Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 26

“Munirudilie”

“Munirudilie”

“Munirudilie, na mimi nitawarudilia.”​—MAL. 3:7.

WIMBO 102 “Mwasaidie Walio Dhaifu”

KIFUPI CHA HABARI *

1. Yehova anajisikia namna gani wakati kondoo wake mumoja anamurudilia?

KAMA vile tuliona mu habari yenye ilitangulia, Yehova anajilinganisha na muchungaji muzuri mwenye anahangaikia kwa upendo kila kondoo wake. Na anatafuta kila kondoo mwenye anapotea. Yehova aliambia hivi Waisraeli wenye walimuacha: “Munirudilie, na mimi nitawarudilia.” Tunajua kama angali anahangaikia kondoo wake kwa sababu anasema hivi: “Sibadilike.” (Mal. 3:6, 7) Yesu alisema kama Yehova na malaika wanafurahi sana wakati hata mutumishi wake mumoja anamurudilia.​—Lu. 15:10, 32.

2. Tutazungumuzia nini katika habari hii?

2 Tuzungumuzie basi mifano tatu kati ya mifano ya Yesu, yenye inaonyesha namna ya kusaidia wale wenye wamemuacha Yehova. Tutazungumuzia sifa fulani zenye tunapaswa kuwa nazo ili kusaidia kondoo wenye wamepotea wamurudilie Yehova. Na tutaona juu ya nini bidii yenye tunafanya ili kusaidia watu wenye kuwa zaifu haiko ya bure.

KUTAFUTA FEZA YA KICHELE YENYE ILIPOTEA

3-4. Juu ya nini mwanamuke mwenye kutajwa mu andiko ya Luka 15:8-10, alitafuta kwa uangalifu feza ya drakma yenye ilipotea?

3 Tunapaswa kujikaza sana ili kutafuta wale wenye wanapenda kumurudilia Yehova. Katika mufano wenye kuwa mu Injili ya Luka, Yesu anaonyesha namna mwanamuke fulani anatafuta kitu cha maana sana chenye kilipotea, ni kusema feza ya kichele ya drakma. Katika mufano huu, jambo lenye linakaziwa ni namna alitafuta ile feza ya drakma.​—Soma Luka 15:8-10.

4 Yesu anaonyesha namna ule mwanamuke anajisikia wakati anapata feza ya kichele ya drakma yenye ilipotea. Katika siku za Yesu, inaonekana mama fulani Wayahudi walikuwa wanapatia mutoto mwanamuke feza kumi za vichele vya drakma siku ya ndoa yake. Pengine ile feza ya kichele ilikuwa moja kati ya zile feza kumi za vichele zenye mama yake alimupatiaka. Ule mwanamuke anawaza kama feza yake ya kichele ilianguka chini mu nyumba yake. Kwa hiyo, anawasha taa na kutafuta-tafuta, lakini haione. Pengine taa yake ya mafuta haina mwangaza wa kutosha ili kumusaidia aone ile feza ya kidogo ya kichele. Ku mwisho, anafagia kwa uangalifu nyumba yote. Katika mavumbi yenye alikusanya, anaona drakma yake ya maana sana inangaa katika mwangaza wa taa. Anajisikia mwenye kutulia wakati anaiona! Anaita marafiki wake na majirani wake ili kuwaambia ile habari njema.

5. Juu ya nini inaweza kuwa nguvu kupata wale wenye wameacha kutaniko?

5 Kama vile mufano wa Yesu unaonyesha, inaomba kujikaza sana ili kupata kitu chenye kilipotea. Vilevile, inaweza kuomba tujikaze sana ili kupata wale wenye wameacha kutaniko. Pengine kumepita miaka mingi tangu wakati waliacha kutaniko. Pengine hata wamehamia mahali fulani kwenye ndugu na dada hawawajue. Lakini kwa wakati huu, tuko hakika kama watu fulani kati ya wale wenye hawatende tena wanapenda kumurudilia Yehova. Wanapenda kumutumikia Yehova pamoja na ndugu na dada zao, lakini wako na lazima ya musaada wetu.

6. Namna gani watu wote mu kutaniko wanaweza kusaidia ili kutafuta wale wenye hawatende tena?

6 Ni nani anaweza kusaidia kutafuta wale wenye hawatende tena? Sisi wote, ni kusema, wazee wa kutaniko, mapainia, wale wenye katika familia yao kuko watu wenye hawatende tena, na wahubiri katika kutaniko, tunaweza kusaidia kutafuta wale wenye hawatende tena. Uko na rafiki ao mutu wa jamaa mwenye hatende tena? Umekutana na mutu mwenye hatende tena wakati ulikuwa unahubiri nyumba kwa nyumba ao mahali pa watu wengi? Umuambie mutu huyo kama ikiwa atapenda kutembelewa, akupatie adresi yake na namba yake ya telefone ili uipatie wazee wa kutaniko lako.

