Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

HABARI YA KUJIFUNZA YA 28

Ukuwe Hakika Kama Mambo Yenye Unaamini Ni ya Kweli

Ukuwe Hakika Kama Mambo Yenye Unaamini Ni ya Kweli

“Endelea kufuata mambo yenye ulijifunza na yenye ulisadikishwa kuamini.”​—2 TI. 3:14.

WIMBO 56 Fanya Kweli Iwe Njia Yako ya Maisha

KIFUPI CHA HABARI *

1. Neno “kweli” maana yake nini?

“ULIJUA kweli namna gani?” “Ulikomalia katika kweli?” “Umefanya miaka ngapi katika kweli?” Pengine wamekwisha kukuuliza ile maulizo ao pengine umeuliza wengine ile maulizo. Neno “kweli” maana yake nini? Kwa kawaida, tunatumia ile neno ili kuzungumuzia mambo yenye tunaamini, namna yetu ya kuabudu, na namna yetu ya kuishi. Watu wenye kuwa “katika kweli” wanajua mambo yenye Biblia inafundisha, na wanaishi kupatana na kanuni zake. Kwa hiyo, wamekuwa huru kutokana na uongo wa dini na wanafurahia maisha ya muzuri zaidi kwa kadiri inawezekana katika ulimwengu huu wa Shetani.​—Yoh. 8:32.

2. Kulingana na Yohana 13:34, 35, ni jambo gani la kwanza lenye linaweza kuvutia mutu katika kweli?

2 Ni jambo gani lilikuvutia katika kweli kwa mara ya kwanza? Pengine mwenendo muzuri wa watu wa Yehova njo wenye ulikuvutia. (1 Pe. 2:12) Ao pengine ni upendo wenye walionyesha. Wengi waliona upendo huo kwenye mukutano wenye walihuzuria kwa mara ya kwanza, na wanaendelea kukumbuka upendo huo kuliko mambo ingine yote yenye ilizungumuziwa kwenye mukutano siku hiyo. Jambo hilo halitushangaze kwa sababu Yesu alisema kama upendo wenye wanafunzi wake wako nao kati yao njo ungewatambulisha kuwa wanafunzi wake. (Soma Yohana 13:34, 35.) Lakini tunapaswa kufanya mambo mingi zaidi kama tunapenda kuwa na imani yenye nguvu.

3. Ni jambo gani linaweza kutokea kama imani yetu kwa Mungu inategemea tu upendo wa Kikristo wenye ndugu na dada wanaonyesha?

3 Imani yetu haipaswe kutegemea tu upendo wa Kikristo wenye watu wa Mungu wanaonyesha. Sababu gani? Wazia kama mwamini mwenzako, ao hata muzee ao painia, anafanya zambi nzito. Ao pengine ndugu ao dada fulani anakukwaza katika njia fulani. Ao tena pengine mutu fulani anakuwa muasi-imani na anasema kama mambo yenye tunaamini haiko ya kweli. Ikiwa mambo kama ile inatokea, utakwazika na kuacha kumutumikia Yehova? Jambo lenye tunajifunza hapa ni hili: Imani yako kwa Mungu haitakuwa nguvu kama inategemea namna watu wengine wanatenda kuliko kutegemea urafiki wako pamoja na Yehova. Kuwa na mawazo ya muzuri kuhusu Yehova na watu wake kunaweza kutia nguvu imani yako kwa kiasi fulani. Lakini ni jambo la lazima kujifunza sana Biblia, kuelewa muzuri mambo yenye unajifunza, na kutafuta habari mbalimbali zenye zitakusaidia kuwa hakika kama mambo yenye unajifunza kuhusu Yehova ni ya kweli kabisa. Unapaswa kujihakikishia wewe mwenyewe kama Biblia iko na mafundisho ya kweli juu ya Yehova.​—Ro. 12:2.

