tangu wakati huo hadi leo, Mashahidi Wakristo waaminifu wa Yehova wamekuwa wakiteswa na watu wanaopinga ibada safi. (2 Tim. 3:12) Kadiri mwisho wa mfumo huu wa mambo unavyozidi kukaribia, tunatarajia kwamba maadui wetu watazidi kutupinga zaidi na zaidi.​—Mt. 24:9.

2-3. (a) Tunapaswa kutambua nini kuhusu woga? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Tunaweza kujitayarishaje sasa kwa ajili ya mateso? Hatuhitaji kuwazia kuhusu mambo yote mabaya yanayoweza kutupata. Ikiwa tungefanya hivyo, tungelemewa na woga na mahangaiko. Tungekuwa tunaruhusu mambo mabaya ya kuwaziwa yatulemee hata kabla ya kukabili majaribu halisi. (Met. 12:25; 17:22) Woga ni silaha yenye nguvu sana ambayo ‘adui yetu Ibilisi’ hujitahidi kutumia ili kutushambulia. (1 Pet. 5:8, 9) Tunaweza kufanya nini sasa ili kujiimarisha?

3 Katika makala hii, tutachunguza jinsi tunavyoweza kuimarisha urafiki wetu pamoja na Yehova na kwa nini ni muhimu kufanya hivyo sasa. Pia, tutazungumzia mambo tunayoweza kufanya ili tuwe jasiri zaidi. Na mwishowe, tutachunguza jinsi tunavyoweza kukabiliana na chuki kutoka kwa wapinzani wetu.

JINSI YA KUIMARISHA URAFIKI WAKO PAMOJA NA YEHOVA

4. Kulingana na Waebrania 13:5, 6, ni lazima tusadiki nini, na kwa nini?

4 Sadiki kwamba Yehova anakupenda na hatakuacha kamwe. (Soma Waebrania 13:5, 6.) Miaka mingi iliyopita, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilieleza hivi: “Mtu anayemjua Mungu vizuri sana atamtumaini zaidi wakati wa jaribu.” Huo ni ukweli mtupu! Ili tukabiliane kwa mafanikio na mateso, ni lazima tumpende Yehova na kumtumaini kikamili na tusitilie shaka kamwe kwamba anatupenda.​—Mt. 22:36-38; Yak. 5:11.

5. Ni nini kitakachokusaidia uhisi upendo wa Yehova?

5 Soma Biblia kila siku ukiwa na lengo la kumkaribia Yehova zaidi. (Yak. 4:8) Unapoisoma, kazia fikira sifa zinazoonyesha wororo wa Yehova. Jitahidi kuhisi upendo na hisia zake nyororo zinazoonyeshwa kupitia mambo anayosema na kutenda. (Kut. 34:6) Baadhi ya watu huona kuwa vigumu kuamini kwamba Mungu anawapenda kwa sababu hawajawahi kupendwa. Ikiwa unahisi hivyo, jitahidi kuorodhesha kila siku mambo yanayoonyesha jinsi Yehova anavyokutendea kwa rehema na fadhili. (Zab. 78:38, 39; Rom. 8:32) Unapofikiria kuhusu mambo aliyokutendea na kutafakari kuhusu yale unayosoma katika Neno la Mungu, inaelekea utaorodhesha mambo mengi sana ambayo Yehova amekutendea. Kadiri unavyozidi kuthamini mambo ambayo Yehova amekutendea, ndivyo urafiki wako pamoja naye utakavyozidi kuimarika.​—Zab. 116:1, 2.

6. Kulingana na Zaburi 94:17-19, sala za kutoka moyoni zinaweza kukusaidiaje?

6 Sali kwa ukawaida. Wazia mvulana mdogo aliyekumbatiwa kwa upendo na baba yake. Mvulana huyo anahisi akiwa salama sana hivi kwamba anazungumza na baba yake kwa uhuru kuhusu mambo mazuri na mabaya yaliyompata siku hiyo. Unaweza kufurahia urafiki wa aina hiyo pamoja na Yehova ikiwa utamkaribia kwa sala za kutoka moyoni kila siku. (Soma Zaburi 94:17-19.) Unaposali kwa Yehova, “umwage moyo wako kama maji” mbele zake na umwambie Baba yako anayekupenda kuhusu woga na mahangaiko yako yote. (Omb. 2:19) Ni nini kitakachotendeka? Utajionea kile ambacho Biblia inaita “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.” (Flp. 4:6, 7) Kadiri unavyozidi kusali kwa njia hiyo, ndivyo utakavyohisi ukiwa karibu zaidi na Yehova.​—Rom. 8:38, 39.

