Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 39

Watie Moyo Wanawake Wakristo

Watie Moyo Wanawake Wakristo

“Wanawake wanaotangaza habari njema ni jeshi kubwa.”—ZAB. 68:11.

WIMBO 137 Wanawake Waaminifu, Dada Wakristo

MUHTASARI *

Dada zetu wenye bidii na walio na shughuli nyingi, wanashiriki katika mikutano, katika huduma, wanasaidia kudumisha Jumba lao la Ufalme, na wanawajali waabudu wenzao (Tazama fungu la 1)

1. Akina dada Wakristo wanalitegemeza tengenezo kwa njia zipi, lakini wengi wao wanakabili changamoto gani? (Tazama picha kwenye jalada.)

TUNAFURAHI sana kuwa na dada wengi wanaofanya kazi kwa bidii kutanikoni! Kwa mfano, wanashiriki katika mikutano na katika huduma. Baadhi yao wanashiriki katika udumishaji wa Jumba lao la Ufalme, na wanawaonyesha upendezi wa kibinafsi waabudu wenzao. Hapana shaka kwamba wanakabili changamoto. Baadhi yao wanawatunza wazazi waliozeeka. Wengine wanavumilia upinzani kutoka kwa watu wa familia. Na wengine wanafanya kazi kwa bidii ili kuwaandalia watoto wao, hata ingawa wako katika familia ya mzazi mmoja.

2. Kwa nini tunapaswa kuwatia moyo dada zetu Wakristo?

2 Kwa nini tunapaswa kukazia fikira kuwatia moyo dada zetu Wakristo? Kwa sababu mara nyingi ulimwengu hauwapi wanawake heshima wanayostahili. Lakini Biblia inatukumbusha tuwatie moyo. Kwa mfano, mtume Paulo aliliambia kutaniko la Roma, limkaribishe Fibi na “kumpa msaada wowote ambao huenda alihitaji.” (Rom. 16:1, 2) Alipokuwa Farisayo, huenda Paulo alizama katika utamaduni ambao uliwaona wanawake kuwa duni. Lakini baada ya kuwa Mkristo, alimwiga Yesu na kuwatendea wanawake kwa heshima na fadhili.—1 Kor. 11:1.

3. Yesu aliwatendeaje wanawake, na aliwaonaje wanawake waliofanya mapenzi ya Mungu?

3 Yesu aliwaheshimu wanawake wote. (Yoh. 4:27) Hakuwatendea wanawake kama viongozi wa kidini wa siku zake walivyowatendea. Isitoshe, kitabu kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema: “Yesu hakuwahi kusema jambo lolote lililowashushia heshima wanawake.” Yesu aliwaheshimu hata zaidi wanawake waliofanya mapenzi ya Baba yake. Vilevile, aliwaona kama dada zake na kuwataja pamoja na wanaume ambao aliwaona kuwa sehemu ya familia yake ya kiroho.—Mt. 12:50.

4. Tutachunguza nini katika makala hii?

4 Sikuzote Yesu alikuwa tayari kuwasaidia dada zake wa kiroho. Aliwathamini na kuwatetea. Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kumwiga Yesu inapohusu kuwaonyesha dada zetu ufikirio.

WAONYESHE UFIKIRIO DADA ZETU WENYE THAMANI

5. Kwa nini huenda ikawa vigumu kwa baadhi ya akina dada kufaidika na ushirika wenye kujenga wa ndugu na dada?

5 Sisi sote, iwe ni ndugu au dada, tunahitaji ushirika mzuri. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda ikawa vigumu kwa akina dada kutimiza uhitaji huo. Kwa nini? Fikiria maelezo yafuatayo. Dada mmoja anayeitwa Jordan * anasema hivi: “Kwa sababu mimi ni mseja, mara nyingi inakuwa vigumu kwangu kutambua sehemu yangu kutanikoni na ninahisi sichangamani vizuri na wengine.” Kristen, dada painia ambaye alihamia eneo lingine ili kupanua huduma yake alisema hivi: “Unapohamia kutaniko jipya huenda ukahisi upweke.” Huenda baadhi ya akina ndugu wakahisi vivyo hivyo. Huenda wale wanaoishi katika familia iliyogawanyika kidini wakahisi kwamba wametengwa kwa kiasi fulani na watu wa familia zao, na wakati huohuo wanaweza kuhisi wakiwa wapweke wanapokuwa pamoja na ndugu na dada zao. Baadhi ya akina dada huenda wakahisi upweke kwa sababu ni wagonjwa na hivyo hawawezi kutoka nyumbani, au kwa sababu wanawatunza watu wa familia ambao ni wagonjwa. Annette anasema hivi: “Nisingeweza kukubali mialiko ya kwenda kwenye tafrija, kwa sababu mimi ndiye niliyekuwa nikitumia muda mwingi kumtunza mama.”

