Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 30

Endelea Kutembea Katika Kweli

Endelea Kutembea Katika Kweli

“Sina shangwe kubwa kuliko hii: kwamba nisikie watoto wangu wanaendelea kutembea katika kweli.”—3 YOH. 4.

WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”

MUHTASARI *

1. Kama inavyoonyeshwa kwenye 3 Yohana 3, 4, ni jambo gani linalotupatia furaha?

JE, UNAWEZA kuwazia jinsi mtume Yohana alivyofurahi aliposikia kwamba wale aliowasaidia kujifunza kweli walikuwa wakiendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu? Walikabili matatizo mengi, na Yohana alikuwa akijitahidi sana kuimarisha imani ya Wakristo hao washikamanifu ambao aliwaona kuwa watoto wake wa kiroho. Sisi pia tunafurahi wakati watoto wetu, iwe ni watoto wetu halisi au wa kiroho, wanapojiweka wakfu kwa Yehova na kuendelea kumtumikia.—Soma 3 Yohana 3, 4.

2. Kusudi la barua ambazo Yohana aliandika lilikuwa nini?

2 Katika mwaka wa 98 W.K., inaelekea Yohana alikuwa akiishi katika jiji la Efeso au karibu na jiji hilo. Huenda alihamia huko baada ya kuachiliwa huru kutoka kifungoni katika kisiwa cha Patmo. Karibu na kipindi hicho, roho takatifu ya Yehova ilimwongoza aandike barua tatu. Kusudi la barua hizo lilikuwa kuwachochea Wakristo washikamanifu wadumishe imani yao katika Yesu na waendelee kutembea katika kweli.

3. Tutajibu maswali gani?

3 Yohana alikuwa mtume wa mwisho kuwa hai, na alihangaishwa na jinsi walimu wa uwongo walivyokuwa wakiliathiri kutaniko. * (1 Yoh. 2:18, 19, 26) Waasi-imani hao walidai kwamba wanamjua Mungu, lakini hawakutii amri za Yehova. Acheni tuchunguze shauri lililoongozwa na roho ya Mungu ambalo Yohana aliandika. Tunapofanya hivyo, tutapata majibu ya maswali haya matatu: Kutembea katika kweli kunamaanisha nini? Tunakabili changamoto gani? Na tunaweza kusaidiana jinsi gani ili tudumu katika kweli?

KUTEMBEA KATIKA KWELI KUNAMAANISHA NINI?

4. Kulingana na 1 Yohana 2:3-6 na 2 Yohana 4, 6, tunahitaji kufanya nini ili tutembee katika kweli?

4 Ili tutembee katika kweli tunahitaji kuijua kweli inayopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Pia, ni lazima ‘tuzishike amri za Yehova,’ yaani, tunahitaji kuzitii. (Soma 1 Yohana 2:3-6; 2 Yohana 4, 6.) Yesu alituwekea mfano mkamilifu wa kumtii Yehova. Hivyo, njia moja muhimu tunayoonyesha kwamba tunamtii Yehova ni kwa kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu kadiri iwezekanavyo.—Yoh. 8:29; 1 Pet. 2:21.

5. Ni lazima tusadiki nini?

5 Ili tuendelee kutembea katika kweli, ni lazima tusadiki kwamba Yehova ni Mungu wa kweli, kwamba kila kitu anachotuambia katika Neno lake, Biblia, ni cha kweli. Na ni lazima pia tusadiki kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa. Leo, watu wengi hutilia shaka kwamba Yesu ametiwa mafuta kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Yohana alionya kwamba kungekuwa na “wadanganyifu wengi,” ambao wangeweza kuwapotosha wale ambao hawako tayari kutetea ukweli kumhusu Yehova na Yesu. (2 Yoh. 7-11) Yohana aliandika hivi: “Ni nani aliye mwongo kama si yule anayekana kwamba Yesu ndiye Kristo?” (1 Yoh. 2:22) Njia pekee ya kuepuka kudanganywa ni kujifunza Neno la Mungu. Ni kwa kufanya hivyo tu, ndipo tutakapomjua Yehova na Yesu. (Yoh. 17:3) Na ndipo tu tutakaposadiki kwamba tuna kweli.

TUNAKABILI CHANGAMOTO GANI?

