Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 5

Tutaenda Pamoja Nanyi

Tutaenda Pamoja Nanyi

“Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.”—ZEK. 8:23.

WIMBO 26 Mlinitendea Mimi

MUHTASARI *

Kondoo wengine (“watu kumi”) wana pendeleo la kumwabudu Yehova pamoja na watiwa-mafuta (“Myahudi”) (Tazama fungu la 1 na 2)

1. Ni jambo gani ambalo Yehova alitabiri kwamba lingetendeka wakati wetu?

YEHOVA alitabiri hivi kuhusu wakati wetu: “Watu kumi kutoka katika lugha zote za mataifa watashika, naam, watashika kwa nguvu joho la Myahudi, wakisema: ‘Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.’” (Zek. 8:23) Hapa “Myahudi” anawakilisha wale ambao Mungu amewatia mafuta kwa roho takatifu. Pia, wanaitwa “Israeli wa Mungu.” (Gal. 6:16) “Watu kumi” wanawakilisha wale walio na tumaini la kuishi milele duniani. Wanajua kwamba Yehova amekichagua kikundi hicho cha watiwa-mafuta na wanahisi kwamba ni pendeleo kumwabudu yeye pamoja nao.

2. ‘Watu kumi wanaenda pamoja’ na watiwa-mafuta jinsi gani?

2 Hata ingawa si rahisi kujua majina ya kila mtiwa-mafuta aliye duniani leo, * wale walio na tumaini la kuishi duniani wanaweza “kwenda pamoja” na watiwa-mafuta. Jinsi gani? Biblia inasema kwamba “watu kumi [wangeshika] kwa nguvu joho la Myahudi, wakisema: ‘Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa maana tumesikia kwamba Mungu yupo pamoja nanyi.’” Sehemu ya kwanza ya mstari huo wa Biblia inataja Myahudi mmoja. Lakini sehemu inayofuata inatumia kiwakilishi “nanyi.” Hilo linamaanisha kwamba Myahudi huyo si mtu mmoja, bali anawakilisha kikundi kizima cha watiwa-mafuta. Wale ambao hawajatiwa mafuta wanamtumikia Yehova pamoja na watiwa-mafuta. Hata hivyo, hawawaoni watiwa-mafuta kuwa viongozi wao, bali wanatambua kwamba Yesu ndiye Kiongozi wao.—Mt. 23:10.

3. Tutajibu maswali gani katika makala hii?

3 Kwa kuwa bado kuna Wakristo watiwa-mafuta miongoni mwa watu wa Mungu leo, huenda wengine wakajiuliza: (1) Wakristo watiwa-mafuta wanapaswa kuwa na maoni gani kujihusu? (2) Wale wanaoshiriki mifano kwenye Ukumbusho wanapaswa kutendewa jinsi gani? (3) Je, tuhangaishwe ikiwa idadi ya wanaoshiriki mifano inaongezeka? Makala hii itajibu maswali hayo.

WATIWA-MAFUTA WANAPASWA KUWA NA MAONI GANI KUJIHUSU?

4. Ni onyo gani linalopatikana kwenye 1 Wakorintho 11:27-29 ambalo watiwa-mafuta wanapaswa kuchukulia kwa uzito, na kwa nini?

4 Watiwa-mafuta wanapaswa kuchukulia kwa uzito onyo linalopatikana kwenye 1 Wakorintho 11:27-29. (Soma.) Ni katika njia gani mtiwa-mafuta anaweza kula mifano ya Ukumbusho “isivyofaa”? Atakuwa akila mifano hiyo isivyofaa ikiwa haishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Yehova. (Ebr. 6:4-6; 10:26-29) Watiwa-mafuta wanatambua kwamba ni lazima waendelee kuwa waaminifu ikiwa wanataka kupokea “tuzo ya mwito wa Mungu wa kwenda juu kupitia Kristo Yesu.”—Flp. 3:13-16.

