Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 1

“Kwa Hiyo, Muende, na Mufanye Wanafunzi”

“Kwa Hiyo, Muende, na Mufanye Wanafunzi”

ANDIKO LETU LA MWAKA WA 2020: “Kwa hiyo, muende, na mufanye wanafunzi . . . , na muwabatize.”​—MT. 28:19.

WIMBO 79 Wafundishe Kusimama Imara

KIFUPI CHA HABARI *

1-2. Malaika anaambia wanamuke nini ku kaburi la Yesu, na Yesu mwenyewe anawapatia maagizo gani?

NI ASUBUI sana, tarehe 16 Mwezi wa Nisani, mwaka wa 33. Wanamuke wenye huzuni na wenye kumuogopa Mungu wanaenda ku kaburi kwenye mwili wa Bwana Yesu Kristo ulikuwa umelalishwa kumepita siku moja na nusu. Wakati wanafika ku kaburi, wako na kusudi la kutia manukato na mafuta yenye marashi ku mwili wa Yesu lakini wanashangaa kuona kama kaburi liko wazi! Malaika mumoja anaambia wanamuke hao kama Yesu amefufuliwa kutoka kwa wafu na anaongeza hivi: “Anawatangulia kuingia Galilaya. Mutamuona kule.”​—Mt. 28:1-7; Lu. 23:56; 24:10.

2 Kisha wanamuke hao kutoka ku kaburi, Yesu mwenyewe anawakaribia na anawapatia maagizo hii: “Muende, mujulishe ndugu zangu ili waende Galilaya, na kule wataniona.” (Mt. 28:10) Yesu anapaswa kuwa na maagizo fulani ya maana sana ya kupatia wanafunzi wake, juu mukutano huo njo jambo la kwanza lenye anafanya kisha ufufuo wake!

NI NANI YESU ALIPATIA AMRI YA KUFANYA WANAFUNZI?

Wakati Yesu alifanya mukutano pamoja na mitume wake na watu wengine katika Galilaya kisha ufufuo wake, aliwaamuru ‘waende . . . na kufanya wanafunzi’ (Ona fungu la 3-4)

3-4. Juu ya nini tunaweza kusema kama haiko mitume tu njo walipewa amri yenye kuwa mu Matayo 28:19, 20? (Ona picha ku jalada la gazeti hili.)

3 Soma Matayo 28:16-20. Ku mukutano huo wenye Yesu alipanga, alizungumuzia kazi ya maana yenye wanafunzi wake wangefanya wakati huo, na njo kazi yenye sisi pia tuko tunafanya leo. Yesu alisema hivi: “Kwa hiyo, muende, na mufanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na muwafundishe kushika mambo yote yenye nimewaamuru ninyi.”

4 Yesu anapenda wanafunzi wake wote wahubiri. Haiko tu mitume waaminifu 11 njo aliamuru wafanye kazi hiyo. Ni nini inatuhakikishia vile? Ni mitume tu njo walikuwa pale wakati alitoa amri ya kufanya wanafunzi ku mulima katika Galilaya? Kumbuka kama malaika aliambia wale wanamuke hivi: “Mutamuona [katika Galilaya].” Kwa hiyo, inawezekana wanamuke waaminifu walikuwa pia ku mukutano huo. Lakini haiko ile tu. Mutume Paulo anaonyesha kama Yesu “alitokea ndugu zaidi ya mia tano (500) kwa wakati mumoja.” (1 Ko. 15:6) Walikuwa wapi?

5. Andiko la 1 Wakorinto 15:6 linatufundisha nini?

5 Tuko na sababu za muzuri za kuwaza kama Paulo alikuwa anafikiria mukutano wenye ulifanywa katika Galilaya wenye kuzungumuziwa mu Matayo sura ya 28. Ni sababu gani? Sababu ya kwanza ni hii: wengi kati ya wanafunzi wa Yesu walikuwa Wagalilaya. Kwa hiyo, ingekuwa mwepesi kufanya mukutano wa watu wengi ku mulima katika Galilaya kuliko kufanya mukutano huo mu nyumba ya mutu fulani katika Yerusalemu. Sababu ya pili ni hii: kisha kufufuliwa kwake, Yesu alikuwa amekutana na mitume wake 11 katika nyumba ya mutu fulani katika Yerusalemu. Kama Yesu alipenda kuamuru mitume wake tu njo wahubiri na kufanya wanafunzi, angefanya vile katika Yerusalemu; hangeomba mitume wake na wale wanamuke na watu wengine wakutane naye katika Galilaya.​—Lu. 24:33, 36.

