Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 14

Shambulizi Kutoka Kaskazini!

Shambulizi Kutoka Kaskazini!

“Taifa limeivamia nchi yangu.”—YOE. 1:6.

WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka

MUHTASARI *

1. Ndugu Russell na wenzake walitumia mbinu gani ya kujifunza, na kwa nini ilikuwa nzuri?

ZAIDI ya karne moja iliyopita, kikundi kidogo cha wanafunzi wa Neno la Mungu, yaani, Ndugu C. T. Russell pamoja na wenzake, walianza kukutanika pamoja. Walitaka kuona ikiwa wangeweza kujua mambo ambayo Biblia inafundisha hasa kumhusu Yehova Mungu, Yesu Kristo, hali ya wafu, na fidia. Mbinu waliyotumia kujifunza ilikuwa rahisi. Mmoja wao angeuliza swali, na kisha kikundi hicho kingechunguza kila andiko linalohusiana na habari hiyo. Mwishowe, wangeandika mambo waliyojifunza. Yehova aliwasaidia wanaume hao wanyoofu kuelewa kweli nyingi za msingi za Biblia ambazo tunazithamini hadi leo.

2. Ni nini ambacho huenda nyakati nyingine kikafanya tufikie mkataa usio sahihi tunapojitahidi kuelewa unabii fulani wa Biblia?

2 Hata hivyo, punde si punde wanafunzi hao wa Biblia waligundua kwamba kuna tofauti kati ya kujifunza mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu fundisho fulani, na kuelewa kwa usahihi maana ya unabii fulani wa Biblia. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba kwa kawaida unabii wa Biblia hueleweka vizuri zaidi unapokuwa ukitimia au baada ya kutimia. Lakini kuna sababu nyingine. Ili kuelewa unabii kwa usahihi, kwa ujumla tunahitaji kuchunguza muktadha wote. Ikiwa tutakazia sehemu moja tu ya unabii huo na kupuuza sehemu nyingine, huenda tukafikia mkataa usio sahihi. Inaonekana hivyo ndivyo hali ilivyokuwa kuhusiana na unabii ulio katika kitabu cha Yoeli. Acheni tuchunguze unabii huo na tuzungumzie kwa nini tunahitaji kurekebisha uelewaji wetu wa sasa.

3-4. Kufikia sasa, tumekuwa tukiuelewaje unabii ulio kwenye Yoeli 2:7-9?

3 Soma Yoeli 2:7-9. Yoeli anatabiri kwamba shambulizi la nzige litaharibu nchi ya Israeli. Nzige hao wenye pupa na walio na meno na mataya kama ya simba, watakula na kumaliza kabisa kila kitu kilicho mbele yao! (Yoe. 1:4, 6) Kwa miaka mingi, tulielewa kwamba unabii huo ulitabiri kwa njia ya mfano jinsi watu wa Yehova walio kama kundi kubwa la nzige lisiloweza kudhibitiwa, wanavyoshiriki katika kazi ya kuhubiri. Tulielewa kwamba “nchi,” au watu walio chini ya uongozi wa viongozi wa kidini wangechomwa sana moyoni kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri. *

4 Uelewaji huo ungekuwa sahihi ikiwa tungekazia tu andiko la Yoeli 2:7-9. Hata hivyo, tunapochunguza unabii huo kulingana na muktadha wake, tunatambua kwamba tunahitaji kuuelewa kwa njia tofauti. Acheni tuchunguze sababu nne zinazoonyesha kwa nini tunasema hivyo.

SABABU NNE ZA KUFANYA MABADILIKO

5-6. Ni swali gani linalozuka tunapochunguza (a) Yoeli 2:20? (b) Yoeli 2:25?

5 Kwanza kabisa, ona ahadi hii ya Yehova kuhusu shambulizi la nzige: “Nitamfukuza mbali nanyi mkaaji wa kaskazini [yaani, nzige].” (Yoe. 2:20) Ikiwa nzige wanafananisha Mashahidi wa Yehova wanaotii amri ya Yesu ya kuhubiri na kufanya wanafunzi, kwa nini Yehova aahidi kwamba atawafukuza mbali? (Eze. 33:7-9; Mt. 28:19, 20) Ni wazi kwamba Yehova hawafukuzi mbali watumishi wake waaminifu, bali kitu au mtu ambaye ni adui ya watu wake.

