Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 27

Usijifikirie Mwenyewe Sana Kuliko Vile Inaomba Kufikiri

Usijifikirie Mwenyewe Sana Kuliko Vile Inaomba Kufikiri

“Ninaambia kila mutu pale kati yenu asijifikirie yeye mwenyewe sana kuliko vile inaomba kufikiri, lakini afikiri ili akuwe na akili ya muzuri.”​—RO. 12:3.

WIMBO 130 Uwe Mwenye Kusamehe

KIFUPI CHA HABARI *

1. Kulingana na Wafilipi 2:3, namna gani unyenyekevu unatusaidia tukuwe na uhusiano muzuri pamoja na wengine?

TUNAMUTII Yehova kwa unyenyekevu, kwa sababu tunaelewa kama sikuzote yeye anajua mambo yenye inaweza kutuletea faida. (Efe. 4:22-24) Unyenyekevu unatuchochea kutia mapenzi ya Yehova pa nafasi ya kwanza kuliko mambo yenye tunapenda, na unatuchochea pia kuona wengine kuwa wazuri zaidi kuliko sisi. Ile inafanya tukuwe na uhusiano wa muzuri pamoja na Yehova na ndugu na dada zetu.​—Soma Wafilipi 2:3.

2. Mutume Paulo alijua nini, na tutazungumuzia nini katika habari hii?

2 Lakini kama hatuko waangalifu, tunaweza kuchochewa na watu wa ulimwengu wa Shetani wenye wako na majivuno na wenye kujipenda wenyewe. * Inawezekana Wakristo fulani wa karne ya kwanza (1-100) kisha kuzaliwa kwa Yesu, walikuwa katika hatari hiyo; njo maana mutume Paulo aliandikia Waroma hivi: “Ninaambia kila mutu pale kati yenu asijifikirie yeye mwenyewe sana kuliko vile inaomba kufikiri, lakini afikiri ili akuwe na akili ya muzuri.” (Ro. 12:3) Paulo alijua kama kila mutu anapaswa kujifikiria kwa kiasi fulani. Lakini, unyenyekevu utatusaidia tukuwe na maoni yenye usawaziko juu yetu wenyewe. Mu habari hii tutaona namna unyenyekevu utatusaidia kuepuka kujifikiria sana sisi wenyewe katika mambo tatu. Ile mambo ni (1) ndoa yetu, (2) mapendeleo yetu ya utumishi, na (3) namna tunatumia site za Enternete za kupashana habari.

ONYESHA UNYENYEKEVU KATIKA NDOA YAKO

3. Juu ya nini wenye kuoana wanaweza kukosa kuelewana, na bibi na bwana fulani wanatenda namna gani wakati ile hali inatokea?

3 Yehova alianzisha ndoa juu iletee bibi na bwana furaha. Lakini kwa sababu hawakamilike wanaweza kukosa kuelewana juu ya mambo fulani. Kwa kweli, Paulo aliandika kama wale wenye wanaoa ao kuolewa watakuwa na taabu fulani. (1 Ko. 7:28) Bibi na bwana fulani wanabishana kila mara, na wanaweza kuwaza kama hawangepaswa kuoana. Kama wamechochewa na ulimwengu, watawaza haraka kama wanapaswa kuvunja ndoa yao. Wanaweza kujifikiria tu wao wenyewe na wanaweza kuwaza kama watakuwa na furaha ikiwa tu wanavunja ndoa yao.

