Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 45

Namna Roho Takatifu Inatusaidia

Namna Roho Takatifu Inatusaidia

“Kwa mambo yote niko na nguvu kupitia ule mwenye ananipatia nguvu.”​—FLP. 4:13.

WIMBO 104 Roho Takatifu​—Zawadi Kutoka kwa Mungu

KIFUPI CHA HABARI *

1-2. (a) Ni nini inatusaidia kuvumilia magumu ya kila siku? Fasiria. (b) Tutajifunza nini mu habari hii?

“WAKATI ninafikiria magumu yenye nilishapata, ninajua kama singeweza kuvumilia kwa nguvu zangu mwenyewe.” Umekwisha kusema maneno kama ile? Wengi kati yetu wamekwisha kusema vile. Pengine ulisema vile kisha kufikiria namna uliweza kuvumilia ugonjwa hatari ao kifo cha mupendwa wako. Wakati unafikiria ile magumu, unaona kama uliweza kuivumilia kila siku kwa sababu tu roho takatifu ya Yehova ilikupatia “nguvu zenye kupita zile za kawaida.”​—2 Ko. 4:7-9.

2 Tunategemea pia roho takatifu ili kupinga vishawishi vya ulimwengu huu muovu. (1 Yo. 5:19) Tena, tunapaswa kupigana na “pepo wachafu.” (Efe. 6:12) Tutazungumuzia sasa ni katika njia gani mbili roho takatifu inatusaidia kuvumilia ile magumu yote. Kisha tutazungumuzia mambo yenye tunaweza kufanya ili roho takatifu itusaidie kabisa.

ROHO TAKATIFU INATUPATIA NGUVU

3. Ni katika njia gani moja Yehova anatusaidia kuvumilia magumu?

3 Roho takatifu ya Yehova inatusaidia kwa kutupatia uwezo ao nguvu za kutimiza madaraka yetu hata kama tuko na magumu. Mutume Paulo aliona kama aliweza kuendelea kumutumikia Yehova hata kama alikuwa na magumu kwa sababu alitegemea “nguvu za Kristo.” (2 Ko. 12:9) Wakati wa safari yake ya pili ya umisionere, Paulo alitumika sana katika kazi ya kuhubiri habari njema na pia alitumika sana ili kupata feza za kutimiza mahitaji yake ya kimwili. Alibakia Korinto mu nyumba ya Akila na Prisila. Walikuwa wanafanya kazi ya kutengeneza mahema. Kwa sababu Paulo naye alikuwa anajua ile kazi, alikuwa anatumika nao siku fulani. (Mdo. 18:1-4) Roho takatifu ilimupatia Paulo nguvu za kutumika kazi ya kimwili na nguvu za kutimiza utumishi wake.

4. Kulingana na 2 Wakorinto 12:7b-9, Paulo alikuwa na tatizo gani?

4 Soma 2 Wakorinto 12:7b-9. Katika andiko hili, Paulo alipenda kusema nini wakati alisema kama alikuwa na “mwiba katika mwili”? Kama mwiba unakuingia mu mwili, utakuwa na maumivu mingi. Kwa hiyo, alipenda kusema kama alikuwa na tatizo fulani lenye lilikuwa linamuletea maumivu. Aliita tatizo hilo “malaika wa Shetani” mwenye aliendelea ‘kumupiga kofi’ (‘kumupiga,’ maelezo ya chini). Pengine haiko Shetani ao pepo wachafu njo walikuwa wanamuletea Paulo mateso, yenye ilikuwa kama vile kumuingiza mwiba katika mwili wake. Lakini wakati pepo wachafu waliona ule “mwiba,” pengine walifurahia kuingiza ule mwiba ndani zaidi ya mwili kwa njia ya mufano, ili kumuongezea Paulo mateso. Paulo alifanya nini?