Tunapata ujasiri tunapokuwa na imani katika Yehova na Ufalme wake

Stanley Jones alijiimarisha kwa ujuzi thabiti kuhusu Ufalme wa Mungu (Tazama fungu la 7)

7. Kwa nini ni lazima usadiki kwamba ahadi ambazo Mungu anatoa kuhusu Ufalme wake zitatimia?

7 Sadiki kwamba baraka za Ufalme wa Mungu zitatimia. (Hes. 23:19) Ikiwa imani yako kuhusu ahadi hizo ni dhaifu, itakuwa rahisi kwa Shetani na mawakala wake kukuogopesha. (Met. 24:10; Ebr. 2:15) Unaweza kuimarishaje sasa imani yako katika Ufalme wa Mungu? Weka mradi wa kujifunza kuhusu ahadi za Mungu za Ufalme wake na uchunguze sababu zinazokusadikisha kwamba zitatimia. Utanufaikaje kwa kufanya hivyo? Fikiria mfano wa Stanley Jones, ambaye alifungwa gerezani kwa miaka saba kwa sababu ya imani yake. * Ni nini kilichomsaidia avumilie kwa uaminifu? Alisema hivi: “Singeweza kuyumbishwa kamwe kwa sababu nilikuwa nimeimarishwa na ujuzi kuhusu Ufalme wa Mungu, nilisadiki kabisa mambo ambayo ungetimiza, na sikuwa na shaka yoyote kuuhusu.” Ukiwa na imani yenye nguvu kuhusu ahadi za Mungu, utamkaribia Yehova zaidi, na hutashindwa na woga.​—Met. 3:25, 26.

8. Mtazamo wetu kuhusu uhudhuriaji wa mikutano ni kipimo kizuri cha nini? Eleza.

8 Hudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Mikutano hutusaidia kumkaribia Yehova zaidi. Mtazamo wetu kuhusu uhudhuriaji wa mikutano ni kipimo kizuri kinachoweza kutusaidia kujua ikiwa tutafanikiwa kukabiliana na mateso wakati ujao au la. (Ebr. 10:24, 25) Kwa nini? Ikiwa tunaruhusu mambo madogo yatuzuie kuhudhuria mikutano sasa, itakuwaje wakati ujao tutakapolazimika kuhatarisha usalama wetu ili kukutana na waamini wenzetu? Kwa upande mwingine, ikiwa tumeazimia kwa uthabiti kuhudhuria mikutano, hatutaacha kukutana pamoja hata wapinzani wakijaribu kutuzuia kufanya hivyo. Sasa ndio wakati wa kujifunza kuipenda mikutano yetu. Tukijifunza kuipenda mikutano yetu, hakuna upinzani wowote, au hata marufuku ya serikali itakayoweza kutufanya tuwatii wanadamu badala ya kumtii Mungu.​—Mdo. 5:29.

Kukariri sasa maandiko na nyimbo za Ufalme ni jambo linaloweza kukusaidia wakati wa mateso (Tazama fungu la 9) *

9. Kwa nini kukariri maandiko ni njia nzuri ya kujitayarisha kwa ajili ya mateso?

9 Kariri maandiko unayopenda. (Mt. 13:52) Huenda usiwe na kumbukumbu nzuri sana, lakini Yehova anaweza kutumia roho yake takatifu yenye nguvu kukusaidia kuyakumbuka maandiko hayo. (Yoh. 14:26) Ndugu mmoja aliyefungwa gerezani katika kifungo cha upweke huko Ujerumani Mashariki, alisema hivi: “Ilikuwa baraka kubwa kwamba kufikia wakati huo, nilikuwa nimekariri mamia kadhaa ya maandiko! Nilitumia kipindi hicho cha upweke kutafakari kuhusu habari mbalimbali za Biblia.” Maandiko hayo yalimsaidia ndugu yetu kubaki karibu na Yehova, na kuvumilia kwa uaminifu.

(Tazama fungu la 10) *

10. Kwa nini tunapaswa kukariri nyimbo zetu?

10 Kariri na uimbe nyimbo zinazomsifu Yehova. Walipokuwa wamefungwa gerezani huko Filipi, Paulo na Sila waliimba nyimbo za kiroho ambazo walikuwa wamekariri. (Mdo. 16:25) Vivyo hivyo, ndugu zetu walioishi katika nchi zilizokuwa katika Muungano wa Sovieti walijiimarishaje walipopelekwa uhamishoni Siberia? Dada Mariya Fedun alieleza hivi: “Tuliimba nyimbo zote tulizojua katika kitabu chetu cha nyimbo.” Alisema kwamba nyimbo hizo ziliwatia moyo ndugu wote na kuwasaidia wahisi wakiwa karibu zaidi na Yehova. Je, wewe hutiwa nguvu unapoimba nyimbo za kiroho unazopenda? Basi, zikariri sasa nyimbo hizo!​—Tazama sanduku “ Nipe Ujasiri.”