6. Vijana Wakristo wanakabili changamoto gani?

6 Ni lazima Wakristo wote wawe macho ili wasipotoshwe na falsafa za wanadamu. (1 Yoh. 2:26) Kihususa, vijana Wakristo wanapaswa kujihadhari ili wasinaswe na mtego huo. Alexia, * dada mwenye umri wa miaka 25 kutoka Ufaransa anasema hivi: “Nilipokuwa mtoto, mawazo ya ulimwengu kama vile nadharia ya mageuzi na falsafa za wanadamu, yalinisumbua. Nyakati nyingine, nilivutiwa na mafundisho hayo. Lakini nilihisi kwamba nisingeweza kusikiliza tu mambo niliyokuwa nikifundishwa shuleni na kumnyima Yehova nafasi ya kuzungumza.” Alexia alijifunza kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? Ndani ya majuma machache, aliacha kuwa na shaka. Alexia anasema, “Nilijithibitishia mwenyewe kwamba Biblia ina kweli. Na nilitambua kwamba kuishi kulingana na viwango vyake kungenipa shangwe na amani.”

7. Ni lazima tuepuke kushinikizwa kufanya nini, na kwa nini?

7 Ni lazima Wakristo wote, vijana kwa wazee, waepuke kushinikizwa kuishi maisha ya kinafiki. Yohana alitaja wazi kwamba hatuwezi kutembea katika kweli na wakati huohuo tuishi maisha mapotovu kiadili. (1 Yoh. 1:6) Ikiwa tunataka kuwa na kibali cha Mungu sasa na wakati ujao, tunahitaji kuishi kana kwamba kila kitu tunachofanya kimemulikwa waziwazi. Kwa maana hiyo, hakuna dhambi yoyote inayoweza kuwa siri kwa sababu Yehova anaona mambo yote tunayofanya.—Ebr. 4:13.

8. Ni lazima tuepuke nini?

8 Tunapaswa kuepuka mtazamo wa ulimwengu kuhusu dhambi. Mtume Yohana aliandika hivi: “Ikiwa tunasema, ‘Hatuna dhambi,’ tunajipotosha wenyewe na kweli haimo ndani yetu.” (1 Yoh. 1:8) Katika siku za Yohana, waasi-imani walidai kwamba mtu angeweza kufuata njia ya dhambi kimakusudi na bado awe na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Leo, tunaishi miongoni mwa watu wenye maoni hayo. Watu wengi hudai kwamba wanamwamini Mungu, lakini hawakubaliani na maoni ya Yehova kuhusu dhambi, na hasa inapohusu suala la ngono. Mambo ambayo Yehova anayaona kuwa dhambi wanasema kuwa ni uchaguzi wa kibinafsi, au mtindo mwingine tu wa maisha.

Vijana, chunguzeni ni kwa nini Yehova anakataza mambo fulani na kukubali mengine. Kisha mtaweza kutetea imani yenu (Tazama fungu la 9) *

9. Vijana hunufaikaje wanaposhikamana na mambo wanayoamini yanayotegemea Biblia?

9 Kihususa, huenda vijana Wakristo wakashinikizwa na wanafunzi au wafanyakazi wenzao waunge mkono maoni yao kuhusu upotovu wa maadili katika ngono. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Aleksandar. Anaeleza hivi: “Baadhi ya wasichana shuleni walijaribu kunishinikiza nifanye ngono pamoja nao. Walisema kwamba kwa kuwa sikuwa na rafiki wa kike, basi lazima mimi ni shoga.” Ikiwa unakabili majaribu kama hayo, kumbuka kwamba unaposhikamana na mambo unayoamini yanayotegemea Biblia, unalinda heshima yako, afya yako, hali yako ya kihisia, na uhusiano wako pamoja na Yehova. Na kila mara unapopinga kishawishi, itakuwa rahisi zaidi kwako kufanya lililo sawa. Pia, kumbuka kwamba Shetani ndiye chanzo cha maoni yaliyopotoka ya ulimwengu huu kuhusu ngono. Hivyo, unapokataa kuunga mkono mtazamo wa ulimwengu huu, ‘unamshinda yule mwovu.’—1 Yoh. 2:14.

