Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 28

Endelea Kumwabudu Yehova Chini ya Marufuku

Endelea Kumwabudu Yehova Chini ya Marufuku

“Sisi hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”​—MDO. 4:19, 20.

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

MUHTASARI *

1-2. (a) Kwa nini hatupaswi kushangaa ibada yetu inapopigwa marufuku? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

KATIKA mwaka wa 2018, zaidi ya wahubiri wa habari njema wapatao 223,000 waliishi katika nchi ambazo utendaji wetu wa kiroho ulikuwa umepigwa marufuku au kuwekewa vizuizi vikali. Hilo halitushangazi. Kama tulivyojifunza katika makala iliyotangulia, Wakristo wa kweli wanatarajia kwamba watateswa. (2 Tim. 3:12) Haidhuru tunaishi wapi, ghafla na bila kutarajia, serikali zinaweza kutuzuia kumwabudu Yehova, Mungu wetu mwenye upendo.

2 Ikiwa serikali ya nchi unayoishi inaamua kupiga marufuku ibada yetu kwa Yehova, huenda ukajiuliza maswali kama haya: ‘Je, mateso yanamaanisha kwamba tumepoteza kibali cha Mungu? Je, marufuku yatakomesha ibada yetu kwa Yehova? Je, nihamie nchi nyingine ambapo nitaweza kumwabudu Mungu kwa uhuru?’ Tutazungumzia maswali hayo katika makala hii. Tutazungumzia pia jinsi tunavyoweza kumwabudu Yehova kazi yetu inapopigwa marufuku na mitego tunayopaswa kuepuka.

JE, MATESO YANAMAANISHA KWAMBA TUMEPOTEZA KIBALI CHA MUNGU?

3. Kulingana na 2 Wakorintho 11:23-27, mtume mwaminifu Paulo alikabili mateso gani, na mfano wa Paulo unatufundisha nini?

3 Serikali ikipiga marufuku ibada yetu, huenda tukafikia mkataa kimakosa kwamba hatuna kibali cha Mungu. Lakini kumbuka kwamba kukabili mateso hakumaanishi kwamba Yehova amechukizwa nasi. Kwa mfano, mfikirie mtume Paulo. Kwa hakika alikuwa na kibali cha Mungu. Alipata pendeleo la kuandika barua 14 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, na alikuwa mtume kwa mataifa. Ingawa hivyo, alikabili mateso makali. (Soma 2 Wakorintho 11:23-27.) Mambo ambayo mtume Paulo alipitia yanatufundisha kwamba Yehova huruhusu watumishi wake waaminifu wapatwe na mateso.

4. Kwa nini tunachukiwa na ulimwengu?

4 Yesu alieleza kwa nini tunapaswa kutarajia upinzani. Alisema kwamba tutachukiwa kwa sababu sisi si sehemu ya ulimwengu. (Yoh. 15:18, 19) Kukabili mateso si ishara ya kwamba tumepoteza kibali cha Yehova. Badala yake, kunaonyesha kwamba tunafanya mambo yaliyo sahihi!

JE, MARUFUKU YATAKOMESHA IBADA YETU KWA YEHOVA?

5. Je, wanadamu duni wanaweza kukomesha ibada ya Yehova? Eleza.

5 Wanadamu duni wanaotupinga hawawezi kufutilia mbali ibada ya Yehova, Mungu Mweza-Yote. Wengi wamejaribu kufanya hivyo na wameshindwa. Fikiria kilichotukia wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wakati huo, serikali za nchi nyingi ziliwatesa vikali watu wa Mungu. Kazi ya Mashahidi wa Yehova haikupigwa marufuku tu na Wanazi nchini Ujerumani, bali pia na serikali ya Australia, Kanada, na serikali za nchi nyingine. Lakini ona kilichotokea. Katika mwaka wa 1939 vita vilipoanza, kulikuwa na wahubiri 72,475 ulimwenguni pote. Ripoti zinaonyesha kwamba vita vilipokwisha mwaka wa 1945, kwa baraka za Yehova, kulikuwa na wahubiri 156,299. Idadi ya wahubiri ilikuwa imeongezeka zaidi ya mara mbili!

