Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 23

“Jina Lako na Litakaswe”

“Jina Lako na Litakaswe”

“Ee Yehova, jina lako linadumu milele.”—ZAB. 135:13.

WIMBO 10 Msifuni Yehova Mungu Wetu!

MUHTASARI *

1-2. Ni masuala gani muhimu sana ambayo huwasisimua Mashahidi wa Yehova?

SUALA la enzi kuu na kutakaswa kwa jina la Mungu ni masuala mawili muhimu sana yanayotukabili leo. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunapenda kuzungumzia habari hizo zenye kusisimua. Lakini je, suala la enzi kuu ya Mungu na kutakaswa kwa jina lake ni mambo mawili ambayo hayana uhusiano wowote? Hapana.

2 Sisi sote tumejionea kwamba ni lazima jina la Mungu litakaswe. Pia, tumejifunza kwamba enzi kuu ya Yehova, au njia yake ya kutawala inapaswa kuthibitishwa kuwa bora kabisa. Tunapaswa kuyachukulia kwa uzito masuala hayo yote mawili.

3. Jina Yehova linatia ndani nini?

3 Ukweli wa mambo ni kwamba jina Yehova linahusisha mambo yote yanayomhusu Mungu wetu, kutia ndani njia yake ya kutawala. Hivyo, ikiwa tunasema kwamba kutakaswa kwa jina la Yehova ndilo suala muhimu zaidi, tunamaanisha pia kwamba ni lazima njia ya Yehova ya kutawala ithibitishwe kuwa ndiyo njia bora zaidi. Jina la Yehova linahusiana kwa ukaribu sana na njia yake ya kutawala akiwa Mungu Mwenye Enzi Kuu na mweza yote.—Tazama sanduku “ Mambo Yanayohusika Katika Lile Suala Kuu.”

4. Zaburi 135:13 inafafanuaje jina la Mungu, na tutajibu maswali gani katika makala hii?

4 Jina la Yehova ni la pekee. (Soma Zaburi 135:13.) Kwa nini jina la Mungu ni la muhimu sana? Jina la Mungu lilichongewa kwa mara ya kwanza jinsi gani? Mungu analitakasaje? Nasi tunaweza kufanya nini ili kulitetea? Acheni tuzungumzie maswali hayo.

UMUHIMU WA JINA

5. Huenda tukajiuliza nini inapohusu kutakaswa kwa jina la Mungu?

5 “Jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Yesu alisema kwamba jambo hilo linapaswa kuwa mojawapo ya mambo muhimu zaidi katika sala zetu. Lakini maneno ya Yesu yanamaanisha nini? Kutakasa kitu kunamaanisha kukifanya kiwe kitakatifu, safi, au bila unajisi. Hata hivyo, huenda wengine wakajiuliza, ‘Je, si tayari jina la Yehova ni takatifu, safi, na halina unajisi?’ Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kufikiria jina linahusisha mambo gani?

6. Ni jambo gani linalofanya jina liwe na thamani?

6 Jina linahusisha mengi zaidi ya mkusanyo wa herufi zilizoandikwa kwenye karatasi au zinazotamkwa. Biblia inasema hivi: “Ni afadhali kuchagua jina jema kuliko mali nyingi.” (Met. 22:1; Mhu. 7:1) Kwa nini jina lina thamani sana hivyo? Kwa sababu linahusisha sifa ya mtu, yaani, jinsi wengine wanavyomwona yule mwenye jina hilo. Hivyo, jinsi jina linavyoandikwa—au hata jinsi linavyotamkwa—si jambo muhimu zaidi; jambo muhimu zaidi ni mambo ambayo watu hufikiria wanapoliona au kulisikia.

7. Watu wamelishambuliaje jina la Mungu?

7 Watu wanaposema uwongo kumhusu Yehova, wanashambulia sifa yake. Kwa kufanya hivyo, wanalipaka matope jina lake. Jina la Mungu na sifa yake ilishambuliwa kwa mara ya kwanza mwanzoni mwa historia ya wanadamu. Shambulizi hilo dhidi ya jina la Mungu linatufundisha nini?

JINSI JINA LA MUNGU LILIVYOCHONGEWA KWA MARA YA KWANZA

8. Adamu na Hawa walijua nini, na ni maswali gani yanayozuka?

8 Adamu na Hawa walijua jina la Yehova, na vilevile walijua kweli muhimu kumhusu Yule anayeitwa kwa jina hilo. Walimjua kuwa Muumba wao, yule aliyewapa uhai, makao maridadi ya Paradiso, na mwenzi mkamilifu. (Mwa. 1:26-28; 2:18) Hata hivyo, je, wangeendelea kutumia akili yao kamilifu kutafakari mambo yote ambayo Yehova alikuwa amefanya kwa ajili yao? Je, wangeendelea kumpenda na kumshukuru Yule aliyewakilishwa na jina hilo? Majibu ya maswali hayo yalikuwa wazi adui ya Mungu alipowajaribu.