10. Andiko la 1 Yohana 1:9, linatusaidiaje tumtumikie Yehova tukiwa na dhamiri safi?

10 Tunakubali kwamba Yehova ana haki ya kutuamulia mambo tunayopaswa kuyaona kuwa dhambi. Na tunafanya yote tuwezayo ili tusifanye dhambi. Lakini tukifanya dhambi, tutaungama dhambi zetu kwa Yehova katika sala. (Soma 1 Yohana 1:9.) Na ikiwa tunafanya dhambi nzito, tutatafuta msaada wa wazee ambao Yehova amewaweka rasmi watutunze. (Yak. 5:14-16) Hata hivyo, hatupaswi kulemewa na hisia za hatia kwa sababu ya makosa tuliyofanya zamani. Kwa nini? Kwa sababu Baba yetu anayetupenda aliandaa dhabihu ya fidia ya Mwana wake ili dhambi zetu ziweze kusamehewa. Yehova anaposema kwamba atawasamehe watenda dhambi wanaotubu, hivyo ndivyo anavyomaanisha. Hivyo, hakuna jambo linaloweza kutuzuia kumtumikia Yehova tukiwa na dhamiri safi.—1 Yoh. 2:1, 2, 12; 3:19, 20.

11. Tunaweza kulindaje akili zetu ili tusiathiriwe na mafundisho yanayoweza kudhuru imani yetu?

11 Ni lazima tukatae mafundisho ya waasi-imani. Tangu kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, Ibilisi amekuwa akitumia wadanganyifu wengi kupanda mbegu za shaka katika akili za watumishi waaminifu wa Mungu. Hivyo, tunahitaji kujua jinsi ya kutambua tofauti kati ya mambo yaliyo ya kweli na ya uwongo. * Huenda adui zetu wakatumia Intaneti au mitandao ya kijamii kujaribu kudhoofisha tumaini letu kwa Yehova na upendo tulio nao kwa ndugu zetu. Kumbuka ni nani anayeendeleza propaganda hizo, na uzikatae!—1 Yoh. 4:1, 6; Ufu. 12:9.

12. Kwa nini tunapaswa kuimarisha imani yetu kuhusiana na kweli ambazo tumejifunza?

12 Ili tupinge mashambulizi ya Shetani, tunahitaji kuimarisha imani yetu katika Yesu na katika jukumu analotimiza kuhusiana na kusudi la Mungu. Pia, tunahitaji kuitumaini njia pekee ambayo Yehova anatumia ili kuliongoza tengenezo lake leo. (Mt. 24:45-47) Tunaimarisha imani yetu kwa kujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida. Tukifanya hivyo, imani yetu itakuwa kama mti wenye mizizi yenye kina kirefu. Paulo alizungumzia jambo kama hilo alipoliandikia kutaniko la Kolosai. Alisema hivi: “Kama vile ambavyo mmempokea Kristo Yesu aliye Bwana, endeleeni kutembea katika muungano naye, mkiwa mmetia mizizi na kujengwa katika yeye na kuimarishwa katika imani.” (Kol. 2:6, 7) Hakuna chochote ambacho Shetani au wale waliopotoshwa naye wanaweza kufanya ili kumyumbisha Mkristo ambaye ameimarisha imani yake.—2 Yoh. 8, 9.

13. Tunapaswa kutazamia nini, na kwa nini?

13 Ni lazima tutarajie kwamba ulimwengu utatuchukia. (1 Yoh. 3:13) Yohana anatukumbusha kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Mfumo huu wa mambo unapokaribia kufika mwisho wake, hasira ya Shetani inazidi kuwaka. (Ufu. 12:12) Shetani hatumii tu mashambulizi yaliyojificha, kama vile kishawishi cha kufanya uasherati au uwongo wa waasi-imani. Yeye hutumia pia mashambulizi ya moja kwa moja, kama vile mateso ya kikatili. Shetani anajua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati cha kujaribu kukomesha kazi yetu ya kuhubiri au kuvunja imani yetu. Hivyo, haishangazi kwamba kazi yetu imewekewa vizuizi au kupigwa marufuku katika nchi kadhaa. Licha ya hayo, ndugu na dada zetu katika nchi hizo wanaendelea kuvumilia. Wanathibitisha kwamba haidhuru yule mwovu anatushambulia kwa njia gani, tunaweza kuibuka tukiwa washindi!

TUSAIDIANE ILI TUDUMU KATIKA KWELI

14. Taja njia moja ambayo tunaweza kuwasaidia ndugu na dada zetu wadumu katika kweli.

14 Ili tuwasaidie ndugu na dada zetu wadumu katika kweli, ni lazima tuwaonyeshe huruma. (1 Yoh. 3:10, 11, 16-18) Hatupaswi kuonyeshana upendo wakati tu hali ni nzuri, bali pia wakati ambapo matatizo yametokea. Kwa mfano, je, unamfahamu yeyote ambaye amefiwa na mpendwa wake na anahitaji faraja au msaada hususa? Au je, umepata habari kwamba waamini wenzako wamepoteza mali zao kwa sababu ya majanga ya asili na wanahitaji msaada wa kujenga upya Majumba yao ya Ufalme au nyumba zao? Tunaonyesha kina cha upendo na huruma tuliyo nayo kwa ndugu na dada zetu kupitia mambo tunayosema, lakini la muhimu hata zaidi, kupitia mambo tunayowatendea.