4. Kulingana na Matayo 13:3-6, 20, 21, watu fulani wanafanya nini wakati magumu inatokea?

4 Yesu alisema kama watu fulani wangekubali kweli “kwa furaha,” lakini imani yao ingekuwa zaifu wakati magumu inatokea. (Soma Matayo 13:3-6, 20, 21.) Pengine hawakutambua kama kumufuata Yesu kungewaletea pia magumu na matatizo. (Mt. 16:24) Ao pengine waliwaza kama kuwa Mukristo kutawafanya waishi maisha ya raha, ni kusema, maisha yenye kuwa na baraka tu, bila magumu. Lakini katika ulimwengu huu wa Shetani, tunapaswa kujua kama magumu haikosake. Hali zinaweza kubadilika, na kufanya furaha yetu ipunguke kwa wakati fulani.​—Zb. 6:6; Muh. 9:11.

5. Namna gani ndugu na dada wengi wanaonyesha kama wako hakika kuwa mambo yenye wanaamini ni ya kweli?

5 Ndugu na dada wengi wanaonyesha kama wako hakika kuwa mambo yenye wanaamini ni ya kweli. Namna gani? Imani yao haitikisike hata wakati Mukristo mwenzao anawakwaza ao anajiingiza katika mwenendo wenye hauko wa Kikristo. (Zb. 119:165) Kila mara wakati wanapata magumu, kuliko imani yao ikuwe zaifu, inakuwa nguvu zaidi. (Yak. 1:2-4) Namna gani tunaweza kukomalisha imani ya vile?

PATA “UJUZI WENYE HAUNA MAKOSA WA MUNGU”

6. Imani ya Wakristo wa karne ya kwanza ilitegemea nini?

6 Imani ya Wakristo wa karne ya kwanza (1-100) ilitegemea ujuzi wa Maandiko na mafundisho ya Yesu Kristo yenye walikuwa nayo, ni kusema, “kweli ya habari njema.” (Gal. 2:5) Kweli hiyo ni mafundisho yote yenye sisi Wakristo tunaamini, inatia ndani mafundisho juu ya bei ya ukombozi ya Yesu na ufufuo wake. Mutume Paulo alikuwa hakika kama ile mafundisho yote ilikuwa kweli. Juu ya nini tunasema vile? Juu alitumia Maandiko wakati alikuwa anafundisha watu. Alikuwa anawahakikishia “kwa kutumia mambo yenye kuandikwa kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na afufuliwe kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:2, 3) Wanafunzi wa karne ya kwanza waliamini ile mafundisho na walitegemea roho takatifu ili iwasaidie kuelewa Neno la Mungu. Walijihakikishia wao wenyewe kama ile mafundisho ilitegemea Maandiko. (Mdo. 17:11, 12; Ebr. 5:14) Imani yao haikutegemea tu mawazo yao na namna walijisikia, na hawakumutumikia Yehova juu tu walijisikia muzuri wakati walikuwa wanakutana na waamini wenzao. Lakini, imani yao ilitegemea “ujuzi wenye hauna makosa wa Mungu.”​—Kol. 1:9, 10.

7. Imani yetu katika kweli za Biblia itatusaidia namna gani?

7 Kweli za Neno la Mungu hazibadilike. (Zb. 119:160) Kwa mufano, hazibadilike kama Mukristo mwenzetu anatukwaza ao wakati anafanya zambi nzito. Na hazibadilike wakati tunapata magumu. Kwa hiyo, tunapaswa kujua muzuri sana mafundisho ya Biblia na kuwa hakika kama ni ya kweli. Imani yetu yenye kuwa nguvu na yenye kutegemea kweli za Biblia inatusaidia tusimame imara wakati tunajaribiwa, kama vile tu nanga inasaidia mashua ibakie imara wakati wa upepo mukali. Namna gani unaweza kutia nguvu imani yako kama mambo yenye unaamini ni ya kweli?

UJIHAKIKISHIE MAMBO YENYE UNAAMINI

8. Kama vile 2 Timoteo 3:14, 15 inaonyesha, namna gani Timoteo alifikia kuwa hakika kama mambo yenye aliamini ilikuwa ya kweli?

