Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jitihada za Kutafuta Kweli

Jitihada za Kutafuta Kweli

Tunaweza kuokoa uhai wetu tukijua ukweli. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo maisha yetu yamebadilika kwa kupata jibu la swali hili, Magonjwa ya kuambukiza huenezwa jinsi gani?

Kwa maelfu ya miaka, hakuna yeyote aliyejua jibu la swali hilo. Hivyo, magonjwa ya kuambukiza yalisababisha vifo vya mamilioni ya watu. Hatimaye wanasayansi walijua ukweli. Waligundua kwamba mara nyingi magonjwa yalikuwa yakisababishwa na viini, yaani, vijidudu vidogo kama vile bakteria au virusi. Kutambua ukweli huo kumesaidia kukinga na kutibu magonjwa mengi, na hilo limefanya mabilioni ya watu waboreshe afya zao na waishi kwa muda mrefu.

Namna gani kuhusu maswali mengine muhimu, kama vile;

  • Mungu ni nani?

  • Yesu Kristo ni nani?

  • Ufalme wa Mungu ni nini?

  • Maisha yatakuwaje wakati ujao?

Mamilioni ya watu wamepata majibu ya maswali hayo, na hilo limewasaidia kuboresha maisha yao. Wewe pia unaweza kunufaika kwa kupata majibu ya maswali hayo.

JE, UNAWEZA KUPATA UKWELI?

Huenda ukajiuliza, ‘Je, inawezekana kupata ukweli kuhusu jambo lolote?’ Isitoshe, inaonekana kwamba kadiri muda unavyokwenda, ndivyo inavyokuwa vigumu zaidi kupata ukweli kuhusu mambo mengi. Kwa nini?

Watu wengi hawaamini kwamba serikali, wafanyabiashara au vyombo vya habari vinaweza kuwaambia ukweli. Wanaona kuwa vigumu kutambua ikiwa habari inayoelezwa ni ya kweli au ni maoni ya watu fulani au ikiwa habari hizo zina ukweli nusu-nusu au zimepotoshwa kabisa. Kwa sababu ya hali hiyo ya kutoaminiana na kupotoshwa kwa habari nyingi, maoni ya watu kuhusu ukweli yanatofautiana na hawatambui ikiwa ukweli unaweza kuwanufaisha katika maisha yao.

Licha ya changamoto hizo, tunaweza kupata majibu ya kweli ya maswali muhimu zaidi maishani. Jinsi gani? Kwa kutumia mbinu za kawaida maishani.

JITIHADA ZA KUTAFUTA UKWELI

Kwa kadiri fulani, wewe hutafuta ukweli kila siku. Fikiria kisa cha Jessica. Anasema hivi: “Binti yangu ana mzio unaosababishwa na karanga (nafaka). Hata kiasi kidogo tu cha karanga kinaweza kumsababishia madhara makubwa.” Kila wakati anaponunua chakula, Jessica anahitaji kuhakikisha hakitamwathiri binti yake. Anaendelea kusema: “Jambo la kwanza ninalofanya kabla ya kununua chakula ni kuangalia kwa makini bidhaa zilizotumiwa kukitayarisha. Kisha ninafanya utafiti zaidi na hata ninawasiliana na watayarishaji wa chakula hicho, ili kuthibitisha kwamba hakina hata chembe ya karanga. Pia, ninafanya utafiti kupitia vyanzo vingine vyenye kutegemeka ili kujihakikishia kwamba kampuni hiyo inategemeka.”

Inawezekana jitihada zako za kutafuta ukweli katika shughuli za kila siku zisiwe za kina kama za Jessica, lakini kama yeye unaweza kutumia mbinu zifuatazo ili kupata majibu ya maswali yako:

  • Tafuta habari kamili.

  • Fanya utafiti zaidi.

  • Hakikisha unapata habari kupitia vyanzo vinavyotegemeka.

Mbinu hizi zinaweza kukusaidia kupata majibu ya kweli ya maswali muhimu katika maisha. Jinsi gani?

KITABU CHA PEKEE CHA KWELI

Alipokuwa akitafuta majibu ya maswali muhimu maishani, Jessica alitumia mbinu zilezile ambazo hutumia anapotafuta chakula ambacho hakitamdhuru binti yake. Anasema hivi, “Kusoma kwa makini na kufanya utafiti kwa bidii kulinisaidia kupata majibu ya kweli.” Kama Jessica, mamilioni ya watu wamepata majibu ya maswali yafuatayo kwenye Biblia:

  • Kwa nini tuliumbwa?

  • Inakuwaje tunapokufa?

  • Kwa nini tunateseka?

  • Mungu anafanya nini ili kukomesha mateso?

  • Unaweza kufanya nini ili familia yako iwe na furaha?

Unaweza kupata majibu ya kweli ya maswali haya na mengine mengi kwa kusoma Biblia na kufanya utafiti zaidi kwenye tovuti ya www.pr418.com.