Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

“Sisi Hapa! Tutume Sisi!”

“Sisi Hapa! Tutume Sisi!”

JE, UNAPANGA kupanua huduma yako kwa kuhamia eneo lenye uhitaji, labda kwenye nchi ya kigeni? Ikiwa ndivyo, simulizi la Ndugu na Dada Bergame litakunufaisha.

Jack na Marie-Line wamekuwa katika utumishi wa wakati wote pamoja tangu mwaka wa 1988. Kwa kuwa wanajulikana kwa sifa ya kubadilikana kulingana na hali, wamepewa migawo mingi tofauti-tofauti nchini Guadeloupe na Guiana ya Ufaransa. Kwa sasa maeneo yote mawili yako chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Ufaransa. Acheni tuwaulize Jack na Marie-Line maswali machache.

Ni nini kilichokuchochea uanze utumishi wa wakati wote?

Marie-Line: Nilipokuwa nikikua nchini Guadeloupe, nilizoea kuhubiri siku nzima na mama yangu, ambaye alikuwa Shahidi mwenye bidii. Ninawapenda watu, hivyo mara tu nilipomaliza shule mwaka wa 1985, nilianza upainia.

Jack: Nikiwa kijana, nilizungukwa na watumishi wengi wa wakati wote ambao walipenda huduma. Nilikuwa na kawaida ya kufanya upainia msaidizi wakati wa likizo za shule. Nyakati nyingine wakati wa miisho juma, tungesafiri kwa basi ili kwenda kuungana na mapainia wengine katika eneo lao. Tulihubiri siku nzima na kisha tulienda kwenye ufuo wa bahari. Tulifurahia sana siku hizo!

Muda mfupi baada ya kufunga ndoa na Marie-Line mwaka wa 1988, nilijiambia, ‛Sisi tuko huru, kwa nini tusifanye mengi zaidi katika huduma?’ Nilijiunga na Marie-Line katika utumishi wa upainia. Mwaka mmoja baadaye, baada ya kuhudhuria shule ya mapainia, tuliwekwa rasmi kuwa mapainia wa pekee. Tulifurahia migawo mbalimbali nchini Guadeloupe kabla ya kuombwa tuhamie Guiana ya Ufaransa.

Mmebadilishiwa migawo mara nyingi kwa miaka hiyo yote. Ni nini kilichowasaidia kuzoea hali mpya?

Marie-Line: Akina ndugu katika Betheli ya Guiana ya Ufaransa, walijua kwamba andiko tunalolipenda sana ni Isaya 6:8. Hivyo walipotupigia simu, kwa kawaida wangeanza kwa kusema hivi kwa ucheshi, “Je, mnakumbuka andiko mnalolipenda sana?” Tulijua kwamba hilo lilimaanisha tungepata badiliko la mgawo hivyo tungejibu, “Sisi Hapa! Tutume Sisi!”

Sisi huepuka kulinganisha mgawo wetu mpya na migawo iliyopita kwa sababu hilo lingetufanya tusifurahie mgawo tulio nao. Pia, sisi huchukua hatua ya kwanza kuwajua vizuri ndugu na dada zetu.

Jack: Wakati uliopita, baadhi ya rafiki zetu wasio na nia mbaya walijaribu kutuvunja moyo ili tusihame kwa sababu walitaka tuendelee kuishi karibu nao. Lakini tulipoondoka Guadeloupe, ndugu mmoja alitukumbusha maneno ya Yesu yaliyo kwenye Mathayo 13:38: “Shamba ni ulimwengu.” Hivyo, tunapopata mgawo mpya tunajikumbusha kwamba bado tunaendelea kutumikia kwenye shamba lilelile haidhuru tuko wapi. Isitoshe, jambo muhimu zaidi ni watu tunaokutana nao na eneo tunalotumikia!

Tunapofika katika eneo jipya, tunaona kwamba wengine wamefaulu kuishi hapo kwa furaha. Hivyo, tunajitahidi kuishi kama wenyeji wanavyoishi. Vyakula vinaweza kuwa tofauti, lakini tunakula wanachokula na kunywa wanachokunywa, huku tukizingatia usalama wa afya yetu. Tunajitahidi kuzungumzia mambo mazuri kuhusu kila mgawo tunaopata.

Marie-Line: Pia, tunajifunza mambo mengi kutoka kwa ndugu wenyeji. Ninakumbuka tulipowasili Guiana ya Ufaransa kwa mara ya kwanza. Mvua kubwa ilikuwa ikinyesha, hivyo nilifikiri kwamba tulihitaji kusubiri ili mvua iache kunyesha ndipo twende kuhubiri. Lakini dada mmoja akaniuliza, “Tunaweza kwenda?” Nilimjibu kwa mshangao, “Tutaendaje?” Akaniambia, “Chukua mwavuli wako, na tutaenda kwa baiskeli zetu.” Hivyo, nikajifunza kuendesha baiskeli huku nimeshika mwavuli. Ikiwa nisingejifunza mbinu hiyo, nisingehubiri kamwe katika msimu wa mvua!

