Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 9

Acha Yehova Akubembeleze

Acha Yehova Akubembeleze

“Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.”—ZAB. 94:19.

WIMBO 44 Sala ya Mtu wa Hali ya Chini

MUHTASARI *

1. Ni mambo gani yanayoweza kusababisha mahangaiko, na mahangaiko yanaweza kutuathirije?

JE, UMEWAHI kulemewa na mahangaiko? * Huenda una mahangaiko kwa sababu umeumizwa na mambo ambayo wengine wamesema au kukutendea. Au huenda una mahangaiko kwa sababu ya mambo uliyosema au kutenda. Kwa mfano, huenda umefanya kosa fulani, na una wasiwasi kwa sababu unahisi kwamba Yehova hatakusamehe kamwe. Jambo baya hata zaidi, huenda ukahisi kwamba kwa kuwa mahangaiko yamekulemea, basi huna imani ya kutosha—hivyo lazima wewe ni mtu mbaya. Lakini, je, jambo hilo ni kweli?

2. Ni mifano gani ya Kimaandiko inayoonyesha kwamba kuwa na mahangaiko hakumaanishi kwamba hatuna imani?

2 Fikiria mifano michache katika Biblia. Hana, ambaye alikuja kuwa mama ya nabii Samweli, alikuwa mwanamke mwenye imani kubwa. Licha ya hilo, alilemewa na mahangaiko wakati mtu wa familia yake alipomtendea isivyofaa. (1 Sam. 1:7) Mtume Paulo alikuwa na imani yenye nguvu, lakini alilemewa na ‘mahangaiko kwa ajili ya makutaniko yote.’ (2 Kor. 11:28) Mfalme Daudi alikuwa na imani yenye nguvu hivi kwamba Yehova alimpenda sana. (Mdo. 13:22) Hata hivyo, Daudi alifanya makosa yaliyosababisha alemewe na mahangaiko yaliyomtaabisha sana. (Zab. 38:4) Yehova alimfariji na kumbembeleza kila mmoja wao. Acheni tuchunguze mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mifano yao.

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKA KWA MWANAMKE MWAMINIFU, HANA

3. Maneno ya wengine yanaweza kutusababishiaje mahangaiko?

3 Wengine wanapozungumza kwa ukali au kutenda bila fadhili, wanaweza kutusababishia mahangaiko. Na hilo ni kweli, hasa ikiwa aliyetuumiza ni rafiki yetu wa karibu au mtu wa ukoo. Huenda tukawa na wasiwasi kwamba uhusiano wetu na mtu huyo umeharibika. Nyakati nyingine, huenda mtu aliyetuumiza alizungumza bila kufikiri na kusababisha tuhisi kana kwamba tumechomwa kwa upanga! (Met. 12:18) Au huenda mtu akaamua kimakusudi kutumia maneno yatakayokuumiza. Dada mmoja kijana alikabili changamoto hiyo. Anasema hivi: “Miaka kadhaa iliyopita dada ambaye nilidhani alikuwa rafiki yangu alianza kueneza habari za uwongo kunihusu kwenye mtandao. Jambo hilo liliniumiza na kunihangaisha. Sikuelewa kwa nini rafiki niliyemwamini alinisaliti kiasi hicho.” Ikiwa umeumizwa na rafiki wa karibu au mtu wa ukoo, unaweza kujifunza mengi kutoka kwa Hana.

4. Hana alilazimika kukabiliana na hali zipi?

4 Hana alilazimika kukabiliana na hali fulani ngumu. Kwa miaka mingi hakuweza kupata watoto. (1 Sam. 1:2) Katika utamaduni wa Waisraeli, watu waliamini kwamba mwanamke aliyekuwa tasa alikuwa amelaaniwa. Jambo hilo lilimfanya aaibike sana. (Mwa. 30:1, 2) Mambo yalikuwa mabaya hata zaidi kwa Hana kwa sababu mume wake alikuwa na mke mwingine aliyeitwa Penina, ambaye alikuwa amemzalia watoto. Penina alimwonea wivu Hana na “alimdhihaki daima ili kumkasirisha.” (1 Sam. 1:6) Mwanzoni, hali hiyo ngumu ilimhuzunisha sana Hana. Aliumia sana hivi kwamba “alilia na kushindwa kula.” Akawa na “uchungu mwingi sana” moyoni. (1 Sam. 1:7, 10) Hana alipata wapi faraja?

