Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 47

Mambo Tunayojifunza Katika Kitabu cha Mambo ya Walawi

Mambo Tunayojifunza Katika Kitabu cha Mambo ya Walawi

“Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.”—2 TIM. 3:16.

WIMBO 98 Maandiko—Yaliongozwa na Roho ya Mungu

MUHTASARI *

1-2. Kwa nini Wakristo leo wanapaswa kupendezwa na kitabu cha Mambo ya Walawi?

MTUME Paulo alimkumbusha Timotheo, rafiki yake kijana kwamba “kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Tim. 3:16) Maandiko hayo yanatia ndani kitabu cha Mambo ya Walawi. Unakionaje kitabu hicho? Huenda wengine wakakiona kuwa kitabu kilicho na orodha ndefu ya sheria ambazo hazituhusu sisi leo, hata hivyo Wakristo wa kweli wana maoni tofauti.

2 Kitabu cha Mambo ya Walawi kiliandikwa miaka 3,500 hivi iliyopita, licha ya hilo Yehova alikihifadhi “ili kutufundisha.” (Rom. 15:4) Kwa sababu kitabu hicho kinatufunulia njia ya Yehova ya kufikiri, tunapaswa kuwa na hamu ya kukichunguza. Ukweli ni kwamba kuna mambo mengi tunayoweza kujifunza kutokana na kitabu hicho kilichoongozwa na roho ya Mungu. Acheni tuchunguze masomo manne.

JINSI TUNAVYOPATA KIBALI CHA YEHOVA

3. Kwa nini dhabihu zilitolewa kila mwaka katika Siku ya Kufunika Dhambi?

3 Somo la kwanza: Ili dhabihu zetu zikubaliwe na Yehova tunahitaji kuwa na kibali chake. Kila mwaka, katika Siku ya Kufunika Dhambi, taifa la Israeli lilikusanyika pamoja, na dhabihu za wanyama zilitolewa. Dhabihu hizo ziliwakumbusha Waisraeli kwamba walihitaji kusafishwa dhambi zao. Lakini siku hiyo, kabla ya kuhani mkuu kuingia na damu yoyote ya dhabihu katika Patakatifu Zaidi, alihitaji kwanza kufanya jambo fulani ambalo kwa kweli lilikuwa muhimu hata zaidi kuliko msamaha wa dhambi za taifa la Israeli.

(Tazama fungu la 4) *

4. Kama inavyotajwa kwenye Mambo ya Walawi 16:12, 13, kuhani mkuu alifanya nini alipoingia kwa mara ya kwanza katika Patakatifu Zaidi kwenye Siku ya Kufunika Dhambi? (Tazama picha kwenye jalada.)

4 Soma Mambo ya Walawi 16:12, 13. Wazia jinsi hali ilivyokuwa katika Siku ya Kufunika Dhambi: Kuhani mkuu anaingia kwenye hema la ibada. Hiyo ni mara ya kwanza kati ya mara tatu anazopaswa kuingia katika Patakatifu Zaidi siku hiyo. Kwenye mkono mmoja amebeba chombo kilichojaa uvumba uliotiwa manukato, na kwenye mkono mwingine amebeba chetezo cha dhahabu kilichojaa makaa yenye moto. Anasimama mbele ya pazia linalofunika mlango wa Patakatifu Zaidi. Kwa heshima kubwa, anaingia katika Patakatifu Zaidi na kusimama mbele ya sanduku la agano. Kwa njia ya mfano, amesimama mbele za Yehova mwenyewe! Sasa kuhani anatia kwa makini ule uvumba mtakatifu juu ya yale makaa ya moto, na chumba kinajaa harufu tamu. * Baadaye, ataingia tena katika Patakatifu Zaidi akiwa na damu ya dhabihu za dhambi. Ona kwamba anafukiza uvumba kabla ya kutoa damu ya dhabihu za dhambi.