5. Namna gani Yehova alijibu sala za Paulo?

5 Kwanza, Paulo alipenda Yehova atoshe ule “mwiba.” Alisema hivi: ‘Mara tatu (3) nilimuomba Bwana [Yehova] . . . kwamba uondoke kwangu.’ Lakini, hata kama Paulo aliendelea kusali, ule mwiba uliendelea kubakia katika mwili wake. Ni kusema kama Yehova hakujibu sala za Paulo? Hapana kabisa. Alijibu sala zake. Yehova hakutosha tatizo hilo, lakini alimupatia Paulo nguvu za kuvumilia tatizo hilo. Yehova alisema hivi: “Nguvu zangu zinakamilishwa katika uzaifu.” (2 Ko. 12:8, 9) Na alimusaidia Paulo aendelee kuwa na furaha na amani ya akili!​—Flp. 4:4-7.

6. (a) Namna gani Yehova anaweza kujibu sala zetu? (b) Mu maandiko yenye kupatikana katika fungu hili, ni uhakikisho gani wenye unakupatia nguvu?

6 Kama vile Paulo, je, umekwisha kumuomba Yehova akutoshee tatizo fulani? Kama ulisali sana lakini tatizo lako likaendelea, ao hata hali ikakuwa mubaya zaidi, uliwaza kama pengine Yehova hakufurahie tena? Kama ni vile, ukumbuke mufano wa Paulo. Kama vile Yehova alijibu sala za Paulo, kwa kweli, atajibu sala zako pia! Pengine Yehova hatatosha tatizo lako. Lakini kupitia roho yake takatifu, atakupatia nguvu zenye uko nazo lazima ili uvumilie tatizo hilo. (Zb. 61:3, 4) Unaweza ‘kuangushwa chini,’ lakini Yehova hatakuacha.​—2 Ko. 4:8, 9; Flp. 4:13.

ROHO TAKATIFU INATUSAIDIA TUENDELEE KUMUTUMIKIA YEHOVA

7-8. (a) Namna gani roho takatifu iko kama vile upepo? (b) Namna gani Petro alifasiria namna roho takatifu inafanya kazi?

7 Roho takatifu inatusaidia katika njia gani ingine? Tunaweza kulinganisha roho takatifu na upepo. Upepo unaweza kusaidia mashua yenye iko na tanga (kitambaa kikubwa chenye kinafungwa kwenye mashua na kinasukumwa na upepo ili mashua iende mbele) ifike salama kwenye iko inaenda hata kama kuko zoruba katika bahari. Vilevile, roho takatifu inatusaidia tuendelee kumutumikia Yehova hata kama tuko na matatizo mupaka tufike katika ulimwengu mupya wenye Mungu ametuahidi.

8 Kwa sababu mutume Petro alikuwa muvuvi wa samaki, alikuwa anajua mambo mingi juu ya kusafiri mu mashua. Njo maana wakati alizungumuzia namna roho takatifu inafanya kazi, alitumia neno lenye linaonekana kuwa linahusiana na kusafiri mu bahari. Aliandika hivi: “Unabii haukuletwa wakati wowote kwa mapenzi ya mwanadamu, lakini wanadamu walisema yenye yalitoka kwa Mungu wakiongozwa na roho takatifu.” Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “wakiongozwa” linamaanisha neno kwa neno “wakielekezwa; wakipelekwa.”​—2 Pe. 1:21; maelezo ya chini.

