Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 7

Tunampenda Sana Yehova, Baba Yetu

Tunampenda Sana Yehova, Baba Yetu

“Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.”—1 YOH. 4:19.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

MUHTASARI *

1-2. Kwa nini Yehova alitufungulia njia ya kuwa sehemu ya familia yake, na alifanya hivyo jinsi gani?

YEHOVA ametualika tujiunge na familia ya watu wake wanaomwabudu. Huo ni mwaliko mzuri sana! Familia yetu inatia ndani watu ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu na walio na imani katika dhabihu ya fidia ya Mwana wake. Sisi ni familia yenye furaha. Tunafurahia maisha yenye kusudi sasa na tunashangilia kwa sababu tuna tumaini la kuishi milele—iwe ni mbinguni au katika Paradiso duniani.

2 Akisukumwa na upendo na kwa gharama kubwa, Yehova alitufungulia njia ya kuwa sehemu ya familia yake. (Yoh. 3:16) ‘Tulinunuliwa kwa bei.’ (1 Kor. 6:20) Kupitia fidia, Yehova alifanya iwezekane kwetu kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Tuna pendeleo la kumwita Mtu mkuu zaidi katika ulimwengu wote, Baba. Na kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, Yehova ndiye Baba bora zaidi kuliko wote.

3. Huenda tukajiuliza maswali gani? (Tazama pia sanduku “ Je, Yehova Ananiona?”)

3 Huenda tukajiuliza hivi kama mwandikaji mmoja wa Biblia: “Nitamlipa Yehova nini kwa mema yote aliyonitendea?” (Zab. 116:12) Jibu ni kwamba hatuwezi kamwe kumlipa Baba yetu wa mbinguni. Ingawa hivyo, tunachochewa kumpenda. Mtume Yohana aliandika hivi: “Sisi tuna upendo, kwa sababu alitupenda kwanza.” (1 Yoh. 4:19) Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunampenda Baba yetu wa mbinguni?

ENDELEA KUKAA KARIBU NA YEHOVA

Tunaonyesha jinsi tunavyompenda sana Baba yetu wa mbinguni, Yehova, kwa kuendelea kumkaribia katika sala, kwa kumtii, na kwa kuwasaidia wengine wampende (Tazama fungu la 4 hadi 14)

4. Kulingana na Yakobo 4:8, kwa nini tunapaswa kujitahidi kumkaribia Yehova?

4 Yehova anataka tumkaribie na tuwe tukiwasiliana naye. (Soma Yakobo 4:8.) Anatuhimiza ‘tudumu katika sala,’ naye anahakikisha kwamba anapatikana nyakati zote. (Rom. 12:12) Yehova hana shughuli nyingi hivi kwamba ashindwe kutusikiliza na hachoki kufanya hivyo. Nasi tunamsikiliza tunaposoma Neno lake, Biblia, pamoja na machapisho yanayotusaidia kulielewa. Pia, tunamsikiliza Yehova tunaposikiliza kwa makini katika mikutano yetu ya Kikristo. Kama tu ambavyo mawasiliano mazuri huwafanya watoto waendelee kuwa karibu na wazazi wao, ndivyo kuwasiliana kwa ukawaida pamoja na Yehova kunavyotusaidia tuendelee kuwa karibu naye.

Tazama fungu la 5

5. Tunaweza kuboreshaje sala zetu?

5 Fikiria kuhusu ubora wa sala zako. Yehova anataka tummwagie moyo wetu katika sala. (Zab. 62:8) Inafaa tujiulize swali hili: ‘Je, sala zangu ni za kijuujuu tu kama ujumbe ulionakiliwa tena na tena, au ni kama barua iliyoandikwa kutoka moyoni?’ Bila shaka unampenda sana Yehova, na unataka kudumisha uhusiano wako pamoja naye ukiwa imara. Ili ufanye hivyo, lazima uwasiliane naye kwa ukawaida. Mweleze hisia zako za ndani kabisa. Mweleze mambo unayofurahia na yanayokuumiza. Uwe na uhakika kwamba unaweza kumfikia ili kupata msaada.

