Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 24

“Unganisha Moyo Wangu Ili Niliogope Jina Lako”

“Unganisha Moyo Wangu Ili Niliogope Jina Lako”

“Unganisha moyo wangu ili niliogope jina lako. Ninakusifu, Ee Yehova Mungu wangu, kwa moyo wangu wote.” —ZAB. 86:11, 12.

WIMBO 7 Yehova, Nguvu Yetu

MUHTASARI *

1. Inamaanisha nini kumwogopa Mungu, na kwa nini woga huo ni muhimu kwa wale wanaompenda Yehova?

WAKRISTO wanampenda Mungu, na pia wanamwogopa. Kwa wengine, huenda hayo yakaonekana kuwa mambo mawili yanayopingana. Hata hivyo, hatuzungumzii aina ya woga unaoweza kukutisha. Tutazungumzia aina ya pekee ya woga. Watu walio na woga wa aina hiyo wanamhofu sana Mungu na kumheshimu sana kutoka moyoni. Hawangependa kumchukiza Baba yao wa mbinguni kwa sababu hawataki kuharibu urafiki wao pamoja naye.—Zab. 111:10; Met. 8:13.

2. Kwa msingi wa maneno ya Mfalme Daudi kwenye Zaburi 86:11, tutazungumzia mambo gani mawili?

2 Soma Zaburi 86:11. Unapoyatafakari maneno hayo, unaweza kutambua kwamba mfalme mwaminifu Daudi alielewa umuhimu wa kumwogopa Mungu. Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuyatumia maneno ya Daudi yaliyoongozwa na roho ya Mungu. Kwanza, tutachunguza kwa nini tunapaswa kuliheshimu sana jina la Mungu. Pili, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunaliheshimu sana jina la Mungu katika maisha yetu ya kila siku.

KWA NINI TUNAPASWA KULIHESHIMU SANA JINA LA YEHOVA?

3. Ni tukio gani ambalo huenda lilimsaidia Musa aendelee kuliheshimu sana jina la Mungu?

3 Fikiria jinsi Musa alivyohisi alipokuwa amejikunyata kwenye shimo ndani ya mwamba na kuona maono ya utukufu wa Yehova ulipokuwa ukipita. Huenda hilo lilikuwa tukio lenye kustaajabisha zaidi ambalo mwanadamu amewahi kuona kabla ya kuja kwa Yesu duniani! Musa alisikia maneno haya ambayo inaelekea yalisemwa na malaika: “Mimi Yehova, Yehova, ni Mungu mwenye rehema na huruma, si mwepesi wa hasira, nina upendo mwingi mshikamanifu na kweli, ninawatendea maelfu kwa upendo mshikamanifu, ninasamehe makosa na uovu na dhambi.” (Kut. 33:17-23; 34:5-7) Huenda Musa alikumbuka tukio hilo alipotumia jina la Yehova. Haishangazi kwamba baadaye Musa aliwaonya Waisraeli, watu wa Mungu, ‘waliogope jina hilo tukufu na lenye kuogopesha.’—Kum. 28:58.

4. Ni nini kinachoweza kutusaidia tumheshimu Yehova hata zaidi?

4 Tunapofikiria kuhusu jina Yehova, tunapaswa pia kutafakari kuhusu Yule anayeitwa kwa jina hilo. Tunapaswa kutafakari kuhusu sifa zake kama vile nguvu, hekima, haki, na upendo wake. Kutafakari kuhusu sifa hizo na sifa nyingine kunaweza kutuchochea tumheshimu hata zaidi.—Zab. 77:11-15.

5-6. (a) Jina la Mungu linamaanisha nini? (b) Kulingana na Kutoka 3:13, 14 na Isaya 64:8, Yehova hutumia njia gani ili kusababisha mapenzi yake yatendeke?

5 Tunajua nini kuhusu maana ya jina la Mungu? Wasomi wengi wanakubali kwamba inaonekana jina Yehova linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.” Maana hiyo inatukumbusha kwamba hakuna chochote kinachoweza kumzuia Yehova kutimiza mapenzi yake, na anaweza kusababisha chochote kitendeke. Jinsi gani?

6 Yehova husababisha mambo yatendeke kwa kuwa chochote kinachohitajika ili kutimiza kusudi lake. (Soma Kutoka 3:13, 14.) Mara nyingi tumetiwa moyo tutafakari kuhusu sehemu hiyo yenye kustaajabisha ya utu wa Yehova. Pia, Yehova anaweza kusababisha watumishi wake wasio wakamilifu wawe kile kinachohitajika ili wamtumikie na kutimiza kusudi lake. (Soma Isaya 64:8.) Kwa njia hizo, Yehova husababisha mapenzi yake yatimizwe. Hakuna kinachoweza kumfanya Yehova ashindwe kusababisha kutimizwa kwa makusudi yake.—Isa. 46:10, 11.

