Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 27

Usijifikirie Mwenyewe Kuliko Ilivyo Lazima

Usijifikirie Mwenyewe Kuliko Ilivyo Lazima

“Ninamwambia kila mtu kati yenu asijifikirie mwenyewe kuliko ilivyo lazima kufikiri, bali afikiri ili awe na akili timamu.”—ROM. 12:3.

WIMBO 130 Uwe Mwenye Kusamehe

MUHTASARI *

1. Kulingana na Wafilipi 2:3, kwa nini tutakuwa na uhusiano mzuri pamoja na wengine ikiwa tuna sifa ya unyenyekevu?

SISI hujitiisha kwa viwango vya Yehova, tukitambua kwamba sikuzote Yehova anajua mambo yanayotufaa zaidi. (Efe. 4:22-24) Sifa ya unyenyekevu hutuchochea tutangulize mapenzi ya Yehova badala ya kutanguliza mapenzi yetu na tuwaone wengine kuwa bora kuliko sisi. Hivyo, tunafurahia uhusiano mzuri pamoja na Yehova na waamini wenzetu.​—Soma Wafilipi 2:3.

2. Mtume Paulo alitambua nini, na tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Hata hivyo, tusipokuwa waangalifu tunaweza kuathiriwa na watu wenye kiburi na wenye ubinafsi walio katika mfumo huu wa Shetani. * Inaonekana kwamba baadhi ya Wakristo katika karne ya kwanza waliathiriwa na hali hiyo, kwa sababu mtume Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Roma: “Ninamwambia kila mtu kati yenu asijifikirie mwenyewe kuliko ilivyo lazima kufikiri, bali afikiri ili awe na akili timamu.” (Rom. 12:3) Paulo alitambua kwamba kwa njia fulani tunahitaji kujifikiria wenyewe. Hata hivyo, unyenyekevu utatusaidia tuwe na maoni yenye usawaziko kujihusu. Makala hii itazungumzia maeneo matatu ambayo sifa ya unyenyekevu itatusaidia tuepuke kujifikiria wenyewe kupita kiasi. Maeneo hayo ni (1) ndoa, (2) mapendeleo yetu ya utumishi, na (3) matumizi yetu ya mitandao ya kijamii.

ONYESHA UNYENYEKEVU KATIKA NDOA YAKO

3. Kwa nini migogoro inaweza kutokea katika ndoa, na wengine hutendaje inapotokea?

3 Yehova alianzisha ndoa ili iwe chanzo cha furaha kwa mume na mke. Hata hivyo, hakuna yeyote aliye mkamilifu, hivyo migogoro inaweza kutokea. Isitoshe, Paulo aliandika kwamba wale wanaofunga ndoa wanaweza kutarajia kupata dhiki kwa kiwango fulani. (1 Kor. 7:28) Baadhi ya wenzi wa ndoa wana desturi ya kugombana mara kwa mara, na huenda wakafikia mkataa kwamba ni afadhali wasingeoana. Ikiwa wameathiriwa na ulimwengu, watafikiria haraka-haraka kwamba suluhisho ni kutalikiana. Watajifikiria wenyewe tu na watafikiri kwamba wanaweza kuwa na furaha ikiwa tu watatalikiana.

4. Ni lazima tuepuke nini?

4 Ni lazima tuepuke fikira za kwamba ndoa yetu imeshindikana. Tunatambua kwamba msingi pekee wa Kimaandiko wa talaka ni uasherati. (Mt. 5:32) Hivyo, tunapokabiliana na dhiki ambayo Paulo alizungumzia, hatungependa kuruhusu kiburi kitufanye tuanze kujiuliza: ‘Je, ndoa hii inanitimizia mahitaji yangu? Je, ninapendwa kama ninavyostahili? Je, ninaweza kufurahia zaidi nikiwa na mtu mwingine?’ Ona jinsi maswali hayo yanavyokazia sifa ya ubinafsi. Hekima ya ulimwengu huu itakuchochea ufuate moyo wako na ufanye mambo yanayokufurahisha wewe, hata ikiwa hilo litamaanisha uvunje ndoa yako. Hekima kutoka kwa Mungu inasema kwamba unapaswa ‘kuangalia, si faida zako mwenyewe, bali pia faida za wengine.’ (Flp. 2:4) Yehova anataka udumishe ndoa yako, si uivunje. (Mt. 19:6) Anataka umfikirie yeye kwanza badala ya kujifikiria mwenyewe.

