Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Simulizi la Maisha

Kujifunza Kutokana na Mifano Mizuri Kuliniletea Baraka Nyingi

Kujifunza Kutokana na Mifano Mizuri Kuliniletea Baraka Nyingi

Nilipokuwa kijana, kazi ya kuhubiri haikuwa rahisi kwangu. Kadiri nilivyoendelea kukua, nilipata migawo ambayo nilihisi kwamba sistahili kuifanya. Sasa acheni niwasimulie baadhi ya mifano mizuri iliyonisaidia kushinda woga wangu na kufurahia baraka nyingi katika kipindi cha miaka 58 ya utumishi wangu wa wakati wote.

Nilizaliwa nchini Kanada katika jiji la Quebec City, kwenye jimbo la Quebec, lenye wakazi wanaozungumza Kifaransa. Wazazi wangu, Louis na Zélia, walinilea katika mazingira yenye upendo. Baba yangu alikuwa mtu mkimya na alipenda kusoma. Nilipenda kuandika na nilikuwa na ndoto ya kuwa mwandishi wa habari.

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, Rodolphe Soucy, mmoja wa watu waliofanya kazi na Baba, alitutembelea nyumbani pamoja na rafiki yake. Walikuwa Mashahidi wa Yehova. Sikujua mengi kuhusu Mashahidi na sikupendezwa sana na dini yao. Hata hivyo, nilivutiwa na jinsi walivyojibu maswali kwa njia inayopatana na akili wakitumia Biblia. Wazazi wangu pia walivutiwa, hivyo tukakubali kujifunza Biblia.

Wakati huo, nilikuwa katika shule ya Kikatoliki. Pindi kwa pindi, nilizungumza pamoja na wanafunzi wenzangu kuhusu mambo niliyokuwa nikijifunza katika Biblia. Mwishowe, walimu wangu ambao walikuwa makasisi waligundua jambo hilo. Badala ya kutumia Maandiko kupinga mambo niliyokuwa nikisema, mmoja wao alinishutumu mbele ya darasa zima kwamba nilikuwa mwanamapinduzi! Ingawa nilipata mkazo kwa sababu ya hali hiyo, jambo hilo lilikuwa baraka kwangu kwa sababu lilinisaidia kuona kwamba mafundisho ya kidini ya shule hiyo yalipingana na mambo ambayo Biblia inasema. Nilitambua kwamba sikupaswa kuwa hapo. Kwa ruhusa ya wazazi wangu, nilihamia shule nyingine.

NAJIFUNZA KUPENDA HUDUMA

Niliendelea kujifunza Biblia lakini nilifanya maendeleo ya kiroho polepole kwa sababu niliogopa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kanisa Katoliki lilikuwa na ushawishi mkubwa sana na lilipinga vikali kazi yetu ya kuhubiri. Maurice Duplessis, mwanasiasa wa Quebec, alikuwa rafiki wa karibu wa viongozi wa kanisa hilo. Alivisaidia vikundi vya wafanya ghasia kuwasumbua na hata kuwashambulia Mashahidi. Wakati huo, mtu alihitaji kuwa jasiri sana ili kuhubiri.

Ndugu aliyenisaidia kushinda woga wangu alikuwa John Rae, mhitimu wa darasa la tisa la Shule ya Gileadi. John, ndugu mwenye uzoefu sana alikuwa mtu mpole, mwenye kiasi, na aliyefikika kwa urahisi. Hakuwa na mazoea ya kunishauri moja kwa moja, lakini mfano wake mzuri ulizungumza mengi. John hakujua Kifaransa vizuri, hivyo niliandamana pamoja naye katika huduma mara kwa mara na kumsaidia kujifunza lugha hiyo. Kutumia muda mwingi pamoja na John kulinisaidia kuchukua msimamo thabiti upande wa kweli. Nilibatizwa, Mei 26, 1951, miaka kumi baada ya kukutana na Mashahidi.

