Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Upole​—Unatunufaishaje?

Upole​—Unatunufaishaje?

Sara * anaeleza hivi: “Kiasili mimi ni mtu mwenye haya na sijiamini sana. Hivyo, sijihisi huru ninapokuwa pamoja na watu wanaojiamini sana na washupavu. Lakini ninajihisi huru ninapokuwa pamoja na mtu mpole na mnyenyekevu. Ninaweza kumfunulia moyo wangu, kumweleza hisia zangu, na kuzungumzia matatizo yangu. Rafiki zangu wa karibu zaidi wako hivyo.”

Maelezo ya Sara yanaonyesha kwamba tukiwa na sifa ya upole wengine watavutiwa nasi. Pia, sifa ya upole humfurahisha Yehova. Neno lake linatuhimiza hivi: “Jivikeni . . . upole.” (Kol. 3:12) Upole ni nini? Yesu alionyeshaje upole? Na sifa hiyo inaweza kufanyaje maisha yetu yawe yenye furaha zaidi?

UPOLE NI NINI?

Upole ni hali ya moyoni ya kuwa mwenye amani. Mtu mwenye upole hushughulika na wengine kwa wororo, kwa njia yenye fadhili na anaweza kukabiliana na mambo yenye kuudhi maishani kwa utulivu na akiwa na sifa ya kujizuia.

Upole si ishara ya udhaifu. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “upole” lilitumiwa kumfafanua farasi aliyechukuliwa kutoka mwituni na kufugwa. Farasi anabaki na nguvu zilezile, lakini amezoezwa kudhibiti nguvu zake. Vivyo hivyo, tunapoonyesha upole, tunadhibiti mielekeo yetu isiyo mikamilifu na kushughulika na wengine kwa amani.

Huenda tukasema kwamba ‘kiasili mimi sina sifa ya upole.’ Tunaishi katika ulimwengu ambamo watu wengi ni washupavu na hawana subira, hivyo huenda tukaona kuwa changamoto kuonyesha sifa ya upole. (Rom. 7:19) Ni wazi kwamba jitihada inahitajika ili kusitawisha sifa ya upole, lakini roho takatifu ya Yehova itatusaidia kuimarisha azimio letu la kufikia mradi huo. (Gal. 5:22, 23) Kwa nini tunapaswa kujitahidi kusitawisha sifa ya upole?

Upole ni sifa inayowavutia watu. Kama Sara aliyenukuliwa awali, sisi pia tunahisi tukiwa tumestarehe tunaposhirikiana na mtu mpole. Yesu ni mfano bora wa mtu ambaye ni mpole na mwenye fadhili. (2 Kor. 10:1) Hata watoto ambao hawakumjua walitaka kuwa karibu naye.—Marko 10:13-16.

Upole hutulinda sisi na wale wanaotuzunguka. Ikiwa sisi ni wapole, hatutaudhika upesi au kutenda kwa hasira. (Met. 16:32) Na tukifanya hivyo, tutaepuka hisia za hatia tunazopata baada ya kumuumiza mtu mwingine—hasa mtu tunayempenda. Pia, sifa ya upole huwalinda wale wanaotuzunguka kwa kuwa tutatenda kwa upole na hivyo kuepuka kuwaumiza.

MFANO MKAMILIFU WA MTU ALIYEONYESHA UPOLE

Licha ya majukumu yake mazito na ratiba yenye mambo mengi, Yesu aliwatendea watu wote kwa upole. Watu wengi katika siku zake walikuwa wakitaabika na kulemewa na mizigo, na walihitaji kuburudishwa. Hapana shaka kwamba walifarijika Yesu alipowaambia: “Njooni kwangu, . . . kwa maana mimi ni mpole na mnyenyekevu moyoni”!—Mt. 11:28, 29.