6. Badala ya kutuogopesha, upinzani unaweza kuleta matokeo gani mazuri? Toa mfano.

6 Badala ya kutuogopesha, upinzani unaweza kutuchochea tumtumikie Yehova kikamili zaidi. Kwa mfano, wenzi fulani wa ndoa na mtoto wao mdogo waliishi katika nchi ambayo serikali iliamua kupiga marufuku ibada yetu. Badala ya kuogopa, wenzi hao waliamua kuwa mapainia wa kawaida. Hata mke aliamua kuacha kazi yake yenye mshahara mnono ili awe painia. Mume anasema kwamba marufuku hayo yaliwafanya watu wengi wawe na maswali mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova. Kwa sababu hiyo, ilikuwa rahisi zaidi kwake kuanzisha mafunzo ya Biblia. Marufuku hayo yalikuwa na matokeo mazuri kwa wengine pia. Mzee wa kutaniko katika nchi hiyohiyo alisema kwamba wengi waliokuwa wameacha kumtumikia Yehova walianza kuhudhuria mikutano na wakaanza kuhubiri.

7. (a) Andiko la Mambo ya Walawi 26:36, 37 linatufundisha nini? (b) Utafanya nini ukiwa chini ya marufuku?

7 Maadui wetu wanapopiga marufuku ibada yetu, lengo lao ni kutuogopesha tusimtumikie Yehova. Mbali na marufuku, wanaweza kueneza habari zisizo za kweli kutuhusu, kuwatuma wenye mamlaka kukagua nyumba zetu, kutupeleka mahakamani, au hata kuwafunga gerezani baadhi yetu. Wanatarajia kwamba tutaogopa kwa sababu wamefanikiwa kuwafunga gerezani wachache miongoni mwetu. Iwapo tutawaruhusu wafanye mioyo yetu iingiwe na woga, huenda sisi wenyewe tukaanza kuipiga “marufuku” ibada yetu. Hatungependa kuwa kama watu wanaotajwa kwenye Mambo ya Walawi 26:36, 37. (Soma.) Hatutaruhusu woga utufanye tupunguze au kuacha utendaji wetu wa kiroho. Tunamtumaini Yehova kikamili na hatutakubali kuingiwa na wasiwasi. (Isa. 28:16) Tutamwomba Yehova mwongozo kupitia sala. Tunajua kwamba, kwa msaada wake, hata serikali zenye nguvu zaidi za kibinadamu haziwezi kutuzuia kumwabudu Mungu wetu kwa uaminifu.​—Ebr. 13:6.

JE, NIHAMIE NCHI NYINGINE?

8-9. (a)  Ni uamuzi gani wa kibinafsi ambao kila kichwa cha familia au mtu mmojammoja anahitaji kufanya? (b) Ni nini kinachoweza kumsaidia mtu kufanya uamuzi wa hekima?

8 Ikiwa serikali katika nchi unayoishi inapiga marufuku ibada yetu, huenda ukajiuliza ikiwa unapaswa kuhamia katika nchi ambayo unaweza kumtumikia Yehova kwa uhuru. Huo ni uamuzi wa kibinafsi ambao hakuna mtu yeyote anayeweza kukufanyia. Huenda baadhi ya ndugu na dada zetu wakafikiria jambo ambalo Wakristo katika karne ya kwanza walifanya walipokabili mateso. Baada ya maadui kumuua Stefano kwa kumpiga kwa mawe, wanafunzi huko Yerusalemu walihamia na kutawanyika kotekote katika maeneo ya Yudea na Samaria, na hata kufika mpaka Foinike, Kipro, na Antiokia. (Mt. 10:23; Mdo. 8:1; 11:19) Hata hivyo, huenda Wakristo wengine wakatambua kwamba baada ya wimbi lingine la mateso kuwapata Wakristo wa karne ya kwanza, mtume Paulo aliamua kubaki katika maeneo ambayo kazi ya kuhubiri ilipingwa. Badala ya kuhama, alihatarisha usalama wake ili kutangaza habari njema na kuwaimarisha akina ndugu katika majiji ambako kulikuwa na mateso makali.​—Mdo. 14:19-23.