Timoteo alikuwa hakika kama mambo yenye aliamini ilikuwa ya kweli. Ni nini ilimusaidia aamini vile? (Soma 2 Timoteo 3:14, 15.) Mama yake na tate (nkambo) yake walikuwa wa kwanza kumufundisha “maandishi matakatifu.” Lakini, bila shaka yeye mwenyewe pia alijifunza kwa bidii ile maandishi. Kwa hiyo, ‘alisadikishwa kuamini’ kama ile maandishi ilikuwa ya kweli. Kisha, Timoteo, mama yake, na tate yake walijifunza mafundisho ya Kikristo. Kwa kweli, Timoteo alivutiwa na upendo wenye wafuasi wa Yesu walionyesha, na alifurahia sana kupitisha wakati pamoja na ndugu na dada katika kutaniko na kuwasaidia. (Flp. 2:19, 20) Hata hivyo, imani yake haikutegemea upendo wenye alikuwa nao juu ya watu, lakini ilitegemea mafundisho ya kweli yenye ilimusaidia amukaribie Yehova. Wewe pia unapaswa kujifunza Biblia na kujihakikishia kama mambo yenye Biblia inafundisha kumuhusu Yehova ni ya kweli.

9. Ni kweli gani tatu za maana zenye unapaswa kujihakikishia?

9 Ili kufanya vile, unapaswa kwanza kujihakikishia kweli tatu za musingi. Kwanza, ni lazima ukuwe hakika kama Yehova Mungu ni Muumbaji wa kila kitu. (Kut. 3:14, 15; Ebr. 3:4; Ufu. 4:11) Pili, unapaswa kujihakikishia kama Biblia ni ujumbe wa Mungu kwa wanadamu wenye uliongozwa na roho yake. (2 Ti. 3:16, 17) Na tatu, ni lazima ukuwe hakika kama Yehova iko na kikundi cha watu wenye kupangwa muzuri wenye kumuabudu chini ya uongozi wa Kristo, na kama Mashahidi wa Yehova njo kile kikundi. (Isa. 43:10-12; Yoh. 14:6; Mdo. 15:14) Ili kujihakikishia kweli hizo haiombe ujue mambo yote juu ya Biblia. Kusudi lako linapaswa kuwa kutumikisha “nguvu [zako] za kufikiri” ili kutia nguvu imani yako kama mambo yenye unaamini ni ya kweli.​—Ro. 12:1.

UJITAYARISHE ILI KUSAIDIA WENGINE WAKUWE HAKIKA NA MAMBO YENYE WANAAMINI

10. Zaidi ya kujua kweli, tunapaswa kuwa na uwezo wa kufanya nini?

10 Kisha kujihakikishia zile kweli tatu za musingi kuhusu Mungu, Biblia, na watu wa Mungu, unapaswa kuwa na uwezo wa kutumia Maandiko ili kuhakikishia wengine zile kweli. Sababu gani? Sababu sisi Wakristo tuko na daraka la kufundisha kweli zenye tunajifunza kwa wale wenye watatusikiliza. * (1 Ti. 4:16) Na wakati tunajikaza kuhakikishia wengine kweli za Biblia, tunatia nguvu imani yetu katika kweli hizo.

11. Mutume Paulo alituwekea mufano gani katika kazi ya kufundisha?

11 Wakati mutume Paulo alifundisha watu, alikuwa “akiwasadikisha juu ya Yesu kwa kutumia Sheria ya Musa na pia Manabii.” (Mdo. 28:23) Namna gani tunaweza kumuiga Paulo wakati tunafundisha watu kweli? Zaidi ya kuambia wanafunzi wetu wa Biblia mambo yenye Biblia inafundisha, kuko jambo lingine lenye tunapaswa kufanya. Tunapaswa kuwasaidia wafikiri juu ya Maandiko ili wamukaribie Yehova. Tunapenda wakubali kweli, haiko juu wanatufurahia, lakini juu wamejihakikishia wao wenyewe kama mambo yenye wako wanajifunza juu ya Mungu ni ya kweli.

Wazazi, musaidie watoto wenu watie nguvu imani yao kwa kuwafundisha “mambo mazito ya Mungu” (Ona fungu la 12-13) *

12-13. Namna gani wazazi wanaweza kusaidia watoto wao waendelee kubakia katika kweli?

