Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 17

“Nimewaita Rafiki”

“Nimewaita Rafiki”

“Nimewaita rafiki, kwa sababu nimewajulisha mambo yote niliyosikia kutoka kwa Baba yangu.”—YOH. 15:15.

WIMBO 13 Kristo, Kielelezo Chetu

MUHTASARI *

1. Unasitawishaje urafiki wa karibu pamoja na wengine?

KWA kawaida, hatua ya kwanza ya kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na mtu ni kutumia wakati pamoja naye. Kadiri mnavyozungumza pamoja na kushiriki mawazo na hisia zenu, ndivyo mnavyozidi kuwa marafiki. Hata hivyo, tunakabili changamoto mbalimbali inapohusu kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yesu. Baadhi ya changamoto hizo ni zipi?

2. Taja changamoto ya kwanza ambayo tunakabili.

2 Changamoto ya kwanza ni kwamba hatujawahi kukutana na Yesu ana kwa ana. Wakristo wengi wa karne ya kwanza walikabili changamoto hiyo pia. Ingawa hivyo, mtume Petro alisema hivi: “Mnampenda ingawa hamkumwona kamwe. Ijapokuwa hammwoni sasa, bado mnaonyesha imani katika yeye.” (1 Pet. 1:8) Hivyo, inawezekana kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yesu hata ingawa hatujawahi kukutana naye kibinafsi.

3. Taja changamoto ya pili ambayo tunakabili.

3 Changamoto ya pili ni kwamba hatuwezi kuzungumza na Yesu. Tunaposali, tunamweleza Yehova mawazo yetu. Ni kweli kwamba tunasali katika jina la Yesu, lakini hatuzungumzi na Yesu. Isitoshe, Yesu hataki tusali kwake. Kwa nini? Kwa sababu sala ni tendo la ibada, na ni Yehova peke yake anayepaswa kuabudiwa. (Mt. 4:10) Licha ya hilo, tunaweza kumwonyesha Yesu upendo wetu.

4. Changamoto ya tatu tunayokabili ni ipi, na tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Changamoto ya tatu ni kwamba Yesu anaishi mbinguni, hivyo hatuwezi kutumia wakati pamoja naye kihalisi. Lakini bado tunaweza kujua mengi kumhusu Yesu ingawa hatuko pamoja naye kihalisi. Tutachunguza mambo manne tunayoweza kufanya ili tuimarishe urafiki wetu pamoja naye. Lakini kwanza, acheni tuchunguze kwa nini ni muhimu kwetu kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Kristo.

KWA NINI TUNAHITAJI KUWA RAFIKI ZA YESU?

5. Kwa nini ni lazima tuwe rafiki za Yesu? (Pia, tazama sanduku “ Urafiki Pamoja na Yesu Huongoza Kwenye Urafiki Pamoja na Yehova” na “ Maoni Yenye Usawaziko Kuhusu Jukumu la Yesu.”)

5 Ikiwa tunataka kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, ni lazima tuwe rafiki za Yesu. Kwa nini? Fikiria sababu hizi mbili. Kwanza, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mmenipenda.” (Yoh. 16:27) Pia, alisema hivi: “Hakuna mtu anayekuja kwa Baba bila kupitia kwangu.” (Yoh. 14:6) Kujaribu kuwa rafiki ya Yehova bila kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Yesu ni kama kujaribu kuingia katika jengo fulani bila kupitia mlangoni. Yesu alitumia mfano kama huo alipojifafanua mwenyewe kuwa “mlango wa kondoo.” (Yoh. 10:7) Sababu ya pili ni kwamba Yesu aliiga kikamilifu sifa za Baba yake. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Yeyote ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yoh. 14:9) Hivyo, njia moja muhimu ya kumjua Yehova ni kujifunza kuhusu maisha ya Yesu. Kadiri tunavyojifunza kumhusu Yesu, ndivyo tutakavyozidi kumpenda. Na kadiri urafiki wetu pamoja naye unavyozidi kusitawi, ndivyo tutakavyozidi kumpenda Baba yake pia.