JINSI YA KUWA JASIRI ZAIDI

11-12. (a) Kulingana na 1 Samweli 17:37, 45-47, kwa nini Daudi alikuwa na ujasiri? (b) Mfano wa Daudi unatufundisha somo gani muhimu?

11 Ili ukabiliane na mateso, unahitaji ujasiri. Ikiwa unahisi kwamba huna ujasiri, unaweza kufanya nini? Kumbuka kwamba ujasiri wa kweli hautegemei umbo, nguvu, au uwezo ulio nao. Fikiria mfano wa kijana Daudi alipokabiliana na Goliathi. Kwa kulinganishwa na jitu hilo, Daudi alikuwa mdogo na dhaifu sana, na silaha zake zilikuwa duni. Hakuwa hata na upanga. Licha ya hilo, alikuwa na ujasiri mwingi. Kwa ujasiri, Daudi alikimbia haraka kulielekea jitu hilo lenye kiburi ili kupigana nalo.

12 Kwa nini Daudi alikuwa na ujasiri mwingi hivyo? Aliamini kabisa kwamba Yehova alikuwa pamoja naye. (Soma 1 Samweli 17:37, 45-47.) Daudi hakukazia fikira jinsi Goliathi alivyokuwa na umbo kubwa kwa kulinganishwa naye. Badala yake, alikazia fikira jinsi Goliathi alivyokuwa mdogo sana akilinganishwa na Yehova. Simulizi hilo linatufundisha nini? Tutakuwa jasiri ikiwa tuna uhakika kwamba Yehova yuko pamoja nasi na ikiwa tuna uhakika kwamba wapinzani wetu ni wadogo sana kwa kulinganishwa na Mungu Mweza-Yote. (2 Nya. 20:15; Zab. 16:8) Tunaweza kuimarishaje ujasiri wetu sasa, kabla ya kupatwa na mateso?

13. Tunaweza kuimarishaje ujasiri wetu? Eleza.

13 Tunaweza kuimarisha ujasiri wetu sasa kwa kuhubiri hadharani habari njema ya Ufalme wa Mungu. Kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu kuhubiri hutufundisha kumtumaini Yehova na kushinda woga wowote wa wanadamu. (Met. 29:25) Kama tu ambavyo misuli yetu huimarika tunapofanya mazoezi, ndivyo pia ujasiri wetu huimarika tunapohubiri isivyo rasmi, nyumba kwa nyumba, maeneo ya umma, na katika maeneo ya biashara. Tukisitawisha ujasiri wa kuhubiri sasa, tutakuwa tayari kuendelea kuhubiri hata kazi yetu ikipigwa marufuku.​—1 The. 2:1, 2.

Nancy Yuen alikataa kuacha kuhubiri habari njema (Tazama fungu la 14)

14-15. Tunajifunza nini kutoka kwa Nancy Yuen na Valentina Garnovskaya?

14 Tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa dada wawili waaminifu walioonyesha ujasiri wa pekee. Nancy Yuen alikuwa na urefu usiozidi mita moja na nusu hivi, lakini hakuogopeshwa kwa urahisi. * Alikataa kuacha kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. Matokeo ni kwamba alifungwa kwa takriban miaka 20 huko China wakati wa utawala wa Kikomunisti. Maofisa waliomhoji walisema kwamba alikuwa “ndiye mtu msumbufu zaidi” nchini!

Valentina Garnovskaya alisadiki kwamba Yehova alikuwa pamoja naye (Tazama fungu la 15)

15 Pia, Valentina Garnovskaya alifungwa katika pindi tatu tofauti-tofauti kwa jumla ya takriban miaka 21 chini ya ule uliokuwa Muungano wa Sovieti. * Kwa nini? Alikuwa ameazimia kabisa kuendelea kuhubiri hivi kwamba maofisa walimwita “mhalifu hatari sana.” Ni nini kilichofanya wanawake hao waaminifu wawe na ujasiri mwingi hivyo? Walikuwa wamesadiki kabisa kwamba Yehova alikuwa pamoja nao.

16. Siri ya ujasiri wa kweli ni nini?

16 Kama tulivyojifunza, ili tuimarishe ujasiri wetu hatupaswi kukazia fikira nguvu tulizo nazo au uwezo wetu. Badala yake, tunapaswa kuamini kwamba Yehova yuko pamoja nasi na ndiye anayetupigania. (Kum. 1:29, 30; Zek. 4:6) Hiyo ndiyo siri ya ujasiri wa kweli.

UNAWEZA KUFANYA NINI UNAPOCHUKIWA NA WATU?

17-18. Kama inavyotajwa kwenye Yohana 15:18-21, Yesu alitupatia onyo gani? Eleza.

