Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 13

Pendaneni Sana

Pendaneni Sana

“Pendaneni sana kutoka moyoni.”—1 PET. 1:22.

WIMBO 109 Pendaneni Sana Kutoka Moyoni

MUHTASARI *

Katika usiku wa mwisho pamoja na mitume wake, Yesu alikazia kuhusu upendo (Tazama fungu la 1 na 2)

1. Yesu aliwapa wanafunzi wake amri gani hususa? (Tazama picha kwenye jalada.)

USIKU uliotangulia kifo chake, Yesu aliwapa wanafunzi wake amri hususa. Aliwaambia hivi: “Kama vile ambavyo nimewapenda, nanyi mpendane vivyo hivyo.” Kisha aliongeza hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.”—Yoh. 13:34, 35.

2. Kwa nini ni muhimu kuwaonyesha wengine upendo?

2 Yesu alisema kwamba wanafunzi wake wa kweli wangetambuliwa waziwazi ikiwa wangeonyesha upendo uleule ambao yeye alionyesha. Maneno hayo yalithibitika kuwa ya kweli katika karne ya kwanza, na ni ya kweli hata leo. Hivyo, ni jambo la maana sana kwamba tushinde changamoto zozote zinazoweza kutuzuia kuwaonyesha wengine upendo!

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Kwa kuwa sisi si wakamilifu ni vigumu kwetu kuwapenda sana wengine. Licha ya hilo, ni lazima tujitahidi kumwiga Kristo. Katika makala hii, tutazungumzia jinsi upendo unavyotusaidia kuwa wafanya amani, kutokuwa na ubaguzi, na kuwa wakaribishaji wageni. Unapojifunza habari hii, jiulize hivi: ‘Ninajifunza nini kutoka kwa ndugu na dada ambao wameendelea kuonyesha upendo licha ya changamoto mbalimbali?’

UWE MWENYE KUFANYA AMANI

4. Kulingana na Mathayo 5:23, 24, kwa nini tunapaswa kufanya amani pamoja na ndugu aliye na jambo fulani dhidi yetu?

4 Yesu alitufundisha umuhimu wa kufanya amani pamoja na ndugu aliye na jambo fulani dhidi yetu. (Soma Mathayo 5:23, 24.) Alikazia kwamba tunahitaji kudumisha uhusiano mzuri pamoja na wengine ikiwa tunataka kumpendeza Mungu. Yehova anafurahi tunapojitahidi kufanya yote tuwezayo ili kufanya amani pamoja na ndugu zetu. Hatakubali ibada yetu ikiwa tutaendelea kuwa na kinyongo na kukataa hata kujaribu kufanya amani.—1 Yoh. 4:20.

5. Ni nini kilichofanya iwe vigumu kwa ndugu mmoja kufanya amani?

5 Huenda ikawa vigumu kwetu kufanya amani. Kwa nini? Fikiria jambo lililompata Mark. * Aliumia sana wakati ndugu mmoja alipomchambua na kuwaeleza wengine kutanikoni mambo mabaya kumhusu. Mark alitendaje? Anasema hivi: “Nilishindwa kujizuia nami nikazungumza naye kwa hasira.” Hata hivyo, baadaye, Mark alijutia jambo alilofanya na akajaribu kumwomba msamaha ndugu huyo ili kurudisha amani pamoja naye. Lakini ndugu huyo alikataa kufanya amani pamoja na Mark. Mwanzoni, Mark alijiambia hivi, ‘Kwa nini mimi niendelee kufanya jitihada ikiwa yeye hataki kufanya amani?’ Hata hivyo, mwangalizi wa mzunguko alimtia moyo Mark asikate tamaa. Mark alichukua hatua gani?

6. (a) Mark alifuatiliaje amani? (b) Mark alitumiaje kanuni ya Wakolosai 3:13, 14?

6 Mark alipochanganua njia yake ya kufikiri, alitambua kwamba alikuwa amekosa unyenyekevu na alikuwa na mwelekeo wa kujiona kuwa mwadilifu kupita kiasi. Aligundua kwamba alihitaji kubadili mtazamo wake. (Kol. 3:8, 9, 12) Kwa unyenyekevu, alienda kwa ndugu huyo tena na kumwomba msamaha kwa jambo alilokuwa amefanya. Pia, Mark alimwandikia ndugu huyo barua kadhaa, akitaja jinsi alivyosikitika na jinsi alivyotamani warudishe tena urafiki waliokuwa nao. Mark hata alimpa ndugu huyo zawadi ndogo-ndogo ambazo alihisi kwamba zingemfurahisha. Kwa kusikitisha, ndugu huyo aliendelea kuwa na kinyongo. Hata hivyo, Mark aliendelea kutii amri ya Yesu ya kumpenda ndugu yake na kuwa mwenye kusamehe. (Soma Wakolosai 3:13, 14.) Hata wengine wasipoitikia vizuri jitihada zetu za kufanya amani, upendo wa kweli wa Kikristo utatusaidia tuendelee kuwasamehe na kusali ili tuwe na amani pamoja nao tena.—Mt. 18:21, 22; Gal. 6:9.