6. Kwa nini ni lazima tuwe na uhusiano wa karibu pamoja na Yesu? Eleza.

6 Ili sala zetu zijibiwe, ni lazima tuwe na uhusiano mzuri pamoja na Yesu. Hilo linamaanisha kwamba ni lazima tufanye mengi zaidi ya kuhitimisha tu sala zetu kidesturi kwa kusema, “katika jina la Yesu.” Ni lazima tutambue jinsi Yehova anavyomtumia Yesu kujibu sala zetu. Yesu aliwaambia hivi mitume wake: “Lolote mtakaloomba katika jina langu nitalifanya.” (Yoh. 14:13) Ingawa Yehova ndiye anayesikia na kujibu sala zetu, amempa Yesu mamlaka ya kutekeleza maamuzi Yake. (Mt. 28:18) Hivyo, kabla ya Mungu kujibu sala zetu, yeye hutazama ili aone ikiwa tumetii shauri ambalo Yesu alitoa. Kwa mfano, Yesu alisema hivi: “Mkiwasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia; lakini msipowasamehe watu makosa yao, naye Baba yenu hatawasamehe makosa yenu.” (Mt. 6:14, 15) Hivyo, ni jambo la muhimu sana tuwatendee wengine kwa fadhili kama Yehova na Yesu wanavyotutendea!

7. Ni nani wanaonufaika na dhabihu ya fidia ya Yesu?

7 Ni wale tu walio na urafiki wa karibu pamoja na Yesu watakaonufaika na dhabihu yake ya fidia. Tunajuaje? Yesu alisema kwamba ‘angetoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake.’ (Yoh. 15:13) Watu waaminifu walioishi kabla ya Yesu kuja duniani watahitaji kujifunza kumhusu na kuanza kumpenda. Wanaume na wanawake waaminifu kama Abrahamu, Sara, Musa, na Rahabu watafufuliwa, lakini hata watumishi hao waadilifu wa Yehova watahitaji kusitawisha urafiki pamoja na Yesu ili wapate uzima wa milele.—Yoh. 17:3; Mdo. 24:15; Ebr. 11:8-12, 24-26, 31.

8-9. Kama andiko la Yohana 15:4, 5 linavyoeleza, uhusiano wetu pamoja na Yesu unatuwezesha kutimiza nini, na kwa nini ni lazima tuendelee kukaa katika muungano pamoja na Yesu?

8 Tuna shangwe ya kushirikiana pamoja na Yesu katika kazi ya kuhubiri na kufundisha habari njema ya Ufalme. Yesu alikuwa mwalimu alipokuwa duniani. Na tangu aliporudi mbinguni, Yesu, akiwa kichwa cha kutaniko amekuwa akiendelea kuongoza kazi ya kuhubiri na kufundisha. Anaona na anathamini jitihada zako za kuwasaidia watu wengi kadiri uwezavyo wamjue yeye pamoja na Baba yake. Ukweli ni kwamba njia pekee tunayoweza kutimiza kazi hiyo ni kwa msaada wa Yehova na Yesu.—Soma Yohana 15:4, 5.

9 Neno la Mungu linafundisha wazi kwamba ni lazima tumpende Yesu na kudumisha upendo huo, ili tumpendeze Yehova. Hivyo, acheni tuchunguze mambo manne tunayoweza kufanya ili tuwe rafiki za Yesu.

JINSI YA KUSITAWISHA URAFIKI PAMOJA NA YESU

Unaweza kuwa rafiki ya Yesu (1) kwa kumjua vizuri zaidi, (2) kwa kuiga njia yake ya kufikiri na kutenda, (3) kwa kuwaunga mkono ndugu za Kristo, na (4) kwa kuunga mkono mipango ya kutaniko (Tazama fungu la 10 hadi 14) *