6. Namna gani Matayo 28:20 inaonyesha kama haiko Wakristo wa wakati wa Yesu tu njo walipewa amri ya kufanya wanafunzi, na namna gani watu wako wanatii amri hiyo leo?

6 Sababu ingine ya tatu ya maana ni hii: haiko Wakristo wenye waliishi wakati wa Yesu tu njo walipewa amri ya kufanya wanafunzi. Ni nini inaonyesha vile? Yesu alimalizia maagizo yenye alipatia wanafunzi wake kwa kusema hivi: “Niko pamoja na ninyi sikuzote mupaka umalizio wa mupangilio wa mambo.” (Mt. 28:20) Kama vile Yesu alisema, watu wengi leo wako wanafanya kazi ya kufanya wanafunzi. Fikiria kidogo jambo hili! Kila mwaka, karibu watu 300 000 wako wanakuwa wanafunzi wa Yesu Kristo, wanabatizwa, na kuwa Mashahidi wa Yehova!

7. Tutazungumuzia sasa nini, na juu ya nini?

7 Watu wengi wenye wanajifunza Biblia wanafanya maendeleo na wanafikia kubatizwa. Lakini, watu fulani wenye wanajifunza Biblia pamoja na sisi kwa ukawaida wanaogopa kuwa wanafunzi wa Yesu. Wanafurahia kujifunza Biblia, lakini hawafanye maendeleo ili wafikie kubatizwa. Kama uko unaongoza funzo la Biblia, tuko hakika kama unapenda kusaidia mwanafunzi wako atumie mambo yenye anajifunza na akuwe mwanafunzi wa Kristo. Habari hii inazungumuzia namna tunaweza kugusa moyo wa mwanafunzi wetu na namna tunaweza kumusaidia afanye maendeleo ya kiroho. Juu ya nini ni lazima tuzungumuzie jambo hilo? Juu wakati fulani, inaweza kuomba tuamue ikiwa tutaendelea kujifunza na mutu ao hapana.

UJIKAZE KUGUSA MOYO

8. Juu ya nini inaweza kuwa nguvu kugusa moyo wa mwanafunzi wetu?

8 Yehova anapenda watu wamutumikie kwa sababu wanamupenda. Kwa hiyo, kusudi letu ni kusaidia wanafunzi wetu waelewe kama Yehova anahangaikia sana kila mumoja wao na anawapenda sana. Tunapenda kuwasaidia wamuone Yehova kuwa “Baba ya watoto wenye hawana baba na mulinzi wa wajane.” (Zb. 68:5) Wakati wanafunzi wako wanafikia kuona kama Mungu anawapenda, inawezekana wataguswa moyo na watamupenda Yehova zaidi. Wanafunzi fulani wanaweza kuona kama ni nguvu kumuona Yehova kuwa Baba mwenye upendo juu baba zao hawakuwaonyesha upendo. (2 Ti. 3:1, 3) Kwa hiyo, wakati unajifunza nao, kazia sifa za muzuri sana za Yehova. Saidia wanafunzi wako waelewe kama Mungu wetu mwenye upendo anapenda wapate uzima wa milele, na iko tayari kuwasaidia wafikie kusudi hilo. Ni jambo gani lingine tunaweza kufanya?

9-10. Ni vichapo gani vyenye tunapaswa kutumia ili kuongoza mafunzo ya Biblia, na juu ya nini tunapaswa kutumia vichapo hivyo?

9 Utumie vitabu “Biblia Inatufundisha Nini?” na “Namna ya Kubakia Katika Upendo wa Mungu.” Vitabu hivyo vimeandikwa zaidi sana ili kutusaidia kugusa mioyo ya wanafunzi wetu. Kwa mufano, sura ya 1 ya kitabu Inatufundisha inajibu hii maulizo: Mungu anatuhangaikiaka?, Mungu anajisikia namna gani wakati watu wanateseka?, na Unaweza kuwa rafiki ya Yehova? Halafu kitabu Namna ya Kubakia Katika Upendo wa Mungu? Kitabu hicho kitasaidia mwanafunzi aelewe namna kutumia kanuni za Biblia kunaweza kufanya maisha yake ikuwe muzuri zaidi na kumusaidia amukaribie Yehova zaidi. Hata kama umekwisha kuongoza mafunzo mingi kwa kutumia vitabu hivyo, utayarishe muzuri kila funzo, na ufikirie mahitaji ya kila mwanafunzi.