5. Tunajifunza nini kutokana na matumizi ya uvumba katika Siku ya Kufunika Dhambi?

5 Tunajifunza nini kutokana na matumizi ya uvumba katika Siku ya Kufunika Dhambi? Biblia inaonyesha kwamba sala zinazokubalika za waabudu waaminifu wa Yehova ni kama uvumba. (Zab. 141:2; Ufu. 5:8) Kumbuka kwamba kuhani mkuu aliingia mbele za Yehova kwa heshima kubwa akiwa na uvumba. Vivyo hivyo, tunapomfikia Yehova katika sala, tunafanya hivyo tukiwa na heshima kubwa. Tunamwonyesha staha kubwa. Tunathamini sana kwamba Muumba wa ulimwengu anaturuhusu tumfikie na kumkaribia, kama inavyokuwa kwa mtoto na baba yake. (Yak. 4:8) Anatukubali kuwa rafiki zake! (Zab. 25:14) Tunathamini sana pendeleo hilo hivi kwamba hatungependa kumhuzunisha.

6. Kitendo cha kuhani mkuu kufukiza uvumba kabla ya kutoa dhabihu kinatufundisha nini?

6 Kumbuka kwamba kuhani mkuu alipaswa kufukiza uvumba kabla ya kutoa dhabihu. Kwa njia hiyo, alihakikisha kwamba alikuwa na kibali cha Mungu alipokuwa akitoa dhabihu. Tunajifunza nini? Alipokuwa duniani, Yesu alihitaji kufanya jambo fulani muhimu kabla ya kutoa uhai wake kuwa dhabihu, jambo muhimu kuliko hata kuandaa wokovu kwa ajili ya wanadamu. Lilikuwa jambo gani? Alipaswa kuwa mtimilifu kwa kumtii Yehova kwa ushikamanifu katika kipindi chote cha maisha yake duniani ili Yehova aweze kuikubali dhabihu yake. Kwa kufanya hivyo, Yesu angethibitisha kwamba kufanya mambo kulingana na njia ya Yehova ndiyo njia bora zaidi ya maisha. Yesu angeitetea, yaani, angethibitisha kwamba enzi kuu ya Baba yake au njia yake ya kutawala ndiyo sahihi na ya haki.

7. Kwa nini maisha ya Yesu duniani yalimpendeza Baba yake?

7 Katika kipindi chote cha maisha yake duniani, Yesu alitii kikamilifu viwango vya Yehova vya uadilifu. Hakuna kishawishi au jaribu lolote ambalo lingeweza kudhoofisha tamaa yake ya kutetea njia ya Baba yake ya kutawala, hata kifo chenye maumivu makali hakingeweza kumzuia. (Flp. 2:8) Alipokabili majaribu, Yesu alisali “kwa vilio vyenye nguvu na machozi.” (Ebr. 5:7) Sala zake za kutoka moyoni zilionyesha kwamba alikuwa mshikamanifu kwa Yehova na ziliimarisha azimio lake la kuendelea kuwa mtiifu. Machoni pa Yehova, sala za Yesu zilikuwa kama uvumba wenye harufu tamu. Katika maisha yake yote, Yesu alimpendeza sana Baba yake na alitetea enzi Yake kuu.

8. Tunaweza kuiga maisha ya Yesu jinsi gani?

8 Tunaweza kumwiga Yesu kwa kufanya yote tuwezayo ili kuwa watimilifu na washikamanifu kwa njia na sheria za Yehova. Tunapokabili majaribu, tunasali kwa Yehova kwa bidii ili atusaidie kwa sababu tunataka kumfurahisha. Kwa kufanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunaunga mkono njia ya Yehova ya kutawala. Tunatambua kwamba Yehova hatakubali sala zetu ikiwa tutajihusisha na mwenendo unaomchukiza. Lakini tukiishi kulingana na viwango vya Yehova, tunaweza kuwa na uhakika kwamba sala zetu za kutoka moyoni zitakuwa kama uvumba wenye harufu tamu mbele za Yehova. Na tunaweza kuwa na uhakika kwamba utimilifu na utii wetu mshikamanifu unamfurahisha Baba yetu wa mbinguni.—Met. 27:11.