Kama Yesu, tunaweza kuwaonyesha dada zetu waaminifu kwamba tunawajali sana (Tazama fungu la 6 hadi 9) *

6. Kulingana na Luka 10:38-42, Yesu aliwasaidia Martha na Maria jinsi gani?

6 Yesu alitumia wakati wake pamoja na dada zake wa kiroho, naye alikuwa rafiki wa kweli. Fikiria urafiki wake pamoja na Maria na Martha, ambao inaelekea walikuwa waseja. (Soma Luka 10:38-42.) Ni wazi kwamba kupitia maneno na matendo yake, Yesu aliwastarehesha. Maria alijihisi huru kuketi miguuni pake kama wanafunzi wengine. * Na Martha alipokwazika kwa sababu Maria hakuwa akimsaidia kutayarisha chakula, alikuwa huru kumweleza Yesu hisia zake. Katika kikusanyiko hicho kisicho rasmi, Yesu aliweza kuwasaidia kiroho wanawake hao. Na alionyesha kwamba aliwajali wanawake hao na ndugu yao Lazaro, kwa kuwatembelea kwa ukawaida. (Yoh. 12:1-3) Haishangazi kwamba Lazaro alipokuwa mgonjwa sana Maria na Martha walijua kwamba wangeweza kumwomba Yesu awasaidie.—Yoh. 11:3, 5.

7. Taja njia moja tunayoweza kuwatia moyo dada zetu.

7 Kwa baadhi ya akina dada, mikutano ndiyo fursa kuu ya kuwa pamoja na waabudu wenzao. Hivyo, tungependa kutumia pindi hizo kuwafanya wajihisi huru, kuzungumza nao, na kuwaeleza jinsi tunavyowajali. Jordan, aliyetajwa mapema, anasema hivi: “Ninathamini sana wengine wanaponipongeza kwa maelezo yangu, wanapopanga kushiriki pamoja nami katika utumishi, au wanapoonyesha kwamba wananijali kwa njia nyingine.” Ni lazima tuwaonyeshe dada zetu kwamba wao ni muhimu sana kwetu. Kia anasema hivi: “Ikiwa nitakosa kufika mikutanoni, ninajua nitapata ujumbe mfupi kutoka kwa baadhi ya ndugu na dada wanaotaka kunijulia hali. Jambo hilo linanionyesha kwamba ndugu na dada zangu wananijali.”

8. Tunaweza kumwiga Yesu katika njia gani nyingine?

8 Kama Yesu, sisi pia tunaweza kutenga wakati wa kuwa na ushirika pamoja na dada zetu. Labda tunaweza kuwaalika nyumbani kwa ajili mlo au tafrija. Tunapofanya hivyo, tungependa mazungumzo yetu yawe yenye kujenga. (Rom. 1:11, 12) Wazee wanapaswa kuwa na mtazamo kama wa Yesu. Yesu alitambua kwamba useja unaweza kuwa changamoto kwa baadhi ya watu, lakini aliweka wazi kwamba furaha ya kweli haitegemei kufunga ndoa au kupata watoto. (Luka 11:27, 28) Badala yake, furaha ya kudumu inatokana na kutanguliza utumishi wetu kwa Yehova maishani.—Mt. 19:12.

9. Wazee wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia akina dada?

9 Wazee hasa wanapaswa kuwatendea wanawake Wakristo kama dada na mama zao wa kiroho. (1 Tim. 5:1, 2) Wazee wanapaswa kutenga muda wa kuzungumza na akina dada kabla na baada ya mikutano. Kristen anasema hivi: “Mzee mmoja alitambua kwamba nilikuwa na shughuli nyingi na alitaka kuelewa jinsi nilivyoratibu shughuli zangu. Nilithamini sana kwamba alikuwa ananijali.” Wazee wanapotenga wakati wa kuzungumza na dada zao wa kiroho kwa ukawaida, wanathibitisha kwamba wanawajali. * Annette aliyetajwa mapema, anaeleza faida moja ya kuzungumza na wazee kwa ukawaida. Anasema hivi: “Ninapata fursa ya kuwajua vizuri na wao pia wanapata fursa ya kunijua vizuri zaidi. Kisha, ninapopata matatizo ninajihisi huru kuwafikia ili kupata msaada.”