Huenda tukahitaji kufanya zaidi ya jambo moja ili kurudisha amani (Tazama fungu la 7 na 8) *

7. (a) Yesu alituhimiza tufanye nini? (b) Dada mmoja alikabili hali gani ngumu?

7 Yesu alituhimiza tuendelee kuwatendea wengine kama ambavyo tungependa tutendewe. Pia, alisema kwamba hatupaswi kuwapenda tu wale wanaotupenda. (Luka 6:31-33) Ingawa si jambo la kawaida, vipi ikiwa ndugu au dada kutanikoni anakuepuka na kukataa kukusalimia? Dada Lara alikabili hali kama hiyo. Anaeleza hivi: “Dada fulani aliniepuka, na sikujua sababu. Nilipatwa na mkazo mkubwa sana na sikufurahia kwenda mikutanoni.” Mwanzoni, Lara alijiambia hivi: ‘Sijakosea. Isitoshe, wengine kutanikoni wanahisi pia kwamba dada huyo ana tabia za ajabu.’

8. Lara alifanya nini ili kurudisha amani, na kisa chake kinatufundisha nini?

8 Lara aliamua kuchukua hatua za kufanya amani. Alisali kwa Yehova na akaamua kuzungumza na dada huyo. Walizungumzia tatizo hilo, wakakumbatiana, na kufanya amani. Kila kitu kilionekana kuwa sawa. Lara anaeleza hivi: “Lakini baadaye, dada huyo alianza kunitendea kama alivyokuwa akinitendea mwanzoni. Nilivunjika moyo sana.” Mwanzoni, Lara alihisi kwamba angekuwa na furaha ikiwa tu dada huyo angebadili mtazamo wake. Hata hivyo, mwishowe Lara alitambua kwamba jambo bora zaidi la kufanya ni kuendelea kumtendea kwa upendo dada huyo na ‘kumsamehe kwa hiari.’ (Efe. 4:32–5:2) Lara alikumbuka kwamba upendo wa kweli wa Kikristo “hauweki hesabu ya ubaya. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” (1 Kor. 13:5, 7) Lara alipata tena amani ya akili. Baada ya muda, yule dada alianza kumwonyesha urafiki zaidi. Uwe na hakika kwamba unapofuatilia amani pamoja na ndugu na dada zako na kuendelea kuwapenda, ‘Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nawe.’—2 Kor. 13:11.

USIWE NA UBAGUZI

9. Kulingana na Matendo 10:34, 35, kwa nini hatupaswi kuwa wabaguzi?

9 Yehova hana ubaguzi. (Soma Matendo 10:34, 35.) Tusipowabagua wengine, tunathibitisha kwamba sisi ni watoto wa Yehova. Tunatii amri ya kuwapenda jirani zetu kama tunavyojipenda, na tunadumisha amani katika familia yetu ya kiroho.—Rom. 12:9, 10; Yak. 2:8, 9.

10-11. Dada mmoja alishindaje hisia zisizofaa?

10 Huenda isiwe rahisi kwa baadhi ya ndugu na dada kuendelea kutokuwa na ubaguzi. Kwa mfano, fikiria hali iliyompata dada anayeitwa Ruth. Alipokuwa kijana, mtu fulani kutoka nchi nyingine aliitendea familia yake jambo fulani baya sana. Jambo hilo lilimwathirije? Ruth anakiri hivi: “Nilichukia mambo yote kuhusu nchi hiyo. Nilifikiri kwamba watu wote kutoka huko, hata ndugu na dada walikuwa hivyo.” Ruth alishindaje hisia hizo zisizofaa?