9. Wakati Petro alitumia neno “wakipelekwa,” alifanya watu wafikirie nini katika akili?

9 Maneno ya Petro “wakipelekwa” ilifanya watu wafikirie nini katika akili? Luka, muandikaji wa kitabu cha Matendo, alitumia neno la Kigiriki lenye kufanana na hilo, ili kuzungumuzia mashua yenye ‘kusukumwa’ na upepo. (Mdo. 27:15) Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia alisema kama, wakati Petro aliandika kama waandikaji wa Biblia ‘walipelekwa,’ alitumia neno la mufano lenye lilifanya watu wafikirie safari za mu bahari. Petro alipenda kusema kwamba, kama vile mashua inapelekwa na upepo ili kusafiri mupaka kwenye inaenda, manabii na waandikaji wa Biblia walipelekwa na roho takatifu ili kutimiza kazi yao. Mutu huyo mwenye elimu alisema tena hivi: “Manabii walipandisha tanga zao kwa njia ya mufano.” Yehova alifanya sehemu yake: Aliwapatia “upepo,” ao roho takatifu. Na waandikaji wa Biblia walifanya sehemu yao: Walifuata muongozo wa roho hiyo.

JAMBO LA 1: Ufanye kwa ukawaida mambo ya kiroho

JAMBO LA 2: Ufanye ile mambo ya kiroho kulingana na uwezo wako wote (Picha hii inapatana na fungu la 11) *

10-11. Ni mambo gani mbili yenye tunapaswa kufanya ili roho takatifu ituongoze? Leta mufano.

10 Kwa kweli, leo Yehova hatumie tena roho yake takatifu ili kuongoza watu waandike vitabu vya Biblia. Lakini, angali anatumia roho takatifu ili kuongoza watumishi wake. Yehova angali anafanya sehemu yake. Tunapaswa kufanya nini ili roho takatifu ituongoze? Tunapaswa kuendelea kufanya sehemu yetu. Namna gani?

11 Fikiria mufano huu. Kama mutu mwenye kuongoza mashua anapenda upepo umusaidie, anapaswa kufanya mambo mbili. Jambo la kwanza, anapaswa kupeleka mashua nafasi kwenye upepo unavuma. Lakini, mashua yake haitaenda nafasi yoyote kama inabakia mahali kwenye mashua zinaegesha mbali na nafasi kwenye upepo unavuma. Jambo la pili, anapaswa kupandisha na kufungua kabisa tanga zake. Kwa kweli, hata kama mashua yake iko nafasi kwenye upepo unavuma, itaenda mbele wakati tu tanga zinajaa upepo. Vilevile, tutaendelea kumutumikia Yehova ikiwa tu tuko na musaada wa roho takatifu. Ili roho takatifu itusaidie, tunapaswa kufanya mambo mbili. Jambo la kwanza, tunapaswa kuenda nafasi kwenye roho ya Mungu inavuma, kwa kufanya mambo yenye inafanya roho takatifu ituongoze. Jambo la pili, tunapaswa “kupandisha tanga zetu” kabisa, kwa kufanya ile mambo kulingana na uwezo wetu wote. (Zb. 119:32) Wakati tunafanya ile mambo, roho takatifu itatusaidia kushinda upinzani na majaribu yenye kuwa kama zoruba na itatusaidia kuvumilia kwa uaminifu mupaka tufike katika ulimwengu mupya wa Mungu.

12. Tutazungumuzia nini sasa?

12 Tumeona kama roho takatifu inatusaidia katika njia mbili. Roho takatifu inatupatia nguvu na inatusaidia tubakie waaminifu wakati tunapata majaribu. Pia, roho takatifu inatuongoza na inatusaidia tubakie katika njia yenye kuongoza kwenye uzima wa milele. Sasa tutazungumuzia mambo ine yenye tunapaswa kufanya ili roho takatifu itusaidie kabisa.