WATHAMINI DADA ZETU

10. Ni jambo gani linaweza kuwaimarisha dada zetu?

10 Sisi sote, iwe ni wanaume au wanawake, tunaimarishwa wengine wanapotambua uwezo wetu mbalimbali, na kutuambia kwamba wanathamini kazi tunayofanya. Kwa upande mwingine, ikiwa hakuna mtu anayethamini vipawa vyetu au kazi yetu, tunavunjika moyo. Abigail, dada mseja na ambaye ni painia, anakiri kwamba nyakati nyingine anahisi kwamba anapuuzwa. Anasema hivi: “Watu wananiona tu kuwa dada ya fulani au binti ya fulani. Nyakati nyingine ninahisi ni kana kwamba hakuna anayeniona.” Hata hivyo, mfikirie dada anayeitwa Pam. Akiwa mseja alitumikia akiwa mmishonari kwa miaka mingi. Baadaye, alirudi nyumbani ili kuwatunza wazazi wake. Sasa akiwa na miaka sabini na kitu, bado anaendelea kutumikia akiwa painia. Pam anasema hivi: “Jambo ambalo limekuwa likinitia moyo ni wengine wanaponiambia kwamba wanathamini kazi ninayofanya.”

11. Yesu alionyeshaje kwamba aliwathamini wanawake waliofuatana naye katika huduma?

11 Yesu alithamini msaada kutoka kwa wanawake wanaomwogopa Mungu waliomhudumia “kwa mali zao.” (Luka 8:1-3) Hakuwapa tu pendeleo hilo, bali pia aliwafunulia kweli za kiroho zenye kina. Kwa mfano, aliwaambia kwamba angekufa na kisha kufufuliwa. (Luka 24:5-8) Aliwatayarisha wanawake hao ili wakabiliane na majaribu yaliyokuwa mbele yao, kama tu alivyofanya kwa mitume. (Marko 9:30-32; 10:32-34) Inafaa kukumbuka kwamba ingawa mitume walikimbia Yesu alipokamatwa, baadhi ya wanawake waliokuwa wakimfuata walikuwa kando yake alipokuwa akifa kwenye mti wa mateso.—Mt. 26:56; Marko 15:40, 41.

12. Yesu aliwakabidhi wanawake kazi gani?

12 Yesu aliwakabidhi wanawake kazi muhimu. Kwa mfano, wanawake waliomwogopa Mungu walikuwa mashahidi wa kwanza wa ufufuo wake. Aliwapa wanawake hao mgawo wa kuwaambia mitume wake kwamba alikuwa amefufuliwa kutoka kwa wafu. (Mt. 28:5, 9, 10) Inaelekea wanawake walikuwepo roho takatifu ilipomiminwa kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Ikiwa ndivyo, dada hao waliotoka tu kutiwa mafuta waliweza kupokea kimuujiza uwezo wa kuzungumza lugha za kigeni na kuwaambia wengine kuhusu “mambo makuu ya Mungu.”—Mdo. 1:14; 2:2-4, 11.

13. Wanawake Wakristo wanatimiza nini leo, na tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini mambo wanayofanya?

13 Dada zetu wanastahili kupongezwa kwa yote wanayofanya katika utumishi wa Yehova. Utumishi huo unatia ndani kujenga na kudumisha majengo, kuunga mkono vikundi vya lugha ya kigeni, na kujitolea kufanya kazi Betheli. Wanasaidia katika kazi ya kutoa misaada, wanatafsiri machapisho yetu na kutumikia wakiwa mapainia na wamishonari. Kama tu ilivyo kwa akina ndugu, akina dada pia wanahudhuria shule ya mapainia, Shule ya Waeneza Injili wa Ufalme, na Shule ya Gileadi. Kwa kuongezea, wake wanawasaidia waume zao ili watimize majukumu yao mazito katika kutaniko na katika tengenezo. Ndugu hao wenye majukumu wasingeweza kutumikia kikamili ‘wakiwa zawadi’ ikiwa wake zao hawangewaunga mkono. (Efe. 4:8) Je, unaweza kufikiria njia mbalimbali za kuwaunga mkono dada zetu kwa kazi wanazofanya?