7. Maelezo ya muzee mwenye kuitwa Thomas inakufundisha nini?

7 Ni mambo gani wazee wanaweza kufanya ili kutafuta wale wenye wanapenda kumurudilia Yehova? Ona maelezo ya muzee mumoja mwenye kuitwa Thomas, * mwenye anaishi mu inchi ya Uhispania. Amesaidia Mashahidi zaidi ya 40 kurudia katika kutaniko. Thomas anasema hivi: “Kwanza, ninauliza ndugu na dada mbalimbali kama wanajua kwenye watu fulani wenye hawatende tena wanaishi sasa. Ao ninauliza wahubiri ikiwa wanakumbuka mutu fulani mwenye hahuzurie tena mikutano. Wengi katika kutaniko wanafurahi sana wakati wanaona kama nao wanaweza kusaidia kutafuta wenye wamepotea. Kisha, wakati ninatembelea ndugu ao dada wenye hawatende tena, ninawauliza habari juu ya watoto wao na watu wengine wa jamaa. Watu fulani wenye hawatende tena walizoea kuja na watoto wao ku mikutano, na pengine watoto hao walikuwa wahubiri wakati fulani. Watoto hao wanaweza pia kusaidiwa ili wamurudilie Yehova.”

SAIDIA WATOTO WA YEHOVA WENYE WALIPOTEA WARUDIE KATIKA KUTANIKO

8. Katika mufano wa mwana mupotevu, wenye kuwa mu Luka 15:17-24, namna gani baba alimutendea mwana wake mwenye alitubu?

8 Tunapaswa kuwa na sifa gani ili tuweze kusaidia wale wenye wanapenda kumurudilia Yehova? Mufano wa Yesu wa mwana mupotevu unaweza kutufundisha mambo fulani. (Soma Luka 15:17-24.) Yesu anafasiria namna mwana mupotevu alifikia kurudiwa na ufahamu na akaamua kurudia ku nyumba. Baba yake alikimbia ili kukutana naye na akamukumbatia kwa furaha, ili kumuonyesha kama alikuwa anamupenda. Zamiri ya ule mutoto iliendelea kumusumbua na alijisikia kuwa hastahili kutendewa kama mwana. Baba alimusikilia huruma mwana wake, na mwana naye akamuonyesha baba yake namna alikuwa anajisikia mu moyo. Kwa hiyo, baba alifanya mambo fulani ili kumuhakikishia mwana wake kuwa hangemutendea kama mufanyakazi wa kulipwa, lakini angemutendea kama mwana mupendwa. Alifanya karamu na akamupatia mwana wake mwenye alitubu nguo za muzuri sana.

9. Ni sifa gani tunapaswa kuonyesha ili kusaidia wale wenye hawatende tena wamurudilie Yehova? (Ona kisanduku “ Namna ya Kusaidia Wale Wenye Wanapenda Kurudia.”)

9 Yehova iko kama baba mwenye kuzungumuziwa katika mufano huo. Anapenda ndugu na dada zetu wenye hawatende tena na anapenda wamurudilie. Kama tunamuiga Yehova, tunaweza kuwasaidia warudie. Ili tufanye vile, inaomba tuwaonyeshe uvumilivu, huruma, na upendo. Juu ya nini tunapaswa kuonyesha sifa hizo, na namna gani tunaweza kufanya vile?

10. Juu ya nini tunapaswa kuonyesha uvumilivu wakati tunasaidia mutu fulani apone katika hali ya kiroho?

10 Tunapaswa kuonyesha uvumilivu kwa sababu inaomba wakati ili mutu apone katika hali ya kiroho. Watu wengi wenye hawakukuwa wanatenda tena wanaonyesha kama iliomba wazee na wengine mu kutaniko wawatembelee mara mingi mbele wamurudilie Yehova. Dada mumoja mwenye kuitwa Nancy, wa Asia ya Kusini-Mashariki, anaandika hivi: “Rafiki mumoja wa sana mu kutaniko alinisaidia sana. Alinipenda sawa vile mutu anapendaka dada yake mukubwa. Alinikumbusha wakati muzuri wenye tulipitisha pamoja zamani. Alikuwa ananisikiliza kwa uvumilivu wakati nilikuwa ninamuelezea namna nilikuwa ninajisikia, na hakusita kunishauria. Alionekana kuwa rafiki wa kweli, mwenye kuwa tayari kusaidia wakati wowote.”

