Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 4

“Roho Yenyewe Hutoa Ushahidi”

“Roho Yenyewe Hutoa Ushahidi”

“Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu.”​—ROM. 8:16.

WIMBO 25 Mali ya Pekee

MUHTASARI *

Katika siku ya Pentekoste, Yehova aliwamiminia roho yake takatifu kwa njia ya pekee Wakristo 120 hivi (Tazama fungu la 1 na 2)

1-2. Ni tukio gani la pekee linalotokea siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?

NI JUMAPILI asubuhi huko Yerusalemu. Ni siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kikundi cha wanafunzi 120 kimekusanyika kwenye chumba cha juu. (Mdo. 1:13-15; 2:1) Siku chache zilizopita, Yesu alikuwa amewaagiza wabaki Yerusalemu kwa sababu wangepokea zawadi ya pekee. (Mdo. 1:4, 5) Ni nini kinachotokea?

2 ‘Ghafla kunatokea kelele kutoka mbinguni, kama ya upepo wenye nguvu unaovuma.’ Sauti hiyo inajaa nyumba yote. Kisha “ndimi kama za moto” zinaonekana juu ya vichwa vya wanafunzi hao, na wote ‘wanajazwa roho takatifu.’ (Mdo. 2:2-4) Yehova anatumia njia hiyo ya pekee kukijaza kikundi hicho roho yake takatifu. (Mdo. 1:8) Wanakuwa watu wa kwanza kutiwa mafuta kwa roho takatifu * na kupewa tumaini la kutawala pamoja na Yesu mbinguni.

NI NINI AMBACHO HUTUKIA MTU ANAPOTIWA MAFUTA?

3. Kwa nini wanafunzi katika siku ya Pentekoste hawakuwa na shaka kwamba walikuwa wametiwa mafuta kwa roho takatifu?

3 Ikiwa ungekuwa miongoni mwa wanafunzi hao waliokusanyika katika chumba cha juu, usingesahau kamwe siku hiyo. Kitu fulani kinachofanana na ndimi za moto kinakuja na kutua juu ya kichwa chako, nawe unaanza kusema katika lugha mbalimbali! (Mdo. 2:5-12) Ni wazi kwamba hungekuwa na shaka kwamba umetiwa mafuta kwa roho takatifu. Lakini, je, wale wote wanaotiwa mafuta kwa roho takatifu wanapokea roho hiyo kwa njia ileile? Hapana. Tunajuaje?

4. Watiwa-mafuta katika karne ya kwanza walipokea mwito wao wakati gani? Eleza.

4 Acheni tuzungumzie suala la wakati. Si kikundi hicho pekee cha Wakristo 120 hivi kilichotiwa mafuta kwa roho takatifu siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K. Baadaye siku hiyo, watu wengine 3,000 hivi walipokea roho takatifu. Walitiwa mafuta kwa roho takatifu walipobatizwa. (Mdo. 2:37, 38, 41) Katika miaka iliyofuata, si Wakristo wote watiwa-mafuta waliotiwa mafuta siku ya ubatizo. Wasamaria walitiwa mafuta wakati fulani baada ya kubatizwa. (Mdo. 8:14-17) Katika kisa cha pekee, Kornelio na watu wa nyumba yake walitiwa mafuta hata kabla ya kubatizwa.—Mdo. 10:44-48.

5. Kulingana na 2 Wakorintho 1:21, 22, ni nini ambacho hutokea mtu anapotiwa mafuta kwa roho takatifu?

5 Pia, acheni tuzungumzie kinachotokea mtu anapotiwa mafuta kwa roho takatifu. Mwanzoni, huenda baadhi ya watiwa-mafuta wakasita kukubali kwamba Yehova amewachagua. Huenda wakajiuliza, ‘Kwa nini Mungu amenichagua mimi?’ Huenda wengine wasihisi hivyo. Vyovyote vile, mtume Paulo anaeleza kinachowapata watiwa-mafuta wote: “Baada ya kuamini, mlitiwa muhuri * kupitia kwake kwa roho takatifu iliyoahidiwa, ambayo ni rehani ya mapema ya urithi wetu.” (Efe. 1:13, 14; maelezo ya chini) Hivyo, Yehova anatumia roho yake takatifu kuwajulisha waziwazi Wakristo hao kwamba amewachagua. Kwa njia hiyo, roho takatifu ni “rehani [dhamana au ahadi]” inayotolewa ili kuwahakikishia kwamba wataishi milele mbinguni wakati ujao.—Soma 2 Wakorintho 1:21, 22.