10. Taja hatua ya kwanza ya kusitawisha urafiki pamoja na Yesu.

10 (1) Jifunze kumhusu Yesu. Tunaweza kufanya hivyo kwa kusoma vitabu vya Biblia vya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Tunapotafakari kuhusu masimulizi ya Biblia yanayozungumzia maisha ya Yesu, tutaanza kumpenda na kumheshimu Yesu kwa sababu ya jinsi alivyoshughulika na watu kwa njia ya fadhili. Kwa mfano, ingawa alikuwa Bwana juu ya wanafunzi wake, hakuwatendea kama watumwa. Badala yake, aliwafunulia mawazo na hisia zake za ndani kabisa. (Yoh. 15:15) Yesu alihisi maumivu yao na alilia pamoja nao. (Yoh. 11:32-36) Hata wapinzani wake walikiri kwamba alikuwa rafiki ya wale walioitikia vizuri ujumbe wake. (Mt. 11:19) Tunapoiga jinsi Yesu alivyoshughulika na wanafunzi wake, tunaboresha uhusiano wetu pamoja na wengine, tunaridhika na kuwa wenye furaha zaidi, na tutampenda na kumheshimu Kristo hata zaidi.

11. Taja hatua ya pili ya kusitawisha urafiki pamoja na Yesu. Kwa nini hatua hiyo ni muhimu?

11 (2) Iga jinsi Yesu alivyotenda na kufikiri. Kadiri tunavyoijua na kuiiga njia yake ya kufikiri, ndivyo urafiki wetu pamoja naye utakavyokuwa wa karibu zaidi. (1 Kor. 2:16) Tunaweza kumwigaje Yesu? Fikiria mfano mmoja. Yesu alifikiria zaidi kuhusu kuwasaidia wengine kuliko kujipendeza mwenyewe. (Mt. 20:28; Rom. 15:1-3) Kwa sababu alikuwa na mtazamo huo wa akili, Yesu alikuwa tayari kujidhabihu na kuwasamehe wengine. Hakuwa mwepesi wa kuudhika kwa sababu ya mambo ambayo watu walimwambia. (Yoh. 1:46, 47) Na hakushikilia au kuruhusu kosa ambalo mtu alifanya zamani liathiri mtazamo wake wa sasa kumwelekea. (1 Tim. 1:12-14) Yesu alisema hivi: “Wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.” (Yoh. 13:35) Ni vema ujiulize swali hili: “Je, ninaiga mfano wa Yesu kwa kufanya yote niwezayo ili kudumisha amani pamoja na ndugu na dada zangu?”

12. Taja hatua ya tatu ya kusitawisha urafiki pamoja na Yesu. Tunaweza kuchukuaje hatua hiyo?

12 (3) Waunge mkono ndugu za Kristo. Yesu huona mambo tunayowatendea ndugu zake watiwa-mafuta kuwa mambo tunayomtendea yeye binafsi. (Mt. 25:34-40) Njia kuu tunayoonyesha kwamba tunawaunga mkono watiwa-mafuta ni kwa kushiriki kikamili katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi ambayo Yesu aliwaagiza wafuasi wake waifanye. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 10:42) Ndugu za Kristo wanaweza tu kutimiza kampeni hiyo ya kuhubiri ulimwenguni pote kwa msaada wa “kondoo wengine.”(Yoh. 10:16) Ikiwa wewe ni mmoja wa kondoo wengine, tambua kwamba kila mara unaposhiriki katika kazi hiyo, hauonyeshi tu kwamba unawapenda watiwa-mafuta, bali pia unaonyesha kwamba unampenda Yesu.

13. Tunaweza kutumiaje shauri la Yesu linalopatikana kwenye Luka 16:9?

13 Pia, tunasitawisha urafiki pamoja na Yehova na Yesu kwa kutumia pesa zetu ili kutegemeza kazi wanayoongoza. (Soma Luka 16:9.) Kwa mfano, tunaweza kutoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, na michango hiyo inaweza kutumiwa kutegemeza kazi ya kuhubiri habari njema katika maeneo ya mbali zaidi, kutegemeza ujenzi na udumishaji wa majengo yanayotegemeza ibada ya kweli, na kuwasaidia wale ambao wameathiriwa na majanga ya asili. Tunaweza pia kulitegemeza kutaniko letu kifedha na kuwasaidia wale ambao tunajua kibinafsi kwamba wana uhitaji. (Met. 19:17) Tunaweza kuwaunga mkono ndugu za Kristo katika njia hizo.