UTUMISHI WETU KWA YEHOVA HUCHOCHEWA NA UTHAMINI NA UPENDO WETU KWAKE

(Tazama fungu la 9) *

9. Kwa nini dhabihu za ushirika zilitolewa?

9 Somo la pili: Tunamtumikia Yehova kwa sababu tunathamini mambo anayotutendea. Ili kuelewa vizuri sababu hiyo, acheni tuzungumze kuhusu dhabihu za ushirika, ambazo zilikuwa sehemu muhimu ya ibada ya kweli katika taifa la kale la Israeli. * Katika kitabu cha Mambo ya Walawi tunajifunza kwamba Mwisraeli angeweza kutoa dhabihu ya ushirika “ili kuonyesha shukrani.” (Law. 7:11-13, 16-18) Alitoa dhabihu hiyo si kwa sababu alilazimika kufanya hivyo, bali kwa kuwa alitamani kufanya hivyo. Hiyo ilikuwa dhabihu ya hiari ambayo mtu alitoa kwa sababu alimpenda Yehova, Mungu wake. Mtu aliyetoa dhabihu hiyo, familia yake, na makuhani wangekula nyama ya mnyama aliyetolewa dhabihu. Lakini sehemu fulani za mnyama huyo wa dhabihu zilitolewa tu kwa ajili ya Yehova. Sehemu gani hizo?

(Tazama fungu la 10) *

10. Dhabihu za ushirika zinazofafanuliwa kwenye Mambo ya Walawi 3:6, 12, 14-16 zinatufundisha nini kuhusu nia ya Yesu ya kufanya mapenzi ya Baba yake?

10 Somo la tatu: Tunampa Yehova kilicho bora kwa sababu tunampenda. Yehova aliyaona mafuta kuwa sehemu bora kabisa ya mnyama. Pia, alitaja kihususa kwamba viungo muhimu kama vile figo, vilikuwa na thamani ya pekee. (Soma Mambo ya Walawi 3:6, 12, 14-16.) Hivyo, Yehova alifurahi sana Mwisraeli alipomtolea kwa hiari viungo hivyo muhimu pamoja na mafuta. Mwisraeli aliyetoa dhabihu hiyo alionyesha tamaa yake ya kutoka moyoni ya kumtolea Mungu kitu kilicho bora kabisa. Kwa njia hiyohiyo, Yesu alimtolea Yehova kwa hiari kitu kilicho bora kabisa kwa kumtumikia kwa nafsi yote kwa sababu alimpenda. (Yoh. 14:31) Yesu alifurahia kufanya mapenzi ya Mungu; aliipenda sana sheria ya Mungu. (Zab. 40:8) Hapana shaka kwamba Yehova alifurahi sana kumwona Yesu akimtumikia kwa hiari!

Kumpenda Yehova hutuchochea tumpe kilicho bora (Tazama fungu la 11 na 12) *

11. Utumishi wetu ni kama dhabihu za ushirika jinsi gani, na ulinganisho huo unatufariji jinsi gani?

11 Kama dhabihu hizo za ushirika, utumishi wetu wa hiari tunaofanya kwa ajili ya Yehova unaonyesha jinsi tunavyohisi kumhusu. Tunampa Yehova kilicho bora kabisa, na tunafanya hivyo kwa sababu tunampenda kwa moyo wetu wote. Yehova anafurahi sana anapoona mamilioni ya waabudu wake wakimtumikia kwa hiari kwa sababu wanampenda sana yeye na njia zake! Tunafarijika kwa kukumbuka kwamba Yehova anaona na anathamini matendo na nia yetu. Kwa mfano, ikiwa umri wako umesonga na hauwezi kufanya mengi kama ulivyokuwa ukifanya awali, uwe na hakika kwamba Yehova anaelewa hali yako. Huenda ukahisi kwamba huwezi kutimiza mengi kwa ajili ya Yehova, lakini Yehova anaona upendo wako mwingi unaokuchochea kufanya yote unayoweza. Anakubali kwa furaha kupokea kilicho bora kutoka kwako kulingana na uwezo wako.

