Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 20

Mfalme wa Kaskazini” Ni Nani Leo?

Mfalme wa Kaskazini” Ni Nani Leo?

“Atasonga kufikia mwisho wake, na hakuna atakayemsaidia.” —DAN. 11:45.

WIMBO 95 Nuru Inazidi Kuongezeka

MUHTASARI *

1-2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

LEO, kuliko wakati mwingine wowote, kuna uthibitisho mwingi zaidi unaoonyesha kwamba tunaishi mwishoni mwa siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Hivi karibuni, Yehova na Yesu Kristo wataangamiza serikali zote zinazopinga Ufalme wa Mungu. Kabla ya jambo hilo kutokea, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wataendelea kupambana wao kwa wao na dhidi ya watu wa Mungu.

2 Katika makala hii, tutazungumzia unabii wa Danieli 11:40–12:1. Tutajifunza mfalme wa kaskazini ni nani leo, na kuzungumzia kwa nini tunaweza kukabiliana na matatizo ya wakati ujao tukiwa na uhakika.

MFALME MPYA WA KASKAZINI AIBUKA

3-4. Mfalme wa kaskazini ni nani leo? Eleza.

3 Baada ya Muungano wa Sovieti kuvunjika mwaka wa 1991, watu wa Mungu katika eneo hilo kubwa walipata “msaada kidogo,” yaani, kipindi fulani cha uhuru. (Dan. 11:34) Kwa sababu hiyo, walifanikiwa kuhubiri kwa uhuru, na baada ya muda mfupi idadi ya wahubiri katika eneo hilo lililokuwa chini ya Ukomunisti ikaongezeka kufikia mamia ya maelfu. Lakini baada ya miaka kadhaa, serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zikawa mfalme wa kaskazini. Kama tulivyojifunza katika makala iliyopita, ili serikali iweze kuwa mfalme wa kaskazini au wa kusini, ni lazima itimize mambo haya matatu: (1) iwatawale au kuwatesa watu wa Mungu, (2) ionyeshe kwa matendo yake kwamba ni adui ya Yehova na watu wake, na (3) ipambane na mfalme mwingine.

4 Zifuatazo ni sababu zinazofanya tuseme kwamba mfalme wa kaskazini leo, ni serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono. (1) Zimewaathiri moja kwa moja watu wa Mungu kwa kupiga marufuku kazi ya kuhubiri na kuwatesa mamia ya maelfu ya ndugu na dada wanaoishi katika maeneo yaliyo chini ya mamlaka yao. (2) Matendo hayo yanaonyesha kwamba wanamchukia Yehova na watu wake. (3) Zimekuwa zikipambana na mfalme wa kusini, yaani, Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Acheni tuone jinsi serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zimethibitika kuwa mfalme wa kaskazini.

MFALME WA KASKAZINI NA MFALME WA KUSINI WAENDELEA KUSUKUMANA

5. Andiko la Danieli 11:40-43 linafafanua kipindi gani cha wakati, na nini kinachotukia katika kipindi hicho?

5 Soma Danieli 11:40-43. Sehemu hii ya unabii inazungumzia wakati wa mwisho. Unabii huu unazungumza kuhusu pambano kati ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Kama Danieli alivyotabiri, katika wakati wa mwisho, mfalme wa kusini “atasukumana” na mfalme wa kaskazini au “atamenyana” naye.—Dan. 11:40; maelezo ya chini.

6. Kuna uthibitisho gani kwamba mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wamekuwa wakisukumana?

6 Mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wanaendelea kushindana ili serikali zao ziwe zenye nguvu zaidi duniani. Kwa mfano, fikiria kilichotukia baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu wakati ambapo Muungano wa Sovieti na nchi zilizouunga mkono zilipokuwa na mamlaka kubwa juu ya sehemu nyingi za Ulaya. Matendo ya mfalme wa kaskazini yalimlazimisha mfalme wa kusini aanzishe muungano wa kijeshi wa kimataifa, unaoitwa NATO. Mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini wanaendelea kushindana wakitumia pesa nyingi ili kujipatia silaha na jeshi lenye nguvu. Mfalme wa kaskazini alipigana na mpinzani wake kwa kuunga mkono upande tofauti katika vita na maasi yaliyokuwa yakiendelea barani Afrika, Asia, na Amerika ya Latini. Katika miaka ya hivi karibuni mamlaka au nguvu ya serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono imeongezeka kotekote duniani. Pia, mfalme wa kaskazini amemshambulia mfalme wa kusini kwa kutumia kompyuta. Wafalme hao wamekuwa wakilaumiana wenyewe kwa wenyewe kwamba wametumia programu za kompyuta zilizo na madhara ambazo zimekusudiwa kuharibu mifumo yao ya kiuchumi na ya kisiasa. Na kama Danieli alivyotabiri, mfalme wa kaskazini anaendelea kuwashambulia watu wa Mungu.—Dan. 11:41.

