Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 40

“Linda Yote Uliyokabidhiwa”

“Linda Yote Uliyokabidhiwa”

“Timotheo, linda yote uliyokabidhiwa.”—1 TIM. 6:20.

WIMBO 29 Kuishi Kulingana na Jina Letu

MUHTASARI *

1-2. Kulingana na andiko la 1 Timotheo 6:20, Timotheo alikuwa amepewa nini?

MARA nyingi tunawakabidhi watu wengine vitu vyetu vyenye thamani ili watutunzie. Kwa mfano, huenda tukahifadhi pesa zetu katika benki. Tunapofanya hivyo tunatarajia kwamba pesa zetu zitatunzwa kwa usalama na hazitapotea au kuibiwa. Hivyo, tunaelewa kile kinachomaanishwa na kumkabidhi mtu mwingine vitu tunavyoona kuwa vyenye thamani.

2 Soma 1 Timotheo 6:20. Mtume Paulo, alimkumbusha Timotheo kwamba alikuwa amepokea kitu fulani chenye thamani, yaani, ujuzi sahihi kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu. Timotheo pia alikuwa amekabidhiwa pendeleo la ‘kulihubiri neno’ na “kufanya kazi ya mweneza-injili.” (2 Tim. 4:2, 5) Paulo alimhimiza Timotheo alinde yote aliyokabidhiwa. Kama Timotheo, sisi pia tumekabidhiwa vitu vyenye thamani. Ni vitu gani hivyo? Na kwa nini ni lazima tulinde hazina hiyo ambayo tumepewa na Yehova?

TUMEKABIDHIWA KWELI ZENYE THAMANI

3-4. Kwa nini kweli za Biblia ni zenye thamani?

3 Yehova ametupatia pendeleo la kupata ujuzi sahihi wa kweli zenye thamani zinazopatikana katika Neno lake, Biblia. Kweli hizo ni zenye thamani kwa sababu zinatufundisha jinsi ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, na zinaeleza mambo yanayoweza kutupatia furaha ya kweli maishani. Tunapokubali kweli hizo na kuishi kulingana nazo, tunawekwa huru kutokana na utumwa wa mafundisho ya uwongo na mwenendo mpotovu kiadili.—1 Kor. 6:9-11.

4 Sababu nyingine inayofanya kweli zinazopatikana katika Neno la Mungu ziwe zenye thamani ni kwamba Yehova anazifunua tu kwa watu wanyenyekevu na ‘walio na mwelekeo unaofaa.’ (Mdo. 13:48) Watu hao wanakubali njia anayoitumia kuwafundisha kweli hizo leo. (Mt. 11:25; 24:45) Hatuwezi kujifunza kweli hizo peke yetu, na hakuna jambo lingine lolote linaloikaribia thamani ya kuelewa kweli hizo.—Met. 3:13, 15.

5. Yehova ametupatia pendeleo gani lingine?

5 Yehova pia ametukabidhi pendeleo la kuwafundisha wengine kweli kumhusu Yeye na makusudi yake. (Mt. 24:14) Ujumbe tunaohubiri ni wenye thamani sana kwa sababu unawasaidia watu wawe sehemu ya familia ya Yehova na kuwapatia fursa ya kupata uzima wa milele. (1 Tim. 4:16) Iwe tunashiriki katika huduma kwa kiwango kidogo au kikubwa, tunaunga mkono kazi muhimu zaidi inayofanywa katika kipindi hiki. (1 Tim. 2:3, 4) Ni pendeleo kubwa sana kuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu!—1 Kor. 3:9.

LINDA MAMBO ULIYOKABIDHIWA!

Timotheo alihitaji kusimama imara katika kweli wengine walipochagua kuiacha (Tazama fungu la 6)

6. Ni nini kilichowapata baadhi ya watu walioshindwa kuthamini pendeleo lao la kuwa wafanyakazi wenzi wa Mungu?

6 Baadhi ya Wakristo walioishi kipindi kimoja na Timotheo hawakuthamini pendeleo lao la kuwa wafanyakazi wenzi pamoja na Mungu. Kwa kuwa Dema aliupenda ulimwengu aliacha pendeleo lake la kutumikia pamoja na Paulo. (2 Tim. 4:10) Inaelekea Figelo na Hermogene waliacha huduma yao kwa sababu waliogopa kwamba wangekabili minyanyaso kama Paulo. (2 Tim. 1:15) Himenayo, Aleksanda na Fileto walikuja kuwa waasi-imani nao wakaacha kweli. (1 Tim. 1:19, 20; 2 Tim. 2:16-18) Mwanzoni, watu hao wote walikuwa imara kiroho, lakini waliacha kuyaona mambo waliyokabidhiwa kuwa yenye thamani.