5. Sala ilimsaidiaje Hana?

5 Hana alimmwagia Yehova hisia zake katika sala. Baada ya kusali, alimweleza Kuhani Mkuu Eli hali aliyokuwa akipitia. Eli alimwambia hivi: “Nenda kwa amani, na Mungu wa Israeli akupe ulichoomba.” Ikawaje? Hana “akaenda zake, akala chakula, na uso wake haukuwa na huzuni tena.” (1 Sam. 1:17, 18) Sala ilimsaidia Hana apate tena amani.

Kama Hana, sisi leo tunawezaje kupata tena amani ya moyoni na kuidumisha? (Tazama fungu la 6 hadi 10))

6. Tunajifunza mambo gani kuhusu sala kutoka kwa Hana na pia Wafilipi 4:6, 7?

6 Tunaweza kupata amani tena ikiwa tutadumu katika sala. Hana alitumia muda mwingi sana kuzungumza na Baba yake wa mbinguni. (1 Sam. 1:12) Sisi pia tunaweza kuzungumza kwa kirefu sana pamoja na Yehova kuhusu mahangaiko yetu, hofu tuliyo nayo, na udhaifu wetu. Si lazima sala zetu ziwe zimeandaliwa kama shairi au kwa ufasaha sana. Huenda hata tukajikuta tukizungumza kwa uchungu huku tukilia kwa huzuni. Ingawa hivyo, Yehova hatachoka kamwe kutusikiliza. Zaidi ya kusali kuhusu matatizo yetu, tunahitaji kukumbuka ushauri unaopatikana kwenye Wafilipi 4:6, 7. (Soma.) Paulo alitaja kihususa kwamba tunapaswa kutoa sala za shukrani, au za kuonyesha uthamini. Tuna sababu nyingi sana za kumshukuru Yehova. Kwa mfano, tunaweza kumshukuru kwa sababu ya zawadi ya uhai, kazi zake za uumbaji, upendo wake mshikamanifu, na tumaini zuri ajabu tulilo nalo. Tunajifunza nini kingine kutoka kwa Hana?

7. Hana na mume wake walikuwa na kawaida ya kufanya nini?

7 Licha ya matatizo yake, Hana alienda kwa ukawaida pamoja na mume wake huko Shilo, mahali pa Yehova pa ibada. (1 Sam. 1:1-5) Alipokuwa katika hema la ibada, ndipo Kuhani Mkuu Eli alipomtia moyo kwa kumwambia kwamba Yehova angejibu sala yake.—1 Sam. 1:9, 17.

8. Mikutano inaweza kutusaidiaje? Eleza.

8 Tunaweza kupata amani tena kwa kuendelea kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Kwa kawaida, tunapoanza mikutano sala hutolewa ili kuomba roho takatifu ya Mungu iwe pamoja nasi. Amani ni sehemu ya tunda la roho hiyo. (Gal. 5:22) Tunapohudhuria mikutano yetu licha ya mkazo tulio nao, tunampa Yehova na pia ndugu na dada zetu fursa ya kututia moyo na kutusaidia tupate tena amani ya akili na ya moyoni. Sala na mikutano ni njia muhimu ambazo Yehova anatumia kutubembeleza. (Ebr. 10:24, 25) Fikiria somo lingine tunaloweza kujifunza kutoka kwa Hana.