MFALME WA KASKAZINI AINGIA KATIKA “NCHI YA LILE PAMBO”

7. “Nchi ya lile Pambo” ni nini?

7 Andiko la Danieli 11:41 linasema kwamba mfalme wa kaskazini ataingia katika “nchi ya lile Pambo.” Ni nchi gani hiyo? Katika nyakati za kale, nchi halisi ya Israeli ilionwa kuwa nchi “nzuri sana kuliko nchi zote.” (Eze. 20:6) Lakini jambo hususa lililoifanya nchi hiyo iwe ya pekee sana ni kwamba ibada ya kweli iliendelezwa humo. Tangu Pentekoste 33 W.K., “nchi” hiyo si eneo fulani halisi la kijiografia; hapana, kwa sababu watu wa Yehova wameenea kotekote duniani. Badala yake, leo “nchi ya lile Pambo” ni utendaji wote wa watu wa Yehova unaotia ndani mambo kama vile ibada yao kwa Yehova kupitia mikutano na huduma ya shambani.

8. Mfalme wa kaskazini ameingiaje katika “nchi ya lile Pambo”?

8 Katika kipindi cha siku za mwisho, mfalme wa kaskazini ameingia tena na tena katika “nchi ya lile Pambo.” Kwa mfano, Ujerumani ya Wanazi ilipokuwa mfalme wa kaskazini, na hasa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, mfalme huyo aliingia katika “nchi ya lile Pambo” kwa kuwatesa na kuwaua watu wa Mungu. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, wakati Muungano wa Sovieti ulipokuwa mfalme wa kaskazini, mfalme huyo aliingia katika “nchi ya lile Pambo” kwa kuwatesa watu wa Mungu na kuwapeleka uhamishoni.

9. Katika miaka ya karibuni, serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zimeingiaje katika “nchi ya lile Pambo”?

9 Pia, katika miaka ya hivi karibuni, Serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono zimeingia katika “nchi ya lile Pambo.” Jinsi gani? Katika mwaka wa 2017, mfalme huyo wa sasa wa kaskazini alipiga marufuku kazi ya watu wa Yehova na kuwatupa gerezani baadhi ya ndugu na dada zetu. Pia, aliyapiga marufuku machapisho yetu, kutia ndani Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Isitoshe, alichukua kwa lazima ofisi yetu ya tawi huko Urusi na pia Majumba ya Ufalme na Majumba ya Makusanyiko. Baada ya vitendo hivyo, katika mwaka wa 2018 Baraza Linaloongoza lilitambulisha serikali ya Urusi na nchi zinazoiunga mkono kuwa mfalme wa kaskazini. Hata wanapoteswa vikali, watu wa Yehova hawatajihusisha kwa vyovyote na vitendo vya kujaribu kupindua au kubadili serikali za wanadamu. Badala yake, wanafuata shauri la Biblia la kusali kwa ajili ya “wote wenye vyeo vya juu,” hasa wanapofanya maamuzi yanayoweza kuathiri uhuru wa ibada.—1 Tim. 2:1, 2.

JE, MFALME WA KASKAZINI ATAMSHINDA MFALME WA KUSINI?

10. Je, mfalme wa kaskazini atamshinda mfalme wa kusini? Eleza.

10 Unabii wa Danieli 11:40-45 unakazia hasa utendaji wa mfalme wa kaskazini. Je, hilo linamaanisha kwamba mfalme huyo atamshinda mfalme wa kusini? Hapana. Mfalme wa kusini atakuwa angali “hai” Yehova na Yesu watakapoangamiza serikali zote za wanadamu katika vita vya Har–Magedoni. (Ufu. 19:20) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika huo? Fikiria mambo yanayotajwa katika unabii wa Danieli na Ufunuo.