Tunaweza kusitawishaje upole ambao Yesu alionyesha? Tunahitaji kujifunza Neno la Mungu ili kujifunza jinsi Yesu alivyowatendea watu na jinsi alivyoshughulika na hali ngumu. Kisha tunapokabili hali zinazojaribu upole wetu, tunajitahidi kutenda kama Yesu. (1 Pet. 2:21) Fikiria mambo matatu yaliyomsaidia Yesu kuwa mpole.

Yesu alikuwa mnyenyekevu moyoni. Yesu alisema kwamba alikuwa “mpole na mnyenyekevu moyoni.” (Mt. 11:29) Biblia inazitaja sifa hizo mbili pamoja kwa sababu kuna uhusiano wa karibu kati ya upole na unyenyekevu. (Efe. 4:1-3) Jinsi gani?

Unyenyekevu hutusaidia tuepuke kujiona kuwa watu wa maana mno na kuepuka kuwa wenye kuchokozeka haraka. Yesu alitendaje watu walipomkosoa isivyo haki kwa kumwita “mlafi na mwenye mazoea ya kunywa divai”? Aliacha mfano wake uthibitishe ukweli wa mambo, na kwa upole akawaambia kwamba “hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kupitia kazi zake.”—Mt. 11:19.

Ikiwa mtu atasema jambo fulani lisilofaa kuhusu jamii yako, jinsia, au malezi yako, kwa nini usijitahidi kumjibu kwa upole? Peter, mzee wa kutaniko kutoka Afrika Kusini, anasema hivi: “Mtu anaponiudhi kwa sababu ya jambo alilosema, mimi hujiuliza, ‘Yesu angetendaje katika hali hiyo?’” Anaongeza hivi: “Nimejifunza kutojifikiria kupita kiasi.”

Yesu alielewa udhaifu wa wanadamu. Wanafunzi wa Yesu walikuwa na nia nzuri, lakini kwa kuwa hawakuwa wakamilifu, nyakati nyingine walishindwa kutenda yale waliyokusudia. Kwa mfano, usiku uliotangulia kifo chake, Petro, Yakobo, na Yohana walishindwa kumpa Yesu utegemezo wa kihisia aliokuwa amewaomba. Yesu alitambua kwamba “bila shaka, roho inataka lakini mwili ni dhaifu.” (Mt. 26:40, 41) Kwa kuwa alitambua jambo hilo, Yesu hakukasirishwa na mitume wake.

Mandy ni dada aliyekuwa na kawaida ya kudai mengi sana kutoka kwa wengine, lakini sasa anajitahidi sana kuiga sifa ya Yesu ya upole. Anasema hivi: “Ninajitahidi kukumbuka kwamba wanadamu wote si wakamilifu na ninajitahidi kukazia sifa zao nzuri, jambo ambalo Yehova hufanya.” Je, mtazamo wenye huruma wa Yesu kuhusu udhaifu wa wanadamu unaweza kukusaidia wewe pia ushughulike na wengine kwa upole?

Yesu aliacha mambo yote mikononi mwa Yehova. Alipokuwa duniani, Yesu aliacha watu wamtendee isivyo haki. Watu walimwelewa vibaya, walimdharau, na walimtesa. Ingawa hivyo, aliendelea kuwa mpole kwa sababu “alijikabidhi mkononi mwa Yule anayehukumu kwa uadilifu.” (1 Pet. 2:23) Yesu alijua kwamba Baba yake wa mbinguni angemsaidia na kwamba kwa wakati unaofaa, angeshughulikia ukosefu huo wa haki.

Ikiwa tutakasirika na kujaribu kupigania haki yetu, ni rahisi kuchukua hatua ambayo itafanya mambo yawe mabaya hata zaidi. Hiyo ndiyo sababu Maandiko yanatukumbusha hivi: “Hasira ya mwanadamu haitokezi uadilifu wa Mungu.” (Yak. 1:20) Hata ikiwa tuna msingi wa kukasirika, kwa kuwa hatujakamilika tunaweza kutenda kwa njia isiyofaa.

