Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAISHA YA MKRISTO

Jinsi ya Kusitawisha Upendo kwa Mungu na Jirani

Jinsi ya Kusitawisha Upendo kwa Mungu na Jirani

Ingawa si lazima Wakristo wafuate Sheria ya Musa, zile sheria mbili kuu zaidi, yaani, kumpenda Mungu na kumpenda jirani, bado zinaonyesha mambo ambayo Yehova anataka kutoka kwetu. (Mt 22:37-39) Hatuwezi kurithi upendo kama huo. Lazima tuusitawishe. Jinsi gani? Njia moja muhimu ni kupitia kusoma Biblia kila siku. Tunapochunguza sifa mbalimbali za utu wa Mungu kama zinavyofunuliwa katika Maandiko, tunaweza kuutazama “uzuri wa Yehova.” (Zb 27:4) Kwa sababu hiyo, upendo wetu kumwelekea utaongezeka na tutaanza kufikiri kama yeye. Hilo litatuchochea kutii sheria za Mungu, kutia ndani sheria ya kuwa na upendo wa kujidhabihu kuelekea wengine. (Yoh 13:34, 35; 1Yo 5:3) Yafuatayo ni mapendekezo matatu ya kufanya usomaji wa Biblia ufurahishe hata zaidi:

  • Tumia uwezo wako wa kuwazia, na uhusishe hisi zako. Jiwazie ukiwa hapo. Unaona nini? Unasikia nini? Unanusa nini? Huenda wahusika wana hisia zipi?

  • Tumia mbinu mbalimbali. Zifuatazo ni baadhi ya mbinu hizo: Soma kwa sauti, au ufuatane na usomaji uliorekodiwa. Soma kuhusu mhusika katika Biblia au kuhusu kichwa fulani badala ya kusoma sura moja baada ya nyingine. Kwa mfano, tumia Nyongeza A7 au B12 katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya kusoma kumhusu Yesu. Soma sura nzima ambayo andiko la siku limetolewa. Soma vitabu vya Biblia kulingana na wakati vilipoandikwa.

  • Soma ili uelewe. Inafaa zaidi kusoma sura moja tu, kuielewa, na kutafakari kuihusu, kuliko kusoma sura nyingi ili tu kumaliza. Chunguza muktadha. Changanua mambo hususa yaliyotajwa. Tumia ramani na marejeo ya pambizoni. Fanya utafiti kuhusu angalau jambo moja ambalo huelewi. Ikiwezekana, muda unaotumia kutafakari uwe sawa na unaotumia kusoma.