14. Kulingana na Zaburi 68:11, wazee wenye hekima wanafanya nini?

14 Wazee wenye hekima wanatambua kwamba akina dada ni “jeshi kubwa” la wafanyakazi walio tayari, na kwamba mara nyingi wao ni wahubiri stadi wa habari njema. (Soma Zaburi 68:11.) Hivyo, wazee hujitahidi kujifunza kutokana na uzoefu wao. Abigail, aliyetajwa mapema, anatiwa moyo akina ndugu wanapomuuliza kuhusu njia zenye matokeo anazotumia kuwafikia watu katika eneo lake. Anasema hivi: “Jambo hilo linanisaidia kuona kwamba Yehova amenipa sehemu katika tengenezo lake.” Kwa kuongezea, wazee wanatambua kwamba dada waaminifu na wakomavu wana mchango mkubwa katika kuwasaidia dada vijana kukabiliana na changamoto mbalimbali. (Tito 2:3-5) Bila shaka, dada zetu wanastahili kuthaminiwa!

WATETEE NA KUWASAIDIA DADA ZETU

15. Ni nyakati gani ambazo dada zetu wanaweza kuhitaji mtu wa kuwatetea?

15 Nyakati nyingine huenda akina dada wakahitaji mtu wa kuwatetea wanapokabiliana na changamoto fulani hususa. (Isa. 1:17) Kwa mfano, huenda dada mjane au aliyetalikiwa akahitaji mtu wa kuzungumza kwa niaba yake na kumsaidia kufanya baadhi ya kazi ambazo mume wake alikuwa akifanya. Huenda dada mwenye umri mkubwa akahitaji mtu wa kumsaidia kuzungumza na wataalamu wa afya. Au huenda dada painia anayeshiriki katika miradi mingine ya kitheokrasi akahitaji mtu wa kumtetea endapo wengine watahoji kwa nini hashiriki katika huduma kwa ukawaida kama mapainia wengine. Tunaweza kuwasaidia dada zetu katika njia zipi nyingine? Kwa mara nyingine tena, acheni tuchunguze mfano wa Yesu.

16. Kama inavyotajwa kwenye Marko 14:3-9, Yesu alimteteaje Maria?

16 Yesu alikuwa mwepesi wa kuwatetea dada zake wa kiroho wengine walipowaelewa vibaya. Kwa mfano, alimtetea Maria, Martha alipomkosoa. (Luka 10:38-42) Kwa mara nyingine tena, Yesu alimtetea Maria watu walipomshutumu kwa kufanya jambo ambalo waliliona kuwa si sawa. (Soma Marko 14:3-9.) Yesu alielewa nia ya Maria na alimpongeza kwa kusema hivi: “Amenitendea jambo jema. . . . Amefanya alichoweza.” Na hata alitabiri kwamba tendo lake la ukarimu lingetajwa popote ambapo “habari njema itahubiriwa ulimwenguni,” kama tu makala hii inavyofanya. Inapendeza sana kwamba Yesu alihusianisha ukubwa wa kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, na tendo lisilo la ubinafsi la mwanamke huyo! Ni wazi kwamba maneno hayo ya Yesu yalimtia moyo sana Maria baada ya kuhukumiwa isivyo haki!

17. Toa mfano wa hali ambayo huenda tukahitaji kumtetea dada yetu.

17 Je, wewe huwatetea dada zako kunapokuwa na uhitaji? Kwa mfano, fikiria hali ifuatayo. Baadhi ya wahubiri humwona dada ambaye mume wake si Shahidi akichelewa mikutanoni mara kwa mara, na kuondoka mara tu baada ya mikutano kuisha. Na wanamwona akiambatana na watoto wake mara chache sana. Hivyo, wanahoji kwa nini hachukui msimamo thabiti na kumwambia mume wake amruhusu kwenda na watoto mikutanoni, na wanaanza kumchambua. Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba dada huyo anafanya yote awezayo. Hana mamlaka kamili juu ya ratiba yake wala juu ya watoto wake. Unaweza kufanya nini ili kumtetea? Ikiwa utampongeza dada huyo na kutaja kwa wengine mambo mazuri anayofanya, huenda wakaacha kumchambua.