9. Kulingana na Mwanzo 2:16, 17 na 3:1-5, Yehova aliwaambia nini wenzi wa kwanza wa ndoa, na Shetani alipotoshaje ukweli?

9 Soma Mwanzo 2:16, 17 na 3:1-5. Akizungumza kupitia nyoka, Shetani alimuuliza Hawa swali hili: “Je, ni kweli kwamba Mungu alisema msile matunda ya kila mti wa bustani?” Swali hilo lilikuwa na uwongo uliojificha uliokuwa kama sumu isiyoonekana. Lakini jambo ambalo Mungu alikuwa amesema ni kwamba wangeweza kula matunda ya kila mti, isipokuwa mti mmoja. Kulikuwa na matunda mengi ya aina mbalimbali ambayo Adamu na Hawa wangeweza kula. (Mwa. 2:9) Naam, kwa hakika Yehova ni mkarimu. Hata hivyo, Mungu alikuwa amewakataza Adamu na Hawa kula matunda ya mti mmoja aliokuwa ameuchagua. Hivyo, swali la Shetani lilipotosha ukweli. Shetani alifanya ionekane kwamba Mungu hakuwa mkarimu. Huenda Hawa alijiuliza, ‘Je, Mungu ananinyima jambo fulani zuri?’

10. Shetani alilichongeaje moja kwa moja jina la Mungu, na matokeo yalikuwaje?

10 Kufikia wakati huo, bado Hawa alimwona Yehova kuwa Mtawala wake. Alimjibu Shetani kwa kurudia tena agizo la wazi ambalo Mungu alikuwa ametoa. Hata aliongeza kusema kwamba hawakupaswa kuugusa mti huo. Alijua kwamba kutotii onyo hilo la Mungu kungesababisha kifo. Lakini Shetani alimwambia: “Hakika hamtakufa.” (Mwa. 3:2-4) Sasa uwongo wa Shetani ulikuwa wazi. Alikuwa akilichongea moja kwa moja jina la Mungu; kwa maneno mengine alikuwa akimwambia Hawa kwamba Yehova ni mwongo. Hivyo, Shetani akawa Ibilisi, yaani, mchongezi. Hawa alidanganywa kabisa; alimwamini Shetani. (1 Tim. 2:14) Hawa alimtumaini zaidi Shetani kuliko Yehova. Jambo hilo lilifanya iwe rahisi kwa Hawa kufanya uamuzi mbaya sana. Aliamua kutomtii Yehova. Alianza kula matunda ya mti ambao Yehova alikuwa amemkataza kula. Baadaye, Hawa akampa Adamu baadhi ya matunda hayo.—Mwa. 3:6.

11. Wazazi wetu wa kwanza wangeweza kufanya nini, lakini walishindwa kufanya nini?

11 Fikiria kidogo jambo ambalo Hawa alipaswa kumwambia Shetani. Wazia ikiwa angesema hivi: “Sijui wewe ni nani, lakini ninamjua Baba yangu, Yehova, na ninampenda na kumtumaini. Amenipa mimi pamoja na Adamu kila kitu tulicho nacho. Unawezaje kuthubutu kusema mambo mabaya hivyo kumhusu? Ondoka hapa!” Yehova angefurahi sana kusikia maneno hayo ya ushikamanifu kutoka kwa binti yake mpendwa! (Met. 27:11) Lakini Hawa hakuwa na upendo mshikamanifu kwa Yehova; Adamu pia hakuongozwa na sifa hiyo. Kwa kuwa Adamu na Hawa hawakumpenda Baba yao kwa ushikamanifu, walishindwa kutetea jina lake alipochongewa.

12. Shetani alipandaje mbegu za shaka katika akili ya Hawa, na Adamu na Hawa walishindwa kufanya nini?

12 Kama tulivyoona, Shetani alianza kwa kupanda mbegu za shaka katika akili ya Hawa. Alimfanya amtilie shaka Yule aliyewakilishwa na jina Yehova. Kisha Adamu na Hawa wakashindwa kutetea jina la Yehova pamoja na sifa yake. Kwa njia hiyo, wakafanya iwe rahisi kwao kumsikiliza Shetani alipopendekeza wamwasi Baba yao. Shetani anatumia mbinu hizohizo leo. Analishambulia jina la Yehova kwa kulichongea. Watu wanaoamini uwongo wa Shetani hushawishiwa kwa urahisi kuukataa utawala wa Yehova wenye uadilifu.