14. Kama inavyotajwa kwenye Waefeso 4:15, 16, hatua ya nne ya kusitawisha urafiki pamoja na Yesu ni ipi?

14 (4) Unga mkono mipango ya kutaniko la Kikristo. Tunaimarisha urafiki wetu pamoja na Yesu aliye kichwa cha kutaniko tunaposhirikiana na wale ambao amewaweka rasmi ili watutunze. (Soma Waefeso 4:15, 16.) Kwa mfano, kwa sasa tunajitahidi kuhakikisha kwamba Majumba yote ya Ufalme yanatumiwa kikamili. Kwa sababu hiyo, baadhi ya makutaniko yameunganishwa, na mipaka ya maeneo ya makutaniko imebadilishwa. Mpango huo umesaidia tengenezo kuokoa pesa nyingi zilizotolewa kwa ajili ya ibada ya Yehova. Kwa upande mwingine, baadhi ya wahubiri wamelazimika kuzoea hali mpya zilizoletwa na mabadiliko hayo. Huenda wahubiri hao waaminifu walitumikia katika kutaniko fulani kwa miaka mingi na huenda walikuwa na uhusiano wa karibu na ndugu na dada hapo. Lakini sasa wameombwa watumikie katika kutaniko tofauti. Lazima Yesu anafurahi sana anapowaona wahubiri hao washikamanifu wakiunga mkono mpango huo!

TUTAKUWA MARAFIKI WA YESU MILELE

15. Urafiki wetu pamoja na Yesu utazidi kuimarika jinsi gani wakati ujao?

15 Wale waliotiwa mafuta kwa roho takatifu wana tumaini la kuwa pamoja na Yesu milele, wakitawala pamoja naye katika Ufalme wa Mungu. Watakuwa pamoja na Kristo kihalisi, yaani, watamwona, watazungumza naye, na watatumia wakati pamoja naye. (Yoh. 14:2, 3) Pia, Yesu atawaonyesha upendo na kuwakazia uangalifu wale walio na tumaini la kuishi duniani. Ingawa hawatamwona Yesu kihalisi, uhusiano wao pamoja naye utazidi kuimarika kadiri wanavyofurahia maisha ambayo Yehova na Yesu wamewaandalia.—Isa. 9:6, 7.

16. Tunapata baraka gani tunapokuwa rafiki za Yesu?

16 Tunapata baraka nyingi, tunapokubali mwaliko wa Yesu wa kuwa rafiki zake. Kwa mfano, tunanufaika kwa sababu ya upendo na utegemezo anaotupatia leo. Tuna tumaini la kuishi milele. Na jambo muhimu zaidi ya yote ni kwamba urafiki wetu pamoja na Yesu utatuongoza kwenye hazina iliyo bora kupita zote, yaani, kuwa na uhusiano wa kibinafsi na wa karibu sana pamoja na Yehova, Baba ya Yesu. Ni pendeleo kubwa sana kuitwa rafiki za Yesu!

WIMBO 17 “Nataka”

^ fu. 5 Mitume walishirikiana na Yesu kwa miaka kadhaa wakizungumza na kufanya kazi pamoja naye, nao wakawa marafiki wa karibu wa Yesu. Yesu pia anataka tuwe rafiki zake, lakini tunakabili changamoto ambazo mitume hawakuwa nazo. Makala hii itazungumzia baadhi ya changamoto hizo na itatoa mapendekezo ya jinsi tunavyoweza kusitawisha na kudumisha urafiki wa karibu pamoja na Yesu.

^ fu. 55 MAELEZO YA PICHA: (1) Wakati wa ibada ya familia, tunaweza kujifunza kuhusu maisha na huduma ya Yesu. (2) Tunapokuwa kutanikoni, tunaweza kufuatilia amani pamoja na ndugu zetu. (3) Tunaweza kuwaunga mkono ndugu za Kristo kwa kushiriki kikamili katika huduma. (4) Tunaweza kuunga mkono maamuzi ya wazee, makutaniko yanapounganishwa.