6 Fikiria sababu ya pili katika maneno ya Yoeli 2:25. Hapo Yehova anasema hivi: Nitafidia miaka ambayo mazao yenu yaliliwa na nzige wanaoruka katika makundi, tunutu, parare wanaokula sana, na nzige wanaokula sana, jeshi langu kubwa ambalo nililituma miongoni mwenu.” Ona kwamba Yehova anaahidi ‘kufidia’ uharibifu uliosababishwa na nzige. Ikiwa nzige wanafananisha waeneza-injili wa Ufalme, hilo lingemaanisha kwamba ujumbe wanaotangaza husababisha uharibifu. Hata hivyo, ujumbe huo kwa kweli unaweza kuwachochea baadhi ya watu waovu watubu. (Eze. 33:8, 19) Hilo lingekuwa jambo zuri sana kwao!

7. Neno “kisha” kwenye Yoeli 2:28, 29, linamaanisha nini?

7 Soma Yoeli 2:28, 29. Fikiria sababu ya tatu, yaani, mfuatano wa matukio katika unabii huo. Je, umetambua kwamba Yehova anasema: “Kisha nitaimimina roho yangu juu ya kila aina ya mwili”; yaani, baada ya nzige kukamilisha kazi waliyopewa? Ikiwa nzige ni wahubiri wa Ufalme wa Mungu, kwa nini Yehova aimimine roho yake juu yao baada ya wao kumaliza kazi yao ya kutoa ushahidi? Ukweli ni kwamba bila msaada wa roho takatifu ya Mungu yenye nguvu, hawangeweza kuendelea kuhubiri kwa miaka mingi chini ya upinzani na hata marufuku.

Ndugu J. F. Rutherford na watumishi wengine watiwa-mafuta ambao walikuwa mstari wa mbele walitangaza kwa ujasiri hukumu za Mungu dhidi ya mfumo huu mwovu wa mambo (Tazama fungu la 8)

8. Ni nani wanaofananishwa na nzige wanaotajwa kwenye Ufunuo 9:1-11? (Tazama picha kwenye jalada.)

8 Soma Ufunuo 9:1-11. Sasa tuzungumzie sababu ya nne. Hapo awali tulihusianisha unabii wa shambulizi la nzige linalotajwa kwenye Yoeli na kazi yetu ya kuhubiri, kwa sababu ya unabii mwingine unaofanana nao katika kitabu cha Ufunuo. Unabii ulio kwenye Ufunuo unafafanua kundi kubwa la nzige walio na nyuso kama za wanadamu na ‘kitu kinachoonekana kama mataji ya dhahabu’ juu ya vichwa vyao. (Ufu. 9:7) Nzige hao wanawatesa “watu [maadui wa Mungu] wasio na muhuri wa Mungu kwenye mapaji ya nyuso zao” kwa kipindi cha miezi mitano, ambacho ni wastani wa urefu wa maisha ya nzige. (Ufu. 9:4, 5) Inaonekana ufafanuzi huo unawahusu watumishi wa Yehova watiwa-mafuta. Wanatangaza kwa ujasiri hukumu za Mungu dhidi ya mfumo huu mwovu wa mambo, na jambo hilo linawafanya wale wanaouunga mkono wasiwe na amani.

9. Kuna tofauti gani kubwa kati ya nzige ambao Yoeli aliona na wale wanaotajwa na Yohana?

9 Ni kweli kwamba kuna mambo yanayofanana katika unabii ulio kwenye kitabu cha Ufunuo na ule ulio kwenye kitabu cha Yoeli. Hata hivyo, kuna tofauti kadhaa kubwa. Fikiria mambo haya: Katika unabii wa Yoeli, nzige wanaharibu mimea. (Yoe. 1:4, 6, 7) Katika maono ya Yohana, nzige wanaambiwa “wasidhuru majani ya dunia.” (Ufu. 9:4) Nzige ambao Yoeli aliona, walitoka kaskazini. (Yoe. 2:20) Nzige ambao Yohana aliona walitoka kwenye shimo refu lisilo na mwisho. (Ufu. 9:2, 3) Nzige wanaotajwa na Yoeli wanafukuzwa mbali. Kwenye Ufunuo, nzige hawafukuzwi bali wanaruhusiwa wakamilishe kazi yao. Hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba hawana kibali cha Yehova.—Tazama sanduku “ Unabii Kuhusu Nzige—Unafanana Lakini Unatofautiana.”

10. Toa mfano katika Biblia unaoonyesha kwamba nzige wanaotajwa na Yoeli na Yohana wanaweza kufananisha mambo tofauti-tofauti.