11. Juu ya nini tunapaswa kuonyesha huruma ili kufariji mutu fulani mwenye amekwazika?

11 Huruma iko kama vile dawa yenye nguvu; inaweza kusaidia mutu mwenye alikwazika ajisikie muzuri. Watu fulani wenye hawatende tena walikwazwa na mutu fulani mu kutaniko kumepita miaka mingi, na wangali wanajisikia kuwa wenye uchungu na huzuni. Kwa sababu ya kujisikia vile, hawana hamu ya kumurudilia Yehova. Wamoja wanaweza kuwaza kama walitendewa bila haki. Wanaweza kuwa na lazima ya mutu wa kuwasikiliza na kuelewa namna wanajisikia. (Yak. 1:19) María, mwenye hakukuwa anatenda wakati fulani, anasema hivi: “Nilikuwa na lazima ya mutu wa kunisikiliza, kunifariji, kunipatia mashauri na kunisaidia.”

12. Leta mufano wenye kuonyesha namna upendo wa Yehova uko kama kamba.

12 Biblia inaonyesha kama upendo wa Yehova kwa watu wake uko kama vile kamba. Namna gani upendo wa Mungu uko kama vile kamba? Fikiria mufano huu: Wazia kuwa uko unazama mu bahari yenye upepo mukali, na mutu fulani anakutupia nguo yenye inasaidiaka mutu asizame. Kwa kweli, utafurahia ule musaada kwa sababu utakusaidia uendelee kubakia juu ya maji. Lakini, zaidi ya nguo ya kukusaidia usizame utakuwa na lazima ya kitu kingine. Maji iko baridi, na ili kuokoka inaomba ufike ku mashua ya kuokoa watu. Utakuwa na lazima ya mutu wa kukutupia kamba na kukukokota ili uingie mu mashua ya kuokoa watu. Yehova alisema hivi juu ya Waisraeli wenye walimuacha: “Niliendelea kuwavuta . . . kwa kamba za upendo.” (Ho. 11:4) Leo pia, Mungu anajisikia vile juu ya wale wenye wameacha kumutumikia na wenye wanalemewa na magumu na mahangaiko. Anataka wajue kama anawapenda, na anataka kuwasaidia wamurudilie. Na Yehova anaweza kukutumia ili kuwaonyesha kama anawapenda.

13. Leta mufano wenye kuonyesha kama kuonyesha wengine upendo kunaweza kuwasaidia wamurudilie Yehova.

13 Ni jambo la maana kuhakikishia wale wenye hawatende tena kama Yehova anawapenda na kama sisi pia tunawapenda. Pablo, mwenye tulizungumuzia katika habari yenye ilitangulia, aliacha kutenda kwa miaka zaidi ya 30. Anasema hivi: “Siku moja asubui, wakati nilikuwa ninatoka ku nyumba, nilikutana na dada mumoja mwenye fazili mwenye kuzeeka na akazungumuza na mimi kwa njia ya upendo. Nilianza kulia kama mutoto. Nilimuambia kama inaonekana kuwa Yehova njo alimutuma ili kuzungumuza na mimi. Ni wakati huo njo niliamua kumurudilia Yehova.”

SAIDIA KWA UPENDO WALE WENYE KUWA ZAIFU

14. Kulingana na mufano wenye kuwa mu Luka 15:4, 5, muchungaji alifanya nini wakati alipata kondoo mwenye alipotea?

14 Kisha kupata wale wenye hawatende tena, tunapaswa kuendelea kuwasaidia na kuwatia moyo. Kama mwana mupotevu mwenye kuzungumuziwa katika mufano wa Yesu, wanaweza kuwa na maumivu ya moyoni. Na inawezekana wako wazaifu kiroho kwa sababu ya mambo yenye iliwafikia katika ulimwengu wa Shetani. Tunapaswa kuwasaidia ili watie nguvu imani yao katika Yehova. Katika mufano wa kondoo mwenye alipotea, Yesu anaonyesha namna muchungaji anatia kondoo ku mabega yake na kumurudisha kwenye kundi. Muchungaji ametumia wakati na nguvu mingi ili kupata kondoo mwenye alipotea. Lakini, anaona kama anapaswa kumurudisha kwenye kundi juu hana nguvu ya kurudia yeye mwenyewe.​—Soma Luka 15:4, 5.