10 Lakini, utafanya nini kama mwanafunzi anapendezwa na habari ingine yenye inapatikana katika kichapo chenye hakiko kati ya Vyombo Vyetu vya Kufundishia? Pengine unaweza kumutia moyo asome kichapo hicho yeye mwenyewe ili uendelee kuongoza funzo katika kichapo kimoja kati ya vichapo vyenye tumetaja vyenye tunaombwa kutumia ili kuongoza funzo la Biblia.

Sali kila mara mbele ya kuanza kujifunza (Ona fungu la 11)

11. Ni wakati gani tunapaswa kuanza na kumaliza funzo la Biblia kwa sala, na namna gani tunaweza kufasiria mwanafunzi juu ya nini ni muzuri kusali?

11 Sali kila mara mbele ya kuanza kujifunza. Ni muzuri kuanza na kumaliza funzo la Biblia kwa sala haraka kadiri inawezekana, kwa kawaida katika majuma fulani kisha kuanzisha funzo lenye tutakuwa tunaongoza kwa ukawaida. Tunapaswa kusaidia mwanafunzi aelewe kama ni roho takatifu ya Mungu tu njo inaweza kutusaidia kuelewa Neno la Mungu. Ndugu na dada fulani wenye kuongoza mafunzo ya Biblia wanafasiria juu ya nini tunasali mbele ya kujifunza kwa kusoma andiko la Yakobo 1:5, lenye kusema hivi: “Kama mutu yeyote kati yenu anakosa hekima, aendelee kumuomba Mungu.” Kisha wanauliza mwanafunzi hivi: “Namna gani tunaweza kumuomba Mungu hekima?” Inawezekana mwanafunzi atasema kama tunapaswa kusali kwa Mungu.

12. Namna gani unaweza kutumia Zaburi 139:2-4 ili kusaidia mwanafunzi akuwe anazungumuza na Yehova waziwazi katika sala?

12 Fundisha mwanafunzi wako namna ya kusali. Umuhakikishie kama Yehova anapenda kusikia sala zenye anatoa kwa moyo wote. Umufasirie kama katika sala zetu za kipekee, tunaweza kumuambia Yehova namna tunajisikia na kumuambia mambo yenye hatuwezi kupenda kuambia mutu mwingine yeyote. Kumbuka kama tayari Yehova anajua mawazo yetu ya ndani kabisa. (Soma Zaburi 139:2-4.) Tunaweza pia kutia moyo mwanafunzi wetu amuombe Mungu amusaidie kupiganisha mawazo ya mubaya na amusaidie kushinda tabia za mubaya. Kwa mufano, pengine mwanafunzi wako mwenye mumejifunza naye kwa wakati fulani anapenda sikukuu fulani yenye ilianzishwa na wapagani. Anajua kama ni mubaya, lakini angali anafurahia mambo fulani ya sikukuu hiyo. Umutie moyo amuelezee Yehova waziwazi namna anajisikia na kumuomba amusaidie apende tu mambo yenye Mungu anapenda.​—Zb. 97:10.

Alika mwanafunzi wako wa Biblia ahuzurie mikutano (Ona fungu la 13)

13. (a) Juu ya nini tunapaswa kualika wanafunzi wetu ku mikutano haraka kadiri inawezekana? (b) Tunaweza kufanya nini ili mwanafunzi ajisikie muzuri ku Jumba la Ufalme?

13 Alika mwanafunzi wako wa Biblia ahuzurie mikutano haraka kadiri inawezekana. Mambo yenye mwanafunzi wako anasikia na kuona ku mikutano ya Kikristo inaweza kumugusa moyo na kumusaidia afanye maendeleo ya kiroho. Umuonyeshe video Kwa Kawaida Tunafanya Nini Kwenye Jumba la Ufalme? na umualike kwa uchangumufu akuje pamoja na wewe. Kama inawezekana umusaidie kufika ku mikutano. Ni muzuri kualika ndugu na dada mbalimbali wakusindikize wakati unaenda kuongoza funzo lako. Kufanya vile kutasaidia mwanafunzi wako ajuane na wengine katika kutaniko, na inawezekana atajisikia muzuri wakati atakuja ku mikutano.