Katika vita vya Har–​Magedoni, Ufalme wa Mungu, ambao unalinganishwa na jiwe, utakomesha utawala wa wanadamu, ambao unafananishwa na sanamu kubwa (Tazama, fungu la 11)

11. Andiko la Danieli 2:43-45 linaonyesha nini? (Tazama picha kwenye jalada.)

11 Soma Danieli 2:43-45. Nabii Danieli anafafanua mfululizo wa serikali za wanadamu ambazo zimewaathiri watu wa Mungu. Serikali hizo zinafananishwa na sehemu mbalimbali za sanamu kubwa sana. Serikali ya mwisho ya wanadamu katika sanamu hiyo imefananishwa na miguu iliyofanyizwa kwa chuma kilichochanganyika na udongo. Miguu hiyo inafananisha Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Unabii huo unaonyesha kwamba serikali hiyo itakuwa bado ikitawala Ufalme wa Mungu utakapokuja na kuziangamiza serikali za wanadamu.

12. Kichwa cha saba cha mnyama wa mwituni kinafananisha nini, na kwa nini ni muhimu kujua hilo?

12 Mtume Yohana pia anaeleza kuhusu mfululizo wa serikali za ulimwengu ambazo zimewatawala watu wa Yehova. Katika unabii wa Yohana, serikali hizo zinafananishwa na mnyama wa mwituni mwenye vichwa saba. Kichwa cha saba cha mnyama huyo kinafananisha Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Hilo ni jambo muhimu kwa sababu mnyama huyo hatajwi kwamba atatokeza vichwa vingine. Kichwa cha saba cha mnyama huyo kitakuwa bado kinatawala wakati Kristo na majeshi yake ya mbinguni watakapokiangamiza pamoja na sehemu nyingine zote za mnyama huyo. *​—Ufu. 13:1, 2; 17:13, 14.

MFALME WA KASKAZINI ATAFANYA NINI HIVI KARIBUNI?

13-14. “Gogu wa nchi ya Magogu” ni nani, na huenda ni nini kitakachomchochea awashambulie watu wa Mungu?

13 Ezekieli aliandika unabii unaotueleza mambo ambayo huenda yatatukia kabla ya mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kuharibiwa. Inaonekana kwamba unabii wa Ezekieli 38:10-23; Danieli 2:43-45; 11:44–12:1; na Ufunuo 16:13-16, 21 unazungumza kuhusu matukio yanayotukia katika kipindi kilekile cha wakati. Ikiwa hilo ni kweli, inaonekana tunaweza kutarajia kwamba mambo yafuatayo yatatokea.

14 Wakati fulani baada ya dhiki kuu kuanza, “wafalme wa dunia nzima inayokaliwa” wataanzisha muungano wa mataifa. (Ufu. 16:13, 14; 19:19) Biblia inauita muungano huo wa mataifa “Gogu wa nchi ya Magogu.” (Eze. 38:2) Muungano huo wa mataifa utawashambulia watu wote wa Mungu na kujaribu kuwaangamiza kabisa. Ni nini kitakachoyachochea mataifa yawashambulie watu wa Mungu? Akizungumza kuhusu wakati huo, mtume Yohana aliona dhoruba ya mvua kubwa ya mawe isiyo ya kawaida ikiwanyeshea maadui wa Mungu. Huenda mvua hiyo ya mfano ya mawe ikafananisha ujumbe mkali wa hukumu utakaotolewa na watu wa Yehova. Huenda ujumbe huo utamfanya Gogu wa Magogu awashambulie watu wa Mungu akikusudia kuwafutilia mbali kutoka duniani.—Ufu. 16:21.

15-16. (a) Huenda andiko la Danieli 11:44, 45 linarejelea tukio gani? (b) Ni nini kitakachompata mfalme wa kaskazini na mataifa mengine yanayofanyiza Gogu wa Magogu?