Mfano mzuri wa John Rae (A) ulinisaidia mimi (B) kushinda woga wa kuhubiri nyumba kwa nyumba

Wahubiri wengi katika kutaniko letu dogo jijini Quebec City walikuwa mapainia. Mfano wao mzuri ulinichochea kuwa painia. Siku hizo, tulihubiri nyumba kwa nyumba tukitumia Biblia tu. Kwa kuwa hatukuwaachia watu machapisho, tulihitaji kutumia Maandiko kwa ustadi zaidi. Hivyo, nilijitahidi sana kufahamu vizuri mistari ya Biblia ili niweze kuitetea kweli. Hata hivyo, watu wengi walikataa kuisoma hata Biblia yenyewe ikiwa haikuwa na kibali rasmi cha Kanisa Katoliki.

Katika mwaka wa 1952, nilifunga ndoa na Simone Patry, dada mwaminifu kutoka eneo hilo. Tulihamia Montreal, na ndani ya mwaka mmoja tukabarikiwa kumpata binti yetu Lise. Ingawa nilikuwa nimeacha upainia muda mfupi kabla ya kufunga ndoa, mimi pamoja na Simone tulijitahidi kudumisha maisha rahisi ili tushiriki kikamili katika utendaji wa kutaniko tukiwa familia.

Baada ya miaka kumi nilifikiria tena kwa uzito kuhusu kupanua utumishi wangu. Mwaka wa 1962, nilipokuwa nikihudhuria Shule ya Huduma ya Ufalme iliyofanywa kwa mwezi mmoja katika Betheli ya Kanada, tuliishi chumba kimoja na ndugu aliyeitwa Camille Ouellette. Bidii ya Camille katika huduma ilinigusa sana—hasa kwa kuwa alikuwa na familia. Siku hizo, katika jimbo la Quebec halikuwa jambo la kawaida kwa mzazi kuwa painia huku akilea mtoto; ingawa hivyo, Camille alikuwa na lengo hilo. Tulipokuwa tukiishi pamoja, alinitia moyo nifikirie kuhusu hali yangu. Baada ya miezi michache tu, nilitambua kwamba ninaweza kutumikia tena nikiwa painia wa kawaida. Baadhi ya watu walikosoa uamuzi wangu, lakini nilisonga mbele, nikiwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zangu za kushiriki kwa njia kubwa zaidi katika huduma.

TUNARUDI QUEBEC CITY TUKIWA MAPAINIA WA PEKEE

Katika mwaka wa 1964, mimi pamoja na Simone tuliwekwa rasmi kuwa mapainia wa pekee jijini Quebec City, jiji la nyumbani kwetu, ambako tulitumikia kwa miaka kadhaa iliyofuata. Kufikia wakati huo, mazingira ya kuhubiri yalikuwa afadhali, lakini bado tulipata upinzani.

Jumamosi moja mchana, nilikamatwa huko Sainte-Marie, mji mdogo ulio karibu na Quebec City. Ofisa mmoja alinipeleka kwenye kituo cha polisi na kunifunga gerezani kwa sababu nilikuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba bila kibali. Baadaye, nilipelekwa mbele ya hakimu mwenye kuogopesha aliyeitwa Baillargeon. Alitaka kujua ni nani ambaye angeniwakilisha mahakamani. Nilipotaja jina la Glen How, * mwanasheria Shahidi aliyejulikana sana, alisema hivi kwa wasiwasi: “Ah, Hapana! Simtaki huyo!” Wakati huo, Glen How alisifika sana kwa kuwatetea kisheria Mashahidi. Baada ya muda mfupi, mahakama ikanijulisha kwamba ilikuwa imeyafutilia mbali mashtaka dhidi yangu.

Pia, kwa sababu ya upinzani wa kazi yetu huko Quebec ilikuwa vigumu kukodi mahali palipofaa kwa ajili ya mikutano. Kutaniko letu dogo lilifanikiwa tu kupata chumba cha kuegeshea gari ambacho kilikuwa na baridi. Ili kukipasha joto katika majira ya baridi kali, akina ndugu walitumia kipasha-joto kilichotumia mafuta. Kwa kawaida, tulikizunguka kwa saa chache kabla ya mikutano ili kusimuliana mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo.

Ni jambo linalofurahisha sana kuona jinsi kazi ya kuhubiri ilivyositawi kwa miaka hiyo yote. Katika miaka ya 1960, kulikuwa na makutaniko machache madogo jijini Quebec City, eneo la Côte-Nord, na Peninsula ya Gaspé. Leo, kuna zaidi ya mizunguko miwili katika maeneo hayo, na akina ndugu wanafanya mikutano kwenye Majumba maridadi ya Ufalme.

