Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Amua Kuunga Mkono Ufalme wa Mungu!

Amua Kuunga Mkono Ufalme wa Mungu!

Wazia kimbunga kikubwa kinakaribia sana eneo lenu. Serikali inatoa onyo hili: “ONDOKENI HAPA! KIMBILIENI ENEO SALAMA!” Utafanya nini? Bila shaka utakimbilia eneo salama.

Hivi karibuni, sisi sote tutakabili “dhoruba” kubwa ya mfano ambayo Yesu aliita “dhiki kuu.” (Mathayo 24:21) Hatuwezi kuiepuka. Lakini kuna jambo tunaloweza kufanya ili kujilinda. Jambo gani?

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu Kristo aliagiza hivi: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza Ufalme na uadilifu wake.” (Mathayo 6:33) Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Tafuta kwanza Ufalme wa Mungu. Hili linamaanisha kwamba Ufalme wa Mungu unapaswa kuwa jambo muhimu zaidi maishani mwetu. (Mathayo 6:25, 32, 33) Kwa nini tunapaswa kuwa na mtazamo huo? Kwa sababu wanadamu hawawezi kusuluhisha matatizo wanayokabili. Ni Ufalme wa Mungu tu utakaosuluhisha matatizo ya wanadamu.

Tafuta uadilifu wake. Tunapaswa kujitahidi kuishi kulingana na sheria na kanuni za Mungu za uadilifu. Kwa nini? Kwa sababu ikiwa tutaamua kujiwekea viwango vyetu wenyewe vya mema na mabaya, matokeo yatakuwa mabaya. (Methali 16:25) Kwa upande mwingine, ikiwa tutaishi kulingana na viwango vya Mungu, tutampendeza Mungu na kujinufaisha wenyewe.—Isaya 48:17, 18.

Endelea kuutafuta kwanza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake. Yesu alionya kwamba baadhi ya watu watakengeushwa, na kufikiri kwamba kuwa na pesa nyingi kutawapa usalama. Wengine wanaruhusu mahangaiko ya maisha yawalemee hivi kwamba wanakosa muda wa kutafuta Ufalme wa Mungu.—Mathayo 6:19-21, 25-32.

Hata hivyo, Yesu aliahidi kwamba wale wanaounga mkono Ufalme wa Mungu watapata vitu wanavyohitaji sasa, na kufurahia baraka za milele wakati ujao.—Mathayo 6:33.

Ingawa wanafunzi wa Yesu wa karne ya kwanza walitafuta kwanza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake, bado walikabili maumivu na mateso katika maisha yao. Hata hivyo, walikuwa wakilindwa. Jinsi gani?

Wanafunzi wa Yesu waliishi kupatana na viwango vya Mungu vya uadilifu, na hilo liliwasaidia kuepuka matatizo ambayo yaliwapata wale waliopuuza viwango hivyo. Imani yao yenye nguvu kwamba Ufalme wa Mungu ungekuja, iliwasaidia kukabiliana na matatizo makubwa. Na Mungu aliwapa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili waweze kukabiliana na matatizo hayo.—2 Wakorintho 4:7-9.

JE, UTATAFUTA KWANZA UFALME?

Wakristo katika karne ya kwanza walitii amri ya Yesu ya kutafuta kwanza Ufalme. Walihubiri habari njema za Ufalme katika maeneo yote waliyoishi. (Wakolosai 1:23) Je, kuna watu wanaofanya hivyo leo?

Ndiyo! Mashahidi wa Yehova wanatambua kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utachukua hatua ya kuondoa mfumo huu wa mambo. Hivyo, wanajitahidi kadiri wanavyoweza kutii maneno haya ya Yesu: “Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.

Utatendaje ukihubiriwa habari njema? Tunakusihi uwaige wakazi wa jiji la karne ya kwanza la Beroya lililokuwa Makedonia. Waliposikia habari njema ya Ufalme kutoka kwa mtume Paulo, walikubali ujumbe huo “kwa hamu kubwa ya akili.” Kisha, ‘waliyachunguza Maandiko kwa uangalifu’ ili kuthibitisha yale waliyosikia, na walitenda kulingana na mambo waliyojifunza.—Matendo 17:11, 12.

Unaweza kufanya hivyo pia. Ukitafuta kwanza Ufalme wa Mungu na uadilifu wake, utapata ulinzi sasa na utafurahia amani yenye kudumu na usalama wakati ujao.