Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 11

Je, Uko Tayari Kubatizwa?

Je, Uko Tayari Kubatizwa?

“Ubatizo . . . unawaokoa ninyi sasa pia.”—1 PET. 3:21.

WIMBO 28 Kuwa Rafiki ya Yehova

MUHTASARI *

1. Mtu anapaswa kufanya nini kabla ya kuanza kujenga nyumba?

MWAZIE mtu ambaye anaamua kujenga nyumba na amechagua aina ya nyumba ambayo angependa kujenga. Je, ataenda mara moja kununua vifaa na kuanza ujenzi? Hapana. Kabla ya kuanza ujenzi, anapaswa kufanya jambo fulani muhimu—anapaswa kuhesabu gharama itakayohusika. Kwa nini? Kwa sababu anahitaji kujua ikiwa ana pesa za kutosha ili kukamilisha ujenzi wa nyumba hiyo. Akihesabu gharama kwa makini kabla ya kuanza ujenzi, kuna uwezekano mkubwa zaidi kwamba atafanikiwa kukamilisha nyumba yake mpya.

2. Kulingana na Luka 14:27-30, unapaswa kufikiria kwa makini kuhusu nini kabla ya kubatizwa?

2 Je, upendo na uthamini wako kwa Yehova umekuchochea ufikirie kubatizwa? Ikiwa ndivyo, hali yako inafanana na ya mtu anayetaka kujenga nyumba. Kwa nini tunasema hivyo? Fikiria maneno ya Yesu kwenye Luka 14:27-30. (Soma.) Yesu alikuwa akizungumzia maana ya kuwa mwanafunzi wake. Ili tuwe wafuasi wake, ni lazima tuwe tayari kukubali “gharama” zinazohusika, yaani, tuwe tayari kukabili changamoto na kudhabihu mambo fulani. (Luka 9:23-26; 12:51-53) Hivyo kabla ya kubatizwa, unahitaji kufikiria kwa makini mambo yote yanayohusika. Ndipo utakapokuwa tayari zaidi kuendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu ukiwa Mkristo aliyebatizwa.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Je, kuna faida yoyote ya kujitahidi kuwa mwanafunzi wa Kristo aliyebatizwa? Bila shaka! Ubatizo hufungua mlango wa baraka nyingi sana sasa na wakati ujao. Acheni tuzungumzie maswali fulani muhimu kuhusu ubatizo. Kufanya hivyo kutakusaidia kujibu swali hili, “Je, niko tayari kubatizwa?”

MAMBO UNAYOHITAJI KUJUA KUHUSU KUJIWEKA WAKFU NA KUBATIZWA

4. (a) Kujiweka wakfu kunamaanisha nini? (b) Kama inavyotajwa kwenye Mathayo 16:24, ‘kujikana’ wenyewe kunamaanisha nini?

4 Kujiweka wakfu kunamaanisha nini? Kabla ya kubatizwa, ni lazima ujiweke wakfu. Unapojiweka wakfu, unazungumza na Yehova kutoka moyoni katika sala na kumwambia kwamba utatumia maisha yako kumtumikia yeye milele. Unapojiweka wakfu kwa Mungu, ‘unajikana’ mwenyewe. (Soma Mathayo 16:24.) Sasa unakuwa mali ya Yehova, na hilo ni pendeleo kubwa sana. (Rom. 14:8) Unamwambia kwamba kuanzia siku hiyo na kuendelea, utakazia fikira kumtumikia yeye na si kujipendeza mwenyewe. Wakfu wako ni nadhiri—ahadi nzito inayotolewa kwa Mungu. Yehova hatulazimishi kuweka nadhiri hiyo. Lakini tunapofanya hivyo, anatarajia tuitimize.—Zab. 116:12, 14.

5. Kujiweka wakfu kunahusianaje na kubatizwa?

5 Kujiweka wakfu kunahusianaje na kubatizwa? Wakfu wako ni jambo la kibinafsi unalofanya faraghani, na ni kati yako na Yehova. Ubatizo ni jambo linalofanyika hadharani; hufanywa mbele ya watazamaji na kwa kawaida hufanyika makusanyikoni. Unapobatizwa, unawaonyesha wengine kwamba tayari umejiweka wakfu kwa Yehova. * Hivyo, ubatizo wako unawaonyesha wengine kwamba unampenda Yehova Mungu wako kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zako zote, na kwamba umeazimia kumtumikia yeye milele.—Marko 12:30.