9. Ni jambo gani ambalo halikubadilika kuhusu hali ya Hana, lakini ni nini kilichobadilika?

9 Chanzo cha mahangaiko ya Hana hakikuondoka mara moja. Hana aliporudi nyumbani baada ya kumwabudu Yehova kwenye hema la ibada, bado alilazimika kuishi kwenye nyumba ileile pamoja na Penina. Na Biblia haisemi kwamba mtazamo wa Penina ulibadilika. Hivyo, inaonekana kwamba Hana alilazimika kuendelea kuvumilia maneno yenye kuchoma ya Penina. Lakini Hana alifanikiwa kupata tena amani ya moyoni na kuidumisha. Kumbuka kwamba baada ya Hana kuacha jambo hilo mikononi mwa Yehova, hakuendelea tena kulemewa na jambo lililomhangaisha. Aliacha Yehova amfariji na kumbembeleza. Muda fulani baadaye, Yehova alijibu sala ya Hana na akapata watoto wake mwenyewe!—1 Sam. 1:19, 20; 2:21.

10. Tunajifunza nini kutoka kwa Hana?

10 Tunaweza kupata amani tena hata ikiwa chanzo cha mahangaiko yetu hakijatoweka. Hata ingawa huenda tukasali kwa bidii na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, matatizo fulani yanaweza kuendelea. Kutokana na mfano wa Hana, tunajifunza kwamba hakuna kitu chochote kinachoweza kumzuia Yehova kuubembeleza moyo wetu unaotaabika. Yehova hatatusahau kamwe, na wakati utafika ambapo atatuthawabisha kwa sababu ya uaminifu wetu, iwe ni karibuni au baadaye.—Ebr. 11:6.

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKA KWA MTUME PAULO

11. Paulo alikuwa na sababu gani za kuwa na mahangaiko?

11 Paulo alikuwa na sababu nyingi za kuwa na mahangaiko. Kwa mfano, kwa kuwa Paulo aliwapenda ndugu na dada zake, alihangaishwa sana na matatizo yao. (2 Kor. 2:4; 11:28) Katika mgawo wake akiwa mtume, Paulo alilazimika kukabiliana na wapinzani ambao walimpiga na kumtupa gerezani. Pia, alilazimika kuvumilia hali ngumu zilizomsababishia mahangaiko, kama vile “kupungukiwa na chakula.” (Flp. 4:12) Na ukizingatia kwamba alikuwa amevunjikiwa na meli mara tatu hivi kufikia wakati huo, unaweza kuwazia jinsi alivyokuwa na wasiwasi alipokuwa akisafiri kwa mashua. (2 Kor. 11:23-27) Paulo aliyashughulikiaje mahangaiko yake?

12. Ni nini kilichompunguzia Paulo mahangaiko?

12 Paulo alipatwa na mahangaiko ndugu na dada zake walipokabili matatizo, lakini hakujaribu kusuluhisha matatizo yao yote mwenyewe. Paulo alikuwa na kiasi. Alifanya mipango ili wengine wasaidie kulitunza kutaniko. Kwa mfano, aliwakabidhi mamlaka wanaume wenye kutegemeka kama vile Timotheo na Tito. Bila shaka, kazi ya ndugu hao ilimpunguzia Paulo mahangaiko aliyokuwa nayo.—Flp. 2:19, 20; Tito 1:1, 4, 5.

Kama tulivyojifunza kupitia mfano wa mtume Paulo, tunaweza kufanya nini ili tuepuke kulemewa na mahangaiko? (Tazama fungu la 13 hadi 15)

13. Wazee wanaweza kumwigaje Paulo?

13 Waombe wengine msaada. Kama Paulo, leo wazee wengi wenye hisia-mwenzi hupatwa na mahangaiko ndugu na dada zao kutanikoni wanapopatwa na matatizo. Lakini huenda mzee wa kutaniko asiweze kuwasaidia wote. Sifa ya kiasi itamchochea awakabidhi majukumu wanaume wengine wenye kustahili na kuwazoeza vijana ili wamsaidie kulitunza kundi la Mungu.—2 Tim. 2:2.