YEHOVA ANALITAKASA JINA LAKE

13. Andiko la Ezekieli 36:23 linakaziaje ujumbe mkuu wa Biblia?

13 Je, Yehova anaweza kukubali uchongezi kama huo na asijitetee? Hapana, hawezi kukubali! Biblia yote inakazia kuhusu hatua ambazo Yehova amechukua ili kulitakasa jina lake kwa sababu lilichafuliwa katika bustani ya Edeni. (Mwa. 3:15) Hata tunaweza kusema kwa kifupi kwamba ujumbe mkuu wa Biblia ni: Yehova analitakasa jina lake kupitia Ufalme unaotawaliwa na Mwana wake, na kurudisha uadilifu na amani duniani. Biblia ina habari zinazotusaidia kuelewa jinsi Yehova anavyolitakasa jina lake.—Soma Ezekieli 36:23.

14. Njia ambayo Yehova ametumia kushughulikia uasi uliotokea Edeni imetakasaje jina lake?

14 Shetani amefanya yote awezayo ili kumzuia Yehova kutimiza kusudi Lake. Lakini kila mara, Shetani ameshindwa. Biblia inaonyesha jinsi ambavyo Yehova ametenda, na inathibitisha kwamba hakuna yeyote aliye kama Yehova Mungu. Ni kweli kwamba uasi wa Shetani na wale wote wanaomuunga mkono umemuumiza sana Yehova. (Zab. 78:40) Hata hivyo, Yehova ameshughulikia jambo hilo kwa hekima, subira, na haki. Pia, ameonyesha nguvu zake zisizo na mipaka kwa njia nyingi sana. Zaidi ya yote, upendo wake unaonekana waziwazi katika kila jambo analofanya. (1 Yoh. 4:8) Yehova hajaacha kamwe kazi ya kulitakasa jina lake.

Shetani alimwambia Hawa uwongo kumhusu Yehova, na kwa karne nyingi Ibilisi ameendelea kumchongea Mungu (Tazama fungu la 9, 10, na 15) *

15. Shetani analichongeaje jina la Mungu leo, na matokeo ni nini?

15 Shetani bado anaendelea kulichongea jina la Mungu hata leo. Anawafanya watu watilie shaka kwamba Mungu ana nguvu, haki, hekima, na upendo. Kwa mfano, Shetani anajaribu kuwasadikisha watu kwamba Yehova si Muumba. Na ikiwa watu wanaamini kwamba kuna Mungu, Shetani hujaribu kuwafanya waamini kwamba Mungu hutunyima uhuru na si mwenye haki. Hata anawafundisha watu kwamba Yehova ni Mungu mkatili asiye na huruma ambaye huwateketeza watu katika moto wa mateso. Watu wanapoamini uchongezi huo, inakuwa rahisi zaidi kwao kuchukua hatua inayofuata, yaani, kuukataa utawala wa Yehova wenye uadilifu. Shetani hataacha kampeni yake ya uchongezi hadi atakapoangamizwa, na atajitahidi kukufanya wewe pia umwache Yehova. Je, atafanikiwa?

JUKUMU LAKO KATIKA LILE SUALA KUU

16. Unaweza kufanya jambo gani ambalo Adamu na Hawa walishindwa kufanya?

16 Yehova anawaruhusu wanadamu wasio wakamilifu washiriki katika kulitakasa jina lake. Hivyo, unaweza kufanya mambo ambayo Adamu na Hawa walishindwa kufanya. Licha ya kuwa unaishi katika ulimwengu uliojaa watu wanaolichongea jina la Yehova na kulikufuru, una fursa ya kulitetea na kueleza ukweli kwamba Yehova ni mtakatifu, mwadilifu, mwema, na mwenye upendo. (Isa. 29:23) Unaweza kuunga mkono utawala wake. Unaweza kuwasaidia watu waelewe kwamba utawala wa Yehova pekee ndio ulio na uadilifu kikweli, na ndio utakaoleta amani na furaha kwa uumbaji wote.—Zab. 37:9, 37; 146:5, 6, 10.

