Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 29

“Ninapokuwa Dhaifu, Ndipo Ninapokuwa na Nguvu”

“Ninapokuwa Dhaifu, Ndipo Ninapokuwa na Nguvu”

“Ninapendezwa na udhaifu, na matusi, na nyakati za uhitaji, na mateso na shida, kwa ajili ya Kristo.”—2 KOR. 12:10.

WIMBO 38 Atakupa Nguvu

MUHTASARI *

1. Mtume Paulo alikiri nini waziwazi?

MTUME Paulo alieleza waziwazi kwamba nyakati nyingine alihisi akiwa dhaifu. Alikiri kwamba mwili wake ulikuwa ‘ukichakaa,’ na alihitaji kupambana ili kufanya yaliyo sawa, na kwamba si nyakati zote Yehova alijibu sala zake kwa njia ambayo alitarajia. (2 Kor. 4:16; 12:7-9; Rom. 7:21-23) Pia, Paulo alikiri kwamba wapinzani wake walimwona kuwa dhaifu. * Lakini hakuruhusu mtazamo huo mbaya wa wengine au udhaifu wake mwenyewe umfanye ahisi hana thamani.—2 Kor. 10:10-12, 17, 18.

2. Kulingana na 2 Wakorintho 12:9, 10, mtume Paulo alijifunza somo gani muhimu?

2 Paulo alijifunza somo muhimu sana kwamba mtu anaweza kuwa na nguvu hata anapohisi kwamba yeye ni dhaifu. (Soma 2 Wakorintho 12:9, 10.) Yehova alimwambia Paulo kwamba nguvu Zake “zinakamilika katika udhaifu,” akimaanisha kwamba nguvu za Yehova zingejazia mahali ambapo Paulo alipungukiwa. Kwanza, acheni tuone kwa nini hatupaswi kuhangaika wapinzani wetu wanapotutukana.

‘PENDEZWA NA MATUSI’

3. Kwa nini tunaweza kupendezwa na matusi?

3 Sisi sote hatufurahii kutukanwa. Hata hivyo, ikiwa adui zetu wanatutukana na tunahangaishwa kupita kiasi na mambo wanayosema, tunaweza kuvunjika moyo. (Met. 24:10) Hivyo basi, tunapaswa kuwa na mtazamo gani kuhusu matusi ya wapinzani wetu? Kama Paulo, tunaweza ‘kupendezwa na matusi.’ (2 Kor. 12:10) Kwa nini? Kwa sababu watu wanapotutukana na kutupinga hiyo ni ishara ya kwamba sisi ni wanafunzi wa kweli wa Yesu. (1 Pet. 4:14) Yesu alisema kwamba wafuasi wake wangeteswa. (Yoh. 15:18-20) Jambo hilo lilithibitika kuwa kweli katika karne ya kwanza. Wakati huo, wale waliokuwa wameathiriwa na utamaduni wa Kigiriki waliwaona Wakristo kuwa watu wasio na akili na walio dhaifu. Na miongoni mwa Wayahudi, Wakristo walionwa kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu,” kama hali ilivyokuwa kwa Petro na Yohana. (Mdo. 4:13) Wakristo walionekana kuwa dhaifu; hawakuwa na ushawishi wa kisiasa wala nguvu zozote za kijeshi, na walionwa kuwa watu wasiofaa kitu katika jamii.

4. Wakristo wa mapema waliitikiaje wapinzani waliposema mambo mabaya kuwahusu?

4 Je, Wakristo hao wa mapema waliruhusu mtazamo mbaya wa wapinzani wao uwavunje moyo? Hapana. Kwa mfano, mtume Petro na Yohana waliliona kuwa jambo la heshima kuteswa kwa sababu ya kuwa wafuasi wa Yesu na kuwaambia wengine kuhusu mafundisho yake. (Mdo. 4:18-21; 5:27-29, 40-42) Wanafunzi hao hawakuwa na sababu yoyote ya kuaibika. Mwishowe, Wakristo hao wanyenyekevu wa karne ya kwanza waliwatendea wanadamu mambo mengi mema kuliko yaliyotendwa na wapinzani wao. Kwa mfano, vitabu vilivyoongozwa na roho ya Mungu vilivyoandikwa na baadhi ya Wakristo hao, bado vinaendelea kuwasaidia na kuwapa tumaini mamilioni ya watu. Na Ufalme waliotangaza unatawala sasa mbinguni na hivi karibuni utawatawala wanadamu wote. (Mt. 24:14) Kinyume cha hilo, serikali ya kisiasa yenye nguvu ambayo iliwatesa Wakristo hao ilianguka na kubaki historia, ilhali wanafunzi hao washikamanifu sasa ni wafalme mbinguni. Wapinzani wao wamekufa; na ikiwa watafufuliwa, watakuwa raia wa Ufalme ambao ulitangazwa na Wakristo hao ambao waliwachukia.—Ufu. 5:10.