12 Wazazi, bila shaka munapenda watoto wenu waendelee kubakia katika kweli. Munaweza kuwaza kama ikiwa wako na marafiki wazuri katika kutaniko, watafanya maendeleo ya kiroho. Lakini, ili watoto wenu wakuwe hakika kama mambo yenye wanaamini ni ya kweli, ni lazima wafanye jambo fulani la maana kuliko tu kuwa na marafiki wazuri. Wanapaswa kuwa na urafiki wa kipekee pamoja na Mungu na kuwa hakika kama mambo yenye Biblia inafundisha ni ya kweli.

13 Wazazi hawawezi kufundisha muzuri watoto wao kweli juu ya Mungu, kama wao wenyewe hawako mufano muzuri kuhusu kujifunza Biblia. Wanapaswa kufikiri sana juu ya mambo yenye wanajifunza. Wakifanya vile, watoto wao pia wanaweza kuwaiga. Wazazi wanapaswa kufundisha watoto wao namna ya kutumia vifaa vya kusaidia kujifunza Biblia, kama vile tu wanafundishaka wanafunzi wao wa Biblia. Kwa kufanya vile, watasaidia watoto wao wamupende Yehova na wakuwe hakika kama Yehova anatumia “mutumwa muaminifu na mwenye busara” ili kututolea chakula cha kiroho. (Mt. 24:45-47) Wazazi, zaidi ya kufundisha watoto wenu mafundisho ya musingi ya Biblia, munapaswa pia kufanya jambo lingine. Muwasaidie wakuwe na imani yenye nguvu kwa kuwafundisha “mambo mazito ya Mungu” yenye wanaweza kuelewa kulingana na uwezo na miaka yao.​—1 Ko. 2:10.

UJIFUNZE UNABII WA BIBLIA

14. Juu ya nini tunapaswa kujifunza unabii wa Biblia? (Ona pia kisanduku “ Unaweza Kufasiria Unabii Huu?”)

14 Unabii wa Biblia ni sehemu ya maana ya neno la Mungu yenye inatusaidia tutie nguvu imani yetu kwa Yehova. Ni unabii gani ulitia nguvu imani yako? Pengine unaweza kutaja unabii kuhusu “siku za mwisho.” (2 Ti. 3:1-5; Mt. 24:3, 7) Lakini ni unabii gani mwingine wenye umetimia wenye umetia nguvu imani yako? Kwa mufano, unaweza kufasiria unabii wenye kuwa katika Danieli sura ya 2 ao Danieli sura ya 11 na kuonyesha namna umetimia, na namna gani unaendelea kutimia? * Imani yako itaendelea kuwa yenye nguvu sana kama inategemea Biblia. Fikiria mufano wa ndugu zetu wa Ujerumani wenye walipata mateso ya nguvu wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Hata kama hawakuelewa kabisa unabii wa Biblia wenye unahusu siku za mwisho, walikuwa na imani yenye nguvu katika Neno la Mungu.

Kujifunza Biblia na pia unabii wa Biblia, kunaweza kutusaidia kubakia waaminifu kwa Yehova wakati wa magumu (Ona fungu la 15-17) *

15-17. Namna gani kujifunza Biblia kulisaidia ndugu zetu wenye waliteswa na Wanazi?

15 Chini ya utawala wa serikali ya Nazi katika Ujerumani, maelfu ya ndugu na dada zetu walipelekwa katika kambi za mateso. Hitler na Heinrich Himmler, ofisa mumoja mwenye kujulikana sana, walichukia sana Mashahidi wa Yehova. Dada mumoja alisema kama Himmler aliambiaka hivi kikundi cha dada wenye walikuwa katika kambi moja ya mateso: “Yehova wenu anaweza kutawala mbinguni, lakini hapa ku dunia sisi njo tunatawala! Tutaona kati yetu na ninyi ni nani wataendelea kuishi!” Ni nini ilisaidia watu wa Yehova waendelee kubakia waaminifu?

16 Wale wanafunzi wa Biblia walijua kama Ufalme wa Mungu ulianza kutawala katika mwaka wa 1914. Hawakushangaa wakati walipata mateso. Lakini, walikuwa hakika kama hakuna hata serikali moja ya wanadamu yenye inaweza kuzuia kusudi la Mungu kutimia. Hitler hangeweza kumaliza ibada ya kweli ao kuweka serikali yenye ingekuwa na nguvu zaidi kuliko Ufalme wa Mungu. Ndugu zetu waliamini kama siku moja utawala wa Hitler ungefikia mwisho.