7. Shetani anatumia mbinu gani dhidi yetu?

7 Shetani anajaribu jinsi gani kutufanya tuache kuthamini hazina ambazo Yehova ametukabidhi? Fikiria baadhi ya mbinu za Shetani. Anatumia burudani na vyombo vya habari kuendeleza viwango, njia ya kufikiri, na tabia ambazo anaamini kwamba zinaweza kutufanya tulegeze msimamo wetu inapohusu kweli za Biblia. Anajaribu kututisha kupitia watu wanaotushinikiza au kututesa ili tuache kuhubiri. Anajaribu kutushawishi tusikilize “‘ujuzi’ wa uwongo” wa waasi-imani ili tuiache kweli.—1 Tim. 6:20, 21.

8. Tunajifunza nini kutokana na kisa cha ndugu anayeitwa Danieli?

8 Tusipokuwa waangalifu, hatua kwa hatua tunaweza kuiacha kweli. Fikiria kisa cha Danieli, * ambaye alikuwa anapenda kucheza michezo ya kompyuta. Anaeleza hivi: “Nilianza kucheza michezo ya kompyuta nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi. Mwanzoni, nilicheza michezo ambayo haikuwa na madhara. Lakini hatua kwa hatua nilianza kucheza michezo ambayo ilikuwa na ukatili mwingi na uwasiliani-roho.” Mwishowe alikuwa akicheza michezo ya kompyuta kwa saa 15 hivi kila siku. Danieli anaeleza hivi: “Moyoni nilijua kwamba aina ya michezo ya kompyuta niliyokuwa nikicheza, na kiasi cha wakati nilichokuwa nikitumia kilikuwa kikidhoofisha uhusiano wangu na Yehova. Hata hivyo, dhamiri yangu ilikuwa imekufa ganzi na kunifanya niamini kwamba kanuni za Biblia hazikuwa zinanihusu.” Tusipokuwa waangalifu tunaweza kuathiriwa kirahisi na burudani zisizofaa na hivyo hatua kwa hatua tukaiacha kweli. Ikiwa hilo litatokea, huenda mwishowe tukapoteza vitu vyenye thamani ambavyo Yehova ametukabidhi.

JINSI TUNAVYOWEZA KUILINDA KWELI

9. Kulingana na andiko la 1 Timotheo 1:18, 19, Paulo alimlinganisha Timotheo na nani?

9 Soma 1 Timotheo 1:18, 19. Paulo alimlinganisha Timotheo na mwanajeshi, na akamhimiza “[aendelee] kupigana vita vizuri.” Vita hivyo havikuwa halisi, bali vilikuwa vita vya kiroho. Ni kwa njia gani Wakristo ni kama wanajeshi walio kwenye pambano? Tunahitaji kusitawisha sifa gani tukiwa wanajeshi wa Kristo? Acheni tuchunguze mambo matano tunayoweza kujifunza kutokana na mfano ambao Paulo alitoa. Mambo hayo yanaweza kutusaidia tuilinde kweli.

10. Ujitoaji-kimungu ni nini, na kwa nini tunahitaji sifa hiyo?

10 Sitawisha sifa ya ujitoaji-kimungu. Mwanajeshi mzuri ni mshikamanifu. Atapigana kwa bidii ili kumlinda mtu anayempenda au kitu anachokithamini. Paulo alimtia moyo Timotheo asitawishe sifa ya ujitoaji-kimungu, yaani, kushikamana kabisa na Mungu. (1 Tim. 4:7) Kadiri upendo na ujitoaji wetu kwa Mungu unavyoongezeka, ndivyo tamaa yetu ya kuilinda kweli itakavyoongezeka.—1 Tim. 4:8-10; 6:6.