6-7. Kulingana na 1 Petro 3:18-22, ni sababu gani mbili zinazoonyesha kwamba ubatizo ni muhimu?

6 Je, kweli ni lazima mtu abatizwe? Fikiria maneno yaliyo kwenye 1 Petro 3:18-22. (Soma.) Kama tu ambavyo safina ilikuwa uthibitisho unaoonekana ulioonyesha kwamba Noa alikuwa na imani, ubatizo wako ni uthibitisho ulio wazi kwamba umejiweka wakfu kwa Yehova. Lakini je, kweli ni lazima mtu abatizwe? Ndiyo. Petro alieleza sababu. Kwanza, ubatizo ‘unakuokoa.’ Ubatizo unaweza kutuokoa ikiwa tumechukua hatua muhimu za kuonyesha kwamba tunamwamini Yesu na kusadiki kwamba alikufa kwa ajili yetu, alifufuliwa na kwenda mbinguni, na sasa “yuko mkono wa kuume wa Mungu.”

7 Pili, ubatizo hutufanya tuwe na “dhamiri njema.” Tunapojiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa, tunaingia katika uhusiano wa pekee pamoja naye. Mungu anatusamehe dhambi zetu kwa sababu tumetubu kutoka moyoni na tuna imani katika fidia. Hivyo, tunaweza kuwa na dhamiri njema mbele zake.

8. Ni jambo gani la msingi linalopaswa kukuchochea kubatizwa?

8 Ni jambo gani la msingi linalopaswa kukuchochea uchukue hatua ya kubatizwa? Kwa kuwa umekuwa ukijifunza Biblia kwa makini, umejifunza mambo mengi kumhusu Yehova, yaani, utu wake na njia zake. Mambo uliyojifunza kumhusu yamechochea moyo wako na kukusukuma umpende sana. Upendo wako kwa Yehova ndilo jambo la msingi linalopaswa kukuchochea uchukue hatua ya kubatizwa.

9. Kama inavyotajwa kwenye Mathayo 28:19, 20, inamaanisha nini kubatizwa katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu?

9 Pia, uamuzi wako wa kubatizwa unategemea kweli za Biblia ambazo umekubali. Fikiria mambo ambayo Yesu alisema alipotoa amri ya kufanya wanafunzi. (Soma Mathayo 28:19, 20.) Kulingana na Yesu, ni lazima wale wanaobatizwa wafanye hivyo “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” Hilo linamaanisha nini? Ni lazima uamini kwa moyo wako wote kweli za Biblia kumhusu Yehova; Yesu, Mwana wake; na roho takatifu. Kweli hizo ni zenye nguvu na zinaweza kugusa sana moyo wako. (Ebr. 4:12) Acheni tuzungumzie baadhi ya kweli hizo.

10-11. Ni kweli gani kumhusu Baba ambazo umejifunza na kukubali?

10 Fikiria kuhusu wakati ulipojifunza kweli hizi kumhusu Baba: ‘Jina lake ni Yehova,’ yeye ndiye ‘Aliye Juu Zaidi,’ na yeye peke yake ndiye “Mungu wa kweli.” (Zab. 83:18; Isa. 37:16) Yeye ni Muumba wetu, na “wokovu ni wa Yehova.” (Zab. 3:8; 36:9) Amefanya mipango ya kutuokoa kutoka katika dhambi na kifo na kutupatia tumaini la kuishi milele. (Yoh. 17:3) Wakfu na ubatizo wako utakutambulisha kuwa Shahidi wa Yehova. (Isa. 43:10-12) Utakuwa sehemu ya familia ya ulimwenguni pote ya waabudu wa Mungu wanaojivunia kuitwa kwa jina lake na wanaowajulisha wengine kuhusu jina hilo.—Zab. 86:12.

11 Ni pendeleo kubwa sana kuelewa yale ambayo Biblia inafundisha kumhusu Baba! Unapokubali kweli hizo zenye thamani, moyo wako utakusukuma ujiweke wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

12-13. Ni kweli gani kumhusu Mwana ambazo umejifunza na kukubali?