MWALIKO WA KUWA MWANGALIZI WA MZUNGUKO

Mwaka wa 1977, nilihudhuria mkutano kwa ajili ya waangalizi wanaosafiri huko Toronto, Kanada

Mimi na Simone tulialikwa katika kazi ya kuzungukia makutaniko mwaka wa 1970. Kisha mwaka wa 1973, nilipata mgawo wa kuwa mwangalizi wa wilaya. Katika miaka hiyo, nilijifunza mengi kutoka kwa akina ndugu wenye uwezo mkubwa kama vile Laurier Saumur * na David Splane, * ambao walitumikia wakiwa waangalizi wa mzunguko. Baada ya kila kusanyiko, mimi pamoja na David tulikuwa na kawaida ya kupeana mapendekezo kuhusu jinsi ya kuboresha ufundishaji wetu. Ninakumbuka siku moja David akiniambia: “Léonce, nilifurahia hotuba yako ya mwisho. Ilikuwa nzuri, hata hivyo ningeweza kutayarisha hotuba tatu kwa kutegemea habari ulizotumia!” Nilizoea kuzungumzia habari nyingi sana katika hotuba zangu. Nilihitaji kujifunza kuzungumzia mambo machache zaidi.

Nilitumikia katika majiji mbalimbali mashariki mwa Kanada

Waangalizi wa wilaya walipewa mgawo wa kuwatia moyo waangalizi wa mzunguko. Hata hivyo, wahubiri wengi jijini Quebec walinifahamu vizuri sana. Kwa kawaida walitamani kuhubiri pamoja nami nilipotembelea mizunguko. Ingawa nilifurahia kushirikiana nao katika huduma, sikuwa nikitumia muda wa kutosha na mwangalizi wa mzunguko. Pindi moja, mwangalizi mmoja wa mzunguko alinikumbusha hivi: “Ni vizuri kutenga muda wa kuwa pamoja na akina ndugu, lakini usisahau kwamba ulikuja kunitembelea mimi juma hili. Ninahitaji kutiwa moyo pia!” Shauri hilo lenye fadhili lilinisaidia niwe mwenye usawaziko zaidi.

Kwa kusikitisha, mwaka 1976 nilipatwa na tukio lenye kuhuzunisha sana ambalo sikuwa nimetarajia. Mke wangu mpendwa, Simone, aliugua sana na kulala usingizi katika kifo. Roho yake ya kujidhabihu na upendo wake kwa Yehova ni mambo yaliyomfanya awe mwenzi mzuri sana. Kuwa na mengi ya kufanya katika huduma kulinisaidia sana kukabiliana na huzuni ya kumpoteza, na ninamshukuru Yehova kwa kunitegemeza kwa upendo katika kipindi hicho kigumu. Baadaye nilifunga ndoa na Carolyn Elliott, dada painia mwenye bidii aliyezungumza Kiingereza aliyekuja Quebec ili kutumikia katika eneo lenye uhitaji. Carolyn ni dada anayefikika kwa urahisi na anayependezwa kikweli na wengine, hasa wale ambao ni wakimya au wapweke. Alithibitika kuwa baraka kwelikweli alipojiunga nami katika kazi ya kuzunguka.

MWAKA MUHIMU SANA

Januari 1978, niliombwa nifundishe Shule ya kwanza ya Utumishi wa Painia jijini Quebec. Nilikuwa na wasiwasi sana, kwa sababu mtaala ulikuwa mpya kwangu na kwa wanafunzi pia. Ninashukuru sana kwamba darasa la kwanza nililofundisha lilikuwa na mapainia wengi wenye uzoefu. Hata ingawa nilikuwa mwalimu, nilijifunza mengi kutoka kwa wanafunzi!