9 Masimulizi hayo yanatufundisha nini? Kila kichwa cha familia anapaswa kufanya uamuzi wa kibinafsi kuhusu kuhamia nchi nyingine au la. Kabla ya kufanya uamuzi huo, anapaswa kusali na kufikiria kwa makini hali za familia yake, na faida au madhara ambayo yanaweza kuipata familia yake iwapo watahama. Kuhusiana na hilo, kila Mkristo “ataubeba mzigo” wake mwenyewe. (Gal. 6:5) Hatupaswi kuwahukumu wengine kwa maamuzi wanayofanya.

TUTAMWABUDU MUNGU JINSI GANI CHINI YA MARUFUKU?

10. Ofisi ya tawi na wazee wa makutaniko watatoa mwongozo gani?

10 Unaweza kuendelea kumwabudu Yehova chini ya marufuku jinsi gani? Ofisi ya tawi itawapa wazee wa makutaniko mwongozo na mapendekezo wanayoweza kutumia kuhusu jinsi ya kupokea chakula cha kiroho, jinsi ya kukutana pamoja kwa ajili ya ibada, na jinsi ya kuhubiri habari njema. Ikiwa ofisi ya tawi haiwezi kuwasiliana na wazee, wazee watakusaidia wewe pamoja na wote kutanikoni kuendelea kumwabudu Yehova. Watatoa mwelekezo unaopatana na mwongozo unaopatikana katika Biblia na machapisho yetu ya Kikristo.​—Mt. 28:19, 20; Mdo. 5:29; Ebr. 10:24, 25.

11. Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote utakuwa na chakula cha kiroho, na unaweza kufanya nini ili kulinda hazina yako ya chakula cha kiroho?

11 Yehova ameahidi kwamba watumishi wake watalishwa vizuri kiroho. (Isa. 65:13, 14; Luka 12:42-44) Hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba tengenezo Lake litafanya kila liwezalo kuandaa kitia-moyo cha kiroho unachohitaji. Unaweza kufanya nini? Ukiwa chini ya marufuku, tafuta mahali pazuri pa kuficha Biblia yako na chakula kingine chochote cha kiroho ulicho nacho. Uwe mwangalifu usiache machapisho hayo yenye thamani mahali yanapoweza kupatikana kwa urahisi​—iwe ni ya kielektroni au yamechapishwa. Ni lazima kila mmoja wetu afanye yote awezayo ili aendelee kubaki akiwa imara kiroho.

Kwa msaada wa Yehova, tunaweza kukutana kwa ajili ya ibada bila kuogopa (Tazama fungu la 12) *

12. Wazee wanaweza kupangaje mikutano kwa njia ambayo wengine hawatatambua kinachoendelea?

12 Vipi kuhusu mikutano yetu ya ibada ya kila juma? Wazee watapanga jinsi ya kufanya mikutano kwa njia ambayo wapinzani wetu hawatatambua kwa urahisi kinachoendelea. Huenda wakapanga tukutane katika vikundi vidogo, na wanaweza kubadili mara kwa mara muda na mahali pa kukutania. Tunaweza kulinda usalama wa wote wanaohudhuria mikutano kwa kuzungumza kwa sauti ya chini tunapoingia au kutoka mahali pa mikutano. Pia, huenda tukahitaji kuvalia kwa njia ambayo haitavuta fikira za watu.

Hata serikali zikitupiga marufuku, hatutaacha kuhubiri (Tazama fungu la 13) *

13. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa ndugu zetu walioishi katika Muungano wa Sovieti?