5. Kulingana na Yohana 15:19, kwa nini watu wa Yehova hudharauliwa?

5 Leo, tukiwa watu wa Yehova, nyakati nyingine tunadharauliwa na kudhihakiwa kwamba sisi ni watu wasio na akili na walio dhaifu. Kwa nini? Kwa sababu hatuungi mkono mitazamo ya watu wanaotuzunguka. Tunajitahidi kuwa wanyenyekevu, wapole, na watiifu. Kwa upande mwingine, ulimwengu huwasifu watu wenye majivuno, wenye kiburi, na wakaidi. Isitoshe, hatujihusishi na siasa, na hatujiungi na majeshi ya vita ya nchi yoyote. Kwa kuwa haturuhusu ulimwengu utufinyange, tunaonekana kuwa watu duni.—Soma Yohana 15:19; Rom. 12:2.

6. Yehova anatimiza nini kupitia watu wake?

6 Licha ya maoni ya ulimwengu kutuhusu, Yehova anatutumia kutimiza mambo makubwa sana. Anatimiza kazi kubwa zaidi ya kuhubiri katika historia ya wanadamu. Leo, watumishi wake hutokeza machapisho yaliyotafsiriwa na kusambazwa kwa wingi duniani na wanatumia Biblia kuwasaidia mamilioni ya watu waboreshe maisha yao. Utukufu wote unamwendea Yehova ambaye amewezesha mambo hayo yote makubwa yatimizwe, na ambaye ametumia kikundi cha watu wanaoonekana kuwa dhaifu kufanya kazi hizo kubwa. Lakini vipi sisi tukiwa mtu mmoja-mmoja? Je, Yehova anaweza kutusaidia tuwe wenye nguvu? Ikiwa ndivyo, basi ni lazima tufanye nini ili atusaidie? Acheni sasa tuchunguze mambo matatu hususa tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa mtume Paulo.

USITEGEMEE NGUVU ZAKO MWENYEWE

7. Tunajifunza somo gani kutokana na mfano wa Paulo?

7 Somo moja tunalojifunza kutokana na mfano wa Paulo ni: Usitegemee nguvu au uwezo wako mwenyewe unapomtumikia Yehova. Kwa maoni ya wanadamu, Paulo alikuwa na sababu ya kujivuna na kujitegemea. Alilelewa huko Tarso, jiji kuu la mkoa wa Roma. Jiji la Tarso lilikuwa tajiri na kituo mashuhuri cha elimu. Paulo alikuwa msomi—alikuwa amefundishwa na Gamalieli, mmoja wa viongozi wa Kiyahudi aliyeheshimika katika siku zake. (Mdo. 5:34; 22:3) Wakati fulani, Paulo alikuwa na ushawishi mkubwa katika jamii ya Kiyahudi. Alisema hivi: “Nilikuwa nikifanya maendeleo makubwa katika dini ya Kiyahudi kuliko watu wengi wa umri wangu katika taifa langu.” (Gal. 1:13, 14; Mdo. 26:4) Lakini Paulo hakujitegemea mwenyewe.