MAMBO YENYE TUNAPASWA KUFANYA ILI ROHO TAKATIFU ITUSAIDIE KABISA

13. Kulingana na 2 Timoteo 3:16, 17, namna gani Maandiko inaweza kutusaidia, lakini tunapaswa kufanya nini?

13 Jambo la kwanza, tunapaswa kujifunza Neno la Mungu. (Soma 2 Timoteo 3:16, 17.) Neno la Kigiriki lenye kutafsiriwa “limeongozwa na roho ya Mungu” linamaanisha neno kwa neno “limepuliziwa na Mungu.” Mungu alitumia roho yake ili “kupuliza” mawazo yake katika akili ya wale wenye waliandika Biblia. Wakati tunasoma Biblia na kufikiri sana juu ya mambo yenye tunasoma, maagizo ya Mungu inaingia katika akili yetu na moyo wetu. Ile maneno yenye kuongozwa na roho ya Mungu inatuchochea tufanye mabadiliko katika maisha yetu ili tumupendeze Yehova. (Ebr. 4:12) Lakini ili roho takatifu itusaidie kabisa, tunapaswa kupanga wakati wa kujifunza Biblia kwa ukawaida na kufikiri sana juu ya mambo yenye tunasoma. Kama tunafanya vile, Neno la Mungu litachochea mambo yote yenye tunasema ao kufanya.

14. (a) Juu ya nini tunaweza kusema kama “upepo unavuma” ku mikutano yetu ya Kikristo? (b) Tunaweza kufanya nini ili tuhuzurie mikutano na tuko na “matanga yenye kufunguliwa”?

14 Jambo la pili, tunapaswa kumuabudu Mungu pamoja na wengine. (Zb. 22:22) Kwa njia ya mufano, “upepo unavuma” ku mikutano yetu ya Kikristo. Roho ya Yehova iko ku mikutano yetu. (Ufu. 2:29) Juu ya nini tunaweza kusema vile? Juu wakati tunakutana ili kuabudu pamoja na Wakristo wenzetu, tunasali ili kupata roho takatifu, tunaimba nyimbo za Ufalme zenye kutegemea Neno la Mungu, na tunasikiliza mafundisho yenye kutegemea Biblia yenye ndugu wenye wamewekwa na roho takatifu wanafundisha. Na roho takatifu ileile njo inasaidia dada watayarishe na kutoa migao yao. Lakini ili roho takatifu itusaidie kabisa, tunapaswa kujitayarisha ili kutoa majibu ku mikutano. Wakati tunafanya vile, tunahuzuria mikutano na tuko na “tanga zenye kufunguliwa” kwa njia ya mufano.

15. Namna gani roho takatifu inatusaidia katika kazi ya kuhubiri?

15 Jambo la tatu, tunapaswa kuhubiri. Wakati tunatumia Biblia katika kazi ya kuhubiri na kufundisha, tunaruhusu roho takatifu itusaidie katika kazi yetu ya kuhubiri. (Ro. 15:18, 19) Lakini ili roho takatifu ya Mungu ikusaidie kabisa, unapaswa kuhubiri kwa ukawaida na kutumia Biblia kila wakati unapata nafasi ya kufanya vile. Ili kufanya namna yako ya kuhubiri ikuwe muzuri zaidi, unaweza kutumia namna mbalimbali za kuanzisha mazungumuzo zenye kupatikana mu Buku la Mukutano Utumishi na Maisha ya Mukristo.

16. Njia ya moja kwa moja kabisa ya kupata roho takatifu ni gani?

16 Jambo la ine, tunapaswa kusali kwa Yehova. (Mt. 7:7-11; Lu. 11:13) Njia ya moja kwa moja kabisa ya kupata roho takatifu ni kumuomba Yehova roho hiyo katika sala. Hakuna kitu chenye kinaweza kuzuia sala zetu zisimufikie Yehova ao kuzuia zawadi ya muzuri ya roho takatifu ya Mungu isitufikie hata tukuwe katika gereza; na hata Shetani hawezi kuzuia roho ya Mungu isitufikie. (Yak. 1:17) Tunapaswa kusali namna gani ili roho takatifu itusaidie kabisa? Ili kujibu ulizo hilo, tuzungumuzie mambo fulani juu ya sala kwa kuchunguza mufano mumoja wenye kupatikana tu katika Injili ya Luka. *