4. Tunapaswa kuepuka jambo gani?

4 Tunapaswa kuepuka kuwaza kama ndoa yetu imeshindwa. Tunajua kama kulingana na Biblia, sababu moja tu yenye inaweza kufanya ndoa ivunjike ni uasherati. (Mt. 5:32) Kwa hiyo, wakati taabu yenye mutume Paulo alizungumuzia inatufikia, hatutaacha majivuno itufanye tuanze kujiuliza: ‘Hii ndoa iko inatimiza mahitaji yangu? Niko ninapendwa kabisa? Sitakuwa na furaha kabisa kama ninaoana na mutu mwingine?’ Kama tunawaza vile, tunajifikiria tu sisi wenyewe kuliko kufikiria bibi ao bwana yetu. Hekima ya ulimwengu inasema kama unapaswa kufuata moyo wako na kufanya mambo yenye itakufanya ukuwe na furaha, hata kama ile itakuomba uvunje ndoa yako. Hata hivyo, hekima ya Mungu inasema kama unapaswa ‘kuangalia, hapana faida zako wewe mwenyewe tu, lakini pia faida za wengine.’ (Flp. 2:4) Yehova anapenda ulinde ndoa yako, hapana kuivunja. (Mt. 19:6) Yehova anapenda umufikirie yeye kwanza kuliko kujifikiria wewe mwenyewe.

5. Kulingana na Waefeso 5:33, bibi na bwana wanapaswa kutendeana namna gani?

5 Bibi na bwana wanapaswa kutendeana kwa upendo na heshima. (Soma Waefeso 5:33.) Biblia inatufundisha tukaze akili juu ya kutoa kuliko kupokea. (Mdo. 20:35) Ni sifa gani itasaidia bibi na bwana waonyeshane upendo na heshima? Ni sifa ya unyenyekevu. Bibi ao bwana munyenyekevu hatatafuta faida yake mwenyewe tu, lakini atatafuta pia “faida ya ule mutu mwingine.”​—1 Ko. 10:24.

Kuliko kushambuliana, bibi na bwana wanyenyekevu wanatumika pamoja kwa umoja (Ona fungu la 6)

6. Maelezo ya Steven na Stephanie inakufundisha nini?

6 Unyenyekevu umesaidia bibi na bwana wengi Wakristo wapate furaha kubwa katika ndoa yao. Kwa mufano, bwana mumoja mwenye kuitwa Steven anasema hivi: “Kama muko na umoja, mutaungana mukono, zaidi sana wakati kuko magumu. Kuliko kufikiria jambo lenye kuwa la muzuri zaidi kwako utafikiria jambo lenye kuwa la muzuri zaidi kwenu.” Stephanie iko pia na mawazo kama ya bwana yake Steven. Anasema hivi: “Hakuna mwenye anapendaka kuishi pamoja na mutu mwenye kupenda mabishano. Wakati hatuelewane tunatafuta kujua tatizo ni nini. Kisha tunasali, tunatafuta kanuni za Biblia zenye zinaweza kutusaidia, na tunazungumuzia namna ya kumaliza tatizo letu. Hatushambuliane, lakini tunashambulia njo tatizo.” Wakati bibi na bwana hawajifikirie wao wenyewe kuliko vile inaomba kufikiri, wanapata faida kabisa.

UMUTUMIKIE YEHOVA KWA “UNYENYEKEVU WOTE”

7. Ndugu mwenye anapata pendeleo fulani la utumishi anapaswa kufanya nini?

7 Ni pendeleo kumutumikia Yehova katika njia mbalimbali. (Zb. 27:4; 84:10) Ni jambo la muzuri sana ikiwa ndugu anapenda kufanya mingi katika kazi ya Yehova. Kwa kweli, Biblia inasema: “Kama mwanaume anajikaza ili akuwe mwangalizi, anatamani kazi ya muzuri.” (1 Ti. 3:1) Lakini, wakati ndugu anapata pendeleo fulani la utumishi, anapaswa kuepuka kujifikiria yeye mwenyewe sana kuliko vile inaomba kufikiri. (Lu. 17:7-10) Kusudi lake linapaswa kuwa kutumikia wengine kwa unyenyekevu.​—2 Ko. 12:15.