Awali, Cathy, dada kutoka Ujerumani, alikuwa akifikiri kwamba ‘Ikiwa sitachukua hatua ya kujitetea, hakuna yeyote atakayefanya hivyo kwa ajili yangu.’ Lakini alipojifunza kumtumaini Yehova, mtazamo wake ulibadilika. Anaeleza hivi: “Sasa sihitaji tena kujihami. Niko huru kutenda kwa upole, nikijua kwamba Yehova atashughulikia kikamilifu mambo yote.” Ikiwa umewahi kutendewa isivyo haki, kufuata mfano wa Yesu wa kumtumaini Mungu kutakusaidia kudumisha sifa ya upole.

“WENYE FURAHA NI WALE WALIO WAPOLE”

Sifa ya upole inaweza kutusaidiaje tunapokabili changamoto mbalimbali?

Yesu alionyesha kwamba sifa ya upole ni muhimu ili tuwe na furaha. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio wapole.” (Mt. 5:5) Ona jinsi upole unavyotusaidia katika hali zifuatazo.

Upole hupunguza mkazo katika ndoa. Robert, ndugu kutoka Australia anakiri hivi: “Nimewahi kumwambia mke wangu mambo mengi yenye kuumiza ambayo sikumaanisha. Lakini maneno unayosema kwa hasira bila kufikiri hayawezi kurudi kinywani. Nilijihisi vibaya sana kuona jinsi nilivyomuumiza sana.”

“Sisi sote hujikwaa mara nyingi” tunapozungumza, na maneno tunayosema bila kufikiri yanaweza kuhatarisha amani katika ndoa. (Yak. 3:2) Nyakati kama hizo, sifa ya upole hutusaidia tuendelee kuwa watulivu na kuudhibiti ulimi wetu.—Met. 17:27.

Robert alijitahidi sana kusitawisha sifa ya utulivu na ya kujizuia. Matokeo yamekuwaje? Anaeleza hivi: “Siku hizi, mimi na mke wangu tunapokosa kuelewana ninajitahidi kumsikiliza kwa makini, kuzungumza naye kwa upole, na kuepuka kuudhika. Uhusiano wangu pamoja na mke wangu ni mzuri zaidi.”

Sifa ya upole hutusaidia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine. Watu ambao hukasirika upesi hawana marafiki wengi. Hata hivyo, upole hutusaidia “kudumisha . . . kifungo cha muungano cha amani.” (Efe. 4:2, 3) Cathy, dada aliyenukuliwa awali anasema hivi: “Sifa ya upole imenipa nguvu ya kushughulika na kila mtu ninayekutana naye kwa njia nzuri zaidi, hata ingawa si rahisi kushughulika na baadhi ya watu.”

Sifa ya upole hutufanya tuwe na amani ya moyoni. Biblia inahusianisha “hekima inayotoka juu” na sifa ya upole na amani. (Yak. 3:13, 17) Mtu mpole ana “moyo mtulivu.” (Met. 14:30) Martin, ambaye amejitahidi sana kusitawisha sifa ya upole, anaeleza hivi: “Sasa mimi ni mtu ninayenyumbulika zaidi na nimeacha kuwa mshupavu kama awali, na nina amani nyingi zaidi ya moyoni na furaha.”

Ni kweli kwamba huenda tukahitaji kupambana ili tusitawishe sifa ya upole. Ndugu mmoja anasema hivi: “Kusema kweli, hadi leo, nyakati fulani mimi hupandwa na hasira.” Lakini Yehova, anayetutia moyo tufuatilie upole, atatusaidia katika pambano hili. (Isa. 41:10; 1 Tim. 6:11) Anaweza ‘kumaliza mazoezi yetu’; anaweza ‘kutufanya tuwe wenye nguvu.’ (1 Pet. 5:10) Baada ya muda, kama mtume Paulo tunaweza kuiga “upole na fadhili za Kristo.”—2 Kor. 10:1.

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.