Paulo aliyaona mambo yaliyoonekana kuwa faida katika ulimwengu huu kuwa “takataka nyingi” kwa kulinganisha na pendeleo la kumfuata Kristo (Tazama fungu la 8) *

8. Kulingana na Wafilipi 3:8, Paulo aliyaonaje mambo aliyoacha, na kwa nini ‘alipendezwa na udhaifu’?

8 Kwa hiari, Paulo aliacha mambo yaliyomfanya awe mashuhuri kulingana na viwango vya ulimwengu. Hata aliona mambo hayo yaliyoonekana kuwa yenye faida kuwa “takataka nyingi.” (Soma Wafilipi 3:8.) Paulo alipitia hali nyingi ngumu kwa sababu ya kuwa mfuasi wa Kristo. Alichukiwa na watu wa taifa lake mwenyewe. (Mdo. 23:12-14) Na raia wenzake wa Roma walimpiga na kumfunga gerezani. (Mdo. 16:19-24, 37) Zaidi ya hayo, Paulo alisikitishwa sana na mapungufu yake. (Rom. 7:21-25) Lakini badala ya kuruhusu wapinzani wake au mapungufu yake yamdhoofishe, ‘alipendezwa na udhaifu.’ Kwa nini? Kwa sababu alipokuwa dhaifu ndipo alipoona nguvu za Mungu zikitenda kazi maishani mwake.—2 Kor. 4:7; 12:10.

9. Tunapaswa kuyaonaje mambo ambayo yanaonekana kuwa yenye faida lakini sisi hatuna?

9 Ikiwa tunataka kupata nguvu kutoka kwa Yehova, ni lazima tuepuke kufikiri kwamba nguvu zetu za kimwili, elimu yetu, utamaduni wetu, au utajiri wetu ndio unaoamua thamani yetu. Hayo si mambo yanayomfanya Yehova atutumie. Isitoshe, watu wengi wa Mungu si “wenye hekima kwa njia ya kimwili, si wengi wenye nguvu, si wengi wa kutoka familia mashuhuri.” Licha ya hilo, Yehova amechagua kutumia “vitu dhaifu vya ulimwengu.” (1 Kor. 1:26, 27) Hivyo, usihisi kwamba kwa kuwa huna mambo ambayo watu huyaona kuwa yenye faida, basi hicho ni kikwazo cha kumtumikia Yehova. Badala yake, ione hali yako kuwa fursa ya kujionea nguvu za Yehova zikitenda kazi ndani yako. Kwa mfano, ikiwa unawaogopa wale wanaojaribu kukufanya utilie shaka mambo unayoamini, sali kwa Yehova ili akupe ujasiri wa kutetea imani yako. (Efe. 6:19, 20) Ikiwa unapambana na tatizo kubwa la kiafya na linaloendelea, mwombe Yehova akupe nguvu unazohitaji ili uendelee kutimiza mengi kadiri uwezavyo katika utumishi wake. Kila mara unapojionea msaada wa Yehova, imani yako huzidi kukua, nawe unazidi kuimarika.

JIFUNZE KUTOKANA NA MIFANO YA BIBLIA

10. Kwa nini tunapaswa kujifunza kuhusu mifano iliyowekwa na watumishi waaminifu katika Biblia, kama wale wanaotajwa kwenye Waebrania 11:32-34?

10 Paulo alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Maandiko. Alijifunza Maandiko kwa ukawaida, na alijifunza mambo mengi kutoka kwa watu ambao masimulizi yao yameandikwa katika Neno la Mungu. Alipokuwa akiwaandikia Wakristo Waebrania, Paulo aliwaomba wafikirie kuhusu mifano iliyowekwa na watumishi wengi waaminifu wa Yehova. (Soma Waebrania 11:32-34.) Mfikirie mmoja wa watumishi hao, Mfalme Daudi. Hakulazimika tu kukabiliana na upinzani kutoka kwa adui zake, bali pia kutoka kwa baadhi ya watu ambao wakati fulani walikuwa rafiki zake. Tunapochunguza mfano wa Daudi, tunaweza kuona nguvu ambazo huenda Paulo alipata alipotafakari maisha ya Daudi na jinsi tunavyoweza kumwiga Paulo mwenyewe.

Daudi alipokuwa akikabiliana na vitisho vya Goliathi, aligeuza mambo yaliyoonekana kuwa udhaifu, yawe fursa ya kujionea nguvu za Mungu zikitenda (Tazama fungu la 11)

11. Kwa nini Daudi alionekana kuwa dhaifu? (Tazama picha kwenye jalada.)

11 Machoni pa shujaa mwenye nguvu aliyeitwa Goliathi, Daudi alionekana kuwa mtu dhaifu. Goliathi alipomwona Daudi, alianza “kumdhihaki kwa dharau.” Isitoshe, Goliathi alikuwa na umbo kubwa sana, mwenye silaha bora zaidi, na mwenye uzoefu mwingi zaidi wa kivita. Kwa upande mwingine, Daudi alikuwa mvulana tu asiye na uzoefu, mwenye silaha duni za vita. Lakini Daudi aligeuza mambo yaliyoonekana kuwa udhaifu, yawe yenye nguvu. Alitegemea nguvu za Yehova, naye akamshinda adui yake.—1 Sam. 17:41-45, 50.

