Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujizuia—Sifa Muhimu Ili Tupate Kibali cha Yehova

Kujizuia—Sifa Muhimu Ili Tupate Kibali cha Yehova

“Binamu yangu alipoanza kupigana nami, nilimkaba koo na kuanza kumnyonga. Nilitaka kumuua.”—Paul.

“Nikiwa nyumbani, nilikuwa nikikasirika upesi sana bila sababu ya msingi. Ningevunja fanicha, midoli ya watoto, yaani, chochote ambacho ningekiona.”—Marco.

Huenda tusifikie hatua kama hizo. Hata hivyo, nyakati nyingine sisi sote hushindwa kujizuia. Sababu kuu ni kwamba tumerithi mielekeo ya dhambi kutoka kwa mtu wa kwanza, Adamu. (Rom. 5:12) Kama Paul na Marco, baadhi ya watu hushindwa kudhibiti hasira yao. Wengine hupata changamoto kudhibiti mawazo yao. Wao huendelea kufikiria sana mambo yanayowaogopesha au mara kwa mara wanahangaishwa na maoni yasiyofaa kujihusu. Na bado ni changamoto kwa wengine kuzuia tamaa ya kufanya uasherati, kunywa pombe kupita kiasi, au kutumia dawa za kulevya.

Watu wanaoshindwa kudhibiti fikira, tamaa, au matendo yao wanaweza kuharibu maisha yao. Lakini tunaweza kuepuka matokeo hayo. Jinsi gani? Kwa kusitawisha sifa ya kujizuia. Ili tuweze kufanya hivyo, acheni tuzungumzie maswali haya matatu: (1) Kujizuia kunamaanisha nini? (2) Kwa nini ni muhimu kujizuia? (3) Tunaweza kusitawishaje sifa hiyo ambayo ni mojawapo ya sifa za “tunda la roho”? (Gal. 5:22, 23) Kisha tutachunguza mambo ambayo sisi binafsi tunaweza kufanya ikiwa nyakati fulani tunashindwa kuonyesha sifa ya kujizuia.

KUJIZUIA KUNAMAANISHA NINI?

Mtu aliye na sifa ya kujizuia haruhusu moyo wake utosheleze kila tamaa aliyo nayo. Badala yake, anajizuia ili asizungumze au kutenda kwa njia isiyompendeza Mungu.

Kwa hakika Yesu alionyesha sifa ya kujizuia

Yesu alituonyesha maana ya kuwa na sifa ya kujizuia. Biblia inasema hivi: “Alipokuwa akitukanwa, hakujibu kwa kutukana. Alipokuwa akiteseka, hakutoa vitisho, bali alijikabidhi mkononi mwa Yule anayehukumu kwa uadilifu.” (1 Pet. 2:23) Yesu alionyesha sifa hiyo ya kujizuia wapinzani walipomdhihaki akiwa ametundikwa kwenye mti wa mateso. (Mt. 27:39-44) Hapo awali, alijizuia kwa kiwango kikubwa sana viongozi wa kidini wenye chuki walipojaribu kumtega kwa maneno yake. (Mt. 22:15-22) Na alituwekea mfano mzuri sana Wayahudi wenye hasira walipookota mawe ili wampige! Badala ya kulipiza kisasi, “Yesu akajificha na kuondoka hekaluni.”—Yoh. 8:57-59.

Je, tunaweza kuiga mfano wa Yesu? Kwa kiasi fulani tunaweza. Mtume Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Pet. 2:21) Ingawa sisi si wakamilifu, tunaweza kufuata kwa ukaribu kielelezo cha Yesu cha kuonyesha sifa ya kujizuia. Kwa nini ni muhimu kwetu kufanya hivyo?

KWA NINI NI MUHIMU KUJIZUIA?

Tunahitaji kuwa na sifa ya kujizuia ili tuwe na kibali cha Yehova. Hata ikiwa tumemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa muda mrefu, tunaweza kupoteza urafiki wetu pamoja naye ikiwa tutashindwa kujizuia kuhusiana na mambo tunayosema na kutenda.

Mfikirie Musa, ambaye “alikuwa mtu mpole zaidi kuliko watu wote duniani” wakati huo. (Hes. 12:3) Baada ya kuonyesha subira na kuvumilia kwa miaka mingi malalamiko ya Waisraeli, Musa alishindwa kuonyesha sifa ya kujizuia. Alikasirika sana Waisraeli walipolalamika kwa mara nyingine kuhusu uhaba wa maji. Alizungumza na watu kwa ukali, akiwaambia: “Sikilizeni sasa, enyi waasi! Je, ni lazima tuwatolee maji katika mwamba huu?”—Hes. 20:2-11.

Musa alishindwa kujizuia. Hakumpa utukufu Yehova aliyekuwa Chanzo cha maji hayo yaliyotokea kimuujiza. (Zab. 106:32, 33) Matokeo ni kwamba Yehova hakumruhusu aingie katika Nchi ya Ahadi. (Hes. 20:12) Hadi siku aliyokufa, inawezekana kwamba Musa alijutia sana kitendo cha kushindwa kudhibiti hasira yake.—Kum. 3:23-27.