5. Kulingana na Waefeso 5:33, mume na mke wanapaswa kutendeana jinsi gani?

5 Mume na mke wanapaswa kupendana na kuheshimiana. (Soma Waefeso 5:33.) Biblia inatufundisha tukazie fikira zaidi kutoa badala ya kupokea. (Mdo. 20:35) Ni sifa gani itakayowasaidia wenzi wa ndoa wapendane na kuheshimiana? Jibu ni unyenyekevu. Waume na wake walio wanyenyekevu watatafuta, si faida zao wenyewe, bali faida “ya yule mtu mwingine.”—1 Kor. 10:24.

Badala ya kushindana, wenzi walio wanyenyekevu watashirikiana pamoja kama timu (Tazama fungu la 6)

6. Tunajifunza nini kutokana na maelezo ya Steven na Stephanie?

6 Sifa ya unyenyekevu imewasaidia wenzi wengi Wakristo wawe na furaha nyingi zaidi katika ndoa zao. Kwa mfano, mume anayeitwa Steven anasema hivi: “Ikiwa ninyi ni kama timu, mtashirikiana pamoja, hasa matatizo yanapotokea. Badala ya kujiuliza ‘mimi nitafaidikaje?’ utajiuliza ‘sisi tutafaidikaje?’” Stephanie, mke wake, anahisi vivyo hivyo. Anasema hivi: “Hakuna anayependa kuishi na mtu wanayezozana naye. Tunapokosa kuelewana, tunajitahidi kujua chanzo cha tatizo. Kisha tunasali, tunafanya utafiti, na kuzungumzia jinsi ya kulisuluhisha. Tunashambulia tatizo, hatushambuliani.” Waume na wake huwa na furaha zaidi wanapoepuka kujifikiria zaidi wao wenyewe kuliko ilivyo lazima.

MTUMIKIE YEHOVA KWA “UNYENYEKEVU WOTE”

7. Ndugu anapaswa kuwa na mtazamo gani anapopata pendeleo fulani la utumishi?

7 Tunaliona kuwa pendeleo kubwa kumtumikia Yehova kwa njia yoyote tunayoweza. (Zab. 27:4; 84:10) Ikiwa ndugu yuko tayari kutumiwa zaidi na tengenezo la Yehova, hilo ni jambo jema. Isitoshe Biblia inasema hivi: “Ikiwa mwanamume anajitahidi kuwa mwangalizi, anatamani kazi njema.” (1 Tim. 3:1) Hata hivyo, anapopata mgawo fulani, hapaswi kujifikiria mwenyewe kuliko ilivyo lazima. (Luka 17:7-10) Lengo lake linapaswa kuwa kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu.—2 Kor. 12:15.

8. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Diotrefe, Uzia, na Absalomu?

8 Biblia ina mifano ya kuonya ya watu ambao walijifikiria wenyewe kupita kiasi. Kwa kuwa Diotrefe hakuwa mwenye kiasi, alitaka kuwa “wa kwanza” katika kutaniko. (3 Yoh. 9) Kwa kiburi, Uzia alijaribu kufanya kazi ambayo Yehova hakumwambia afanye. (2 Nya. 26:16-21) Kwa hila, Absalomu alijaribu kuwashawishi watu wamuunge mkono kwa sababu alitaka kuwa mfalme. (2 Sam. 15:2-6) Mifano hiyo ya Biblia inaonyesha wazi kwamba Yehova hapendezwi na watu wanaojitafutia utukufu wao wenyewe. (Met. 25:27) Hatimaye, watu wenye kiburi na wenye kujitafutia umashuhuri huishia kwenye matatizo.—Met. 16:18.

9. Yesu alituwekea mfano gani?

9 Tofauti na mifano hiyo ya kuonya, mfikirie Yesu, “ambaye, ingawa alikuwa katika umbo la Mungu, hakufikiria kufanya unyakuzi, yaani, kwamba yeye awe sawa na Mungu.” (Flp. 2:6) Yesu, ambaye ni wa pili kutoka kwa Yehova, hajifikirii mwenyewe kuliko ilivyo lazima. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Anayejiendesha kama mdogo zaidi kati yenu nyote ndiye mkuu.” (Luka 9:48) Ni baraka kubwa sana kutumikia pamoja na mapainia, watumishi wa huduma, wazee wa makutaniko, na waangalizi wa mzunguko wanaomwiga Yesu kwa kuonyesha sifa ya unyenyekevu! Watumishi wanyenyekevu wa Yehova wanachangia roho ya upendo ambayo hutambulisha tengenezo la Mungu.—Yoh. 13:35.