6. Ni lazima tufanye nini ili tuendelee kukaa karibu na Baba yetu wa mbinguni?

6 Ili tuendelee kukaa karibu na Baba yetu wa mbinguni, ni lazima sikuzote tuwe watu wenye shukrani. Tunakubaliana na mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Jinsi ulivyotenda mambo mengi sana, Ee Yehova Mungu wangu, kazi zako zinazostaajabisha na mawazo yako kutuelekea. Hakuna yeyote anayeweza kulinganishwa nawe; ikiwa ningejaribu kusimulia na kuongea kuzihusu, zingekuwa nyingi sana kwangu kusimulia!” (Zab. 40:5) Tunafanya mengi zaidi ya kuwa tu na hisia za shukrani; tunaonyesha shukrani zetu kwa Yehova kupitia maneno na matendo yetu. Jambo hilo hutufanya tuonekane kuwa tofauti na watu wengi leo. Tunaishi katika ulimwengu ambao watu hawathamini mambo yote ambayo Mungu anawafanyia. Jambo moja linaloonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” ni kwamba watu hawana shukrani. (2 Tim. 3:1, 2) Tusiige kamwe mtazamo huo!

7. Yehova anataka tufanye nini, na kwa nini?

7 Wazazi hawapendi watoto wao wagombane bali wawe marafiki. Vivyo hivyo, Yehova anataka watoto wake wote wawe marafiki. Kwa kweli, upendo tulio nao miongoni mwetu hututambulisha kuwa Wakristo wa kweli. (Yoh. 13:35) Tunakubaliana na mtunga zaburi aliyeandika hivi: “Jinsi ilivyo vema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” (Zab. 133:1) Tunapowapenda ndugu na dada zetu, tunamthibitishia Yehova kwamba tunampenda. (1 Yoh. 4:20) Inapendeza sana kuwa katika familia yenye ndugu na dada wenye “fadhili [na] huruma nyororo”!—Efe. 4:32.

ONYESHA UPENDO WAKO KWA KUWA MTIIFU

Tazama fungu la 8

8. Kulingana na 1 Yohana 5:3, sababu kuu inayotufanya tumtii Yehova ni ipi?

8 Yehova anatarajia watoto wawatii wazazi wao, na anatarajia sisi pia tumtii. (Efe. 6:1) Anastahili utii wetu kwa sababu yeye ni Muumba wetu, Mtegemezaji wa uhai wetu, na mwenye hekima kuliko baba yeyote duniani. Hata hivyo, sababu kuu inayotufanya tumtii Yehova ni kwamba tunampenda. (Soma 1 Yohana 5:3.) Ingawa kuna sababu nyingi zinazotufanya tumtii, Yehova hatulazimishi kufanya hivyo. Yehova alitupatia zawadi ya uhuru wa kuchagua, hivyo anafurahi tunapochagua kumtii yeye kwa sababu tunampenda.

9-10. Kwa nini ni muhimu kujua viwango vya Yehova na kuishi kulingana navyo?

9 Wazazi wangependa watoto wao wawe salama. Hiyo ndiyo sababu wanawawekea watoto wao sheria zitakazowanufaisha. Watoto wanapotii sheria hizo, wanaonyesha kwamba wanawatumaini na kuwaheshimu wazazi wao. Hivyo, ni jambo la muhimu hata zaidi kwetu kujua viwango vya Baba yetu wa mbinguni na kuishi kulingana navyo. Tunapofanya hivyo, tunamwonyesha Yehova kwamba tunampenda na kumheshimu na pia tunajinufaisha sisi wenyewe. (Isa. 48:17, 18) Kinyume cha hilo, wale wanaomkataa Yehova na viwango vyake huishia kujiumiza wenyewe.—Gal. 6:7, 8.

10 Tunapoishi kwa njia inayompendeza Yehova, tunalindwa dhidi ya madhara ya kimwili, ya kihisia, na ya kiroho. Yehova anajua mambo yanayotufaa zaidi. Aurora, dada anayeishi Marekani, anasema hivi: “Ninajua kwamba sikuzote kumtii Yehova humfanya mtu awe na maisha bora kabisa.” Na ndivyo ilivyo kwetu sote. Umenufaikaje kwa kutii mwongozo wa Yehova wenye upendo?

11. Sala inaweza kutusaidiaje?

11 Sala hutusaidia kuwa watiifu hata inapokuwa vigumu kufanya hivyo. Nyakati nyingine, ni vigumu kwetu kumtii Yehova, lakini ni lazima sikuzote tupambane na mwelekeo wetu wa kutenda dhambi. Mtunga zaburi alimsihi Mungu hivi: “Chochea ndani yangu utayari wa kukutii.” (Zab. 51:12) Denise, dada ambaye ni painia wa kawaida, anasema hivi: “Ninapohisi kuwa ni vigumu kwangu kutii mojawapo ya amri za Yehova, ninasali ili nipate nguvu za kufanya yaliyo sawa.” Tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yehova atajibu ombi kama hilo.—Luka 11:9-13.