17 Sisi hufurahi wengine wanapotuheshimu, lakini hatupaswi kukosea kwa kufikiri kwamba thamani yetu hutegemea jinsi wengine wanavyotutendea. Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni ninyi watu wanapowachukia, wanapowatenga, wanapowashutumu, na kuwachafulia jina kwa ajili ya Mwana wa binadamu.” (Luka 6:22) Yesu alimaanisha nini?

18 Yesu hakuwa akimaanisha kwamba Wakristo wangefurahia kuchukiwa. Badala yake, alikuwa akitaja tu ukweli wa mambo. Sisi si sehemu ya ulimwengu. Tunaishi kulingana na mafundisho ya Yesu na kuhubiri ujumbe ambao alihubiri. Kwa sababu hiyo, ulimwengu unatuchukia. (Soma Yohana 15:18-21.) Tunataka kumfurahisha Yehova. Wanadamu wakituchukia kwa sababu tunampenda Baba yetu, hiyo ni shauri yao.

19. Tunaweza kuiga mfano wa mitume jinsi gani?

19 Usiruhusu kamwe jambo lolote ambalo wanadamu wanasema au kutenda likufanye uaibikie kuitwa Shahidi wa Yehova. (Mika. 4:5) Tunaweza kujifunza jinsi ya kushinda woga wa wanadamu kwa kuchunguza mfano ambao mitume huko Yerusalemu walituwekea muda mfupi baada ya Yesu kuuawa. Walijua vizuri jinsi walivyochukiwa na viongozi wa kidini wa Kiyahudi. (Mdo. 5:17, 18, 27, 28) Licha ya hilo, walienda hekaluni kila siku na kujitambulisha waziwazi kwamba wao ni wanafunzi wa Yesu. (Mdo. 5:42) Hawakuruhusu woga uwalemee. Sisi pia tunaweza kushinda woga wa wanadamu kwa kujitambulisha hadharani na kwa ukawaida kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova, iwe ni kazini, shuleni, au katika ujirani.​—Mdo. 4:29; Rom. 1:16.

20. Kwa nini mitume walikuwa na furaha licha ya kwamba walichukiwa?

20 Kwa nini mitume walikuwa na furaha? Walijua kwa nini walichukiwa, na waliliona kuwa jambo la heshima watu walipowatesa kwa sababu ya kufanya mapenzi ya Yehova. (Luka 6:23; Mdo. 5:41) Baadaye mtume Petro aliandika hivi: “Hata mkiteseka kwa ajili ya uadilifu, ninyi ni wenye furaha.” (1 Pet. 2:19-21; 3:14) Tunapotambua kwamba tunachukiwa kwa kufanya yaliyo sawa, hatutaruhusu kamwe chuki kutoka kwa wanadamu itufanye tuingiwe na woga na kuacha kumtumikia Yehova.

UTANUFAIKA UKIJITAYARISHA

21-22. (a) Umeamua kufanya nini ili kujitayarisha kwa ajili ya mateso? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

21 Hatujui ni lini wimbi la mateso au marufuku yatakapoathiri ibada yetu kwa Yehova. Hata hivyo, tunajua kwamba tunaweza kujitayarisha sasa kwa kuimarisha uhusiano wetu na Yehova, kwa kuimarisha ujasiri wetu, na kwa kujifunza jinsi ya kukabiliana na chuki kutoka kwa wanadamu. Matayarisho tunayofanya sasa yatatusaidia tusimame imara wakati ujao.

22 Lakini vipi ikiwa ibada yetu inapigwa marufuku? Katika makala inayofuata, tutazungumzia kanuni zitakazotusaidia kuendelea kumtumikia Yehova hata chini ya marufuku.

WIMBO 118 “Tupe Imani Zaidi”

^ fu. 5 Hatupendi kuchukiwa. Lakini wakati utafika, iwe ni karibuni au baadaye, ambapo kila mmoja wetu atalazimika kukabiliana na mateso. Makala hii itatusaidia kukabiliana na mateso kwa ujasiri.

^ fu. 7 Tazama gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1965, uku. 756-767, la Kiingereza.

^ fu. 14 Tazama gazeti Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 1979, uku. 4-7 la Kiingereza. Tazama pia video Jina la Yehova Litatangazwa kwenye JW Broadcasting®. Tafuta kwenye MAHOJIANO NA MAMBO YALIYOONWA.

^ fu. 15 Tazama Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2008, uku. 191-192.

^ fu. 67 MAELEZO YA PICHA: Wakati wa ibada ya familia, wazazi wanatumia kadi zenye maandiko ili kuwasaidia watoto wao kukariri maandiko.

^ fu. 70 MAELEZO YA PICHA: Ukurasa wa 5: Wakiwa njiani kwenda mikutanoni, familia hii inafanya mazoezi ya kuimba nyimbo za Ufalme ndani ya gari.