12 Uliitikiaje ulipojifunza kweli zifuatazo kumhusu Mwana? Yesu ndiye mtu wa pili kwa ukuu katika ulimwengu wote mzima. Alitoa uhai wake kwa hiari kuwa fidia kwa ajili yetu. Tunapoonyesha kwa matendo yetu kwamba tuna imani katika fidia hiyo, tunaweza kusamehewa dhambi zetu, tutaweza kusitawisha urafiki pamoja na Mungu, na kupata uzima wa milele. (Yoh. 3:16) Yesu ni Kuhani wetu Mkuu. Anataka kutusaidia tupate manufaa ya fidia na tuwe na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. (Ebr. 4:15; 7:24, 25) Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, Yehova atamtumia Yesu kulitakasa jina Lake, kukomesha uovu, na kuleta baraka za milele katika Paradiso inayokuja. (Mt. 6:9, 10; Ufu. 11:15) Yesu ni kielelezo chetu. (1 Pet. 2:21) Alituwekea mfano kwa kuyatoa maisha yake yote kwa ajili ya kufanya mapenzi ya Mungu.—Yoh. 4:34.

13 Unapokubali mambo ambayo Biblia inafundisha kumhusu Yesu, unaanza kumpenda Mwana mpendwa wa Mungu. Upendo huo unakuchochea utumie maisha yako kufanya mapenzi ya Mungu, kama Yesu alivyofanya. Hivyo, utasukumwa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

14-15. Ni kweli gani kuhusu roho takatifu ambazo umejifunza na kukubali?

14 Ulifikiria nini ulipojifunza kweli zifuatazo kuhusu roho takatifu? Roho takatifu si mtu bali ni nguvu ya utendaji ya Mungu. Yehova alitumia roho takatifu ili kuwaongoza waandikaji wa Biblia, na roho hiyo hutusaidia kuelewa na kutii mambo tunayosoma katika Biblia. (Yoh. 14:26; 2 Pet. 1:21) Yehova anatumia roho yake kutupatia “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7) Roho hiyo inatupatia nguvu za kuhubiri habari njema, kushinda vishawishi, kukabiliana na hali zenye kuvunja moyo, na kuvumilia matatizo. Inatusaidia kuonyesha sifa maridadi za “tunda la roho.” (Gal. 5:22) Mungu huwapatia bure roho yake wale wanaomtumaini na kumwomba kwa unyoofu roho hiyo.—Luka 11:13.

15 Tunafarijika na kutiwa moyo sana kujua kwamba waabudu wa Yehova wanaweza kuitegemea roho takatifu ili iwasaidie kumtumikia Mungu! Unapokubali kweli ambazo umejifunza kuhusu roho takatifu, utachochewa kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa.

16. Tumejifunza nini kufikia sasa katika mazungumzo yetu?

16 Uamuzi wako wa kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa ni uamuzi muhimu sana. Kama tulivyojifunza, ni lazima tuwe tayari kukubali gharama zinazohusika, yaani, changamoto na mambo tutakayodhabihu. Lakini baraka tutakazopata zinazidi kwa mbali sana gharama zinazohusika. Ubatizo unaweza kukuokoa, na utakufanya uwe na dhamiri njema mbele za Mungu. Jambo kuu linalopaswa kukuchochea uchukue hatua ya kubatizwa ni upendo wako kwa Yehova Mungu. Pia, ni lazima uamini kwa moyo wako wote kweli ulizojifunza kumhusu Baba, Mwana, na roho takatifu. Baada ya kutafakari mambo tuliyozungumzia kufikia sasa, ungejibuje swali hili, “Je, niko tayari kubatizwa?”

MAMBO UNAYOHITAJI KUFANYA KABLA YA KUBATIZWA

17. Taja baadhi ya hatua zinazoongoza kwenye ubatizo.

17 Ikiwa unahisi kwamba uko tayari kubatizwa, bila shaka tayari umechukua hatua kadhaa ili kujenga uhusiano mzuri pamoja na Yehova. * Kujifunza Biblia kwa ukawaida kumekusaidia kujua mambo mengi kumhusu Yehova na Yesu. Umesitawisha imani. (Ebr. 11:6) Unatumaini kikamili ahadi za Yehova zinazopatikana katika Biblia, na unasadiki kwamba kuwa na imani katika dhabihu ya Yesu kunaweza kukuokoa kutokana na dhambi na kifo. Umetubu dhambi zako, yaani, umesikitishwa au kujutia kutoka moyoni makosa uliyofanya, na umemwomba Yehova akusamehe. Umegeuka au umebadili maisha yako, yaani, umeacha kabisa maisha yako mabaya ya awali na umeanza kuishi maisha yanayompendeza Mungu. (Mdo. 3:19) Unatamani kuwaambia wengine kuhusu imani yako. Umestahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa na umeanza kuhubiri pamoja na kutaniko. (Mt. 24:14) Yehova anakuonea fahari kwa sababu ya kuchukua hatua hizo muhimu. Umeufanya moyo wake ushangilie sana.—Met. 27:11.