6. Ni lazima Mkristo mtiwa-mafuta afanye nini ili apate thawabu yake ya kwenda mbinguni?

6 Ikiwa Mkristo ametiwa mafuta kwa roho takatifu, je, inamaanisha kwamba lazima ataenda mbinguni? Hapana. Ana uhakika kwamba amechaguliwa kwenda mbinguni. Hata hivyo, lazima akumbuke himizo hili: “Akina ndugu, jitahidini hata zaidi ili kufanya mwito na kuchaguliwa kwenu kuwe hakika kwa ajili yenu wenyewe, kwa maana mkiendelea kufanya mambo hayo, hamtashindwa kamwe.” (2 Pet. 1:10) Hivyo, ingawa Mkristo mtiwa-mafuta amechaguliwa, au amepata mwito wa kwenda mbinguni, atapata thawabu yake ikiwa tu ataendelea kuwa mwaminifu.—Flp. 3:12-14; Ebr. 3:1; Ufu. 2:10.

MTU ANAJUAJE KWAMBA AMETIWA MAFUTA KWA ROHO TAKATIFU?

7. Watiwa-mafuta wanajuaje kwamba wana mwito wa kwenda mbinguni?

7 Mtu anajuaje kwamba ana mwito wa kwenda mbinguni? Jibu linapatikana katika maneno ya Paulo kwa ndugu waliokuwa Roma ambao ‘waliitwa wawe watakatifu.’ Aliwaambia hivi: “Hamkupokea roho ya utumwa inayosababisha woga tena, bali mlipokea roho ya kufanywa kuwa wana, roho ambayo kupitia hiyo tunapaza sauti: ‘Abba, Baba!’ Roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu.” (Rom. 1:7; 8:15, 16) Hivyo, kupitia roho yake takatifu, Mungu anawajulisha waziwazi watiwa-mafuta kwamba wana mwito wa kwenda mbinguni.—1 The. 2:12.

8. Andiko la 1 Yohana 2:20, 27 linaonyeshaje kwamba Wakristo watiwa-mafuta hawahitaji uthibitisho kutoka kwa watu wengine kwamba wametiwa mafuta?

8 Yehova huondoa shaka yoyote katika akili na mioyo ya wale wanaopokea mwaliko wa kwenda mbinguni. (Soma 1 Yohana 2:20, 27.) Bila shaka, Wakristo watiwa-mafuta wanahitaji kufundishwa na Yehova kupitia kutaniko kama tu watu wengine. Lakini hawahitaji mtu yeyote awathibitishie kwamba wametiwa mafuta. Yehova ametumia nguvu kubwa zaidi katika ulimwengu wote, yaani, roho yake takatifu, kuwathibitishia wazi kwamba wametiwa mafuta!

‘WANAZALIWA UPYA’

9. Kama inavyotajwa katika Waefeso 1:18, ni mabadiliko gani yanayompata mtu anapotiwa mafuta?

9 Huenda ikawa vigumu kwa watumishi wengi wa Mungu leo kuelewa kinachotokea Mungu anapomtia mtu mafuta kwa roho. Hilo ni jambo la kawaida kwa sababu wao wenyewe hawajatiwa mafuta kwa roho. Mungu aliwaumba wanadamu waishi milele duniani na si mbinguni. (Mwa. 1:28; Zab. 37:29) Hata hivyo, Yehova amewachagua baadhi ya watu wakaishi mbinguni. Hivyo, anapowatia mafuta kwa roho, anabadilisha kabisa tumaini lao na njia yao ya kufikiri ili watazamie kwa hamu kuishi mbinguni.—Soma Waefeso 1:18.

10. ‘Kuzaliwa tena’ kunamaanisha nini? (Tazama pia maelezo ya chini.)

10 Wakristo wanapotiwa mafuta kwa roho takatifu, ‘wanazaliwa tena,’ au ‘wanazaliwa kutoka juu.’ * Pia, Yesu alionyesha kwamba ni vigumu kumweleza kihususa mtu ambaye hajatiwa mafuta jinsi mtu ‘aliyezaliwa tena’ au ‘aliyezaliwa kwa roho’ anavyohisi.—Yoh. 3:3-8; maelezo ya chini.