10 Tofauti hizo kubwa kati ya unabii wa Yoeli na Yohana, unafanya tufikie mkataa kwamba unabii huo hauhusiani. Je, tunasema kwamba “nzige” wanaotajwa kwenye Yoeli si sawa na “nzige” wanaotajwa kwenye kitabu cha Ufunuo? Ndiyo. Nyakati nyingine katika Biblia ni jambo la kawaida kwa mfano fulani kuwa na maana mbalimbali ikitegemea jinsi unavyotumiwa. Kwa mfano, kwenye Ufunuo 5:5, Yesu anaitwa “Simba wa kabila la Yuda,” lakini kwenye 1 Petro 5:8, Ibilisi anafafanuliwa kuwa “simba anayenguruma.” Hivyo, kwa msingi wa maswali yanayozushwa na uelewaji wetu wa sasa, tunahitaji kutafuta ufafanuzi mwingine wa unabii wa Yoeli. Unabii huo unamaanisha nini?

UNABII HUO UNAMAANISHA NINI?

11. Andiko la Yoeli 1:6 na 2:1, 8, 11 linatusaidiaje kujua utambulisho wa nzige?

11 Tunapochunguza kwa makini muktadha wa unabii wa Yoeli, tunaelewa kwamba nabii huyo alikuwa akitabiri kuhusu shambulizi la kijeshi. (Yoe. 1:6; 2:1, 8, 11) Yehova alisema kwamba angetumia ‘jeshi lake kubwa’ (wanajeshi wa Babiloni) ili kuwaadhibu Waisraeli waliokosa kutii. (Yoe. 2:25) Jeshi hilo la wavamizi linaitwa kwa usahihi “mkaaji wa kaskazini” kwa sababu Wababiloni wangeivamia Israeli kutoka kaskazini. (Yoe. 2:20) Jeshi hilo linalinganishwa na kundi kubwa la nzige lililojipanga vizuri. Yoeli anasema hivi kulihusu: “Kila [mwanajeshi] hupiga mwendo kwenye njia yake. . . . Wanaingia haraka jijini, nao hukimbia ukutani. Hupanda juu ya nyumba, na kuingia kama mwizi madirishani.” (Yoe. 2:8, 9) Wazia hali hiyo! Wanajeshi wako kila mahali. Hakuna popote pa kujificha. Hakuna yeyote anayeweza kuponyoka upanga wa Wababiloni!

12. Unabii wa Yoeli kuhusu nzige ulitimizwaje?

12 Kama nzige, Wababiloni (au, Wakaldayo) walivamia jiji la Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Biblia inasema hivi: “Mfalme wa Wakaldayo . . . ambaye aliwaua wanaume wao vijana kwa upanga . . . , hakumhurumia kijana wa kiume wala bikira, mzee wala aliye dhaifu. Mungu alitia kila kitu mikononi mwake. Aliiteketeza kabisa nyumba ya Mungu wa kweli, akaubomoa ukuta wa Yerusalemu, akateketeza kwa moto minara yake yote yenye ngome, na kuharibu kila kitu chenye thamani.” (2 Nya. 36:17, 19) Wababiloni walipomaliza kuiharibu nchi, wapita-njia walikuwa wakisema: “Ni nchi yenye ukiwa isiyo na mwanadamu wala mnyama, nayo imetiwa mikononi mwa Wakaldayo.”—Yer. 32:43.

13. Eleza maana ya Yeremia 16:16, 18.

13 Miaka 200 hivi baada ya unabii wa Yoeli, Yehova alimtumia Yeremia kutabiri jambo lingine kuhusu shambulizi hilo. Alisema kwamba wavamizi hao wangewatafuta kwa makini Waisraeli waliofanya mambo maovu—na wote wangekamatwa. “‘Tazama, ninawaita wavuvi wengi,’ asema Yehova, ‘Nao watawavua. Na baada ya hapo nitawaita wawindaji wengi, nao watawawinda kwenye kila mlima na kila kilima na kutoka kwenye mipasuko ya majabali. . . . Nitalipa kiwango kamili kinachostahili kosa lao na dhambi yao.’” Bahari wala misitu isingeweza kamwe kuwaficha Waisraeli wasiotubu dhidi ya shambulizi kutoka kwa Wababiloni.—Yer. 16:16, 18.

KURUDISHWA

14. Unabii wa Yoeli 2:28, 29 ulitimizwaje?

14 Sasa, Yoeli ana habari njema za kutangaza. Nchi itatoa mazao yake tena. (Yoe. 2:23-26) Kisha wakati fulani ujao, chakula kingi cha kiroho kingepatikana. “Nitaimimina roho yangu juu ya kila aina ya mwili,” asema Yehova, “na wana wenu na mabinti wenu watatoa unabii . . . Na hata juu ya watumwa wangu wa kiume na watumwa wa kike nitaimimina roho yangu.” (Yoe. 2:28, 29) Kumiminwa kwa roho hiyo takatifu ya Mungu hakukutendeka mara tu baada ya Waisraeli kurudishwa katika nchi yao kutoka Babiloni. Badala yake, kulitendeka karne nyingi baadaye, kwenye Pentekoste 33 W.K. Tunajuaje?