WASAIDIE WENGINE KUMPENDA BABA YETU

12. Kulingana na Waefeso 5:1, tunapaswa kufanya nini?

12 Soma Waefeso 5:1. Tukiwa “watoto wapendwa” wa Yehova, tunafanya yote tuwezayo ili kumtii yeye. Tunaiga sifa zake tunapowaonyesha wengine upendo, fadhili, na kuwasamehe. Watu wasiomjua Mungu wanapoona mwenendo wetu mzuri, wanaweza kuchochewa wajifunze mengi zaidi kumhusu. (1 Pet. 2:12) Wazazi Wakristo wana sababu nzuri ya kumwiga Yehova inapohusu jinsi wanavyowatendea watoto wao. Wanapomwiga Yehova, watoto wao wanaweza kutamani kuwa na urafiki pamoja na Baba yetu anayetupenda.

Tazama fungu la 13

13. Tunapaswa kukazia fikira nini?

13 Mtoto mdogo hujivunia baba yake na anafurahia kuzungumza kumhusu. Vivyo hivyo, tunajivunia Baba yetu wa mbinguni, Yehova, na tunataka wengine wamjue. Sisi sote tunahisi moyoni kama Mfalme Daudi aliyeandika hivi: “Nitajigamba kwa sababu ya Yehova.” (Zab. 34:2) Lakini vipi ikiwa tuna haya? Tunawezaje kuwa jasiri? Tunapata ujasiri tunapokazia fikira jinsi tunavyoweza kumfurahisha Yehova kwa kuzungumza kumhusu na jinsi wengine watakavyonufaika kwa kujifunza kumhusu. Yehova atatupatia ujasiri tunaohitaji. Aliwasaidia ndugu zetu katika karne ya kwanza kuwa jasiri, naye atatusaidia sisi pia.—1 The. 2:2.

14. Taja sababu zinazoonyesha umuhimu wa kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi.

14 Yehova hana ubaguzi, na anafurahi anapoona tukiwaonyesha wengine upendo, hata iwe wanatoka wapi. (Mdo. 10:34, 35) Mojawapo ya njia bora zaidi tunayoweza kuwaonyesha wengine upendo ni kwa kuwahubiria habari njema. (Mt. 28:19, 20) Kazi hiyo inatimiza nini? Wale wanaotusikiliza wanaweza kuboresha maisha yao sasa na kupata tumaini la kufurahia maisha milele wakati ujao.—1 Tim. 4:16.

MPENDE BABA YETU NA UWE NA FURAHA

15-16. Tuna sababu zipi za kuwa na furaha?

15 Yehova ni Baba mwenye upendo, hivyo anataka familia yake iwe na furaha. (Isa. 65:14) Tuna sababu nyingi za kuwa na shangwe sasa licha ya kwamba tunakabili hali ngumu mbalimbali. Kwa mfano, tuna hakika kwamba Baba yetu wa mbinguni anatupenda sana. Tuna ujuzi sahihi wa Neno la Mungu, Biblia. (Yer. 15:16) Na tuko katika familia ya pekee ya watu wanaompenda Yehova, wanaopenda viwango vyake vya juu vya maadili, na wanaopendana.—Zab. 106:4, 5.

16 Tunaweza kuendelea kuwa na furaha kwa sababu tuna tumaini lililo hakika kwamba maisha yatakuwa mazuri hata zaidi wakati ujao. Tunajua kwamba hivi karibuni Yehova atawaondoa waovu wote na kwamba chini ya mwongozo wa Ufalme wake, dunia itakuwa Paradiso. Pia, tuna tumaini zuri sana kwamba wale waliokufa watafufuliwa na kuungana tena na wapendwa wao. (Yoh. 5:28, 29) Itakuwa shangwe kwelikweli! Na jambo muhimu hata zaidi ni kwamba tuna hakika kuwa hivi karibuni kila mmoja, mbinguni na duniani, atampa Baba yetu anayetupenda heshima, sifa, na ibada anayostahili.

WIMBO 12 Mungu Mkuu, Yehova

^ fu. 5 MUHTASARI Tunajua kwamba Yehova, Baba yetu, anatupenda sana na ametukaribisha katika familia ya watu wake wanaomwabudu. Hivyo, tunachochewa kumpenda. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunampenda Baba yetu anayetujali? Makala hii itazungumzia mambo hususa tunayoweza kufanya.