7. Tunaweza kufanya nini ili uthamini wetu kwa Baba yetu wa mbinguni uongezeke?

7 Tunaweza kufanya uthamini wetu kwa Baba yetu wa mbinguni uongezeke kwa kutafakari kuhusu mambo ambayo amefanya na mambo ambayo ametuwezesha kufanya. Kwa mfano, tunapotafakari kuhusu maajabu ya uumbaji, tunastaajabishwa na mambo ambayo Yehova ametimiza, mambo ambayo amesababisha yawepo. (Zab. 8:3, 4) Na tunapotafakari kuhusu kile ambacho Yehova amesababisha tuwe ili tutimize mapenzi yake, tunachochewa kumpa heshima kubwa hata zaidi. Kwa kweli, jina Yehova ni lenye kuogopesha! Linatia ndani kila kitu kuhusu utu wa Baba yetu, yote aliyofanya, na yote atakayofanya.—Zab. 89:7, 8.

“NITALITANGAZA JINA LA YEHOVA”

Mambo ambayo Musa alifundisha yaliburudisha. Yalikazia kuhusu jina na utu wa Yehova Mungu (Tazama fungu la 8) *

8. Kulingana na Kumbukumbu la Torati 32:2, 3, Yehova ana maoni gani kuhusu jina lake?

8 Muda mfupi kabla ya Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, Yehova alimfundisha Musa maneno ya wimbo fulani. (Kum. 31:19) Kisha Musa alipaswa kuwafundisha watu wimbo huo. (Soma Kumbukumbu la Torati 32:2, 3.) Tunapotafakari mstari wa 2 na wa 3, tunaona wazi kwamba Yehova hataki jina lake lifichwe, kana kwamba halipaswi kutamkwa kwa sababu ni takatifu sana. Anataka jina lake lijulikane na kila mtu! Lilikuwa pendeleo kubwa sana kwa watu kumsikia Musa akiwafundisha kumhusu Yehova na jina Lake tukufu! Mambo ambayo Musa aliwafundisha yaliimarisha imani yao na kuwaburudisha kama mvua ya rasharasha juu ya majani. Tunaweza kuhakikishaje kwamba ufundishaji wetu uko hivyo pia?

9. Tunaweza kuchangiaje kutakaswa kwa jina la Yehova?

9 Tunapohubiri nyumba kwa nyumba au hadharani, tunaweza kutumia Biblia zetu kuwaonyesha watu jina la kibinafsi la Mungu, yaani, Yehova. Tunaweza kuwapa machapisho yetu maridadi, video zetu bora, na habari zilizo katika tovuti yetu zinazomtukuza Yehova. Tunapokuwa kazini, shuleni, au tunaposafiri, tunaweza kutafuta fursa za kuzungumza na wengine kumhusu Mungu wetu mpendwa na jinsi alivyo. Tunapowajulisha watu tunaokutana nao kuhusu kusudi lenye upendo la Yehova kuwaelekea wanadamu na dunia, tunawasaidia wamwone Yehova kwa njia ambayo huenda ni mpya kabisa kwao. Tunapowaambia wengine kweli kumhusu Baba yetu mwenye upendo, tunachangia katika kulitakasa jina la Mungu. Tunawasaidia watu wasahihishe mafundisho ya uwongo na uchongezi kumhusu Yehova ambao huenda wamefundishwa. Tunawapa watu mafundisho bora kabisa yenye lishe na yanayoburudisha.—Isa. 65: 13, 14.

10. Tunapojifunza Biblia pamoja na watu, kwa nini tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kuwafundisha matakwa na viwango vya Mungu?

10 Tunapojifunza Biblia pamoja na wanafunzi wetu, tungependa kuwasaidia wamjue Yehova na kulitumia jina lake. Pia, tungependa kuwasaidia waelewe maana ya jina lake. Je, tutafaulu kutimiza hilo ikiwa tutawafundisha tu maagizo ya Mungu, viwango vyake, na jinsi tunavyopaswa kujiendesha? Huenda mwanafunzi mzuri akajifunza kuhusu sheria za Mungu, na hata akazipenda. Lakini je, atamtii Yehova kwa sababu anampenda Yeye mwenyewe binafsi? Kumbuka, Hawa alijua sheria ya Mungu, lakini hakumpenda kikweli Mungu aliyetoa sheria hiyo; hali ilikuwa vivyo hivyo pia kwa Adamu. (Mwa. 3:1-6) Hivyo, ni lazima tufanye mengi zaidi ya kuwafundisha wengine kuhusu matakwa na viwango vya Mungu vya uadilifu.

11. Tunapowafundisha wanafunzi wetu kuhusu sheria na viwango vya Mungu, tunaweza kuwasaidiaje wampende Yehova, Mpaji-Sheria wetu?