15. Kulingana na Matendo 2:16, 17, Petro alitumia maneno gani tofauti kidogo aliponukuu Yoeli 2:28, na jambo hilo linaonyesha nini?

15 Akiongozwa na roho takatifu, mtume Petro alihusianisha utimizo wa Yoeli 2:28, 29 na tukio lenye kustaajabisha lililotendeka siku ya Pentekoste. Saa tatu hivi asubuhi hiyo, roho takatifu ilimiminwa kimuujiza na kuwafanya wale walioipokea waanze kuzungumza “kuhusu mambo makuu ya Mungu.” (Mdo. 2:11) Chini ya mwongozo wa roho takatifu, Petro alitumia maneno tofauti kidogo alipokuwa akinukuu unabii wa Yoeli. Je, ulitambua tofauti ya maneno aliyotumia? (Soma Matendo 2:16, 17.) Badala ya kuanza na neno “kisha” kama Yoeli alivyofanya, Petro alitumia maneno: “Na katika siku za mwisho”—katika muktadha huu akirejelea siku za mwisho za mfumo wa Kiyahudi—ambapo Mungu angemimina roho yake “juu ya kila aina ya mwili.” Hilo linaonyesha kwamba muda mrefu ungepita kabla ya kutimizwa kwa unabii wa Yoeli.

16. Roho ya Mungu ilitimiza nini kuhusiana na kazi ya kuhubiri katika karne ya kwanza, na vipi kuhusu leo?

16 Baada ya tukio hilo lenye kustaajabisha la kumiminwa kwa roho ya Mungu katika karne ya kwanza, kazi ya kuhubiri ilianza kuenea kwa kiwango kikubwa sana. Kufikia wakati ambapo mtume Paulo aliandika barua yake kwa Wakolosai, karibu mwaka wa 61 W.K., angeweza kueleza kwamba habari njema ilikuwa imehubiriwa “katika uumbaji wote chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Katika siku za Paulo, maneno “uumbaji wote” yalimaanisha ulimwengu uliojulikana wakati huo. Kwa msaada wa roho takatifu ya Yehova yenye nguvu, kazi ya kuhubiri imefanywa kwa kiwango kikubwa hata zaidi katika siku zetu—“mpaka miisho ya dunia”!—Mdo. 13:47; tazama sanduku “ Nitaimimina Roho Yangu.”

NI NINI KILICHOBADILIKA?

17. Uelewaji wetu wa unabii wa Yoeli kuhusu nzige umebadilikaje?

17 Ni nini kilichobadilika? Sasa tunauelewa kwa usahihi zaidi unabii wa Yoeli 2:7-9. Kwa ufupi, mistari hiyo hairejelei kazi yetu ya kuhubiri tunayofanya kwa bidii, bali inarejelea shambulizi la jeshi la Babiloni dhidi ya jiji la Yerusalemu katika mwaka wa 607 K.W.K.

18. Ni nini ambacho hakijabadilika kuhusu watu wa Yehova?

18 Ni nini ambacho hakijabadilika? Watu wa Yehova wanaendelea kuhubiri habari njema kila mahali wakitumia kila njia wawezayo. (Mt. 24:14) Hakuna vizuizi vyovyote vya serikali vinavyoweza kutuzuia kutimiza kazi tuliyopewa ya kuhubiri. Na kwa msaada wa Yehova, leo kuliko wakati mwingine wowote tuna bidii hata zaidi, tukihubiri kwa ujasiri habari njema ya Ufalme! Kwa unyenyekevu tunaendelea kutafuta mwongozo wa Yehova ili kuelewa unabii wa Biblia, tukiwa na uhakika kwamba kwa wakati unaofaa, atatuongoza “kwenye kweli yote”!—Yoh. 16:13.

WIMBO 97 Uhai Unategemea Neno la Mungu

^ fu. 5 Kwa miaka mingi, tumekuwa tukiamini kwamba unabii wa Yoeli sura ya 1 na ya 2 ulitabiri kuhusu kazi yetu ya kuhubiri inayofanywa katika siku zetu. Hata hivyo, kuna sababu nne nzuri zinazoonyesha kwa nini tunahitaji kubadili uelewaji wetu kuhusu sehemu hiyo ya unabii wa Yoeli. Sababu hizo ni zipi?

^ fu. 3 Kwa mfano, tazama makala “Hekima ya Yehova Inaonekana Katika Uumbaji” katika Mnara wa Mlinzi, Aprili 15, 2009, fu. 14-16.