8. Mifano ya Diotrefe, Uzia, na Absalomu inatufundisha nini?

8 Biblia iko na mifano yenye kuonya ya watu wenye walijifikiria sana wao wenyewe. Diotrefe alionyesha kama hakukuwa mwenye kiasi, kwa sababu alitafuta “kuwa wa kwanza” katika kutaniko. (3 Yo. 9) Kwa kiburi, Uzia alijaribu kutimiza mugao fulani wenye hakupewa na Yehova. (2 Ny. 26:16-21) Absalomu alitumia ujanja fulani ili kufanya watu wamuunge mukono kwa sababu alipenda kuwa mufalme. (2 Sa. 15:2-6) Kama vile habari hizo zinaonyesha, Yehova anachukia watu wenye kujitafutia utukufu. (Mez. 25:27) Kiburi na kupenda kusifiwa vinaletaka matatizo.​—Mez. 16:18.

9. Yesu alituachia mufano gani?

9 Yesu hakukuwa kama wale watu wenye majivuno wenye tumetoka kuzungumuzia. Biblia inasema kama “hata kama alikuwa katika umbo ya Mungu, hakufikiria kuchukua nafasi ya Mungu, ni kusema, kwamba yeye akuwe sawa na Mungu.” (Flp. 2:6) Hata kama Yesu njo mutu wa pili mwenye mamlaka kisha Yehova, hakujifikiria yeye mwenyewe sana kuliko vile inaomba kufikiri. Aliambia wanafunzi wake hivi: “Mwenye anajiendesha kama mudogo zaidi katikati yenu ninyi wote ndiye mukubwa.” (Lu. 9:48) Ni baraka kabisa kutumika pamoja na mapainia, watumishi wa huduma, wazee, na waangalizi wa muzunguko, wenye wanamuiga Yesu kwa kuonyesha sifa ya unyenyekevu. Kama tuko wanyenyekevu, tutaonyesha wengine upendo mwingi. Na Yesu alisema kama ile njo sifa yenye ingetambulisha Wakristo wa kweli.​—Yoh. 13:35.

10. Unapaswa kufanya nini ikiwa unaona kama matatizo fulani haihangaikiwe muzuri katika kutaniko?

10 Utafanya nini ikiwa inaonekana kama kuko matatizo fulani katika kutaniko na unaona kama wazee hawaihangaikie muzuri? Kuliko kunungunika, unaweza kuonyesha unyenyekevu kwa kutegemeza wale wenye kuongoza. (Ebr. 13:17) Ili kufanya vile, unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ile matatizo iko nguvu sana hivi kwamba inaomba irekebishwe? Huu njo wakati muzuri wa kuirekebisha? Ni daraka langu kuirekebisha? Kusema kweli, napenda kuendeleza umoja ao napenda tu kuonekana kuwa wa maana?’

Wale wenye kuwa na madaraka hawapaswe kujulikana tu kwa sababu ya uwezo wao lakini pia kwa sababu ya unyenyekevu wao (Ona fungu la 11) *

11. Kulingana na Waefeso 4:2, 3, tutapata matokeo gani kama tunamutumikia Yehova kwa unyenyekevu?

11 Yehova anaona unyenyekevu kuwa wa maana zaidi kuliko uwezo, na anaona umoja kuwa wa maana zaidi kuliko uwezo wa kutimiza muzuri jambo fulani. Kwa hiyo, fanya yako yote ili kumutumikia Yehova kwa unyenyekevu. Ukifanya vile, utaendeleza umoja katika kutaniko. (Soma Waefeso 4:2, 3.) Fanya kazi ya kuhubiri kwa bidii. Tafuta njia za kusaidia wengine kwa kuwafanyia mambo ya muzuri. Ukuwe mukarimu kwa watu wote, kutia ndani wale wenye hawana madaraka katika kutaniko. (Mt. 6:1-4; Lu. 14:12-14) Ukitumika kwa unyenyekevu pamoja na ndugu na dada zako, hawataona tu uwezo wako, lakini wataona pia unyenyekevu wako.