11 Ruth alitambua kwamba alipaswa kushinda mawazo yake yasiyofaa. Alisoma mambo yaliyoonwa na ripoti mbalimbali kuhusu nchi hiyo katika Kitabu cha Mwaka. Anasema hivi: “Nilifanya jitihada kubwa ili niwe na maoni yanayofaa kuhusu watu kutoka katika nchi hiyo. Nilianza kuona kwamba ndugu na dada walikuwa na bidii kwa ajili ya Yehova. Nikatambua wazi kwamba wao pia ni sehemu ya undugu wetu wa ulimwenguni pote.” Hatua kwa hatua, Ruth alitambua kwamba alihitaji kuonyesha upendo zaidi. Anaeleza hivi: “Popote nilipokutana na ndugu na dada kutoka nchi hiyo, nilifanya jitihada ya pekee ya kuwaonyesha urafiki. Nilizungumza nao na nikawafahamu vizuri zaidi.” Ikawaje? Ruth anasema hivi: “Baada ya muda, hisia zangu zisizofaa zilitoweka.”

Ikiwa tunaupenda sana “ushirika mzima wa akina ndugu,” hatutakuwa na ubaguzi (Tazama fungu la 12 na 13) *

12. Dada anayeitwa Sarah alikuwa na tatizo gani?

12 Huenda wengine wakawa na ubaguzi na wasitambue jambo hilo. Kwa mfano, Sarah alifikiri kwamba hana ubaguzi kwa sababu hakuwabagua watu kwa msingi wa rangi yao, hali yao ya kifedha, au mapendeleo waliyokuwa nayo katika tengenezo. Lakini anakiri hivi: “Nilianza kutambua kwamba kwa kweli nilikuwa na ubaguzi.” Jinsi gani? Sarah alilelewa katika familia iliyokuwa na watu wasomi na alipendelea kushirikiana na watu waliokuwa na malezi kama yake. Wakati fulani hata aliwahi kumwambia hivi rafiki yake: “Mimi hushirikiana na waabudu wenzangu ambao ni wasomi. Sishirikiani na ndugu na dada ambao si wasomi.” Kwa kweli, Sarah alihitaji kubadili mtazamo wake. Jinsi gani?

13. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Sarah alivyobadili mtazamo wake?

13 Mwangalizi wa mzunguko alimsaidia Sarah achunguze mtazamo wake. Sarah anaeleza hivi: “Alinipongeza kwa sababu ya kumtumikia Yehova kwa uaminifu, kwa maelezo yangu mazuri, na ujuzi wangu wa Maandiko. Kisha alinieleza kwamba kadiri ujuzi wetu unavyozidi kuongezeka, tunahitaji pia kusitawisha sifa za Kikristo kama vile unyenyekevu, kiasi, na rehema.” Sarah aliyachukulia kwa uzito maneno ya mwangalizi wa mzunguko. Anasema hivi: “Kwa kweli, nilitambua kwamba jambo muhimu zaidi ni kuwa mwenye fadhili na mwenye upendo.” Hivyo, Sarah akaanza kuwaona ndugu na dada zake kwa njia tofauti. Anaeleza hivi: “Nilijitahidi kuelewa sifa zinazowafanya wawe na thamani mbele za Yehova.” Namna gani sisi? Hatungependa kamwe kujiona kuwa bora kuliko wengine kwa sababu ya elimu yetu! Ikiwa tunaupenda sana “ushirika mzima wa akina ndugu,” hatutakuwa na ubaguzi.—1 Pet. 2:17.

UWE MKARIBISHAJI WAGENI

14. Kulingana na Waebrania 13:16, Yehova anahisije tunapoonyesha sifa ya ukaribishaji wageni?

14 Yehova anathamini sana sifa ya ukaribishaji wageni. (Soma Waebrania 13:16.) Anaiona kuwa sehemu ya ibada yetu, hasa tunapowasaidia wale walio na uhitaji. (Yak. 1:27; 2:14-17) Hivyo, Maandiko yanatutia moyo ‘tuwe wakaribishaji wageni.’ (Rom. 12:13) Tunapoonyesha sifa ya ukaribishaji wageni tunaonyesha kwamba tunawajali sana wengine, tunawapenda, na sisi ni rafiki zao. Yehova anafurahi tunaposhiriki vitu vyetu pamoja na wengine, iwe ni chakula chepesi, kinywaji, mlo, au kutumia wakati wetu pamoja nao. (1 Pet. 4:8-10) Hata hivyo, kuna changamoto ambazo huenda zikafanya iwe vigumu kwetu kuonyesha sifa ya ukaribishaji wageni.

“Wakati uliopita, sikuwa mkaribishaji wageni, lakini sasa nimebadilika na ninapata shangwe nyingi sana” (Tazama fungu la 16) *

15-16. (a) Kwa nini huenda wengine wakasita kuwa wakaribishaji wageni? (b) Edit alishindaje mambo yaliyomfanya asite kuwa mkaribishaji wageni?