Mmehama mara 15 hivi. Je, mna mapendekezo yoyote kuhusu kuhama yatakayowasaidia wengine?

Marie-Line: Kuhama kunaweza kuwa changamoto. Ingawa hivyo, ni muhimu kutafuta mahali pazuri pa kuishi patakapokustarehesha baada ya kutoka utumishini.

Jack: Kwa kawaida mimi hupiga rangi upya sehemu ya ndani ya nyumba tunayohamia. Wakitambua kwamba huenda tusikae kwenye mgawo huo kwa muda mrefu sana, nyakati nyingine akina ndugu katika ofisi ya tawi huniambia, “Jack, wakati huu usihangaike kupiga rangi!”

Marie-Line ni stadi wa kufunga mizigo! Anaweka kila kitu kwenye maboksi na kuyaweka lebo zilizoandikwa “bafuni,” “chumba cha kulala,” “jikoni,” na kadhalika. Hivyo, tunapowasili kwenye makao yetu mapya, inakuwa rahisi zaidi kuweka kila boksi kwenye chumba husika. Yeye huorodhesha vitu vilivyomo katika kila boksi ili iwe rahisi kupata kile tunachohitaji.

Marie-Line: Kwa kuwa tumejifunza kupanga mambo vizuri, ni rahisi kuanza utendaji wetu mara moja.

Mnapangaje wakati wenu ili ‘kutimiza kikamili huduma yenu’?—2 Tim. 4:5.

Marie-Line: Siku ya Jumatatu, tunapumzika na kujitayarisha kwa ajili ya mikutano. Kuanzia Jumanne na kuendelea tunaenda kuhubiri.

Jack: Ingawa tuna takwa la saa, hatukazii fikira jambo hilo. Huduma yetu ndilo jambo tunalotanguliza maishani. Kuanzia tunapoondoka nyumbani hadi tunaporudi, tunajitahidi kuzungumza na kila mtu tunayekutana naye.

Marie-Line: Kwa mfano, tunapoenda kwenye matembezi, sikuzote mimi hubeba trakti. Baadhi ya watu huja kutuomba machapisho, hata ingawa hatujawaambia kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova. Hivyo, tunakuwa waangalifu kuhusu kile tunachovaa na jinsi tunavyojiendesha. Watu huona mambo kama hayo.

Jack: Pia, tunatoa ushahidi kwa kuwa majirani wema. Mimi huokota karatasi, ninaondoa takataka, na kukusanya majani nje ya nyumba yetu. Jirani zetu huona jambo hilo na nyakati nyingine wananiuliza, “Unaweza kuwa na Biblia kwa ajili yangu?”

Umehubiri mara nyingi katika maeneo ya mbali. Je, kuna safari yoyote kati ya hizo ambayo unaikumbuka sana?

Jack: Nchini Guiana, kuna baadhi ya maeneo ambayo si rahisi kuhubiri. Mara nyingi tunalazimika kusafiri kilomita 600 kwa juma moja kwenye barabara mbaya. Hatutasahau kamwe ziara yetu huko St. Élie, kwenye msitu wa Amazoni. Tulitumia saa kadhaa ili kufika huko tukitumia gari lenye uwezo wa kupita kwenye maeneo yasiyopitika kwa urahisi na pia mashua yenye injini. Watu wengi walioishi huko walikuwa wachimba-dhahabu. Ili kutushukuru kwa sababu ya machapisho tuliyowapa, baadhi yao walitupatia vipande vidogo vya dhahabu kama mchango! Jioni, tuliwaonyesha mojawapo ya video za tengenezo. Wenyeji wengi walikuja kuiona.

Marie-Line: Hivi karibuni, Jack alipewa mgawo wa kutoa hotuba ya Ukumbusho huko Camopi. Ili kufika huko, tulisafiri kwa saa nne kwa kutumia mashua yenye injini kwenye Mto Oyapock. Ilikuwa safari yenye kusisimua sana.

Jack: Mahali ambapo maji ya mto ni yenye kina kifupi, maporomoko ya maji yanaweza kuwa hatari sana. Nakuhakikishia kwamba inavutia sana kuyatazama maporomoko hayo mashua inapoyakaribia. Mwendesha-mashua anapaswa kujua anachofanya. Lakini lilikuwa tukio lenye kusisimua. Ingawa kulikuwa na Mashahidi 6 tu, watu 50 hivi walihudhuria Ukumbusho, kutia ndani Wahindi wenyeji!

Marie-Line: Vijana wanaweza kufurahia jambo kama hilo lililoonwa lenye kusisimua ikiwa watajitoa zaidi kwa Yehova. Unahitaji kumtumaini Yehova katika hali kama hizo, na imani yako itazidi kuimarishwa. Mara nyingi sisi hujionea mkono wa Yehova ukitenda.

Mmejifunza lugha kadhaa. Je, mna uwezo wa pekee wa kujifunza lugha?