10. Unapaswa kufanya nini ikiwa unahisi kwamba matatizo kutanikoni hayashughulikiwi kwa njia inayofaa?

10 Vipi ikiwa inaonekana kwamba kuna matatizo kutanikoni na unahisi kwamba hayashughulikiwi kwa njia inayofaa? Badala ya kulalamika, unaweza kuonyesha unyenyekevu kwa kuwaunga mkono wale wanaoongoza. (Ebr. 13:17) Ili ufanye hivyo, jiulize: ‘Je, kweli matatizo ninayoona ni makubwa sana hivi kwamba yanahitaji kurekebishwa? Je, huu ndio wakati unaofaa wa kuyarekebisha? Je, ni jukumu langu kuyarekebisha? Kwa unyoofu, je, kweli ninajitahidi kuendeleza umoja, au ninajaribu kujitafutia sifa mimi mwenyewe?’

Wale waliokabidhiwa jukumu fulani hawapaswi tu kujulikana kwa uwezo walio nao bali pia wanapaswa kujulikana kwa unyenyekevu wao (Tazama fungu la 11) *

11. Kulingana na Waefeso 4:2, 3, tunapata matokeo gani tunapomtumikia Yehova kwa unyenyekevu?

11 Yehova humthamini sana mtu mnyenyekevu kuliko mwenye uwezo, na anayedumisha umoja kuliko anayetimiza mambo kwa ufanisi. Hivyo, fanya yote uwezayo ili umtumikie Yehova kwa unyenyekevu. Ukifanya hivyo, utaendeleza umoja katika kutaniko. (Soma Waefeso 4:2, 3.) Uwe na bidii katika huduma. Tafuta fursa za kuwatumikia wengine kwa kuwatendea mambo mema. Uwe mkarimu kwa wote, kutia ndani wale ambao hawana mapendeleo kutanikoni. (Mt. 6:1-4; Luka 14:12-14) Unaposhirikiana pamoja na kutaniko kwa unyenyekevu, ndugu na dada hawataona tu uwezo wako bali pia wataona unyenyekevu wako.

ONYESHA UNYENYEKEVU UNAPOTUMIA MITANDAO YA KIJAMII

12. Je, Biblia inatutia moyo tuwe na marafiki? Eleza.

12 Yehova alituumba ili tufurahie uhusiano mzuri pamoja na marafiki na watu wa familia. (Zab. 133:1) Yesu alikuwa na marafiki wazuri. (Yoh. 15:15) Biblia inafafanua kuhusu manufaa ya kuwa na marafiki wa kweli. (Met. 17:17; 18:24) Na inatuambia kwamba si vizuri kujitenga na wengine. (Met. 18:1) Watu wengi huhisi kwamba mitandao ya kijamii ndiyo njia ya kupata marafiki wengi na kuepuka upweke. Hata hivyo, tunahitaji kujihadhari inapohusu kutumia njia hiyo ya mawasiliano.

13. Kwa nini baadhi ya watu wanaotumia mitandao ya kijamii huhisi upweke na kushuka moyo?

13 Utafiti unaonyesha kwamba watu wanaotumia muda mwingi kwenye mitandao ya kijamii wanaweza kuhisi upweke na kushuka moyo. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba mara nyingi watu huweka picha zinazoonyesha mambo ya pekee katika maisha yao, wakionyesha tu picha nzuri-nzuri za maisha yao, rafiki zao, na sehemu zenye kusisimua walizotembelea. Mtu anapotazama picha hizo anaweza kufikia mkataa kwamba maisha yake ni ya kawaida tu, au hata hayasisimui anapoyalinganisha na mambo anayoona kwenye mitandao ya kijamii. Dada mmoja Mkristo mwenye umri wa miaka 19 anakiri hivi: “Nilianza kuhisi kwamba maisha yangu hayaridhishi nilipowaona watu wengine wakifurahia pindi za miisho-juma wakati mimi nikikaa tu nyumbani.”

14. Shauri la Biblia lililo kwenye 1 Petro 3:8 linaweza kutusaidiaje inapohusu matumizi ya mitandao ya kijamii?

14 Bila shaka, mitandao ya kijamii inaweza kutumiwa kwa kusudi zuri, kama vile kuwasiliana na familia na marafiki. Hata hivyo, je, umetambua kwamba baadhi ya watu wanaoweka maelezo au picha kwenye mitandao ya kijamii wanafanya hivyo ili watu wawasifu? Ni kana kwamba wanasema “hebu nitazame.” Wengine hata wanatumia lugha chafu au isiyo na heshima wanapotolea maelezo picha zao wenyewe au za wengine. Jambo hilo ni kinyume kabisa na sifa ya unyenyekevu na hisia-mwenzi ambazo Wakristo wanatiwa moyo wasitawishe.—Soma 1 Petro 3:8.