18. Tunaweza kuwasaidia dada zetu katika njia gani nyingine?

18 Tunaweza kuonyesha kwamba tunawajali sana dada zetu kwa kuwapa msaada hususa. (1 Yoh. 3:18) Annette, dada ambaye alikuwa akimtunza mama yake aliyekuwa mgonjwa anasema hivi: “Baadhi ya ndugu na dada wangekuja nyumbani kunisaidia ili nifanye mambo mengine au wangeleta chakula. Jambo hilo lilinifanya nihisi ninapendwa, na kwamba mimi ni sehemu ya kutaniko.” Jordan pia alipewa msaada. Ndugu mmoja alimpa madokezo ya jinsi ya kudumisha gari lake. Anasema hivi: “Inafurahisha kujua kwamba ndugu na dada zangu wanajali usalama wangu.”

19. Wazee wanaweza kuwasaidia dada zetu kwa njia gani nyingine?

19 Wazee pia hujitahidi kuwatunza akina dada. Wanajua kwamba Yehova anataka akina dada watendewe kwa njia nzuri. (Yak. 1:27) Hivyo, wanamwiga Yesu kwa kuwa na usawaziko. Wanafanya hivyo kwa kutoweka sheria inapohusu hali ambazo ingefaa zaidi kuonyesha fadhili na ufikirio. (Mt. 15:22-28) Wazee wanaochukua hatua ya kwanza ili kuwasaidia dada zao, huwatia moyo. Mwangalizi wa kikundi cha utumishi cha dada Kia alipotambua kwamba alikuwa akihamia nyumba nyingine, bila kukawia alipanga kwenda kumsaidia. Kia anasema hivi: “Jambo hilo lilinipunguzia sana mkazo niliokuwa nao. Kwa kuwa wazee walinitia moyo na kunipa msaada niliohitaji, walinionyesha kwamba mimi ni sehemu ya kutaniko na kwamba hawataniacha nikabiliane na hali ngumu nikiwa peke yangu.”

DADA ZETU WOTE WA KIROHO WANAHITAJI KUTIWA MOYO

20-21. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawapenda sana dada zetu wote Wakristo?

20 Tunapotazama makutaniko yetu leo, tunaona idadi kubwa ya wanawake Wakristo wenye bidii wanaostahili kitia moyo chetu. Kama tulivyojifunza kutokana na mfano wa Yesu, tunaweza kuwasaidia kwa kutumia wakati wetu pamoja nao na kuwajua vizuri zaidi. Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini mambo wanayofanya katika utumishi wa Mungu. Na tunaweza kuwatetea na kuwasaidia inapohitajika.

21 Mwishoni mwa barua yake kwa Waroma, mtume Paulo aliwataja kihususa wanawake tisa Wakristo. (Rom. 16:1, 3, 6, 12, 13, 15) Bila shaka, wanawake hao walitiwa moyo waliposikia salamu na pongezi zake. Acheni sisi pia tuwatie moyo dada zetu kutanikoni. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba tunawapenda wakiwa sehemu ya familia yetu ya kiroho.

WIMBO 136 “Malipo Kamili Kutoka kwa Yehova”

^ fu. 5 Wanawake Wakristo wanakabili changamoto nyingi. Makala hii itazungumzia jinsi tunavyoweza kuwatia moyo dada hao wa kiroho kwa kuiga mfano wa Yesu. Tutaona jinsi alivyotumia wakati pamoja na wanawake, alivyowathamini, na kuwatetea.

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 6 Kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Wanafunzi waliketi miguuni pa walimu wao. Walifanya hivyo walipokuwa wakijiandaa kuwa walimu. Hata hivyo, wanawake hawakuruhusiwa kuwa walimu. Hivyo, inaelekea wanaume wengi wa Kiyahudi wangeshangazwa kumwona Maria ameketi miguuni pa Yesu, na akiwa na hamu ya kujifunza kutoka kwa Yesu.”

^ fu. 9 Wazee wanahitaji kuwa waangalifu wanapowasaidia akina dada. Kwa mfano, wanapaswa kuepuka kuwatembelea akina dada wakiwa peke yao.

^ fu. 65 MAELEZO YA PICHA: Kama Yesu alivyowaonyesha upendezi wa kibinafsi wanawake waaminifu, ndugu mmoja anawasaidia dada wawili kubadili tairi la gari lao, mwingine anamtembelea dada aliye mgonjwa, na wa tatu anaenda pamoja na mke wake kumtembelea dada fulani pamoja na binti yake ili wafurahie ibada ya familia.