17 Mambo yenye ndugu na dada hao waliamini ilikuwa ya kweli. Kisha miaka fulani, utawala wa Nazi ulianguka, na Heinrich Himmler, ule mwanaume mwenye alisemaka “hapa ku dunia sisi njo tunatawala,” alikuwa anakimbia ili kuokoa uzima wake. Wakati Himmler alikuwa anakimbia, alikutana na Ndugu Lübke, mufungwa wa zamani. Himmler alijua kama Lübke alikuwa Shahidi wa Yehova. Akiwa ameshuka moyo kabisa, Himmler alimuuliza Ndugu Lübke: “Sasa, Mwanafunzi wa Biblia, nini njo inataka kutokea?” Ndugu Lübke alimufasiria Himmler kuwa Mashahidi wa Yehova walijua mbele ya wakati kama utawala wa Nazi ungeshindwa na kama Mashahidi wa Yehova wangekombolewa. Himmler, mwenye alisemaka mambo mingi ya mubaya juu ya Mashahidi wa Yehova, sasa hakujua aseme nini. Wakati kidogo kisha pale akajiua. Ile habari inatufundisha nini? Kujifunza Biblia na pia unabii wa Biblia, kunaweza kutusaidia tukuwe na imani yenye nguvu kwa Mungu na kutusaidia tumutumainie wakati wa majaribu.​—2 Pe. 1:19-21.

18. Kulingana na Yohana 6:67, 68, juu ya nini tuko na lazima ya “ujuzi wenye hauna makosa na utambuzi kamili” wenye Paulo alizungumuzia?

18 Kila mumoja wetu anapaswa kuonyesha upendo wenye unatambulisha Wakristo wa kweli. Lakini, tuko pia na lazima ya “ujuzi wenye hauna makosa na utambuzi kamili.” (Flp. 1:9) Kama hatufanye vile, tunaweza kuchochewa “na kila upepo wa mafundisho kupitia udanganyifu wa watu,” kutia ndani waasi-imani. (Efe. 4:14) Wakati wanafunzi wengi wa karne ya kwanza waliacha kumufuata Yesu, mutume Petro alionyesha kama alikuwa hakika kuwa Yesu alikuwa na “maneno ya uzima wa milele.” (Soma Yohana 6:67, 68.) Hata kama ile wakati Petro hakuelewa kila kitu kuhusu ile maneno, aliendelea kubakia muaminifu kwa sababu alijua kweli juu ya Kristo. Wewe pia unaweza kutia nguvu imani yako katika mambo yenye Biblia inafundisha. Kama unafanya vile, imani yako itaendelea kuwa nguvu hata wakati unapata magumu, na utasaidia wengine wakuwe na imani yenye nguvu.​—2 Yo. 1, 2.

WIMBO 72 Kutangaza Ukweli wa Ufalme

^ fu. 5 Habari hii itatusaidia tupende mafundisho ya kweli ya Neno la Mungu. Itazungumuzia pia namna tunaweza kuwa hakika zaidi kama mambo yenye tunaamini ni ya kweli.

^ fu. 10 Ili kukusaidia ujue namna ya kufikiri na wengine juu ya kweli za musingi za Biblia, ona habari zenye kichwa “Mazungumuzo ya Biblia Pamoja na Jirani,” zenye zilitolewa katika Munara wa Mulinzi kuanzia 2010 mupaka 2015. Kuko habari kama vile “Je, Yesu Ni Mungu?,” “Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Wakati Gani?,” na “Je, Mungu Anawapa Watu Malipizi kwa Kuwaunguza Katika Moto wa Mateso?

^ fu. 14 Maelezo kuhusu unabii huo inapatikana katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 6, 2012, na wa Mwezi wa 5, 2020.

^ fu. 60 MAFASIRIO YA PICHA: Wakati wa ibada ya familia, wazazi wako wanajifunza pamoja na watoto wao unabii wa Biblia kuhusu taabu kubwa.

^ fu. 62 MAFASIRIO YA PICHA: Wakati wa taabu kubwa, familia ileile haitashituka kuona mambo yenye itatokea.