Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 34

Kukabiliana na Mabadiliko Unapopata Mgawo Mpya

Kukabiliana na Mabadiliko Unapopata Mgawo Mpya

“Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—EBR. 6:10.

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

MUHTASARI *

1-3. Taja baadhi ya sababu zinazoweza kufanya migawo ya watumishi wa wakati wote ibadilike.

ROBERT na Mary Jo wanaeleza hivi: “Baada ya kutumikia kwa furaha tukiwa wamishonari kwa miaka 21, wazazi wetu wote wanne walikuwa wamedhoofika kiafya. Tulikuwa tayari kuwatunza. Lakini tulihuzunika sana tulipoondoka kwenye eneo ambalo tulilipenda sana.”

2 William na Terrie wanasimulia hivi: “Tulipoambiwa kwamba afya yetu haingeturuhusu turudi katika mgawo wetu, tulilia sana. Ndoto yetu ya kumtumikia Yehova katika nchi ya kigeni ilikuwa imekwisha.”

3 Aleksey anasema hivi: “Tulijua kwamba wapinzani wetu walikuwa na nia ya kufunga ofisi ya tawi nilikokuwa nikitumikia. Lakini bado nilishtuka sana walipochukua hatua hiyo na tukalazimika kuondoka Betheli.”

4. Tutazungumzia maswali gani katika makala hii?

4 Fikiria pia maelfu ya Wanabetheli pamoja na ndugu na dada wengine ambao wamepokea migawo mipya. * Huenda ndugu na dada hao waaminifu wakaona kuwa vigumu kuacha mgawo wanaopenda sana. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wakabiliane na mabadiliko hayo? Unaweza kuwasaidiaje? Majibu ya maswali hayo yanaweza kutusaidia sisi sote kujua jinsi tunavyoweza kukabiliana na mabadiliko maishani mwetu.

JINSI YA KUKABILIANA NA MABADILIKO

Kwa nini inaweza kuwa changamoto kwa watumishi wa wakati wote wanapolazimika kuacha mgawo wao? (Tazama fungu la 5) *

5. Huenda ndugu na dada zetu wakahisije mgawo wao unapobadilika?

5 Iwe tunatumikia shambani au Betheli, baada ya muda sisi huanza kuwapenda sana watu na hata mahali tunapotumikia. Tunapolazimika kuacha mgawo wetu, mioyo yetu huhuzunika sana. Tunawakosa sana ndugu na dada zetu tunaowaacha, na tunakuwa na wasiwasi kuwahusu, hasa ikiwa tumelazimika kuondoka kwa sababu ya mateso. (Mt. 10:23; 2 Kor. 11:28, 29) Isitoshe, huenda tukalazimika kuzoea utamaduni au hali mpya ya mahali tunapohamia tunapopata mgawo mpya au hata tunapolazimika kurudi nyumbani. Robert na Mary Jo wanasema hivi: “Tulikuwa tumesahau utamaduni wetu na hata kuhubiri katika lugha yetu ya mama. Tulihisi tukiwa wageni katika nchi yetu wenyewe.” Huenda baadhi ya ndugu na dada wanaopata mgawo mpya wakakabili changamoto za kiuchumi ambazo hawakutazamia. Huenda wakavunjika moyo, wakawa na wasiwasi, na wasijue la kufanya. Ni nini kinachoweza kuwasaidia?

Ni muhimu sana tumkaribie Yehova na kumtumaini yeye (Tazama fungu la 6 na 7) *

6. Tunaweza kuendelea kukaa karibu na Yehova jinsi gani?

6 Endelea kukaa karibu na Yehova. (Yak. 4:8) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kwa kumtumaini yeye akiwa “Msikiaji wa sala.” (Zab. 65:2) Andiko la Zaburi 62:8 linasema: “Mwageni mioyo yenu mbele zake.” Yehova anaweza “kufanya kwa wingi zaidi kupita mambo yote tunayoomba au tunayofikiri.” (Efe. 3:20) Yehova hatutimizii tu mambo tunayotaja kihususa katika sala zetu. Anaweza kufanya mambo ambayo hatukutazamia, mambo ambayo hatungeweza kamwe kuyafikiria, ili asuluhishe matatizo yetu.

7. (a) Ni nini kitakachokusaidia uendelee kukaa karibu na Yehova? (b) Kulingana na Waebrania 6:10-12, itakuwaje ikiwa tutaendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu?