12. Daudi alilazimika kukabiliana na changamoto gani nyingine?

12 Daudi alilazimika kukabiliana na changamoto nyingine ambayo ingeweza kumfanya awe dhaifu na asiye na nguvu. Daudi alimtumikia kwa ushikamanifu Sauli, ambaye Yehova alikuwa amemweka rasmi kuwa mfalme wa Israeli. Mwanzoni, Mfalme Sauli alimheshimu Daudi. Lakini baadaye, kiburi kilimfanya Sauli amwonee wivu Daudi. Sauli alimtendea Daudi kwa njia mbaya, hata akajaribu kumuua.—1 Sam. 18:6-9, 29; 19:9-11.

13. Daudi aliitikiaje Mfalme Sauli alipomtendea kwa njia isiyo ya haki?

13 Licha ya Mfalme Sauli kumtendea kwa njia isiyo ya haki, Daudi aliendelea kumheshimu mfalme huyo aliyewekwa rasmi na Yehova. (1 Sam. 24:6) Daudi hakumlaumu Yehova kwa mambo maovu ambayo Sauli alitenda. Badala yake, Daudi alimtegemea Yehova ili ampe nguvu alizohitaji kuvumilia jaribu hilo gumu.—Zab. 18:1, utangulizi.

14. Mtume Paulo alikabili hali gani inayofanana na ya Daudi?

14 Mtume Paulo alikabili hali iliyofanana na ya Daudi. Maadui wa Paulo walikuwa na nguvu nyingi zaidi kuliko zake. Viongozi wengi mashuhuri katika siku zake walimchukia. Mara nyingi, viongozi hao waliagiza apigwe na kutupwa gerezani. Kama Daudi, Paulo alitendewa kwa njia mbaya na watu ambao walipaswa kuwa rafiki zake. Baadhi ya watu katika kutaniko la Kikristo hata walimpinga. (2 Kor. 12:11; Flp. 3:18) Lakini Paulo aliwashinda wote waliompinga. Jinsi gani? Aliendelea kuhubiri licha ya upinzani. Aliendelea kuwa mshikamanifu kwa ndugu na dada zake hata walipomvunja moyo. Na zaidi ya yote, alikuwa mwaminifu kwa Mungu hadi mwisho wa maisha yake. (2 Tim. 4:8) Alishinda vikwazo vikubwa, si kwa sababu alikuwa na nguvu nyingi za kimwili, lakini kwa sababu alimtegemea Yehova.

Uwe na heshima na mwenye fadhili unapojitahidi kujadiliana na wale wanaopinga imani yako ya Kikristo (Tazama fungu la 15) *

15. Lengo letu ni nini, na tunaweza kulitimizaje?

15 Je, unalazimika kukabiliana na matusi au mateso kutoka kwa wanafunzi wenzako, wafanyakazi wenzako, au watu wa familia ambao si Mashahidi? Je, umewahi kutendewa kwa njia mbaya na mtu kutanikoni? Ikiwa ndivyo, kumbuka mfano wa Daudi na Paulo. Unaweza kuendelea “kuushinda uovu kwa wema.” (Rom. 12:21) Lengo lako si kuzamisha jiwe kwenye paji la uso la mtu fulani, kama Daudi alivyofanya, bali kulifanya Neno la Mungu lipenye ndani ya akili na mioyo ya watu walio tayari kulikubali. Unaweza kutimiza lengo hilo kwa kutegemea Biblia unapojibu maswali ya watu, kwa kuwaonyesha heshima na fadhili wale wanaokutendea kwa njia mbaya, na kwa kuwatendea wote mema, hata adui zako.—Mt. 5:44; 1 Pet. 3:15-17.

KUBALI MSAADA KUTOKA KWA WENGINE

16-17. Paulo hakusahau nini?