5. Wakristo watiwa-mafuta wanapaswa kuwa na maoni gani kujihusu?

5 Roho takatifu ya Yehova huwasaidia watumishi wake wawe wanyenyekevu, na si wenye kiburi. (Efe. 4:1-3; Kol. 3:10, 12) Hivyo, watiwa-mafuta hawajioni kuwa bora kuliko wengine. Wanajua kwamba haimaanishi kuwa Yehova huwapatia watiwa-mafuta roho takatifu zaidi kuliko watumishi wake wengine. Hawahisi kwamba wana uelewaji wenye kina zaidi wa kweli za Biblia kuliko mtu mwingine yeyote. Na hawawezi kamwe kumwambia mtu mwingine kwamba ametiwa mafuta na anapaswa kuanza kushiriki mifano kwenye Ukumbusho. Badala yake, wanatambua kwa unyenyekevu kwamba ni Yehova pekee anayewaalika watu kwenda mbinguni.

6. Kulingana na 1 Wakorintho 4:7, 8, Wakristo watiwa-mafuta wanapaswa kujiendeshaje?

6 Ingawa watiwa-mafuta wanaona kuwa ni pendeleo kupata mwaliko wa kwenda mbinguni, hawatarajii wengine wawatendee kwa njia ya pekee. (Flp. 2:2, 3) Pia, wanajua kwamba Yehova alipowatia mafuta, hakuwajulisha wengine. Hivyo, mtu aliyetiwa mafuta hawezi kushangaa ikiwa wengine hawaamini mara moja kwamba ametiwa mafuta. Anatambua kwamba Biblia inatuambia tusiwe wepesi wa kumwamini mtu anayesema kwamba Mungu amempa jukumu la pekee. (Ufu. 2:2) Kwa kuwa hangependa kujielekezea fikira, Mkristo mtiwa-mafuta hatawaambia watu anaokutana nao kwa mara ya kwanza kwamba yeye ni mtiwa-mafuta. Na bila shaka hatajigamba kwa wengine kuhusu jambo hilo.—Soma 1 Wakorintho 4:7, 8.

7. Watiwa-mafuta wataepuka kufanya nini, na kwa nini?

7 Wakristo watiwa-mafuta hawahisi kwamba wanapaswa kushirikiana tu na watiwa-mafuta wenzao, kana kwamba wao ni washiriki wa kikundi fulani cha pekee. Hawawatafuti watiwa-mafuta wenzao wakiwa na lengo la kuzungumzia kutiwa kwao mafuta au kuanzisha vikundi vya kujifunza Biblia pamoja. (Gal. 1:15-17) Kutaniko halingekuwa na umoja ikiwa watiwa-mafuta wangefanya mambo hayo. Wangekuwa wakitenda kinyume cha roho takatifu, ambayo huwasaidia watu wa Mungu kuwa na amani na umoja.—Rom. 16:17, 18.

WATIWA-MAFUTA WANAPASWA KUTENDEWAJE?

Hatupaswi kuwatendea watiwa-mafuta au wengine wanaoongoza kana kwamba wao ni watu mashuhuri (Tazama fungu la 8) *

8. Kwa nini unahitaji kuwa mwangalifu kuhusu jinsi unavyowatendea wale wanaoshiriki mifano kwenye Ukumbusho? (Tazama pia maelezo ya chini.)

8 Tunapaswa kuwatendeaje ndugu na dada waliotiwa mafuta? Lingekuwa kosa kumkweza mtu kupita kiasi, hata ikiwa yeye ni ndugu ya Kristo ambaye ametiwa mafuta. (Mt. 23:8-12) Biblia inapozungumzia wazee wa kutaniko, inatutia moyo ‘tuige imani yao,’ lakini haituambii kwamba tunaweza kumfanya mwanadamu yeyote kuwa kiongozi wetu. (Ebr. 13:7) Ni kweli kwamba Biblia inasema kuwa wengine “wanastahili heshima mara mbili.” Hiyo ni kwa sababu ‘wanasimamia kwa njia nzuri’ na ‘wanafanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha,’ na si kwa sababu wametiwa mafuta. (1 Tim. 5:17) Ikiwa tutawasifu au kuwaelekezea uangalifu watiwa-mafuta kupita kiasi, tutawafanya wasijihisi huru. * Na jambo baya hata zaidi, tunaweza kusababisha wawe na kiburi. (Rom. 12:3) Hakuna yeyote kati yetu ambaye angependa kufanya jambo lolote linaloweza kusababisha ndugu za Kristo waliotiwa mafuta wafanye kosa zito kama hilo!—Luka 17:2.

9. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawaheshimu Wakristo watiwa-mafuta?