7 Pia, ili uendelee kukaa karibu na Yehova, unahitaji kusoma Maandiko kila siku na kuyatafakari. Ndugu mmoja aliyekuwa mmishonari anasema hivi: “Dumisha ratiba yako ya kutayarisha mikutano na ya ibada ya familia, kama tu ulivyokuwa ukifanya hapo awali katika mgawo wako.” Pia, endelea kushirikiana kikamili na kutaniko lako jipya katika kazi ya kuhubiri habari njema. Yehova huwakumbuka wale wote wanaoendelea kumtumikia kwa uaminifu, hata ikiwa wanashindwa kutimiza yote waliyokuwa wakifanya hapo awali.—Soma Waebrania 6:10-12.

8. Andiko la 1 Yohana 2:15-17 linatusaidiaje kuwa na maisha rahisi?

8 Uwe na maisha rahisi. Usiruhusu mahangaiko katika ulimwengu wa Shetani ‘yasonge’ utendaji wako wa kiroho. (Mt. 13:22) Usikubali watu wasiomtumikia Yehova, marafiki, au watu wa ukoo wenye nia nzuri wakushinikize ujitafutie usalama wa kifedha au pesa nyingi katika mfumo huu wa Shetani. (Soma 1 Yohana 2:15-17.) Mtumaini Yehova, ambaye anaahidi kutuandalia mahitaji yetu yote ya kiroho, ya kihisia, na ya kimwili kwa “wakati unaofaa.”—Ebr. 4:16, maelezo ya chini; 13:5, 6.

9. Kulingana na Methali 22:3, 7, kwa nini ni muhimu kuepuka madeni yasiyo ya lazima, na ni nini kinachoweza kutusaidia tufanye maamuzi kwa hekima?

9 Epuka madeni yasiyo ya lazima. (Soma Methali 22:3, 7.) Kuhamia eneo lingine kunaweza kuhusisha gharama nyingi, na ni rahisi kujiingiza katika madeni. Ili uepuke kujiingiza katika madeni isivyo lazima, usikope pesa ili kununua vitu ambavyo kihalisi huhitaji. Tunapokuwa na mkazo wa kihisia, kwa mfano, tunapomtunza mpendwa wetu aliye mgonjwa, huenda ikawa vigumu kwetu kuamua vizuri kiasi cha pesa tunachohitaji kukopa. Katika hali kama hizo, kumbuka kwamba “sala na dua” zinaweza kukusaidia kufanya maamuzi kwa hekima. Yehova atajibu sala yako kwa kukupatia amani “itakayolinda moyo wako na nguvu zako za akili,” nayo itakusaidia kufikiri kwa utulivu ili ufanye uamuzi unaofaa.—Flp. 4:6, 7; 1 Pet. 5:7.

10. Tunaweza kupataje marafiki wapya?

10 Dumisha uhusiano mzuri na wengine. Waeleze marafiki wako wa karibu kuhusu hisia zako na hali unazopitia, hasa wale ambao huenda wamewahi kupitia hali ngumu au hali zenye furaha kama zako. Kufanya hivyo, kunaweza kutusaidia tuwe na hali njema kihisia. (Mhu. 4:9, 10) Marafiki uliowapata katika mgawo wako wa awali wataendelea kuwa marafiki wako. Hata hivyo, utahitaji kutafuta marafiki wengine katika mgawo wako mpya. Kumbuka kwamba ili upate marafiki unahitaji kuwa mwenye urafiki. Unaweza kupataje marafiki wapya? Wasimulie wengine kuhusu mambo yenye kufurahisha uliyojionea katika utumishi wa Yehova, na acha wengine wajionee waziwazi shangwe unayopata katika utumishi wa Yehova. Hata wengine kutanikoni wasipoelewa sababu zinazokufanya upende sana utumishi wa wakati wote, huenda wengine wakavutiwa na mfano wako na wakawa marafiki wako wa karibu. Hata hivyo, uwe mwangalifu usijisifu unapowaeleza wengine kuhusu mambo uliyotimiza awali, na usizungumzie sana mambo yaliyokuvunja moyo.

11. Unaweza kufanya nini ili mwendelee kufurahia ndoa yenu?

11 Ikiwa ulilazimika kuacha mgawo wako kwa sababu ya matatizo ya afya ya mwenzi wako, usimlaumu. Kwa upande mwingine, ikiwa wewe ndiye mwenye matatizo ya afya, usihisi hatia, ukifikiri kwamba umemvunja moyo mwenzi wako. Kumbukeni kwamba ninyi ni “mwili mmoja,” na mliahidi mbele za Yehova kwamba mtategemezana chini ya hali zote. (Mt. 19:5, 6) Ikiwa mlilazimika kuacha mgawo wenu kwa sababu ya ujauzito ambao hamkutarajia, hakikisheni kwamba mtoto wenu anajua kuwa yeye ni mtu muhimu zaidi kwenu kuliko mgawo mliokuwa nao. Mhakikishieni mtoto wenu kwamba yeye ni “thawabu” kutoka kwa Mungu. (Zab. 127:3-5) Wakati huohuo, mwelezeni kuhusu mambo yenye kusisimua mliyofurahia katika mgawo wenu. Kufanya hivyo, kunaweza kumchochea mtoto wenu atumie maisha yake kumtumikia Yehova kwa shangwe kama mlivyofanya.

