Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu aliwekwa kuwa Kuhani Mkuu lini, na je, kuna tofauti kati ya wakati ambapo agano jipya lilihalalishwa na wakati lilipozinduliwa?

Uthibitisho unaonyesha kwamba Yesu aliwekwa kuwa Kuhani Mkuu alipobatizwa katika mwaka wa 29 W.K. Uthibitisho gani? Wakati wa ubatizo wake, Yesu alijitoa mwenyewe kuwa dhabihu kwenye madhabahu ya “mapenzi” ya Mungu. (Gal. 1:4; Ebr. 10:5-10) Kwa kuwa madhabahu hiyo ya mfano imekuwepo tangu Yesu alipobatizwa na kuendelea, ni lazima hekalu kubwa la kiroho pia lilianza kuwapo kuanzia wakati huo. Hekalu hilo linafananisha mpango wa Yehova wa ibada safi kwa msingi wa dhabihu ya fidia. Madhabahu ni sehemu muhimu ya hekalu hilo la kiroho.—Mt. 3:16, 17; Ebr. 5:4-6.

Hekalu hilo kubwa la kiroho lilihitaji kuhani mkuu wa kuhudumu humo. Ili kutimiza uhitaji huo, Yesu alitiwa mafuta “kwa roho takatifu na nguvu.” (Mdo. 10:37, 38; Marko 1:9-11) Hata hivyo, tunawezaje kuwa na uhakika kwamba Yesu aliwekwa rasmi kuwa Kuhani Mkuu kabla ya kifo na ufufuo wake? Tunapata hoja yenye nguvu tunapochunguza mfano wa Haruni na makuhani waliofuata baada yake ambao walitumikia wakiwa makuhani wakuu chini ya Sheria ya Musa.

Kulingana na Sheria, kuhani mkuu peke yake ndiye angeweza kuingia Patakatifu Zaidi katika hema la ibada, na baadaye, katika Patakatifu zaidi kwenye hekalu. Kulikuwa na pazia lililotenganisha Patakatifu Zaidi na Patakatifu. Siku pekee ambayo kuhani mkuu alivuka pazia na kuingia Patakatifu Zaidi ni katika Siku ya Kufunika Dhambi. (Ebr. 9:1-3, 6, 7) Kama tu ambavyo Haruni na makuhani wakuu baada yake walivyotiwa mafuta kuwa makuhani wakuu kabla ya kuingia “kupitia lile pazia [halisi]” la hema la ibada, lazima Yesu pia aliwekwa rasmi kuwa Kuhani Mkuu wa hekalu kubwa la kiroho la Yehova kabla ya kifo chake, na baada ya hapo aliingia “kupitia lile pazia, yaani, mwili wake” na kwenda mbinguni. (Ebr. 10:20) Ndiyo sababu mtume Paulo aliandika kwamba Yesu alikuja “akiwa kuhani mkuu” na kuingia “katika hema kubwa na kamilifu zaidi ambalo halikutengenezwa kwa mikono,” na kuingia “mbinguni kwenyewe.”—Ebr. 9:11, 24.

Hakuna tofauti kati ya wakati agano jipya lilipohalalishwa na wakati lilipozinduliwa. Kwa nini? Yesu alipoenda mbinguni na kumpa Yehova thamani ya uhai wake mkamilifu wa kibinadamu kwa ajili yetu, alianzisha mpango wenye hatua tatu ambao ulihalalisha kisheria agano jipya. Pia, hatua hizohizo zilizindua agano jipya, au kulifanya lianze kutumika. Ni hatua gani hizo?

Kwanza, Yesu alifika mbele za Yehova; kisha, Yesu alimpa Yehova thamani ya dhabihu yake; na mwishowe, Yehova alikubali thamani ya damu ya Yesu iliyomwagwa. Kabla ya hatua hizo kutekelezwa, agano jipya halikuwa limeanza kutumika.

Biblia haituambii wakati hususa ambao Yehova alikubali thamani ya dhabihu ya Yesu. Hivyo, hatuwezi kutaja wakati hususa ambao agano jipya lilihalalishwa na pia lilipoanza kutumika. Hata hivyo, tunajua kwamba Yesu alienda mbinguni siku kumi kabla ya Pentekoste. (Mdo. 1:3) Wakati fulani, ndani ya kipindi hicho kifupi, Yesu alimpa Yehova thamani ya dhabihu yake, na Yehova aliikubali. (Ebr. 9:12) Uthibitisho wa jambo hilo ulikuwa wazi siku ya Pentekoste. (Mdo. 2:1-4, 32, 33) Ni wazi kwamba wakati huo agano jipya lilikuwa limeanzishwa na kuanza kufanya kazi.

Kwa ufupi, agano jipya lilihalalishwa na kuzinduliwa baada ya Yehova kukubali thamani ya damu ya Yesu iliyomwagwa na kuwaingiza Wakristo watiwa-mafuta katika agano hilo. Kisha agano hilo jipya likaanza kufanya kazi Kuhani Mkuu Yesu, akiwa Mpatanishi wa agano hilo.—Ebr. 7:25; 8:1-3, 6; 9:13-15.