12. Tunapata uhakikisho gani kutokana na jinsi Yehova alivyohisi kuhusu dhabihu za ushirika?

12 Tunajifunza nini kutokana na dhabihu za ushirika? Moto ulipokuwa ukiteketeza sehemu bora kabisa za mnyama wa dhabihu, moshi ulipanda juu na Yehova alifurahi. Hivyo, uwe na hakika kwamba Yehova anapendezwa na utumishi wako wa nafsi yote unaofanya kwa hiari. (Kol. 3:23) Wazia jinsi anavyotabasamu akionyesha kibali chake. Anaona jitihada zako za upendo katika utumishi wake, iwe ni jitihada ndogo au kubwa, kuwa kama hazina ambazo atakumbuka na kuthamini milele na milele.—Mt. 6:20; Ebr. 6:10.

YEHOVA ANALIBARIKI TENGENEZO LAKE

13. Kulingana na Mambo ya Walawi 9:23, 24, Yehova alionyeshaje kwamba aliwakubali makuhani?

13 Somo la nne: Yehova anabariki sehemu ya kidunia ya tengenezo lake. Fikiria kilichotokea mwaka wa 1512 K.W.K., hema la ibada lilipotengenezwa chini ya Mlima Sinai. (Kut. 40:17) Musa aliongoza sherehe ya kumweka rasmi Haruni na wanawe kuwa makuhani. Taifa la Israeli lilikusanyika ili kushuhudia makuhani wakitoa dhabihu za wanyama kwa mara ya kwanza. (Law. 9:1-5) Yehova alionyeshaje kwamba aliwakubali makuhani hao wapya? Haruni na Musa walipokuwa wakiwabariki watu, Yehova alishusha moto ambao uliteketeza sehemu ya dhabihu iliyokuwa imebaki kwenye madhabahu.—Soma Mambo ya Walawi 9:23, 24.

14. Kwa nini tunapendezwa kuona kwamba Yehova alikubali ukuhani wa Haruni?

14 Moto ulioshuka kutoka mbinguni wakati wa kumweka rasmi kuhani mkuu ulionyesha nini? Ulionyesha kwamba Yehova aliunga mkono kabisa ukuhani wa Haruni. Waisraeli walipoona uthibitisho huo ulio wazi wa Yehova wa kuwakubali makuhani, walikuwa na sababu nzuri ya kuwaunga mkono kikamili. Je, hilo linatuhusu? Ndiyo! Ukuhani katika taifa la Israeli, ulikuwa kivuli cha ukuhani mkubwa zaidi. Kristo, Kuhani Mkuu zaidi, ana ukuhani wa kifalme ulio na wale 144,000, ambao watatumikia pamoja naye mbinguni.—Ebr. 4:14; 8:3-5; 10:1.

Yehova anabariki na kuliongoza tengenezo lake. Tunaliunga mkono kwa moyo wetu wote (Tazama fungu la 15 hadi 17) *

15-16. Yehova ameonyeshaje kwamba “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ana kibali chake?

15 Katika mwaka wa 1919, Yesu alikiweka rasmi kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta kuwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Mtumwa huyo anasimamia kazi ya kuhubiri na kuwapa wafuasi wa Kristo ‘chakula kwa wakati unaofaa.’ (Mt. 24:45) Je, tunajionea uthibitisho ulio wazi kwamba mtumwa mwaminifu na mwenye busara ana kibali cha Mungu?

16 Shetani na ulimwengu wake umetokeza changamoto nyingi ili mtumwa mwaminifu ashindwe kutimiza kazi yake. Na bila msaada wa Yehova mtumwa huyo asingeweza kuitimiza kazi hiyo. Licha ya vita viwili vya ulimwengu, mateso yasiyokoma, misukosuko ya kiuchumi duniani, na ukosefu wa haki, mtumwa mwaminifu na mwenye busara ameendelea kuwaandalia wafuasi wa Kristo chakula cha kiroho. Fikiria kuhusu chakula kingi cha kiroho kinachopatikana leo, bila malipo, na katika lugha zaidi ya 900! Huo ni uthibitisho usiopingika wa utegemezo kutoka kwa Mungu. Fikiria uthibitisho mwingine wa baraka za Yehova: kazi ya kuhubiri. Kwa kweli, habari njema inahubiriwa “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Bila shaka, Yehova analiongoza na kulibariki kwa ukarimu tengenezo lake leo.

17. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaunga mkono tengenezo ambalo Yehova analitumia?

17 Inafaa kujiuliza, ‘Je, ninathamini kuwa katika sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova?’ Yehova ametupatia uthibitisho wenye kusadikisha kama ule aliompatia Musa na Haruni aliposhusha moto halisi kutoka mbinguni. Kwa kweli, tuna mengi ya kumshukuru Yehova. (1 The. 5:18, 19) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaunga mkono tengenezo ambalo Yehova analitumia? Kwa kufuata mwongozo unaotegemea Biblia unaotolewa kupitia machapisho, mikutano, na makusanyiko yetu. Zaidi ya hayo, tunaweza kuonyesha kwamba tunaunga mkono tengenezo la Yehova kwa kushiriki kikamili kadiri tuwezavyo katika kazi ya kuhubiri na kufundisha.—1 Kor. 15:58.

18. Umeazimia kufanya nini?

18 Acheni tuazimie kutumia mambo tuliyojifunza katika kitabu cha Mambo ya Walawi. Acheni tutafute kibali cha Yehova ili dhabihu zetu zikubaliwe naye. Acheni tumtumikie Yehova kwa sababu tunathamini mambo anayotufanyia. Acheni tuendelee kumpa Yehova kilicho bora kwa sababu tunampenda kwa moyo wetu wote. Na acheni tuunge mkono kwa moyo wote tengenezo analolibariki leo. Kwa kufanya mambo hayo yote, tunamwonyesha Yehova kwamba tunathamini pendeleo tulilo nalo la kumtumikia tukiwa Mashahidi wake!

WIMBO 96 Kitabu cha Mungu Ni Hazina

^ fu. 5 Kitabu cha Mambo ya Walawi kina sheria ambazo Yehova aliwapa Waisraeli wa kale. Tukiwa Wakristo, hatuko chini ya sheria hizo, lakini zinaweza kutunufaisha. Katika makala hii, tutazungumzia mambo muhimu tunayojifunza katika kitabu cha Mambo ya Walawi.

^ fu. 4 Uvumba uliofukizwa katika hema la ibada ulionwa kuwa mtakatifu, na ulitumika katika Israeli la kale katika ibada ya Yehova tu. (Kut. 30:34-38) Hakuna rekodi yoyote inayoonyesha kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walifukiza uvumba kwenye ibada yao.

^ fu. 9 Kwa habari zaidi kuhusu dhabihu za ushirika, tazama Insight on the Scriptures, Buku la 2, uku. 526.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Katika Siku ya Kufunika Dhambi, kuhani mkuu wa Israeli aliingia katika Patakatifu Zaidi akiwa na uvumba na makaa ya moto ili kujaza chumba harufu tamu. Baadaye, aliingia tena katika Patakatifu Zaidi akiwa na damu ya dhabihu za dhambi.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Mwisraeli akimpa kuhani kondoo kwa ajili ya dhabihu ya ushirika ili kuonyesha shukrani za familia yake kwa Yehova.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alionyesha kwamba anampenda sana Yehova kwa kushika amri za Mungu na kwa kuwasaidia wafuasi wake wazishike pia.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Licha ya udhaifu wa kimwili, dada aliyezeeka anampa Yehova kilicho bora kwa kutoa ushahidi kupitia barua.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Februari 2019, Ndugu Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza alitoa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa ya lugha ya Kijerumani mbele ya umati wenye shukrani na shauku. Leo, wahubiri nchini Ujerumani, kama dada hawa wawili, hutumia kwa shangwe Biblia hiyo katika huduma.