JINSI WENGINE WANAVYOWEZA KUKUSAIDIA

12. (a) Tunaweza kuwasaidiaje watumishi wa wakati wote wasonge mbele na migawo yao? (b) Tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia wazoee kwa urahisi mgawo wao mpya?

12 Ni jambo lenye kutia moyo sana kuona makutaniko mengi na ndugu na dada mmojammoja wakifanya yote wawezayo ili kuwasaidia watumishi wa wakati wote waendelee na migawo yao. Wao hufanya hivyo kwa kuwatia moyo wasonge mbele na migawo yao, kwa kuwapa utegemezo wa kifedha au vitu vya kimwili, au kwa kuwatunza watu wao wa familia walio nyumbani. (Gal. 6:2) Ndugu na dada walio katika utumishi wa wakati wote wanapopata mgawo mpya katika kutaniko lenu, usifikiri kwamba walibadilishiwa mgawo kwa sababu walishindwa kuutimiza vizuri au wanatiwa nidhamu kwa sababu ya jambo fulani baya walilofanya. * Badala yake, wasaidie wazoee kwa urahisi hali yao mpya. Wakaribishe kwa uchangamfu na uwapongeze kwa kazi nzuri waliyofanya, hata ikiwa kwa sasa wanashindwa kutimiza mengi kwa sababu ya afya. Jitahidi kufahamiana nao. Jifunze kutokana na ujuzi, mazoezi, na uzoefu wao mwingi.

13. Tunaweza kuwasaidiaje wale wanaopata migawo mipya?

13 Mwanzoni, huenda wale waliopata mgawo mpya wakahitaji uwasaidie kupata nyumba, usafiri, kazi, na mahitaji mengine ya muhimu. Huenda pia wakahitaji kujua habari za karibuni kuhusu maisha ya kila siku, kama vile kulipa kodi mbalimbali na kupata bima. Badala ya kuwasikitikia, jambo muhimu zaidi wanalohitaji kutoka kwetu ni tuelewe hali zao. Huenda wao wenyewe au watu wao wa ukoo wanakabili matatizo ya afya. Huenda wanaomboleza kwa sababu ya kufiwa na mpendwa wao. * Hata wasiposema, huenda pia wanahuzunika kimyakimya kwa sababu wanawakosa sana marafiki waliokuwa nao katika mgawo wao wa awali. Inachukua muda mrefu kukabiliana na hisia hizo zenye nguvu na ambazo mara nyingi humvuruga mtu sana.

14. Wahubiri katika kutaniko fulani walimsaidiaje dada mmoja azoee mgawo wake mpya?

14 Wakati huohuo, mfano wako na utegemezo wako unaweza kuwasaidia wazoee hali yao mpya. Dada mmoja aliyetumikia kwa miaka mingi katika nchi ya kigeni, anasema hivi: “Katika mgawo wangu wa awali, nilikuwa nikijifunza Biblia na watu wengi kila siku. Lakini katika mgawo wangu mpya, ni vigumu hata kupata fursa ya kumsomea mtu andiko la Biblia au kuonyesha video. Hata hivyo, wahubiri kwenye mgawo wangu wa sasa hunialika kwenye ziara zao za kurudia na mafunzo yao ya Biblia. Kuwaona ndugu na dada hao wenye bidii na ujasiri wakijifunza Biblia na watu wanaofanya maendeleo, hunifanya niwe na mtazamo mzuri zaidi kuhusu eneo ninalotumikia. Nimejifunza jinsi ya kuanzisha mazungumzo na watu kwenye eneo langu jipya. Yote hayo yamenisaidia nipate shangwe tena.”

ENDELEA KUSONGA MBELE!

Tafuta njia za kupanua huduma yako katika eneo lako la nyumbani (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. Unaweza kufanya nini ili ufanikiwe katika mgawo wako mpya?