15 Huenda ujumbe huo mkali wa hukumu na shambulizi la mwisho la maadui wa Mungu ni matukio yaleyale yanayorejelewa kwenye Danieli 11:44, 45. (Soma.) Katika andiko hilo, Danieli anasema kwamba “habari kutoka mashariki na kutoka kaskazini” zitamhangaisha mfalme wa kaskazini, ambaye atatoka kwa “hasira kali.” Mfalme wa kaskazini atakusudia “kuwaua wengi.” Inaonekana neno “wengi” linarejelea watu wa Yehova. * Hivyo huenda Danieli anazungumzia shambulizi la mwisho dhidi ya watu wa Mungu.

16 Shambulizi hilo la mfalme wa kaskazini akishirikiana pamoja na serikali nyingine za ulimwengu, litamkasirisha Mweza-Yote na vita vya Har–Magedoni vitaanza. (Ufu. 16:14, 16) Wakati huo, mfalme wa kaskazini pamoja na mataifa mengine yanayofanyiza Gogu wa Magogu, atafikia mwisho wake, na “hakuna atakayemsaidia.”—Dan. 11:45.

Katika vita vya Har–Magedoni, Yesu Kristo na majeshi yake ya mbinguni watauharibu ulimwengu mwovu wa Shetani na kuwaokoa watu wa Mungu (Tazama fungu la 17)

17. Mikaeli “yule mkuu” anayetajwa katika Danieli 12:1 ni nani, naye anafanya nini sasa, na atafanya nini hivi karibuni?

17 Mstari unaofuata katika unabii huo wa Danieli unatupatia habari zaidi kuhusu jinsi mfalme wa kaskazini na wale wanaomuunga mkono watakavyofikia mwisho wao na jinsi tutakavyookolewa. (Soma Danieli 12:1.) Mstari huo unamaanisha nini? Mikaeli ni jina lingine la Mfalme wetu anayetawala, Kristo Yesu. Amekuwa ‘akisimama kwa ajili’ ya watu wa Mungu tangu mwaka wa 1914 wakati ambapo Ufalme wake ulisimamishwa mbinguni. Hivi karibuni, “atasimama,” au atawaangamiza maadui wake katika vita vya Har–Magedoni. Vita hivyo ndivyo vitakavyohitimisha kipindi cha wakati ambacho Danieli alikiita “wakati wa taabu” ambao haujawahi kamwe kutokea katika historia. Unabii wa Yohana katika kitabu cha Ufunuo unakiita kipindi hicho, “ile dhiki kuu.”—Ufu. 6:2; 7:14.

JE, JINA LAKO ‘LITAANDIKWA KATIKA KILE KITABU’?

18. Kwa nini tunaweza kuutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika?

18 Tunaweza kuutarajia wakati ujao tukiwa na uhakika kwa sababu Danieli na Yohana wanatuhakikishia kwamba wale wanaomtumikia Yehova na Yesu, wataokoka wakati huo wa taabu usioweza kulinganishwa na chochote. Danieli anasema kwamba watu watakaookoka ni wale ambao majina yao yatakuwa ‘yameandikwa katika kile kitabu.’ (Dan. 12:1) Tunaweza kufanya nini ili majina yetu yaandikwe katika kitabu hicho? Ni lazima tuthibitishe waziwazi kwamba tuna imani katika Yesu, Mwanakondoo wa Mungu. (Yoh. 1:29) Tunahitaji kujiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa. (1 Pet. 3:21) Na ni lazima tuunge mkono Ufalme wa Mungu kwa kufanya yote tuwezayo ili kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Yehova.

19. Tunapaswa kufanya nini sasa, na kwa nini?

19 Sasa ndio wakati wa kumtumaini Yehova hata zaidi na pia tengenezo lake la watu wanaomtumikia kwa ushikamanifu. Sasa ndio wakati wa kuunga mkono Ufalme wa Mungu. Ikiwa tutafanya hivyo, tutaokolewa wakati mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini watakapoharibiwa na Ufalme wa Mungu.

WIMBO 149 Wimbo wa Ushindi

^ fu. 5 “Mfalme wa kaskazini” ni nani leo, naye atafikiaje mwisho wake? Kujua majibu ya maswali hayo kunaweza kuimarisha imani yetu na kututayarisha kwa ajili ya majaribu tutakayokabili hivi karibuni.

^ fu. 15 Kwa habari zaidi, tazama toleo la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 2015, uku. 29-30.