11. Eleza jinsi ambavyo njia ya kufikiri ya mtu aliyetiwa mafuta hubadilika.

11 Mkristo anapotiwa mafuta, njia yake ya kufikiri hubadilika jinsi gani? Kabla ya kutiwa mafuta na Yehova, Wakristo hao walikuwa na tumaini la kuishi milele duniani. Walikuwa wakitazamia kwa hamu kubwa sana wakati ambapo Yehova ataondoa uovu wote na kuifanya dunia kuwa paradiso. Huenda waliwazia jinsi watakavyowakaribisha watu wa familia au marafiki watakaofufuliwa. Lakini baada ya kutiwa mafuta, walianza kufikiri kwa njia tofauti. Kwa nini? Si kwa sababu hawakuridhishwa na tumaini la kuishi duniani. Wala hawakubadili njia yao ya kufikiri kwa sababu ya mkazo au matatizo ya kihisia. Na hawakuhisi ghafla kwamba kuishi milele duniani kungekuwa jambo lenye kuchosha. Badala yake, Yehova alitumia roho yake takatifu kubadili njia yao ya kufikiri na tumaini walilotazamia kwa hamu.

12. Kulingana na 1 Petro 1:3, 4, Wakristo watiwa-mafuta wanahisije kuhusu tumaini lao?

12 Huenda mtu aliyetiwa mafuta akahisi kwamba hastahili pendeleo hilo la pekee. Lakini hana shaka hata kidogo kwamba Yehova amemchagua. Moyo wake hufurika kwa shangwe na shukrani anapotafakari kuhusu tumaini lake la wakati ujao.—Soma 1 Petro 1:3, 4.

13. Watiwa-mafuta wanahisije kuhusu maisha yao hapa duniani?

13 Je, hilo linamaanisha kwamba watiwa-mafuta wanatamani kufa? Mtume Paulo anajibu swali hilo. Analinganisha mwili wa binadamu na hema na kusema hivi: “Kwa kweli, sisi tulio katika hema hili tunaugua, tukilemewa kwa sababu hatutaki kuuvua huu, bali tunataka kuuvaa ule mwingine, ili uhai ukimeze kile kinachoweza kufa.” (2 Kor. 5:4) Wakristo hao hawajapoteza hamu ya kuishi wala hawatamani kufa haraka. Kinyume chake, wanafurahia kuishi na wanatamani kutumia kila siku kumtumikia Yehova wakiwa pamoja na familia na marafiki. Hata hivyo, haidhuru wanafanya nini, hawawezi kuacha kukumbuka tumaini lao tukufu la wakati ujao.—1 Kor. 15:53; 2 Pet. 1:4; 1 Yoh. 3:2, 3; Ufu. 20:6.

JE, YEHOVA AMEKUTIA MAFUTA?

14. Ni mambo gani ambayo hayathibitishi kwamba mtu ametiwa mafuta kwa roho takatifu?

14 Huenda unajiuliza ikiwa umetiwa mafuta kwa roho takatifu au la. Ikiwa ndivyo, fikiria maswali haya muhimu: Je, una tamaa yenye nguvu ya kufanya mapenzi ya Yehova? Je, unahisi kwamba una bidii sana katika kazi ya kuhubiri? Je, wewe ni mwanafunzi makini wa Neno la Mungu na anayependa kuchunguza “mambo mazito ya Mungu”? (1 Kor. 2:10) Je, unahisi kwamba Yehova amekupatia matokeo mazuri katika kazi ya kuhubiri? Je, unahisi kutoka moyoni kwamba una jukumu la kuwasaidia wengine kiroho? Je, umejionea uthibitisho wa kwamba Yehova amekusaidia katika njia nyingi hususa maishani mwako? Ikiwa jibu la maswali hayo ni ndiyo, je, huo ni uthibitisho kwamba una mwito wa kwenda mbinguni? Hapana. Kwa nini? Kwa sababu watumishi wote wa Mungu wanaweza kuhisi hivyo, iwe wametiwa mafuta au la. Na kupitia roho yake takatifu, Yehova anaweza kumpa mtumishi wake yeyote nguvu ya kutimiza mambo hayo hata iwe ana tumaini gani. Kwa kweli, ikiwa una shaka kama umetiwa mafuta kwa roho takatifu, hilo pekee linaonyesha kwamba hujatiwa mafuta. Wale ambao wamepokea mwito kutoka kwa Yehova hawana shaka lolote kwamba wametiwa mafuta! Wanajua!

Yehova alitumia roho yake takatifu kumpa Abrahamu, Sara, Daudi, na Yohana Mbatizaji uwezo wa kufanya mambo makubwa, lakini hakutumia roho hiyo kuwapa tumaini la kuishi mbinguni (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. Tunajuaje kwamba si wote waliopokea roho ya Mungu wamechaguliwa kwenda mbinguni?