15 Unaweza kupata mafanikio katika mgawo wako mpya. Usifikiri kwamba mgawo wako umebadilika kwa sababu ulikosea au kwa sasa thamani yako imepungua. Tafakari kuhusu jinsi Yehova alivyokuonyesha mkono wake maishani mwako na uendelee kuhubiri. Waige Wakristo waaminifu wa karne ya kwanza. Popote walipokuwa “[walipita] katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.” (Mdo. 8:1, 4) Jitihada zako za kuendelea kuhubiri zinaweza kuzaa matunda. Kwa mfano, mapainia fulani waliofukuzwa katika nchi moja, walihamia nchi jirani iliyokuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri waliozungumza lugha yao. Katika kipindi cha miezi michache, vikundi vipya vilivyofanya maendeleo kwa kasi vilianzishwa.

16. Ni nini kitakachokusaidia kupata shangwe katika mgawo wako mpya?

16 “Shangwe ya Yehova ndiyo nguvu yenu.” (Neh. 8:10, maelezo ya chini) Hata iwe tunaupenda mgawo wetu kadiri gani, chanzo kikuu cha shangwe yetu kinapaswa kuwa uhusiano wetu na Yehova, na si mgawo wetu. Hivyo basi, endelea kutembea pamoja na Yehova, ukizidi kumtegemea yeye ili upate hekima, mwongozo, na msaada wake. Kumbuka kwamba uliupenda sana mgawo wako wa awali kwa sababu ulijitahidi kwa moyo wako wote kuwasaidia watu. Hivyo, jitoe kwa moyo wako wote kwenye mgawo wako wa sasa na ujionee jinsi Yehova atavyokusaidia kuupenda mgawo huu pia.—Mhu. 7:10.

17. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu mgawo wetu wa sasa?

17 Tunapaswa kukumbuka kwamba utumishi wetu kwa Yehova ni wa milele, lakini mgawo wetu wa sasa ni wa muda tu. Katika ulimwengu mpya, huenda sisi sote tutabadilishiwa migawo. Aleksey, ndugu aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, anaamini kwamba mabadiliko aliyopitia yanamtayarisha kwa ajili ya mabadiliko hayo ya wakati ujao. Anasema hivi: “Sikuzote nilijua kwamba Yehova ni halisi na pia ulimwengu mpya, hata hivyo kwa kadiri fulani ulimwengu mpya na pia Yehova alionekana kuwa mbali kidogo. Sasa ninamwona Yehova akiwa mbele kabisa ya macho yangu, na ulimwengu mpya kama kituo kinachofuata katika safari yangu.” (Mdo. 2:25) Hata iwe tuna mgawo gani, acheni tuendelee kutembea pamoja na Yehova. Hatatuacha kamwe, bali atatusaidia tupate shangwe tunapojitahidi kufanya yote tuwezayo katika utumishi wake—mahali popote pale tutakapokuwa.—Isa. 41:13.

WIMBO 90 Tianeni Moyo

^ fu. 5 Nyakati nyingine, akina ndugu na dada walio katika utumishi wa wakati wote hulazimika kuacha mgawo wao, au hupokea mgawo mwingine mpya. Makala hii inazungumzia changamoto wanazokabili na pia mambo yanayoweza kuwasaidia wazoee hali yao mpya. Pia, inazungumzia mambo ambayo wengine wanaweza kufanya ili kuwatia moyo na kuwategemeza, na vilevile kanuni zinazoweza kutusaidia sisi sote kukabiliana na mabadiliko.

^ fu. 4 Pia, baada ya kufikia umri fulani, ndugu wengi wenye majukumu wamewakabidhi ndugu wenye umri mdogo kuliko wao, majukumu waliyokuwa nayo. Tazama makala, “Enyi Wakristo Wenye Umri Mkubwa Yehova Anathamini Sana Ushikamanifu Wenu,” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Septemba 2018, na “Dumisha Amani ya Akili Licha ya Mabadiliko,” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Oktoba 2018.

^ fu. 12 Bila kukawia, wazee wa kutaniko la awali ambalo walikuwa wakitumikia wanapaswa kuandika barua ya kuwatambulisha ili waweze kuendelea kutumikia wakiwa mapainia, wazee, au watumishi wa huduma bila kuchelewa.

^ fu. 13 Tazama mfululizo “Kukabiliana na Huzuni ya Kufiwa,” katika gazeti Amkeni! la mwaka wa 2018, Na. 3.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Wenzi wa ndoa wamishonari waliolazimika kuondoka katika nchi fulani ya kigeni wanatokwa na machozi wanapoagana na kutaniko lao.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Wakiwa nchini kwao, wenzi hao wa ndoa wanadumu katika sala wakimwomba Yehova awasaidie kukabiliana na changamoto wanazopitia.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Kwa msaada wa Yehova wenzi hao wanaanza tena utumishi wa wakati wote. Wanatumia lugha waliyojifunza walipokuwa wamishonari kuwahubiria wahamiaji walio katika eneo la kutaniko lao jipya.