ONYESHA UNYENYEKEVU WAKATI UNATUMIA SITE ZA ENTERNETE ZA KUPASHANA HABARI

12. Je, Biblia inatutia moyo tukuwe na marafiki? Fasiria.

12 Yehova anapenda tufurahie kupitisha wakati pamoja na marafiki na watu wa familia zetu. (Zb. 133:1) Yesu alikuwa na marafiki wazuri. (Yoh. 15:15) Biblia inaonyesha faida za kuwa na marafiki wa kweli. (Mez. 17:17; 18:24) Na inatuonyesha kama haiko muzuri kujitenga na wengine. (Mez. 18:1) Watu wengi wanawaza kama site za Enternete za kupashana habari zinawasaidia kuwa na marafiki wengi na kuepuka kujisikia kuwa peke yao. Lakini, tunapaswa kuwa waangalifu juu ya namna tunatumia site za Enternete za kupashana habari.

13. Juu ya nini watu fulani wenye wanatumia site za Enternete za kupashana habari wanaweza kujisikia kuwa peke yao na wenye kushuka moyo?

13 Uchunguzi fulani unaonyesha kama watu wenye wanapitisha wakati mingi ili kuangalia picha na maelezo yenye watu wametia ku site za Enternete za kupashana habari, wanaweza kujisikia kuwa peke yao na wenye kushuka moyo. Juu ya nini? Pengine ni juu, mara mingi watu wanatia ku Enternete picha zenye kuonyesha matukio fulani ya maana sana katika maisha yao, picha zao za muzuri zaidi, za marafiki wao, na pia picha za fasi za muzuri kwenye walikuwa. Mutu mwenye kuangalia zile picha anaweza kufikia kusema kama maisha yake ni ya kawaida tu, ao hata haiko ya maana kwa kujilinganisha na wengine. Dada mumoja Mukristo wa miaka 19 anasema hivi: “Sikukuwa ninafurahi wakati niliona wengine wanapitisha wakati wa muzuri ku mwisho wa juma, lakini mimi niko tu ku nyumba na sina la kufanya.”

14. Namna gani shauri la Biblia lenye kuwa katika 1 Petro 3:8 linatusaidia wakati tunatumia site za Enternete za kupashana habari?

14 Kwa kweli, site za Enternete za kupashana habari zinaweza kutumiwa kwa njia ya muzuri. Kwa mufano, tunaweza kuzitumia ili kuzungumuza na watu wa familia na marafiki. Lakini, umekwisha kuona kama watu fulani wanatia picha ao video ku site za Enternete za kupashana habari juu tu ya kujionyesha? Ni kama vile wako wanasema hivi: “Muniangalie.” Wengine wanafikia hata kutia maelezo machafu na yenye kukosa adabu ku picha zao ao ku picha zenye wengine wanatia ku Enternete. Kufanya vile pia, ni tofauti kabisa na vile Wakristo wanapaswa kuwa. Wakristo wanapaswa kuonyesha unyenyekevu na kujitia pa nafasi ya wengine.​—Soma 1 Petro 3:8.

Mambo yenye unatia ku Enternete, inafanya wengine wawaze kama uko na majivuno ao uko munyenyekevu? (Ona fungu la 15)

15. Namna gani Biblia inaweza kutusaidia tuepuke kujiona kuwa wa maana zaidi kuliko wengine?

15 Kama unatumia site fulani ya Enternete ya kupashana habari, ujiulize hivi: ‘Maelezo, picha ao video zenye ninatia ku Enternete zinafanya wengine wawaze kama niko na majivuno? Ninafanya wengine wakuwe na wivu?’ Biblia inasema hivi: “Kila kitu chenye kuwa katika ulimwengu​—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mutu kujionyesha mali yake katika maisha—​hakitokane na Baba, lakini kinatokana na ulimwengu.” (1 Yo. 2:16) Tafsiri moja ya Biblia inatafsiri maneno “kujionyesha mali yake katika maisha” kuwa “kupenda kuonekana kuwa wa maana.” Wakristo hawapaswe kujiona kuwa wa maana zaidi kuliko wengine. Wanafuata shauri hili la Biblia lenye kusema hivi: “Tusikuwe tunajisifu, tusichochee mashindano kati yetu, tusisikiliane wivu.” (Gal. 5:26) Unyenyekevu utatusaidia tusiangukie mu mutego wa ulimwengu huu, ni kusema, kujiona kuwa wa maana zaidi kuliko wengine.