ENDELEA KUSALI

17. Tunaweza kujifunza jambo gani juu ya sala kupitia mufano wa Yesu katika Luka 11:5-9, 13?

17 Soma Luka 11:5-9, 13. Mufano wa Yesu unaonyesha namna tunaweza kusali ili kupata roho takatifu. Katika mufano huo, mwanaume huyo alipata mambo yenye alikuwa nayo lazima ‘kwa sababu aliendelea kuomba kwa uhodari.’ Hakuogopa kuomba rafiki yake musaada hata kama ilikuwa usiku sana. * Kupitia mufano huo, Yesu alitufundisha nini juu ya sala? Alisema hivi: “Muendelee kuomba, na mutapewa; muendelee kutafuta, na mutapata; muendelee kupiga hodi, na watawafungulia.” Kwa hiyo, tunajifunza jambo gani? Ili roho takatifu itusaidie, tunapaswa kuendelea kusali ili tupate roho hiyo.

18. Kulingana na mufano wa Yesu, juu ya nini tunaweza kuwa hakika kama Yehova atatupatia roho yake takatifu?

18 Pia, mufano wa Yesu unatusaidia kuelewa juu ya nini Yehova atatupatia roho takatifu. Mwanaume mwenye kuzungumuziwa katika mufano huo alipenda kukaribisha muzuri mugeni wake. Aliona kama alipaswa kupatia chakula mugeni wake mwenye alifika usiku sana, lakini hakukuwa na chakula. Yesu alisema kama jirani alipatia mwanaume huyo mukate kwa sababu aliendelea kuomba. Yesu alipenda kutufundisha nini? Kama mwanadamu mwenye hakamilike iko tayari kusaidia jirani yake mwenye anaendelea kuomba, tunaweza kuwa hakika zaidi kama Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo atasaidia wale wenye wanaendelea kumuomba roho takatifu! Kwa hiyo, tunaweza kuwa hakika kama Yehova atajibu sala zetu wakati tunamuomba roho takatifu.​—Zb. 10:17; 66:19.

19. Juu ya nini tunaweza kuwa hakika kama tutapata ushindi?

19 Tunaweza kuwa hakika na jambo hili: hata kama Shetani anaendelea kutupiganisha, tutapata ushindi. Juu ya nini? Juu roho takatifu inatusaidia katika njia mbili. Njia ya kwanza, inatupatia nguvu zenye tuko nazo lazima ili kushinda matatizo yetu. Njia ya pili, inatupatia nguvu za kuendelea kumutumikia Yehova mupaka tufike mu ulimwengu mupya wa Mungu. Tuache basi roho takatifu itusaidie kabisa!

WIMBO 41 Tafadhali Sikiliza Sala Yangu

^ fu. 5 Habari hii inafasiria namna roho takatifu ya Mungu inaweza kutusaidia kuvumilia. Inazungumuzia pia mambo yenye tunaweza kufanya ili roho takatifu itusaidie kabisa.

^ fu. 16 Kuliko waandikaji wengine wa Injili, Luka njo anaonyesha zaidi kama sala ilikuwa sehemu ya maana sana ya maisha ya Yesu.​—Lu. 3:21; 5:16; 6:12; 9:18, 28, 29; 18:1; 22:41, 44.

^ fu. 17 Ona maelezo kuhusu “kuomba kwa uhodari” katika Vichapo Vyenye Kutajwa Katika Buku la Mukutano Utumishi na Maisha mu Buku la Mukutano la Mwezi wa 7, 2018, ukurasa wa 6.

^ fu. 60 MAFASIRIO YA PICHA: JAMBO LA 1: Ndugu na dada wanafika ku Jumba la Ufalme. Wakati wanakusanyika pamoja na ndugu na dada wenzao, wanapatikana nafasi kwenye roho ya Yehova iko. JAMBO LA 2: Wamejitayarisha ili kutoa majibu ku mukutano. Tunapaswa kufanya vilevile kuhusu mambo ingine yenye tumezungumuzia katika habari hii: kujifunza Neno la Mungu, kuhubiri, na kusali kwa Yehova.