14. Paulo hakuogopa nini, na tunajifunza nini kutokana na mfano wake?

14 Tambua kwamba unahitaji faraja. Paulo alikuwa mnyenyekevu, hivyo alitafuta faraja na alikubali kutiwa moyo na rafiki zake. Ni wazi hakuogopa kwamba angeonwa na watu kuwa dhaifu kwa kukubali faraja kutoka kwa rafiki zake. Kwenye barua yake kwa Filemoni, Paulo alisema hivi: “Nilipata shangwe nyingi na faraja niliposikia kuhusu upendo wako.” (Flm. 7) Paulo aliwataja wafanyakazi wenzake kadhaa ambao walimtia moyo sana katika nyakati za taabu. (Kol. 4:7-11) Tunapokubali kwa unyenyekevu kwamba tunahitaji kutiwa moyo, ndugu na dada zetu watafurahia kutupatia msaada tunaohitaji.

15. Paulo alifanya nini alipokuwa katika hali ngumu yenye kutaabisha?

15 Tegemea Neno la Mungu. Paulo alijua kwamba Maandiko yangemfariji. (Rom. 15:4) Pia, yangempatia hekima ya kukabiliana na jaribu lolote. (2 Tim. 3:15, 16) Alipokuwa amefungwa gerezani kwa mara ya pili huko Roma, Paulo aliona kwamba kifo chake kilikuwa karibu. Akiwa kwenye hali hiyo yenye kutaabisha, Paulo alifanya nini? Alimwomba Timotheo ampelekee haraka “vitabu vya kukunjwa.” (2 Tim. 4:6, 7, 9, 13) Kwa nini? Kwa sababu huenda vitabu hivyo vya kukunjwa vilikuwa na Maandiko ya Kiebrania ambayo Paulo angetumia alipojifunza Biblia kibinafsi. Tunapomwiga Paulo kwa kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida, Yehova atatumia Maandiko kutubembeleza—hata iwe tunakabili matatizo gani.

MAMBO TUNAYOJIFUNZA KUTOKA KWA MFALME DAUDI

Kama ilivyokuwa katika kisa cha Mfalme Daudi, ni nini kinachoweza kutusaidia tukifanya dhambi nzito? (Tazama fungu la 16 hadi 19)

16. Daudi alijisababishia mahangaiko gani?

16 Daudi alikuwa na sababu ya kuwa na mahangaiko kwa kuwa dhamiri yake ilikuwa na hatia. Alikuwa amefanya uzinzi na Bath-sheba, akafanya mipango ili mume wake auawe, na kwa muda fulani akajaribu kuficha dhambi zake. (2 Sam. 12:9) Mwanzoni, Daudi aliipuuza dhamiri yake. Matokeo ni kwamba aliathirika kiroho, kiakili, na kimwili pia. (Zab. 32:3, 4) Ni nini kilichomsaidia Daudi akabiliane na mahangaiko aliyokuwa amejisababishia, na ni nini kinachoweza kutusaidia ikiwa tutafanya dhambi nzito?

17. Maneno yaliyo kwenye Zaburi 51:1-4 yanafunuaje toba ya Daudi ya kutoka moyoni?

17 Sali ili kuomba msamaha. Hatimaye Daudi alisali kwa Yehova. Alitubu kutoka moyoni na kuungama dhambi zake. (Soma Zaburi 51:1-4.) Kwa kufanya hivyo alipata kitulizo kikubwa sana! (Zab. 32:1, 2, 4, 5) Ukifanya dhambi nzito, usijaribu kuificha. Badala yake, ungama waziwazi dhambi hiyo kwa Yehova kupitia sala. Baada ya kufanya hivyo, utapata kitulizo kutokana na mahangaiko yanayosababishwa na dhamiri yenye hatia. Lakini ikiwa unataka kurekebisha uhusiano wako pamoja na Yehova, unahitaji kufanya mengi zaidi ya kusali tu.