11 Viwango na matakwa ya Yehova hutufaa nyakati zote. (Zab. 119:97, 111, 112) Lakini huenda wanafunzi wetu wasione viwango na matakwa ya Yehova kwa njia hiyo, mpaka watakapotambua kwamba Yehova alituwekea sheria hizo kwa sababu anatupenda. Hivyo, tunaweza kuwauliza hivi wanafunzi wetu: “Unafikiri ni kwa nini Mungu anataka watumishi wake wafanye jambo hili, au wasifanye jambo hili? Jambo hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?” Ikiwa tutawasaidia wanafunzi wetu watafakari kumhusu Yehova na kusitawisha upendo wa kweli kwa jina lake tukufu, itakuwa rahisi zaidi kwetu kugusa mioyo yao. Hivyo, wanafunzi wetu hawatazipenda tu sheria za Yehova, bali pia watampenda Yehova mwenyewe, mtoaji wa sheria hizo. (Zab. 119:68) Imani yao itazidi kukua na jambo hilo litawasaidia kuvumilia majaribu makali wakati ujao.—1 Kor. 3:12-15.

“SISI TUTATEMBEA KATIKA JINA LA YEHOVA”

Pindi moja Daudi aliruhusu moyo wake ugawanyike (Tazama fungu la 12)

12. Pindi moja, Daudi alishindwaje kudumisha moyo uliounganika, na matokeo yalikuwa nini?

12 Zaburi 86:11 ina maneno haya muhimu, “unganisha moyo wangu.” Mfalme Daudi aliongozwa na roho ya Mungu kuandika maneno hayo. Wakati wa maisha yake, Daudi alijionea jinsi ilivyo rahisi kwa mtu kuruhusu moyo wake ugawanyike. Pindi moja alipokuwa kwenye paa ya nyumba yake alimwona mke wa mtu mwingine akioga. Je, pindi hiyo moyo wa Daudi ulikuwa umeunganika au umegawanyika? Daudi alijua sheria hii ya Yehova: “Usimtamani mke wa jirani yako.” (Kut. 20:17) Ingawa hivyo, inaonekana kwamba aliendelea kumtazama. Moyo wake ukagawanyika; alimtamani mwanamke huyo, Bath-sheba, na pia alitamani kumpendeza Yehova. Ingawa Daudi alikuwa amempenda na kumwogopa Yehova kwa muda mrefu, alijiruhusu atende kulingana na tamaa yake yenye ubinafsi. Pindi hiyo, Daudi alifuata mkondo mbaya sana. Alililetea suto jina la Yehova. Pia, Daudi aliwasababishia madhara makubwa watu wasio na hatia, kutia ndani familia yake mwenyewe.—2 Sam. 11:1-5, 14-17; 12:7-12.

13. Tunajuaje kwamba moyo wa Daudi uliunganika tena?

13 Yehova alimtia nidhamu Daudi, na uhusiano wake pamoja na Yehova ukawa mzuri tena. (2 Sam. 12:13; Zab. 51:2-4, 17) Daudi alikumbuka huzuni na matatizo yaliyotokea aliporuhusu moyo wake ugawanyike. Maneno yake yaliyoandikwa kwenye Zaburi 86:11 yanaweza pia kumaanisha: “Nipe moyo ambao haujagawanyika.” Je, Yehova alimsaidia Daudi kuufanya moyo wake uwe kamili, au usiogawanyika? Ndiyo, kwa sababu baadaye Neno la Yehova linamrejelea kuwa mtu ambaye ‘moyo wake ulikuwa kamili kwa Yehova Mungu wake.’—1 Fal. 11:4; 15:3.

14. Tunapaswa kujiuliza swali gani, na kwa nini?

14 Mfano wa Daudi unatutia moyo na pia ni onyo kwetu. Kuanguka kwake katika dhambi nzito ni onyo kwa watumishi wa Mungu leo. Iwe tumeanza kumtumikia Yehova hivi karibuni au tumekuwa tukimtumikia kwa miaka mingi, tunapaswa kujiuliza, ‘Je, ninapinga jitihada za Shetani za kutaka kuugawanya moyo wangu?’