Unapoweka picha au maelezo mtandaoni, je, mambo hayo yanawapa wengine picha ya kwamba unajivuna au wewe ni mnyenyekevu? (Tazama fungu la 15)

15. Biblia inaweza kutusaidiaje kuepuka roho ya kujitafutia sifa?

15 Ikiwa unatumia mitandao ya kijamii, jiulize hivi: ‘Je, maelezo, picha, au video ninazoweka kwenye mitandao ya kijamii zinawapa wengine picha ya kwamba mimi ninajivuna? Je, nitawafanya wengine waone wivu?’ Biblia inasema hivi: “Kila kitu katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali zake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.” (1 Yoh. 2:16) Tafsiri moja ya Biblia inatafsiri maneno “mtu kujionyesha mali zake maishani” kuwa “majivuno yasababishwayo na mali.” Wakristo hawahisi kwamba wanahitaji kujitafutia sifa. Wanafuata himizo hili la Biblia: “Tusiwe tukijisifu, tusichochee mashindano kati yetu, wala tusioneane wivu.” (Gal. 5:26) Unyenyekevu utatusaidia tusinaswe na roho ya kujitafutia sifa inayoendelezwa na ulimwengu.

‘FIKIRI ILI UWE NA AKILI TIMAMU’

16. Kwa nini tunapaswa kuepuka majivuno?

16 Tunahitaji kusitawisha sifa ya unyenyekevu kwa sababu wale wanaojivuna hawana “akili timamu.” (Rom. 12:3) Watu wenye majivuno hupenda kubishana na kujisifu. Mara nyingi mawazo na matendo yao husababisha wajiumize wao wenyewe na pia wengine. Ikiwa hawatabadili njia yao ya kufikiri, akili zao zitapofushwa na kupotoshwa na Shetani. (2 Kor. 4:4; 11:3) Kwa upande mwingine, mtu mnyenyekevu ana akili timamu. Ana mtazamo wenye usawaziko kujihusu, akitambua kwamba wengine ni bora kuliko yeye katika njia nyingi. (Flp. 2:3) Na anajua kwamba “Mungu huwapinga wenye majivuno, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili zisizostahiliwa.” (1 Pet. 5:5) Watu walio na utimamu wa akili hawangependa Yehova awe adui yao.

17. Ni lazima tufanye nini ili tuendelee kuwa wanyenyekevu?

17 Ili tuendelee kuwa wanyenyekevu, ni lazima tufuate shauri la Biblia la ‘kuuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na kujivika utu mpya.’ Jitihada kubwa inahitajika ili kufanya hivyo. Tunahitaji kujifunza mfano wa Yesu na kujitahidi kumwiga kwa ukaribu kadiri iwezekanavyo. (Kol. 3:9, 10; 1 Pet. 2:21) Lakini jitihada hizo si za bure. Tunapoendelea kusitawisha unyenyekevu, maisha yetu ya familia yatakuwa bora zaidi, tutaendeleza umoja katika kutaniko, na tutajua jinsi tunavyoweza kuepuka kutumia mitandao ya kijamii kwa njia isiyofaa. Zaidi ya yote, tutapata baraka na kibali cha Yehova.

WIMBO 117 Sifa ya Wema

^ fu. 5 Leo, tunaishi katika ulimwengu uliojaa watu wabinafsi na wenye kiburi. Tunahitaji kuwa waangalifu ili tusiathiriwe na mtazamo wao. Makala hii itazungumzia maeneo matatu ambayo hatupaswi kujifikiria wenyewe kuliko ilivyo lazima.

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Mtu mwenye kiburi hujifikiria mwenyewe zaidi kuliko anavyowafikiria wengine. Kwa hiyo, mtu mwenye kiburi ni mbinafsi. Kwa upande mwingine, sifa ya unyenyekevu humsaidia mtu asiwe mbinafsi. Unyenyekevu ni kuwa huru kutokana na kiburi au majivuno, kuwa na unyenyekevu wa akili.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Mzee wa kutaniko ambaye ni msemaji mzuri kusanyikoni na mwenye uwezo wa kuwasimamia vizuri akina ndugu, anathamini pia pendeleo la kuwa mstari wa mbele katika huduma na kufanya usafi wa Jumba la Ufalme.