17. Yesu aliwajulishaje watu jina la Baba yake?

17 Tunapolitetea jina la Yehova, tunafuata kielelezo cha Yesu Kristo. (Yoh. 17:26) Yesu alilijulisha jina la Baba yake kwa kulitumia jina hilo na kwa kutetea sifa ya Yehova. Kwa mfano, hakukubaliana na Mafarisayo, ambao kwa njia mbalimbali walifanya Yehova aonekane kuwa mkali, mwenye kudai mengi, asiyefikika, na asiye na rehema. Yesu aliwasaidia watu wamwone Baba yake kuwa mwenye usawaziko, subira, upendo, na mwenye kusamehe. Pia, aliwasaidia watu wamjue Yehova kwa kuiga kikamilifu sifa za Baba yake katika maisha yake ya kila siku.—Yoh. 14:9.

18. Tunaweza kupinduaje uwongo na uchongezi unaosemwa dhidi ya Yehova?

18 Kama Yesu, tunaweza kuwajulisha wengine mambo tunayojua kumhusu Yehova, tukiwafundisha kwamba yeye ni Mungu mwenye upendo na fadhili. Kwa kufanya hivyo, tunapindua uwongo na uchongezi unaosemwa dhidi ya Yehova. Tunalitakasa jina la Yehova, tukilifanya kuwa takatifu katika akili na mioyo ya watu. Sisi pia tunaweza kumwiga Yehova. Hilo linawezekana hata ingawa sisi si wakamilifu. (Efe. 5:1, 2) Tunapowaonyesha watu kupitia maneno na matendo yetu jinsi Yehova alivyo kikweli, tunachangia katika kulitakasa jina lake. Tunalitetea jina hilo kwa kuwaweka watu huru kutokana na mafundisho yasiyo ya kweli kumhusu Mungu. * Pia, tunathibitisha kwamba wanadamu wasio wakamilifu wanaweza kudumisha utimilifu wao.—Ayu. 27:5.

Tunataka kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia waelewe utu wa Yehova wenye upendo na fadhili (Tazama fungu la 18 na 19) *

19. Kulingana na Isaya 63:7, lengo kuu la kuwafundisha wengine linapaswa kuwa nini?

19 Fikiria jambo lingine tunaloweza kufanya ili tutakase jina la Yehova. Tunapowafundisha wengine kweli za Biblia, mara nyingi tunakazia kuhusu enzi kuu ya Mungu, kwamba Yehova ana haki ya kutawala ulimwengu, na hilo ni sahihi kabisa. Hata hivyo, ingawa ni jambo muhimu kuwafundisha watu kuhusu sheria za Mungu, lengo letu kuu ni kuwasaidia wampende Yehova, Baba yetu, na wawe washikamanifu kwake. Hivyo, tunahitaji kuwaonyesha wazi sifa za Yehova zenye kuvutia, tukikazia utu wa Yule anayewakilishwa na jina Yehova. (Soma Isaya 63:7.) Tunapofundisha kwa njia hiyo, tutawasaidia wengine wampende Yehova na kumtii kwa sababu watatamani kuwa washikamanifu kwake.

20. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Hivyo basi, tunaweza kuhakikishaje kwamba mwenendo wetu na njia yetu ya kufundisha itawasaidia wengine wawe na maoni mazuri kuhusu jina la Yehova na kuwafanya wamkaribie? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

WIMBO 2 Jina Lako Ni Yehova

^ fu. 5 Ni suala gani muhimu linalowakabili wanadamu na malaika wote? Kwa nini suala hilo ni muhimu sana, na ni jukumu gani tunalotimiza katika kusuluhishwa kwa suala hilo? Kuelewa majibu ya maswali hayo mawili na mengine yanayohusiana nayo, kutatusaidia kuimarisha uhusiano wetu pamoja na Yehova.

^ fu. 18 Pindi fulani machapisho yetu yamefundisha kwamba jina la Yehova halihitaji kutetewa kwa sababu hakuna yeyote ambaye amewahi kutilia shaka haki ya Yehova ya kuitwa kwa jina hilo. Hata hivyo, uelewaji uliorekebishwa ulitolewa kwenye mkutano wa kila mwaka uliofanywa 2017. Mwenyekiti alieleza hivi: “Kwa ufupi, si kosa kusali kwamba jina la Yehova litetewe kwa sababu kwa kweli sifa yake inapaswa kutetewa au kuondolewa lawama.”​—Tazama programu ya Januari 2018 kwenye jw.org®. Tafuta kwenye MAKTABA > JW BROADCASTING®.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: Ibilisi alimchongea Mungu kwa kumwambia Hawa kwamba Mungu ni mwongo. Kwa karne nyingi, Shetani amekuwa akiendeleza mawazo ya uwongo, kama vile fundisho la kwamba Mungu ni mkatili na kwamba hakuwaumba wanadamu.

^ fu. 64 MAELEZO YA PICHA: Ndugu huyu anakazia kuhusu utu wa Mungu anapoongoza funzo la Biblia.