9 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawaheshimu wale waliotiwa mafuta na Yehova? Hatutawaomba watueleze jinsi walivyotiwa mafuta. Hilo ni jambo la kibinafsi, ambalo hatuna haki ya kulijua. (1 The. 4:11; 2 The. 3:11) Na hatupaswi kufikia mkataa kwamba mume au mke, wazazi, au watu wengine wa familia wametiwa mafuta pia. Mtu harithi tumaini lake la kwenda mbinguni kutoka kwa familia yake. Analipokea kutoka kwa Mungu. (1 The. 2:12) Pia, tunapaswa kuepuka kuuliza maswali yanayoweza kuwaumiza wengine. Kwa mfano, haingefaa kumuuliza mke wa ndugu aliyetiwa mafuta kuhusu jinsi anavyohisi kuhusu tumaini lake la kuishi duniani milele bila mume wake. Isitoshe, tuna uhakika kabisa kwamba katika ulimwengu mpya, Yehova ‘atatosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’—Zab. 145:16.

10. Tunajilindaje wenyewe tunapoepuka “kuwastaajabia watu”?

10 Ikiwa hatutawatendea watiwa-mafuta kwa njia inayoonyesha kwamba wao ni muhimu sana kuliko wengine, tutajilinda wenyewe. Jinsi gani? Biblia inatuambia kwamba huenda baadhi ya watiwa-mafuta wasiendelee kuwa waaminifu. (Mt. 25:10-12; 2 Pet. 2:20, 21) Lakini ikiwa tutaepuka “kuwastaajabia watu,” hatutakuwa wafuasi wa watu, iwe ni watiwa-mafuta au Wakristo wanaojulikana sana au wale ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu. (Yuda 16, maelezo ya chini) Hivyo, wakikosa kuwa waaminifu au wakiliacha kutaniko, hatutapoteza imani yetu kwa Yehova au kuacha kumtumikia.

JE, TUNAPASWA KUHANGAISHWA NA IDADI YA WALE WANAOSHIRIKI MIFANO?

11. Hali imekuwaje kuhusiana na idadi ya wale wanaoshiriki mifano kwenye Ukumbusho?

11 Kwa miaka mingi, idadi ya wale wanaoshiriki mifano kwenye Ukumbusho ilikuwa ikipungua. Lakini katika miaka ya hivi karibuni, idadi hiyo imekuwa ikiongezeka kila mwaka. Je, tunapaswa kuhangaishwa na jambo hilo? Hapana. Acheni tuchunguze mambo fulani tunayopaswa kuzingatia.

12. Kwa nini hatupaswi kuhangaishwa na idadi ya wale wanaoshiriki mifano kwenye Ukumbusho?

12 “Yehova anawajua walio wake.” (2 Tim. 2:19) Tofauti na Yehova, akina ndugu wanaohesabu wale wanaoshiriki mifano kwenye Ukumbusho, hawajui ni nani hasa aliyetiwa mafuta kikweli. Hivyo, idadi hiyo inatia ndani wale ambao wanafikiri kwamba wametiwa mafuta ingawa si hivyo. Kwa mfano, baadhi ya watu ambao walikuwa wakishiriki mifano waliacha kufanya hivyo. Wengine wana matatizo ya akili au kihisia yanayowafanya waamini kwamba watatawala pamoja na Kristo mbinguni. Ni wazi kwamba hatujui kihususa idadi ya watiwa-mafuta waliobaki duniani.

13. Je, Biblia inataja idadi ya watiwa-mafuta watakaokuwa duniani dhiki kuu itakapoanza?

13 Kutakuwa na watiwa-mafuta sehemu mbalimbali duniani Yesu atakapokuja kuwachukua ili kwenda mbinguni. (Mt. 24:31) Biblia inasema kwamba katika siku za mwisho, kutakuwa na idadi ndogo ya watiwa-mafuta watakaokuwa wamebaki duniani. (Ufu. 12:17) Lakini haisemi ni watiwa-mafuta wangapi watakaokuwa duniani dhiki kuu itakapoanza.