SAIDIA MWANAFUNZI WAKO AFANYE MAENDELEO YA KIROHO

14. Ni nini inaweza kuchochea mwanafunzi afanye maendeleo ya kiroho?

14 Kusudi letu ni kusaidia wanafunzi wetu wa Biblia wafanye maendeleo ya kiroho. (Efe. 4:13) Wakati mutu fulani anakubali kujifunza Biblia, pengine anapendezwa kwanza na namna funzo litamuletea faida kipekee. Lakini, wakati upendo wake kwa Yehova unaendelea kukomaa, pengine ataanza kufikiria namna anaweza kusaidia wengine, kutia ndani wale wenye tayari wako katika kutaniko. (Mt. 22:37-39) Wakati inafaa kufanya vile, usisite kuambia mwanafunzi wako kama tuko na daraka la kutegemeza kazi ya Ufalme kupitia michango ya feza.

Fundisha mwanafunzi wako mambo ya kufanya wakati matatizo inatokea (Ona fungu la 15)

15. Tunaweza kufanya nini ili kusaidia mwanafunzi wa Biblia afanye mambo yenye kuwa sawa wakati matatizo inatokea?

15 Fundisha mwanafunzi wako wa Biblia mambo ya kufanya wakati matatizo inatokea. Kwa mufano, pengine mwanafunzi wako ni muhubiri mwenye hajabatizwa na anakuambia kama mutu fulani katika kutaniko amemukwaza. Usimuambie ni nani mwenye iko na makosa ao nani mwenye hana makosa, lakini umuonyeshe mambo yenye Biblia inasema yenye anapaswa kufanya. Anaweza kusamehe ndugu ao dada yake, ao kama hawezi kuachilia mambo, anaweza kuzungumuza kwa upole na upendo na mutu huyo; na kusudi lake linapaswa kuwa ‘kumupata ndugu yake.’ (Linganisha na Matayo 18:15.) Usaidie mwanafunzi wako kutayarisha mambo yenye atasema. Umuonyeshe namna ya kutumia JW Library®, kitabu Musaada wa Kutafuta Habari kwa Ajili ya Mashahidi wa Yehova, na jw.org® ili kujua namna anaweza kushugulikia ile hali. Kama anajifunza namna ya kumaliza kukosa kuelewana na wengine mbele abatizwe, inawezekana kabisa atakuwa na uhusiano wa muzuri pamoja na wengine kisha kubatizwa.

16. Juu ya nini ni muzuri kuomba wahubiri wengine wakusindikize wakati unaenda kuongoza funzo la Biblia?

16 Omba wengine katika kutaniko, na pia mwangalizi wa muzunguko wakati anatembelea kutaniko, wakusindikize wakati unaenda kujifunza na mwanafunzi. Juu ya nini? Zaidi ya sababu zenye tumekwisha kuzungumuzia, wahubiri wengine wanaweza kusaidia mwanafunzi katika namna yenye hauwezi kuweza. Kwa mufano, pengine mwanafunzi wako amejikaza sana ili aache kuvuta tumbako lakini ameshindwa mara mingi. Uombe Shahidi mwenye aliweza kuachana na ile tabia kisha kushindwa mara mingi, akusindikize wakati unaenda kuongoza funzo hilo la Biblia. Shahidi mwenzako anaweza kutoa mashauri yenye mwanafunzi wako iko na lazima ya kusikia. Kama unaogopa kuongoza funzo mbele ya ndugu ao dada mwenye kuwa na uzoefu, umuambie yeye aongoze funzo siku hiyo. Wakati unaomba wengine wakusindikize wakati unaenda kujifunza na mwanafunzi wako wa Biblia, anaweza kupata faida kupitia uzoefu wao. Kumbuka kama, kusudi letu ni kusaidia mwanafunzi afanye maendeleo ya kiroho.

NINAPASWA KUACHA KUJIFUNZA NA MUTU FULANI?

17-18. Unapaswa kufikiria nini wakati unaamua ikiwa utaacha kujifunza na mwanafunzi fulani?

17 Kama mwanafunzi wako wa Biblia hafanye maendeleo, wakati fulani unaweza kujiuliza hivi: ‘Ninapaswa kuacha kujifunza naye?’ Wakati unachunguza jambo hilo, unapaswa kufikiria uwezo wa mutu huyo. Inaomba wakati mingi ili watu fulani wafanye maendeleo. Ujiulize hivi: ‘Mwanafunzi wangu iko anafanya maendeleo kwa kiasi fulani kulingana na hali yake?’ ‘Ameanza “kushika,” ao kutumia katika maisha yake, mambo yote yenye iko anajifunza?’ (Mt. 28:20) Inaweza kuomba wakati murefu ili mutu akuwe mwanafunzi. Lakini anapaswa kufanya mabadiliko hatua kwa hatua katika maisha yake.