16 Kabla ya kuwa mwanafunzi wa Kristo, mtume Paulo alikuwa mwanamume kijana mwenye dharau ambaye aliwatesa wafuasi wa Yesu. (Mdo. 7:58; 1 Tim. 1:13) Paulo, ambaye wakati huo alijulikana kuwa Sauli, alizuiwa na Yesu mwenyewe kushambulia kutaniko la Kikristo. Yesu alizungumza na Paulo kutoka mbinguni na kumpiga kwa upofu. Ili arudishiwe uwezo wake wa kuona, Paulo alilazimika kutafuta msaada kutoka kwa watu walewale aliokuwa amewatesa. Kwa unyenyekevu, alikubali msaada wa mwanafunzi aliyeitwa Anania ambaye alimrudishia uwezo wake wa kuona.—Mdo. 9:3-9, 17, 18.

17 Baadaye, Paulo akawa mshiriki wa kutaniko la Kikristo aliyejulikana sana, lakini hakusahau kamwe somo ambalo Yesu alimfundisha alipokuwa kwenye barabara inayoelekea Damasko. Paulo aliendelea kuwa mnyenyekevu, na alikubali kwa hiari msaada wa ndugu na dada zake. Alikiri kwamba walikuwa ‘msaada wa kumtia nguvu.’—Kol. 4:10, 11, maelezo ya chini.

18. Kwa nini huenda tukasita kupokea msaada kutoka kwa wengine?

18 Tunajifunza nini kutoka kwa Paulo? Tulipoanza kushirikiana na watu wa Yehova, huenda tulikuwa tayari kukubali msaada kutoka kwa wengine, tukitambua kwamba tulikuwa watoto kiroho na tulihitaji kujifunza mambo mengi. (1 Kor. 3:1, 2) Lakini namna gani sasa? Ikiwa tumekuwa tukimtumikia Yehova kwa miaka mingi na tumejipatia uzoefu mwingi, huenda tusiwe na utayari uleule wa kukubali msaada kutoka kwa wengine, hasa ikiwa anayetaka kutusaidia ni mtu ambaye amekuwa kwenye kweli kwa muda mfupi kuliko sisi. Hata hivyo, mara nyingi Yehova huwatumia ndugu na dada zetu kutuimarisha. (Rom. 1:11, 12) Ni lazima tutambue ukweli huo ikiwa tunataka kupata nguvu kutoka kwa Yehova.

19. Kwa nini Paulo alifanikiwa?

19 Paulo alitimiza mambo fulani makubwa baada ya kuwa Mkristo. Kwa nini? Kwa sababu alijifunza kwamba mafanikio hayategemei nguvu za kimwili, elimu, mali, au malezi yetu, bali yanategemea unyenyekevu na kumtegemea Yehova. Acheni sote tumwige Paulo (1) kwa kumtegemea Yehova, (2) kwa kujifunza kutokana na mifano ya watu katika Biblia, na (3) kwa kukubali msaada kutoka kwa waamini wenzetu. Hivyo, haidhuru tunahisi tukiwa dhaifu kadiri gani, Yehova atatutia nguvu!

WIMBO 71 Sisi Ni Jeshi la Yehova!

^ fu. 5 Katika makala hii, tutachunguza mfano wa mtume Paulo. Tutaona kwamba ikiwa sisi ni wanyenyekevu, Yehova atatupatia nguvu tunazohitaji ili kuvumilia dhihaka na kushinda udhaifu wetu mbalimbali.

^ fu. 1 UFAFANUZI WA MANENO: Huenda tukahisi tukiwa dhaifu kwa sababu mbalimbali—hatujakamilika, sisi ni maskini, wagonjwa, au tuna elimu ndogo. Zaidi ya hayo, adui zetu wanajaribu kufanya tuhisi tukiwa dhaifu kwa kutushambulia kimwili na kwa maneno.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Paulo alipoanza kuhubiri kumhusu Kristo, aliacha nyuma mambo yaliyokuwa sehemu ya maisha yake akiwa Farisayo. Huenda mambo hayo yalitia ndani vitabu vya kukunjwa vya kilimwengu na kisanduku chenye maandiko.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Wafanyakazi wanajaribu kumshinikiza ndugu yetu asherehekee siku ya kuzaliwa ya mfanyakazi mwenzao.