15. Kama inavyotajwa kwenye 1 Yohana 4:7, 8, tunahitaji kufanya nini?

15 Tunamwiga Baba yetu wa mbinguni anayetupenda tunapoonyeshana upendo. (Soma 1 Yohana 4:7, 8.) Njia moja muhimu ya kuonyeshana upendo ni kusameheana. Kwa mfano, huenda mtu akatuumiza lakini akatuomba msamaha. Tunaonyesha upendo kwa kumsamehe na kusahau kosa lake. (Kol. 3:13) Ndugu anayeitwa Aldo alikabili jaribu hilo alipomsikia ndugu aliyemheshimu akisema jambo fulani baya kuhusu watu wa kabila lake. Aldo anasema hivi: “Nilisali kwa Yehova mara kwa mara ili anisaidie nisiwe na maoni yasiyofaa kuhusu ndugu huyo.” Lakini Aldo alifanya jambo lingine. Aliamua kumwomba ndugu huyo waandamane pamoja katika utumishi. Walipokuwa wakihubiri pamoja, Aldo alimweleza ndugu huyo jinsi alivyoumizwa na maneno yake. Aldo anasema, “Ndugu huyo aliposikia jinsi maneno yake yalivyoniumiza, aliniomba msamaha. Kutokana na jinsi alivyokuwa akizungumza, niliona wazi kwamba alijutia mambo aliyokuwa amesema. Basi tuliachana tukiwa marafiki na kutupilia mbali tatizo letu.”

16-17. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

16 Mtume Yohana aliwapenda sana ndugu zake na alitaka wawe na imani yenye nguvu. Upendo na hangaiko alilokuwa nalo kuwaelekea linaonyeshwa wazi kupitia shauri alilowapa katika barua zake tatu zilizoongozwa na roho ya Mungu. Inatia moyo sana kujua kwamba wanaume na wanawake walio kama Yohana, wametiwa mafuta ili watawale pamoja na Kristo!—1 Yoh. 2:27.

17 Acheni tutafakari kwa uzito shauri ambalo tumezungumzia. Acheni tuazimie kutembea katika kweli, tukimtii Yehova katika kila nyanja ya maisha yetu. Jifunze Neno lake, na ulitumaini. Jenga imani yenye nguvu katika Yesu. Kataa falsafa za wanadamu na mafundisho ya waasi-imani. Epuka kuishi maisha ya kinafiki na usikubali kushinikizwa kutenda dhambi. Ishi kulingana na viwango vya juu vya Yehova kuhusu maadili. Na acheni tuwasaidie ndugu zetu waendelee kuwa na nguvu kwa kuwasamehe wale wanaotuumiza na kuwasaidia walio na uhitaji. Hivyo, licha ya changamoto tunazokabili, tutaendelea kutembea katika kweli.

WIMBO 49 Kufurahisha Moyo wa Yehova

^ fu. 5 Tunaishi katika ulimwengu unaotawaliwa na Shetani, baba ya uwongo. Hivyo, inaweza kuwa vigumu sana kwetu kuendelea kutembea katika kweli. Wakristo walioishi mwishoni mwa karne ya kwanza walikabili changamoto hiyo pia. Ili kuwasaidia wao na sisi pia, Yehova alimwongoza kwa roho mtume Yohana aandike barua tatu. Mambo yaliyo katika barua hizo yatatusaidia kutambua changamoto tunazokabili na kujifunza jinsi ya kuzishinda.

^ fu. 6 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 11 Tazama makala ya funzo “Je, Una Habari Kamili?” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Agosti 2018.

^ fu. 59 MAELEZO YA PICHA: Akiwa shuleni, dada kijana anasikia na kuona mara nyingi propaganda kuhusu ushoga. (Katika baadhi ya tamaduni, rangi za upinde wa mvua hutumiwa kuwa ishara ya ushoga.) Baadaye, anatenga wakati ili afanye utafiti na kuimarisha imani yake ya Kikristo. Kufanya hivyo, kunamsaidia afanye uamuzi unaofaa.