Tunapaswa kutendaje mtu akishiriki mifano kwenye Ukumbusho? (Tazama fungu la 14)

14. Kama inavyotajwa kwenye Waroma 9:11, 16, tunapaswa kuelewa nini kuhusu jinsi watiwa-mafuta wanavyochaguliwa?

14 Yehova ndiye anayeamua ni wakati gani atachagua watiwa-mafuta. (Rom. 8:28-30) Yehova alianza kuwachagua watiwa-mafuta baada ya Yesu kufufuliwa. Inaonekana kwamba katika karne ya kwanza Wakristo wote wa kweli walikuwa watiwa-mafuta. Katika karne zilizofuata, idadi kubwa ya wale waliodai kuwa Wakristo hawakumfuata Kristo kikweli. Ingawa hivyo, katika kipindi hicho Yehova aliwatia mafuta watu wachache ambao walikuwa Wakristo wa kweli. Walikuwa kama ngano ambayo Yesu alisema ingekua pamoja na magugu. (Mt. 13:24-30) Katika siku za mwisho, Yehova ameendelea kuwachagua watu watakaokuwa sehemu ya wale 144,000. * Ikiwa Mungu anaamua kuchagua baadhi ya watu kuwa watiwa-mafuta kabla tu ya mwisho kufika, kwa kweli hatupaswi kutilia shaka hekima yake. (Soma Waroma 9:11, 16.) * Tunapaswa kuwa waangalifu tusitende kama wafanyakazi ambao Yesu aliwataja katika mojawapo ya mifano yake. Walilalamika kuhusu jinsi msimamizi wao alivyowatendea wale walioanza kufanya kazi jioni.—Mt. 20:8-15.

15. Je, watiwa-mafuta wote ni sehemu ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anayetajwa kwenye Mathayo 24:45-47? Eleza.

15 Si watu wote walio na tumaini la kuishi mbinguni ni sehemu ya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Soma Mathayo 24:45-47.) Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, leo Yehova na Yesu wanawatumia ndugu wachache kulisha, au kufundisha, watu wengi. Ni Wakristo watiwa-mafuta wachache tu katika karne ya kwanza waliotumiwa kuandika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Leo, ni Wakristo watiwa-mafuta wachache tu walio na jukumu la kuwapa watu wa Mungu ‘chakula kwa wakati unaofaa.’

16. Umejifunza nini katika makala hii?

16 Makala hii imetufundisha nini? Yehova ameamua kuwapa watumishi wake wengi uzima wa milele duniani na wachache watakaotawala na Yesu, uzima wa milele mbinguni. Yehova huwathawabisha watumishi wake wote—“Myahudi” na pia wale “watu kumi”—naye anataka watii sheria zilezile na waendelee kuwa waaminifu. Ni lazima wote waendelee kuwa wanyenyekevu. Ni lazima wote wamtumikie yeye pamoja, na kwa umoja. Na ni lazima wote wajitahidi kudumisha amani kutanikoni. Kadiri mwisho unavyozidi kukaribia, acheni sisi sote tuendelee kumtumikia Yehova na kumfuata Kristo tukiwa “kundi moja.”—Yoh. 10:16.

^ fu. 5 Mwaka huu, Ukumbusho wa kifo cha Kristo utaadhimishwa Jumanne, Aprili 7. Tunapaswa kuwaonaje wale wanaoshiriki mifano kwenye Ukumbusho? Je, tuhangaishwe ikiwa idadi ya wale wanaoshiriki mifano inazidi kuongezeka? Tutapata majibu ya maswali hayo katika makala hii inayotegemea gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 2016.

^ fu. 2 Kulingana na Zaburi 87:5, 6, huenda wakati ujao Mungu atafunua majina ya wote watakaotawala pamoja na Yesu mbinguni.—Rom. 8:19.

^ fu. 8 Tazama sanduku “Upendo ‘Haujiendeshi Bila Adabu’” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 2016.

^ fu. 14 Ingawa andiko la Matendo 2:33 linataja kwamba roho takatifu inamiminwa kupitia Yesu, Yehova ndiye anayemchagua kila mtu.

^ fu. 14 Kwa habari zaidi, tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” kwenye gazeti Mnara wa Mlinzi la Mei 1, 2007.

WIMBO 34 Kutembea kwa Utimilifu

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Wazia ingekuwaje ikiwa mwakilishi kutoka makao makuu pamoja na mke wake wangezingirwa na akina ndugu na dada wengi wanaowapiga picha kwenye kusanyiko. Huo ni ukosefu mkubwa wa heshima!