‘FIKIRI ILI UKUWE NA AKILI YA MUZURI’

16. Juu ya nini tunapaswa kuepuka majivuno?

16 Tunapaswa kuonyesha unyenyekevu, juu wale wenye kuwa na majivuno hawana “akili ya muzuri.” (Ro. 12:3) Watu wenye kiburi wanapenda mashindano na ni wenye kujipenda wenyewe. Mara mingi, mawazo na matendo yao inawaletea wao wenyewe na pia wengine matokeo ya mubaya. Kama hawabadilishe namna yao ya kufikiri, Shetani atapofusha na kuharibu akili yao. (2 Ko. 4:4; 11:3) Lakini, mutu munyenyekevu, iko na akili ya muzuri. Tena, iko na mawazo yenye kufaa na yenye kusawazika juu yake mwenyewe, na kila mara anaona wengine kuwa wazuri zaidi kuliko yeye. (Flp. 2:3) Pia, anajua kama “Mungu anawapinga wenye majivuno, lakini anawapatia wanyenyekevu fazili zenye hazistahiliwe.” (1 Pe. 5:5) Wale wenye kuwa na akili ya muzuri hawapendi Yehova akuwe adui yao.

17. Tunapaswa kufanya nini ili tuendelee kuwa wanyenyekevu?

17 Ili tuendelee kuwa wanyenyekevu, tunapaswa kutumikisha shauri la Biblia la ‘kuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na kuvaa [sisi wenyewe] utu mupya.’ Inaomba kujikaza sana ili kufanya vile. Tunapaswa kujifunza mufano wa Yesu na kujikaza kumuiga kwa ukaribu. (Kol. 3:9, 10; 1 Pe. 2:21) Tukifanya vile, tutapata faida kubwa. Wakati tunaonyesha unyenyekevu, familia yetu itakuwa na furaha, tutaendeleza umoja mu kutaniko, na tutajua namna ya kuepuka kutumia mubaya site za Enternete za kupashana habari. Na zaidi ya yote, Yehova atatubariki na kutukubali.

WIMBO 117 Sifa ya Wema

^ fu. 5 Leo, tunaishi katika ulimwengu wenye kujaa watu wenye majivuno na wenye kujipenda wenyewe. Tunapaswa kuwa waangalifu ili tusiige tabia hizo. Katika habari hii tutazungumuzia mambo tatu ambamo tunapaswa kuepuka kujifikiria sisi wenyewe kuliko vile inaomba kufikiri.

^ fu. 2 MAFASIRIO YA MANENO FULANI: Mutu mwenye majivuno anajifikiriaka yeye mwenyewe sana kuliko kufikiria wengine. Kwa hiyo, mutu mwenye majivuno ni mwenye kujipenda mwenyewe. Lakini, unyenyekevu unasaidia mutu asikuwe mwenye kujipenda mwenyewe. Unyenyekevu unamaanisha kukosa kuwa na kiburi ao majivuno, na kuepuka kuwaza kama tuko wa maana sana kuliko wengine.

^ fu. 56 MAFASIRIO YA PICHA: Muzee mumoja mwenye kuwa na uwezo wa kutoa hotuba ku mukusanyiko wa eneo na kusimamia ndugu na dada, anafurahia pia pendeleo la kuongoza mukutano kwa ajili ya mahubiri na kazi ya kusafisha Jumba la Ufalme.