15 Huenda tukasita kuwakaribisha wengine kwa sababu ya hali zetu. Fikiria mfano wa mjane anayeitwa Edit. Kabla ya kuwa Shahidi, hakupenda kushirikiana sana na wengine. Edit alihisi kwamba wengine ndio waliokuwa na hali nzuri zaidi za kuwa wakaribishaji wageni.

16 Baada ya kuwa Shahidi wa Yehova, Edit alibadili njia yake ya kufikiri. Alianza kuwa mkaribishaji wageni. Anaeleza hivi: “Jumba letu jipya la Ufalme lilipokuwa likijengwa, mzee fulani wa kutaniko aliniambia kuhusu wenzi fulani wa ndoa ambao wangekuja kusaidia katika mradi huo, na aliniomba ikiwa ningeweza kujitolea walale nyumbani kwangu kwa majuma mawili. Nilikumbuka jinsi Yehova alivyombariki mjane wa Sarefathi.” (1 Fal. 17:12-16) Edit alikubali kuwakaribisha wenzi hao. Je, alibarikiwa? Anaeleza hivi: “Yale majuma mawili yakawa miezi miwili. Katika kipindi hicho, urafiki wetu ulisitawi na kuwa wa karibu sana.” Pia, Edit amepata baraka ya kuwa na marafiki wa karibu kutanikoni. Sasa yeye ni painia wa kawaida na anafurahia kuwakaribisha nyumbani ndugu na dada anaohubiri nao ili wafurahie viburudisho. Anasema hivi: “Kutoa ni jambo linalonifanya nihisi vizuri! Na ukweli ni kwamba ninapata baraka nyingi sana ninapotoa.”—Ebr. 13:1, 2.

17. Luke na mke wake walitambua nini?

17 Huenda tayari sisi ni wakaribishaji wageni, lakini je, tunaweza kuboresha zaidi sifa hiyo? Kwa mfano, Luke na mke wake wanapenda kukaribisha wageni. Walizoea kuwaalika nyumbani kwao wazazi wao, watu wa ukoo, marafiki wa karibu, na mwangalizi wa mzunguko pamoja na mke wake. Hata hivyo, Luke anasema hivi: “Tulitambua kwamba tulikuwa tukiwaalika tu watu wetu wa karibu.” Luke na mke wake waliboreshaje sifa yao ya ukaribishaji wageni?

18. Luke na mke wake waliboreshaje sifa yao ya ukaribishaji wageni?

18 Luke na mke wake walibadili mtazamo wao walipotafakari maneno haya ya Yesu: “Mkiwapenda wale wanaowapenda, mnapata thawabu gani?” (Mt. 5:45-47) Walitambua kwamba walihitaji kumwiga Yehova, ambaye ni mkarimu kwa watu wote. Hivyo, waliamua kuwaalika ndugu na dada ambao hawakuwahi kuwaalika hapo awali. Luke anasema hivi: “Sasa sisi sote hufurahia sana pindi hizo. Kila mmoja huhisi ametiwa moyo na kuimarishwa.”

19. Tunathibitishaje kwamba sisi ni wanafunzi wa Yesu, na umeazimia kufanya nini?

19 Tumechunguza jinsi ambavyo kuwapenda sana ndugu na dada zetu kunavyoweza kutusaidia kuwa wafanya amani, kutokuwa na ubaguzi, na kuwa wakaribishaji wageni. Ni lazima tushinde hisia zozote zisizofaa na tuwapende sana ndugu na dada zetu kutoka moyoni. Tukifanya hivyo, tutakuwa na furaha na tutathibitisha kwamba kwa kweli sisi ni wanafunzi wa Yesu.—Yoh. 13:17, 35.

WIMBO 88 Nijulishe Njia Zako

^ fu. 5 Yesu alisema kwamba upendo ndiyo sifa inayowatambulisha Wakristo wa kweli. Kuwapenda ndugu na dada zetu hutuchochea tuwe wafanya amani, tusiwe na ubaguzi, na tuwe wakaribishaji wageni. Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo sikuzote. Makala hii inatoa mapendekezo hususa ya jinsi tunavyoweza kuendelea kupendana sana kutoka moyoni.

^ fu. 5 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Dada anajitahidi kufanya amani. Mwanzoni hafanikiwi, lakini hakati tamaa. Jitihada zake za kuendelea kuonyesha upendo hatimaye zinazaa matunda.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Ndugu mwenye umri mkubwa anahisi amepuuzwa na wengine kutanikoni.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Dada ambaye mwanzoni alisita kuonyesha sifa ya ukaribishaji wageni anabadili njia yake ya kufikiri, na furaha yake inaongezeka.