13 Kuhusu kazi ya kuhubiri, hali zitatofautiana kutoka eneo moja hadi lingine. Lakini kwa kuwa tunampenda Yehova na tunafurahia kuwaeleza wengine kuhusu Ufalme wake, tutatafuta njia ya kuwahubiria watu. (Luka 8:1; Mdo. 4:29) Akizungumzia kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova katika ule uliokuwa Muungano wa Sovieti, mwanahistoria Emily B. Baran alisema hivi: “Serikali ilipowaambia waumini kwamba hawapaswi kuwahubiria wengine kuhusu imani yao, Mashahidi waliendelea kuwaeleza jirani zao, wafanyakazi wenzao, na marafiki kuhusu imani yao. Matendo yao yalipofanya wafungwe kwenye kambi za kazi ngumu, Mashahidi walitafuta wafuasi miongoni mwa wafungwa wenzao.” Licha ya marufuku, ndugu zetu katika Muungano wa Sovieti hawakuacha kuhubiri. Wewe pia azimia kufanya vivyo hivyo iwapo kazi ya kuhubiri itapigwa marufuku katika eneo unaloishi!

MITEGO YA KUEPUKA

Tunahitaji kujua wakati wa kunyamaza (Tazama fungu la 14) *

14. Andiko la Zaburi 39:1 linaweza kutusaidia tusinaswe na mtego gani?

14 Uwe mwangalifu kuhusu habari unazowaambia wengine. Wakati wa marufuku, tunapaswa kutambua “wakati wa kunyamaza.” (Mhu. 3:7) Tunapaswa kulinda habari za siri, kama vile majina ya ndugu na dada zetu, mahali tunapofanyia mikutano, mbinu zetu za kuhubiri, na jinsi tunavyopokea chakula cha kiroho. Hatuwapi wenye mamlaka habari hizo wala marafiki wenye nia nzuri au watu wa ukoo walio katika nchi yetu au wanaoishi katika nchi nyingine. Tukinaswa na mtego huo, tutahatarisha usalama wa ndugu zetu.​—Soma Zaburi 39:1.

15. Shetani atajitahidi kusababisha nini, na tunaweza kuepukaje mtego huo?

15 Usiruhusu mambo madogo-madogo yatugawanye. Shetani anajua kwamba nyumba iliyogawanyika haiwezi kusimama. (Marko 3:24, 25) Daima atajitahidi kusababisha migawanyiko miongoni mwetu. Kwa njia hiyo, anatarajia kwamba tutaanza kupambana na ndugu zetu badala ya kupambana naye.

16. Dada Gertrud Poetzinger alituwekea mfano gani mzuri?

16 Hata Wakristo wakomavu wanahitaji kuwa waangalifu ili wasinaswe na mtego huo. Wafikirie dada wawili watiwa-mafuta, Gertrud Poetzinger na Elfriede Löhr. Walikuwa wamefungwa pamoja na dada wengine Wakristo katika kambi ya mateso ya Wanazi. Gertrud alimwonea wivu Elfriede kwa sababu aliwatolea hotuba zenye kutia moyo dada wengine kambini. Baadaye, Gertrud aliaibikia jambo hilo na akamsihi Yehova amsaidie. Aliandika hivi: “Tunapaswa kujifunza kukubaliana na uhalisi wa mambo wengine wanapokuwa na uwezo mkubwa zaidi au majukumu mengi zaidi kuliko sisi.” Alishinda wivu huo jinsi gani? Gertrud alikazia fikira sifa nzuri za Elfriede na utu wake wa kirafiki. Kwa njia hiyo, uhusiano wake pamoja na Elfriede ukawa mzuri tena. Wote wawili waliokoka kambi ya mateso na kumtumikia Yehova kwa uaminifu mpaka walipomaliza mwendo wao wa kidunia. Tukijitahidi kabisa kushinda tofauti zilizopo kati yetu na ndugu zetu, tutaepuka mtego unaosababisha migawanyiko miongoni mwetu.​—Kol. 3:13, 14.