Jack: Hapana. Nilijifunza lugha hizo kwa sababu kulikuwa na uhitaji. Nililazimika kuongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi katika lugha ya Sranantongo * hata kabla ya kushughulikia mgawo wa usomaji wa Biblia! Nilimwomba ndugu mmoja anieleze jinsi nilivyoshughulikia mgawo huo. Alisema, “Nyakati nyingine hatukuelewa baadhi ya maneno, lakini ulifanya vizuri sana.” Watoto walinisaidia sana. Nilipokosea wangeniambia, lakini watu wazima hawakufanya hivyo. Nilijifunza mengi kutoka kwa watoto.

Marie-Line: Katika eneo moja, nilijifunza Biblia na watu katika Kifaransa, Kireno, na Kisranantongo. Dada mmoja alinipendekezea nianze kuongoza funzo katika lugha ambayo ni ngumu zaidi kwangu na kumalizia na lugha ninayoifahamu zaidi. Punde si punde nilielewa kwa nini alinipa ushauri huo.

Siku moja, nilijifunza Biblia na mtu katika Kisranantongo na mwingine katika Kireno. Nilipoanza kuongoza funzo la pili, dada tuliyeandamana naye aliniambia, “Marie-Line, kuna shida kidogo!” Nikatambua kwamba nilikuwa nikizungumza Kisranantongo badala ya Kireno na mwanamke kutoka Brazili!

Mnapendwa sana na ndugu na dada mliowatumikia. Mmefauluje kuwa na urafiki wa karibu pamoja nao?

Jack: Methali 11:25 inasema: “Mtu mkarimu atapata ufanisi.” Hatusiti kujitoa wenyewe kwa ajili ya wengine. Tulipokuwa tukifanya udumishaji wa Jumba la Ufalme, baadhi ya akina ndugu waliniambia: “Acha wahubiri wafanye kazi hiyo.” Lakini nikawajibu: “Hata mimi ni mhubiri pia. Hivyo, ikiwa kuna kazi ya kufanya, ningependa kuifanya.” Ingawa sisi sote tunapenda kuwa na faragha, mara kwa mara tunajikumbusha kwamba hatupaswi kuruhusu faragha yetu ituzuie kuwatendea wengine mema.

Marie-Line: Tunajitahidi kuwaonyesha ndugu na dada upendezi wa kibinafsi. Kwa njia hiyo, tunajua ni wakati gani ambao wanahitaji mtu wa kukaa na watoto wao au kuwachukua kutoka shuleni. Hivyo, tunaweza kupanga upya mipango yetu ili tuweze kuwasaidia. Kwa njia hiyo, tunasitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja na wengine kwa kuwa tayari kuwasaidia wanapohitaji msaada.

Mmepata baraka gani kwa kutumikia katika eneo lenye uhitaji?

Jack: Utumishi wa wakati wote umeboresha maisha yetu. Kwa kawaida sisi hupata fursa ya kufurahia uumbaji mbalimbali wa Yehova. Ingawa tumekabili changamoto mbalimbali, tuna amani ya akili kwa sababu tunajua kwamba watu wa Mungu watatutegemeza popote tulipo.

Nikiwa kijana, nilifungwa gerezani katika Guiana ya Ufaransa kwa sababu ya msimamo wangu wa Kikristo wa kutounga mkono upande wowote. Sikuwahi kuwazia kamwe kwamba ningerudi huko siku moja nikiwa mmishonari na kuruhusiwa kuwahubiria wafungwa nikiwa mhudumu wa kidini. Kwa kweli, Yehova hutoa baraka zake kwa ukarimu!

Marie-Line: Shangwe yangu kubwa inatokana na kujitoa kwa ajili ya wengine. Tunafurahia kuwa katika utumishi wa Yehova. Pia, umetufanya tuwe na uhusiano wa karibu zaidi tukiwa wenzi wa ndoa. Nyakati nyingine, Jack angeniuliza ikiwa tunaweza kuwaalika kwa ajili ya chakula wenzi wa ndoa waliovunjika moyo. Mara nyingi ningejibu, “Nilikuwa nikifikiria jambo hilohilo!” Mara nyingi mambo huwa hivyo.

Jack: Karibuni, niligunduliwa kuwa na saratani ya tezi dume. Ingawa Marie-Line hapendi kusikia maneno haya, nimekuwa nikimwambia hivi: “Mpenzi, ikiwa nitakufa kesho, sitakuwa ‘nimeishi maisha marefu.’ Lakini nitakufa nikiwa nimeridhika, nikijua kwamba nimejaza maisha yangu mambo ya kiroho, mambo yaliyo na thamani.”—Mwa. 25:8.

Marie-Line: Yehova amefungua milango ambayo hatukutarajia na kuturuhusu tufanye mambo ambayo hatungeweza kuwazia. Kwa kweli, maisha yetu yamejaa vitu vyema. Tukiwa na uhakika kamili kwa Mungu, popote ambapo tengenezo lake linatuomba twende, huko ndiko tutakapoenda!

^ fu. 32 Lugha ya Sranantongo ni mchanganyiko wa lugha ya Kiingereza, Kiholanzi, Kireno, na lugha kadhaa za Afrika, na ilianzishwa na watumwa.