18. Unahitaji kufanya mambo gani mengine kabla ya kubatizwa?

18 Kabla ya kubatizwa kuna mambo mengine machache ambayo unahitaji kufanya. Kama tulivyojifunza awali, ni lazima ujiweke wakfu kwa Mungu. Sali kutoka moyoni ukiwa faraghani, na umwahidi kwamba utayatumia maisha yako kufanya mapenzi yake. (1 Pet. 4:2) Kisha, mjulishe mratibu wa baraza la wazee kwamba unataka kubatizwa. Atawaomba wazee fulani wa kutaniko wazungumze nawe. Tafadhali usiogope kuzungumza nao. Bila shaka, tayari ndugu hao wapendwa wanakufahamu na wanakupenda. Watapitia pamoja nawe mafundisho ya msingi ya Biblia ambayo umejifunza. Wanataka kuhakikisha kwamba unaelewa mafundisho hayo na unatambua umuhimu wa kujiweka wakfu na kubatizwa. Wakikubaliana kwamba uko tayari kubatizwa, watakujulisha kwamba unaweza kubatizwa katika kusanyiko linalofuata.

MAMBO UNAYOHITAJI KUFANYA BAADA YA KUBATIZWA

19-20. Utahitaji kufanya nini baada ya kubatizwa, na utafanya hivyo jinsi gani?

19 Baada ya kubatizwa, utahitaji kufanya nini? * Kumbuka kwamba kujiweka wakfu ni nadhiri na Yehova anatarajia uitimize. Hivyo, baada ya kubatizwa, unapaswa kuishi kulingana na wakfu wako. Utafanyaje hivyo?

20 Shirikiana kwa ukaribu na kutaniko lako. Ukiwa Mkristo aliyebatizwa, sasa wewe ni sehemu ya ‘ushirika wa akina ndugu.’ (1 Pet. 2:17) Ndugu na dada zako kutanikoni ni familia yako ya kiroho. Utaimarisha uhusiano wako pamoja nao kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Soma Neno la Mungu na ulitafakari kila siku. (Zab. 1:1, 2) Baada ya kusoma sehemu fulani ya Biblia, tenga wakati wa kutafakari kwa kina mambo uliyosoma. Ndipo maneno hayo yatakapopenya moyoni mwako. ‘Sali bila kuacha.’ (Mt. 26:41) Sala zako za unyoofu zitakufanya umkaribie Yehova zaidi. ‘Endelea kuutafuta kwanza Ufalme.’ (Mt. 6:33) Unaweza kufanya hivyo kwa kuitanguliza kazi ya kuhubiri katika maisha yako. Kwa kushiriki kwa ukawaida katika huduma, utafanya imani yako iwe na nguvu, na unaweza kuwasaidia wengine waipate barabara inayoongoza kwenye uzima wa milele.—1 Tim. 4:16.

21. Ubatizo wako utakufungulia njia ya kupata nini?

21 Uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa ndio uamuzi muhimu zaidi utakaowahi kufanya. Ni kweli kwamba kuna gharama zinazohusika. Je, kuna faida yoyote ya kutia jitihada? Bila shaka! Matatizo yoyote ambayo huenda ukakabili katika ulimwengu huu unaopitilia mbali ni ya ‘muda mfupi na ni mepesi.’ (2 Kor. 4:17) Isitoshe, ubatizo wako utakufungulia njia ya kupata maisha yenye kuridhisha sasa na “uzima ulio wa kweli” ulio mbele yetu. (1 Tim. 6:19) Hivyo tafadhali, tafakari kwa makini na usali kuhusu jinsi utakavyojibu swali hili, “Je, niko tayari kubatizwa?”

WIMBO 50 Sala Yangu ya Wakfu

^ fu. 5 Je, unafikiria kubatizwa? Ikiwa ndivyo, makala hii imetayarishwa kihususa kwa ajili yako. Tutazungumzia baadhi ya maswali muhimu kuhusu jambo hilo zito. Majibu yako kwa maswali hayo yatakusaidia kuamua ikiwa uko tayari kubatizwa.

^ fu. 19 Ikiwa bado hujamaliza kujifunza kitabu Biblia Inatufundisha Nini? na Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu, unapaswa kuendelea kujifunza pamoja na mwalimu wako wa Biblia hadi utakapomaliza vitabu hivyo viwili.