17. Kwa nini ni lazima tuepuke kuwa wenye kimbelembele?

17 Epuka kimbelembele. Tukifuata mwongozo tunaopokea kutoka kwa ndugu wanaotumainika na wenye mapendeleo, tutaepuka matatizo. (1 Pet. 5:5) Kwa mfano, katika nchi moja ambapo kazi yetu imepigwa marufuku, ndugu wenye mapendeleo walitoa mwongozo kwamba wahubiri hawapaswi kuwaachia watu machapisho wanapokuwa katika huduma. Licha ya hilo, ndugu mmoja painia katika eneo hilo alifikiri kwamba anafahamu mambo vizuri zaidi hivyo hakutii mwongozo huo. Ikawaje? Muda mfupi baada ya yeye pamoja na wahubiri wengine kumaliza kuhubiri isivyo rasmi, walihojiwa na polisi. Inaonekana kwamba maofisa hao walikuwa wakiwafuatilia nao walifanikiwa kuchukua machapisho yote waliyokuwa wamewaachia watu. Kisa hiki kinatufundisha nini? Tunahitaji kufuata mwongozo hata ikiwa hatukubaliani na mwongozo huo. Sikuzote Yehova hutubariki tunapowaunga mkono ndugu ambao amewaweka rasmi waongoze kati yetu.​—Ebr. 13:7, 17.

18. Kwa nini ni lazima tuepuke kuwawekea wengine sheria zisizo za lazima?

18 Usiwawekee wengine sheria zisizo za lazima. Wazee wakiwawekea wengine sheria zisizo za lazima, zinaweza kuwa mzigo kwao. Ndugu Juraj Kaminský anakumbuka kilichotukia wakati wa marufuku katika nchi ambayo zamani iliitwa Chekoslovakia: “Baada ya ndugu wengi wenye mapendeleo na wazee wengi kukamatwa, baadhi ya ndugu waliokuwa wakiongoza makutanikoni na katika mizunguko walianza kuwawekea wahubiri sheria zao wenyewe kuhusu mambo wanayopaswa kufanya na yale waliyopaswa kuepuka.” Yehova hajatupatia mamlaka ya kuwafanyia wengine maamuzi ya kibinafsi. Mtu anapowawekea ndugu zake sheria zisizo za lazima halindi usalama wao, badala yake anajaribu kuwa bwana wa imani ya ndugu zake.​—2 Kor. 1:24.

USIACHE KAMWE KUMWABUDU YEHOVA

19. Licha ya jitihada za Shetani, andiko la 2 Mambo ya Nyakati 32:7, 8 linatupatia uhakika gani?

19 Adui yetu mkuu, Shetani Ibilisi, hataacha kujaribu kuwatesa watumishi waaminifu wa Yehova. (1 Pet. 5:8; Ufu. 2:10) Shetani na wale wanaomuunga mkono watajaribu kupiga marufuku ibada yetu kwa Yehova. Hata hivyo, hatuna sababu ya kulemewa na woga na kuacha kumtumikia Yehova! (Kum. 7:21) Yehova yuko upande wetu, na ataendelea kutusaidia hata kazi yetu ikipigwa marufuku.​—Soma 2 Mambo ya Nyakati 32:7, 8.

20. Umeazimia kufanya nini?

20 Acheni tuazimie kama walivyoazimia ndugu zetu wa karne ya kwanza, waliowaambia hivi watawala wa siku zao: “Kama ni sawa machoni pa Mungu kuwasikiliza ninyi badala ya Mungu, hukumuni ninyi wenyewe. Lakini sisi hatuwezi kuacha kusema kuhusu mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.”​—Mdo. 4:19, 20.

WIMBO 73 Tupe Ujasiri

^ fu. 5 Tunapaswa kufanya nini serikali ikipiga marufuku ibada yetu kwa Yehova? Makala hii itatoa mapendekezo yanayofaa kuhusu mambo tunayopaswa kufanya na tunayopaswa kuepuka ili tusiache kamwe kumwabudu Mungu wetu!

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Picha zote zinaonyesha Mashahidi wanaotumikia katika nchi ambazo kazi yetu imewekewa vizuizi. Katika picha hii kikundi kidogo kimekusanyika kwa ajili ya mkutano ndani ya stoo ya ndugu mmoja.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Dada Mkristo (kushoto) akizungumzia mambo ya kawaida pamoja na mwanamke fulani huku akitafuta fursa ya kuzungumzia mambo ya kiroho.

^ fu. 63 MAELEZO YA PICHA: Ndugu anayehojiwa na polisi anakataa kutoa habari kuhusu kutaniko lake.