15. Namna gani tunaweza kusaidia na kutia moyo watu wazaifu wenye wanapenda kumurudilia Yehova? (Ona kisanduku “ Chombo cha Maana sana.”)

15 Inaweza kuomba tutumie wakati na nguvu mingi ili kusaidia watu fulani wenye hawatende tena kusudi wakuwe tena na urafiki muzuri pamoja na Yehova. Lakini kwa musaada wa roho ya Yehova, Neno lake, na vichapo vyenye kutolewa na tengenezo lake, tunaweza kuwasaidia ili wakuwe tena nguvu katika hali ya kiroho. (Ro. 15:1) Namna gani tunaweza kufanya vile? Muzee mumoja mwenye uzoefu anasema hivi: “Watu wengi wenye hawatende tena wako na lazima ya funzo la Biblia kisha kuamua kama wanapenda kabisa kumurudilia Yehova.” * Njo maana, kama wazee wanakuomba ujifunze na mutu mwenye hatende tena, ukubali kwa furaha mugao huo kama uko na uwezo. Muzee huyo alisema tena hivi: “Muhubiri mwenye kujifunza na mutu mwenye aliacha kutenda anapaswa kuwa rafiki muzuri; ile itasaidia ule mwenye hatende tena amuambie mambo yenye kuwa mu moyo wake.”

FURAHA MBINGUNI NA KU DUNIA

16. Ni nini inaonyesha kama malaika wanatusaidiaka kutafuta wale wenye hawatende tena?

16 Mambo mingi yenye ilionwa inaonyesha kama malaika wanatumika pamoja na sisi ili kupata wale wenye hawatende tena, wenye wanapenda kabisa kumurudilia Yehova. (Ufu. 14:6) Kwa mufano, Silvio, wa inchi ya Équateur, alimuomba Yehova amutumie mutu fulani wa kumusaidia kurudia katika kutaniko. Wakati alikuwa angali anasali, kengele ya mulango wake ililia. Wazee wawili walikuwa kwenye mulango wake. Wazee hao walifurahi kuanza kumutolea musaada wenye alikuwa nao lazima.

17. Tutapata baraka gani wakati tunasaidia wale wenye kuwa wazaifu kiroho?

17 Tutapata furaha mingi wakati tunasaidia watu wenye kuwa wazaifu kiroho wamurudilie Yehova. Salvador, painia wa pekee mumoja mwenye anahangaikia sana wale wenye hawatende tena, anasema hivi: “Wakati fulani, siwezi kujizuia kulia machozi ya furaha. Ninafurahi sana kuona kama Yehova amekomboa mumoja wa kondoo wake kutoka katika ulimwengu wa Shetani na kuona kama nilipata pendeleo la kufanya ile kazi pamoja naye.”​—Mdo. 20:35.

18. Kama hautende tena, unaweza kuwa hakika na jambo gani?

18 Kama umeacha kutaniko, ukuwe hakika kama Yehova angali anakupenda. Anapenda umurudilie. Itaomba ufanye mambo fulani ili umurudilie. Lakini, kama baba mwenye kuzungumuziwa katika mufano wa Yesu, Yehova iko anangojea urudie, na atakukaribisha kwa furaha.

WIMBO 103 Wachungaji—Zawadi Katika Wanadamu

^ fu. 5 Yehova anapenda wale wenye wameacha kutaniko wamurudilie. Tunaweza kufanya mambo mingi ili kutia moyo wale wenye wanapenda kukubali mwaliko huu wa Yehova: “Munirudilie.” Katika habari hii, tutazungumuzia namna tunaweza kuwasaidia wamurudilie Yehova.

^ fu. 7 Majina fulani imebadilishwa.

^ fu. 15 Watu fulani wenye hawatende tena wanaweza kupata musaada kwa kujifunza sehemu fulani za kitabu Namna ya Kubakia Katika Upendo wa Mungu, lakini wengine wamepata faida kwa kuchunguza sura fulani za kitabu Mkaribie Yehova. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko itaamua ni nani mwenye anastahili kujifunza na mutu fulani mwenye hatende tena.

^ fu. 68 MAFASIRIO YA PICHA: Ndugu mbalimbali watatu wanasaidia ndugu mwenye anapenda kurudia. Wanafanya vile kwa kuendelea kumuita ku telefone, kwa kumuhakikishia kama wanamupenda, na kwa kumusikiliza na kumuelewa.