18. Daudi aliitikiaje alipotiwa nidhamu?

18 Kubali nidhamu. Yehova alipomtuma nabii Nathani akafunue dhambi ya Daudi, Daudi hakujitetea au kujaribu kupunguza uzito wa dhambi yake. Mara moja, alikiri kwamba hakuwa amemtendea dhambi mume wa Bath-sheba tu, lakini jambo baya hata zaidi alikuwa amemtendea dhambi Yehova. (2 Sam. 12:10-14) Ikiwa tumefanya dhambi nzito, tunahitaji kuzungumza na wale ambao Yehova amewaweka rasmi ili kutuchunga. (Yak. 5:14, 15) Na ni lazima tuepuke mwelekeo wa kujitetea. Kadiri tunavyokubali na kutii haraka nidhamu yoyote tuliyopewa, ndivyo tutakavyopata tena amani na shangwe.

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Azimia kutorudia makosa yaleyale. Mfalme Daudi alijua kwamba ili aepuke kurudia dhambi zilezile, alihitaji msaada wa Yehova. (Zab. 51:7, 10, 12) Baada ya kusamehewa na Yehova, Daudi aliazimia kuepuka mawazo yasiyofaa. Matokeo ni kwamba alipata amani ya moyoni.

20. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini msamaha wa Yehova?

20 Tunaonyesha kwamba tunathamini msamaha wa Yehova kwa kuomba tusamehewe, kwa kukubali nidhamu, na kwa kujitahidi kabisa kuepuka kurudia makosa yaleyale. Tukifanya mambo hayo, tutapata tena amani ya moyoni. James, ndugu aliyefanya dhambi nzito, alijionea ukweli wa jambo hilo. Anasema hivi: “Nilipoungama dhambi yangu kwa wazee, nilihisi kana kwamba nimetua mzigo mzito. Nilianza kupata tena amani ya akili.” Ni jambo linalotia moyo sana kujua kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; huwaokoa waliopondeka roho”!—Zab. 34:18.

21. Tunaweza kufanya nini ili Yehova atubembeleze?

21 Kadiri siku hizi za mwisho zinavyokaribia kwisha, ndivyo mambo yanayoleta mahangaiko yatakavyozidi kuongezeka. Unapolemewa na mawazo yanayohangaisha, usikawie kumwomba Yehova msaada. Jifunze Biblia kwa bidii. Jifunze kutokana na mfano wa Hana, Paulo, na Daudi. Mwombe Baba yako wa mbinguni akusaidie kutambua chanzo cha mahangaiko yako. (Zab. 139:23) Mruhusu akubebee mizigo yako, hasa mizigo ambayo inapita uwezo wako. Ukifanya hivyo, utakuwa kama mtunga zaburi aliyemwimbia Yehova hivi: “Mahangaiko yaliponilemea, ulinifariji na kunibembeleza.”—Zab. 94:19.

WIMBO 4 “Yehova Ni Mchungaji Wangu”

^ fu. 5 Nyakati nyingine, sisi sote huwa na wasiwasi au mahangaiko kwa sababu ya matatizo tunayokabili. Makala hii itazungumzia mifano mitatu ya watumishi wa Yehova katika nyakati za Biblia ambao walilemewa na mahangaiko. Pia, itazungumzia jinsi Yehova alivyomfariji na kumbembeleza kila mmoja wao.

^ fu. 1 UFAFANUZI WA MANENO: Kuwa na mahangaiko ni kuwa na hisia za wasiwasi, hofu, au mkazo. Hali hiyo inaweza kusababishwa na matatizo ya kiuchumi, ya kiafya, ya kifamilia, au matatizo mengine. Pia, tunaweza kupatwa na mahangaiko au mkazo kwa sababu ya makosa tuliyofanya zamani, au changamoto ambazo tunahisi huenda tutakabili wakati ujao.