15 Katika Biblia kuna mifano mingi ya watu wenye imani waliopewa roho takatifu lakini hawakuwa na tumaini la kuishi mbinguni. Daudi aliongozwa na roho takatifu. (1 Sam. 16:13) Roho takatifu ilimsaidia kuelewa mambo mazito kumhusu Yehova na ilimwongoza kuandika sehemu fulani za Biblia. (Marko 12:36) Hata hivyo, mtume Petro alisema kwamba Daudi “hakupanda mbinguni.” (Mdo. 2:34) Yohana Mbatizaji ‘alijazwa roho takatifu.’ (Luka 1:13-16) Yesu alisema kwamba hakuna mtu aliyekuwa mkuu kuliko Yohana, lakini pia akasema kwamba Yohana hangekuwa na sehemu katika Ufalme wa mbinguni. (Mt. 11:10, 11) Yehova alitumia roho yake takatifu kuwapa watu hao uwezo wa kutimiza mambo makubwa, lakini hakutumia roho hiyo kuwachagua ili wakaishi mbinguni. Je, hilo linamaanisha kwamba uaminifu wao ulikuwa mdogo kuliko wa wale waliochaguliwa kutawala mbinguni? Hapana. Inamaanisha tu kwamba Yehova atawafufua ili waishi katika Paradiso duniani.—Yoh. 5:28, 29; Mdo. 24:15.

16. Watumishi wengi wa Mungu leo wanatazamia kwa hamu thawabu gani?

16 Watumishi wengi wa Mungu duniani leo hawana tumaini la kuishi mbinguni. Kama Abrahamu, Sara, Daudi, Yohana Mbatizaji, na wanaume na wanawake wengine wengi wa nyakati za Biblia, wanatazamia kwa hamu kuishi duniani wakati ambapo Ufalme wa Mungu utatawala.—Ebr. 11:10.

17. Tutazungumzia maswali gani katika makala inayofuata?

17 Kwa kuwa baadhi ya watiwa-mafuta bado wako miongoni mwa watu wa Mungu leo, maswali fulani huzuka. (Ufu. 12:17) Kwa mfano, watiwa-mafuta wanapaswa kuwa na maoni gani kujihusu? Ikiwa mtu katika kutaniko lenu anaanza kushiriki mifano kwenye Ukumbusho, unapaswa kumtendeaje? Na vipi ikiwa idadi ya wale wanaosema kwamba wametiwa mafuta inazidi kuongezeka? Je, unapaswa kuhangaishwa na jambo hilo? Maswali hayo yatajibiwa katika makala inayofuata.

^ fu. 5 Tangu Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Yehova amewapatia baadhi ya Wakristo tumaini zuri ajabu—tumaini la kutawala pamoja na Mwana wake mbinguni. Hata hivyo, Wakristo hao wanajuaje kwamba wamechaguliwa ili wapate pendeleo hilo la pekee? Ni nini ambacho hutukia mtu anapopata mwaliko huo? Makala hii inategemea makala ya Mnara wa Mlinzi ya Januari 2016 na itajibu maswali hayo yenye kusisimua.

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Kutiwa mafuta kwa roho takatifu: Yehova anatumia roho yake takatifu kumchagua mtu ili akatawale pamoja na Yesu mbinguni. Kwa kutumia roho yake, Mungu anampa mtu huyo ahadi ya wakati ujao, au “rehani ya mapema.” (Efe. 1:13, 14) Wakristo wanaotiwa mafuta wanaweza kusema kwamba roho takatifu “hutoa ushahidi,” au huwajulisha waziwazi kwamba thawabu yao ni ya mbinguni.—Rom. 8:16.

^ fu. 5 UFAFANUZI WA MANENO: Muhuri. Mkristo mtiwa-mafuta hatiwi muhuri wa kudumu hadi wakati fulani kabla ya kufa akiwa mwaminifu au wakati fulani kabla ya dhiki kuu kuanza.—Efe. 4:30; Ufu. 7:2-4; tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 2016.

^ fu. 10 Kwa maelezo zaidi kuhusu maana ya “kuzaliwa tena,” tazama gazeti Mnara wa Mlinzi, Aprili 1, 2009, uku. 3-12.

WIMBO 27 Kufunuliwa kwa Wana wa Mungu

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Iwe tumefungwa gerezani kwa sababu ya imani yetu au tuko huru kuhubiri na kufundisha kweli, tunaweza kutazamia kwa hamu kuishi duniani wakati ambapo Ufalme wa Mungu utatutawala.