Tunajifunza nini? Hata ikiwa tumekuwa katika kweli kwa muda mrefu, hatupaswi kamwe kuzungumza bila heshima na wale wanaotuudhi au wanaohitaji kurekebishwa. (Efe. 4:32; Kol. 3:12) Ni kweli kwamba kadiri umri wetu unavyozidi kusonga, nyakati nyingine inaweza kuwa vigumu zaidi kwetu kuonyesha subira. Lakini mkumbuke Musa. Hatungependa kamwe kuharibu rekodi yetu ya uaminifu ya muda mrefu kwa sababu ya kukosa sifa ya kujizuia. Tunaweza kusitawishaje sifa hiyo muhimu?

JINSI YA KUSITAWISHA SIFA YA KUJIZUIA

Sali upate roho takatifu. Kwa nini? Kwa sababu kujizuia ni sifa ya tunda la roho ya Mungu, na Yehova huwapa roho yake wale wanaomwomba. (Luka 11:13) Kupitia roho yake, Yehova anaweza kutupatia nguvu tunazohitaji. (Flp. 4:13) Pia, anaweza kutusaidia tusitawishe sifa nyingine za tunda la roho, kama vile upendo, ambao utatusaidia tuimarishe uwezo wetu wa kujizuia.—1 Kor. 13:5.

Epuka kitu chochote kinachodhoofisha uwezo wako wa kujizuia

Jiepushe na kitu chochote kinachoweza kudhoofisha uwezo wako wa kujizuia. Kwa mfano, jiepushe na tovuti na burudani zinazoonyesha mwenendo mpotovu. (Efe. 5:3, 4) Na si hivyo tu, ni lazima tujiepushe na kitu chochote kinachoweza kutushawishi tufanye mambo yasiyofaa. (Met. 22:3; 1 Kor. 6:12) Kwa mfano, mtu ambaye ni rahisi kwake kujiingiza katika mwenendo mchafu kingono huenda akahitaji kujiepusha kabisa na vitabu au sinema za mahaba.

Huenda tukahisi kuwa ni vigumu kufuata shauri hilo. Hata hivyo, tukifanya jitihada, Yehova atatupatia nguvu tunazohitaji ili tuweze kujizuia. (2 Pet. 1:5-8) Atatusaidia tudhibiti mawazo, usemi, na matendo yetu. Uthibitisho wa jambo hilo ni Paul na Marco waliotajwa awali; walijifunza kudhibiti hasira kali waliyokuwa nayo. Pia, mfikirie ndugu ambaye mara kwa mara alishindwa kuzuia hasira yake alipokuwa akiendesha gari, hivi kwamba alikuwa akigombana na madereva wengine barabarani. Alishughulikiaje hali yake? Anaeleza hivi: “Nilisali kwa bidii kila siku. Nilisoma na kujifunza makala zinazohusu kujizuia na kukariri mistari ya Biblia ambayo ingeweza kunisaidia. Ingawa nimekuwa nikifanyia kazi jambo hilo kwa miaka mingi, bado mimi hujikumbusha kila asubuhi lengo langu la kuendelea kuwa mtulivu. Ninajitahidi kuondoka nyumbani mapema ili nisiwe na haraka ninapoendesha gari nikielekea kwenye shughuli zangu.”

TUNAPOSHINDWA KUJIZUIA

Nyakati nyingine sisi hushindwa kuonyesha sifa ya kujizuia. Hilo linapotokea, huenda tukaona aibu sana kusali kwa Yehova. Lakini huo ndio wakati tunapohitaji kusali hata zaidi. Hivyo, sali kwa Yehova papo hapo. Msihi akusamehe, mwombe msaada wake, na uazimie kutorudia kosa hilo tena. (Zab. 51:9-11) Yehova hataidharau kamwe sala yako ya unyoofu ya kumwomba akuonyeshe rehema. (Zab. 102:17) Mtume Yohana anatukumbusha kwamba damu ya Mwana wa Mungu “hutusafisha kutoka katika dhambi yote.” (1 Yoh. 1:7; 2:1; Zab. 86:5) Kumbuka kwamba Yehova anawaambia watumishi wake wawe wakisameheana tena na tena. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatusamehe vivyo hivyo pia.—Mt. 18:21, 22; Kol. 3:13.

Yehova hakufurahia Musa aliposhindwa kwa muda mfupi kuonyesha sifa ya kujizuia kule nyikani. Ingawa hivyo, Yehova alimsamehe. Na Neno la Mungu linamtaja Musa kuwa mfano bora wa imani. (Kum. 34:10; Ebr. 11:24-28) Yehova hakumruhusu Musa aingie katika Nchi ya Ahadi, lakini atamkaribisha kwenye dunia Paradiso na kumpa tarajio la kuishi milele. Tunaweza kuwa na tarajio hilohilo ikiwa tutaendelea kujitahidi kusitawisha sifa muhimu ya kujizuia.—1 Kor. 9:25.