Shetani atajaribu kufanya chochote ili kuugawanya moyo wako. Usimruhusu! (Tazama fungu la 15 na 16) *

15. Kumwogopa Mungu kunaweza kutulindaje tunapoona picha zinazoamsha hamu ya ngono?

15 Kwa mfano, unapoona picha kwenye televisheni au Intaneti inayoweza kuamsha hamu ya ngono, wewe hutendaje? Huenda ikawa rahisi kujiambia kwamba picha au sinema hiyo kimsingi si ponografia. Lakini je, inawezekana kwamba Shetani anatumia mambo hayo ili kuugawanya moyo wetu? (2 Kor. 2:11) Tunaweza kufananisha picha hiyo na tindo ambayo mtu hutumia kupasua gogo kubwa. Mwanzoni mtu huigonga tindo ili sehemu nyembamba yenye ncha kali iweze kupenya kwenye gogo. Tindo inapozidi kuzama, hatimaye gogo hupasuka. Je, inawezekana kwamba picha zinazoamsha hamu ya ngono ni kama ile sehemu nyembamba ya tindo? Mwanzoni huenda kutazama mambo hayo kukaonekana kuwa jambo dogo lisilo na madhara, lakini punde si punde jambo hilo linaweza kusababisha mtu afanye dhambi zitakazougawanya moyo wake na kuvunja utimilifu wake. Hivyo, usiruhusu jambo lolote lisilofaa liingie moyoni mwako! Endelea kuunganisha moyo wako ili uogope jina la Yehova!

16. Tunapaswa kujiuliza maswali gani tunapokabili vishawishi?

16 Mbali na picha zinazoamsha hamu ya ngono, Shetani hutumia mambo mengine ili kutushawishi tuingie kwenye makosa. Sisi hutendaje? Ni rahisi kutoa visingizio. Kwa mfano, huenda tukawaza hivi: ‘Sitatengwa na ushirika kwa kufanya jambo hili, basi inaonekana si jambo zito sana.’ Hiyo ni njia mbaya sana ya kufikiri. Ni vema zaidi kujiuliza maswali kama haya: ‘Je, Shetani anajaribu kutumia kishawishi hiki kuugawanya moyo wangu? Ikiwa nitajiruhusu ninaswe na tamaa mbaya, je, nitaliletea suto jina la Yehova? Je, jambo hilo litanifanya niwe karibu zaidi na Mungu wangu, au litanifanya niwe mbali naye? Tafakari maswali kama hayo. Sali ili upate hekima ya kuyajibu kwa unyoofu, bila kujidanganya. (Yak. 1:5) Kufanya hivyo kunaweza kuwa ulinzi mkubwa sana na kutakusaidia upinge vishawishi kwa uthabiti, kama Yesu alivyofanya aliposema: “Nenda zako, Shetani!”—Mt. 4:10.

17. Kwa nini moyo uliogawanyika hauna thamani? Toa mfano.

17 Moyo uliogawanyika hauna thamani yoyote. Wazia kwamba timu fulani ina wachezaji ambao hawaelewani. Baadhi yao wanajitafutia umaarufu wao wenyewe, wachache hawataki kufuata sheria za mchezo, na wengine kadhaa wanamdharau kocha. Ni vigumu kwa timu kama hiyo kushinda. Kinyume chake, timu yenye umoja ina uwezekano mkubwa zaidi wa kushinda. Moyo wako unaweza kuwa kama timu yenye mafanikio, ikiwa mawazo, tamaa, na hisia zako zimeungana ili kumtumikia Yehova. Kumbuka kwamba Shetani angependa kuugawanya moyo wako. Anataka mawazo, tamaa, na hisia zako zipingane na viwango vya Yehova. Hata hivyo, ili umtumikie Yehova unahitaji kuwa na moyo kamili. (Mt. 22:36-38) Kamwe usimruhusu Shetani augawanye moyo wako!

18. Kulingana na maneno ya Mika 4:5, umeazimia kufanya nini?

18 Sali kwa Yehova kama Daudi alivyofanya aliposali: “Unganisha moyo wangu ili niliogope jina lako.” Azimia kuishi kulingana na sala hiyo. Azimia kila siku kuonyesha kwamba unaliheshimu sana jina takatifu la Yehova kupitia maamuzi unayofanya, iwe ni makubwa au madogo. Kwa kufanya hivyo, ukiwa Shahidi wa Yehova, utalitukuza jina la Yehova. (Met. 27:11) Na sisi sote tutaweza kusema hivi kama nabii Mika: “Sisi tutatembea katika jina la Yehova Mungu wetu milele na milele.”—Mika 4:5.

WIMBO 41 Tafadhali Sikiliza Sala Yangu

^ fu. 5 Katika makala hii, tutakazia mambo ambayo Daudi alitaja katika sala yake kwenye Zaburi 86:11, 12. Inamaanisha nini kuliogopa jina la Yehova? Tuna msingi gani wa kuliheshimu sana jina hilo kuu? Na kumwogopa Mungu kunaweza kutulindaje ili tusinaswe na kishawishi?

^ fu. 53 MAELEZO YA PICHA: Musa aliwafundisha watu wa Mungu wimbo uliomtukuza Yehova.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Hawa hakupinga tamaa mbaya. Tofauti naye, sisi tunakataa kutazama picha au jumbe ambazo zinaweza kuchochea tamaa mbaya na kuliletea suto jina la Mungu.