18 Lakini, halafu kama mutu mwenye tumejifunza naye kwa wakati fulani haonyeshe kama anapendezwa kabisa na funzo? Fikiria hali hii: Mwanafunzi wako amemaliza kitabu Inatufundisha na pengine hata ameanza kitabu Upendo wa Mungu, lakini hajafika ku mukutano hata moja wa kutaniko, ao hata ku Ukumbusho! Na mara mingi haheshimie programu ya kujifunza juu ya sababu zenye haziko za maana. Katika hali hiyo, inaomba kuzungumuza waziwazi na mwanafunzi wako. *

19. Ni mambo gani yenye unaweza kuambia mutu mwenye haonyeshe kabisa kama anapendezwa na funzo la Biblia, na unapaswa kufikiria nini?

19 Unaweza kuanza kwa kumuuliza hivi: “Ni jambo gani la nguvu sana lenye unapaswa kufanya ili ukuwe Shahidi wa Yehova?” Mwanafunzi anaweza kujibu hivi: “Ninapenda kujifunza Biblia, lakini sitakuwaka Shahidi wa Yehova hata siku moja!” Kama ile njo mawazo yenye iko nayo kisha kujifunza kwa wakati fulani, hakuna sababu ya kuendelea kujifunza na mwanafunzi huyo. Ao pengine kwa mara ya kwanza, mwanafunzi wako anaweza kufunua mambo yenye kumuzuia asifanye maendeleo. Kwa mufano, pengine anawaza kama hawezi kuhubiri nyumba kwa nyumba. Sasa, kisha kujua mawazo yake, utajua muzuri namna ya kumusaidia.

Usitumie wakati mingi ili kuongoza funzo lenye halifanye maendeleo (Ona fungu la 20)

20. Namna gani kuelewa maneno yenye kuwa katika Matendo 13:48 kunatusaidia kuamua ikiwa tutaacha kuongoza funzo fulani ao hapana?

20 Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, wanafunzi fulani wa Biblia wako kama Waisraeli wa siku za Ezekieli. Juu yao, Yehova alimuambia Ezekieli hivi: “Angalia! Wewe ni kama wimbo wa mapenzi kwao, wenye kuimbwa kwa sauti ya muzuri na kuchezwa kwa ufundi kwa chombo cha kamba. Watasikia maneno yako, lakini hakuna mutu yeyote mwenye atayatenda.” (Eze. 33:32) Inaweza kuwa nguvu kuambia mutu kama tutaacha kujifunza naye. Lakini, “wakati wenye unabakia umepunguka.” (1 Ko. 7:29) Kuliko kutumia wakati mingi ili kuongoza funzo lenye halifanye maendeleo, tunapaswa kutafuta mutu mwenye kuonyesha kama iko na “muelekeo wenye kufaa kwa ajili ya uzima wa milele.”​—Soma Matendo 13:48.

Kunaweza kuwa watu katika eneo lako wenye wanasali ili wapate musaada (Ona fungu la 20)

21. Andiko letu la mwaka wa 2020 ni andiko gani, na juu ya nini linafaa?

21 Katika mwaka 2020, andiko letu la mwaka litatusaidia tufikirie namna tunaweza kufanya muzuri zaidi kazi yetu ya kufanya wanafunzi. Liko na maneno fulani yenye Yesu alisema wakati wa mukutano wa maana wenye ulifanywa kwenye mulima katika Galilaya. Alisema hivi: “Kwa hiyo, muende, na mufanye wanafunzi . . . , na muwabatize.”​Mt. 28:19.

Tujikaze kufikiria namna tunaweza kufanya muzuri zaidi kazi yetu ya kufanya wanafunzi na kusaidia wanafunzi wetu wafikie kubatizwa (Ona fungu la 21)

WIMBO 70 Tafuteni Wanaostahili

^ fu. 5 Andiko letu la mwaka wa 2020 linatutia moyo ‘tufanye wanafunzi.’ Watumishi wote wa Yehova wanapaswa kutii amri hiyo. Namna gani tunaweza kugusa mioyo ya wanafunzi wetu ili wakuwe wanafunzi wa Kristo? Habari hii itatuonyesha namna tunaweza kusaidia wanafunzi wetu wa Biblia wamukaribie Yehova zaidi. Tutazungumuzia pia namna ya kuamua ikiwa tutaendelea kujifunza Biblia na mutu fulani ao hapana.

^ fu. 18 Angalia ku JW Télédiffusion video Kuacha Kuongoza Mafunzo Yenye Haifanye Maendeleo.