Baadaye mwaka wa 1978, Kusanyiko la Kimataifa la “Imani Ishindayo” lilifanywa katika Uwanja wa Olimpiki wa Montreal. Lilikuwa kusanyiko kubwa kuwahi kufanywa jijini Quebec, kwani zaidi ya watu 80,000 walihudhuria. Nilipewa mgawo katika Idara ya Vyombo vya Habari. Nilizungumza na waandishi wengi wa habari na nilisisimka sana kuona jinsi walivyoandika mambo mengi mazuri kutuhusu. Walifanya mahojiano pamoja nasi kwenye vipindi vya televisheni na redio vilivyorushwa kwa jumla ya zaidi ya saa 20, na mamia ya makala zilichapishwa. Ushahidi mkubwa sana ulitolewa!

KUHAMIA KWENYE ENEO LINGINE

Nilipata mabadiliko makubwa mwaka wa 1996. Baada ya kutumikia katika eneo la Quebec lenye watu wanaozungumza Kifaransa, nilipata mgawo wa kutumikia katika eneo la Toronto lenye watu wanaozungumza Kiingereza. Nilihisi sistahili na niliogopa kutoa hotuba kwa kutumia Kiingereza changu kibovu. Nilihitaji kutoa sala mara nyingi zaidi na kumtegemea Yehova kikamili zaidi.

Ninapokumbuka mambo yaliyopita, kwa kweli ninaweza kusema kwamba nilifurahia miaka miwili niliyotumikia katika eneo la Toronto. Carolyn alinisaidia kwa subira nizungumze Kiingereza kwa kujiamini zaidi, na akina ndugu walinisaidia sana na kunitia moyo. Tulipata haraka marafiki wengi wazuri.

Mbali na utendaji wa ziada na matayarisho kwa ajili ya kusanyiko wakati wa mwisho juma, mara nyingi nilihubiri pia nyumba kwa nyumba kwa saa moja hivi Ijumaa jioni. Huenda wengine walijiuliza, ‘Kwa nini mtu aende kwenye utumishi kabla tu ya kusanyiko la mwisho juma lenye mambo mengi?’ Lakini nilijionea kwamba kuwa na mazungumzo mazuri na watu kwenye huduma kuliniburudisha. Hata sasa, kushiriki katika utumishi wa shambani hunichangamsha.

Katika mwaka wa 1998, mimi na Carolyn tulipata mgawo wa kuwa mapainia wa pekee huko Montreal. Kwa miaka kadhaa, mgawo wangu ulihusisha kupanga mahubiri ya pekee ya hadharani na kufanya kazi na vyombo vya habari ili kurekebisha maoni mabaya ambayo watu wanayo kuhusu Mashahidi wa Yehova. Kwa sasa mimi na Carolyn tunafurahia kuwahubiria wageni waliohamia Kanada hivi karibuni na ambao mara nyingi wana hamu ya kujifunza mengi zaidi kuhusu Biblia.

Pamoja na mke wangu Carolyn

Ninapotafakari kuhusu miaka 68 ya kuwa mtumishi wa Yehova aliyebatizwa, ninahisi kwamba nimebarikiwa kwelikweli. Kujifunza kufurahia huduma na kuwasaidia wengine wajifunze kweli ni mambo ambayo yamenithawabisha sana. Baada ya binti yangu Lise, pamoja na mume wake kulea watoto wao, walianza kutumikia wakiwa mapainia wa kawaida. Ninapoona bidii yake nyingi kwa ajili ya huduma, moyo wangu huchangamka. Ninawashukuru sana Wakristo wenzangu ambao mfano wao mzuri na mashauri yao yenye hekima yamenisaidia kukua kiroho na kutimiza migawo mbalimbali ya kitheokrasi. Nimejionea kwamba tunaweza kuendelea kutimiza migawo yetu kwa uaminifu ikiwa tu tutategemea roho takatifu ya Yehova yenye nguvu. (Zab. 51:11) Ninaendelea kumshukuru Yehova kwa kunipatia pendeleo lenye thamani la kulisifu jina lake!—Zab. 54:6.

^ fu. 16 Tazama simulizi la maisha la W. Glen, “Vita Si Yenu Bali Ni ya Mungu,” katika Amkeni!, Aprili 22, 2000.

^ fu. 20 Tazama simulizi la maisha la Laurier Saumur, I Found Something Worth Fighting For,” katika gazeti Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 1976, la Kiingereza.

^ fu. 20 David Splane ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.