Baada ya siku ndefu yenye shughuli nyingi, huenda tukahitaji kujilazimisha ili tuhudhurie mkutano, lakini tunapata baraka tunapofanya hivyo! (Tazama fungu la 11)

11. Kwa nini tunahitaji sifa ya kujitia nidhamu?

11 Sitawisha sifa ya kujitia nidhamu. Ni lazima mwanajeshi ajitie nidhamu ili sikuzote awe tayari kwa ajili ya pambano. Timotheo aliendelea kuwa imara kiroho kwa sababu alifuata ushauri wa Paulo wa kukimbia tamaa mbaya, kufuatilia sifa zinazompendeza Mungu, na kushirikiana na waamini wenzake. (2 Tim. 2:22) Ili afanye hivyo alihitaji kujitia nidhamu. Tunahitaji kujitia nidhamu ili tushinde vita dhidi ya tamaa zetu za mwili. (Rom. 7:21-25) Isitoshe, tunahitaji kujitia nidhamu ili tuendelee kujitahidi kuuvua utu wa zamani na kuvaa utu mpya. (Efe. 4:22, 24) Na tunapokuwa tumechoka baada ya siku yenye shughuli nyingi, huenda tukahitaji kujilazimisha ili tuhudhurie mkutano.—Ebr. 10:24, 25.

12. Tunaweza kuboreshaje uwezo wetu wa kufundisha Biblia?

12 Mwanajeshi anahitaji kufanya mazoezi ya kutumia silaha zake. Ili awe na ustadi, anahitaji kufanya hivyo kwa ukawaida. Vivyo hivyo, sisi pia tunahitaji kuwa stadi inapohusu kulitumia Neno la Mungu. (2 Tim. 2:15) Tunaweza kujifunza baadhi ya stadi hizo kwenye mikutano yetu. Lakini ikiwa tunataka kuwasadikisha wengine kwamba kweli za Biblia ni zenye thamani sana, tunahitaji kushikamana kabisa na ratiba yetu ya kujifunza Biblia kibinafsi. Tunahitaji kulitumia Neno la Mungu kuimarisha imani yetu. Hilo linahusisha mengi zaidi ya kusoma tu Biblia. Tunahitaji kutafakari mambo tunayosoma na kufanya utafiti katika machapisho yetu ili tuyaelewe Maandiko na kuyatumia kwa usahihi. (1 Tim. 4:13-15) Kisha tutafaulu kulitumia Neno la Mungu kuwafundisha wengine. Hilo pia linahusisha mengi zaidi ya kusoma tu andiko la Biblia. Tungependa kuwasaidia wale wanaotusikiliza walielewe andiko hilo na jinsi ya kulitumia. Kwa kushikamana na ratiba yetu ya kujifunza Biblia kibinafsi, tutaweza kuboresha uwezo wetu wa kulitumia Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu ili kuwafundisha wengine.—2 Tim. 3:16, 17.

13. Kulingana na Waebrania 5:14, kwa nini ni lazima tuwe na utambuzi?

13 Uwe na utambuzi. Ni lazima mwanajeshi awe na uwezo wa kuona hatari kimbele na kuiepuka. Ni lazima sisi pia tujifunze kutambua hali zinazoweza kutudhuru na kisha tuziepuke. (Met. 22:3; soma Waebrania 5:14.) Kwa mfano, tunahitaji kutumia hekima tunapochagua burudani na tafrija tutakazoshiriki. Mara nyingi, vipindi vya televisheni na sinema zinaonyesha upotovu wa maadili. Mwenendo huo unamchukiza Mungu na bila shaka unaleta madhara. Hivyo, tunaepuka burudani zinazoweza kudhoofisha upendo wetu kwa Mungu hatua kwa hatua.—Efe. 5:5, 6.

14. Sifa ya utambuzi ilimsaidiaje Danieli?

14 Danieli aliyetajwa awali, alianza kutambua kwamba kucheza michezo ya kompyuta yenye jeuri na uwasiliani-roho ni jambo lisilofaa. Alifanya utafiti kwenye Watchtower Library ili kupata habari zitakazomsaidia kushughulikia tatizo lake. Matokeo yalikuwa nini? Aliacha kucheza michezo isiyofaa ya kompyuta. Alifuta usajili wake wa kupokea michezo ya kompyuta mtandaoni na aliacha kushirikiana na wachezaji wengine. Danieli anasema: “Badala ya kutumia wakati wangu ndani ya nyumba nikicheza michezo ya kompyuta, nilianza kufanya shughuli nje ya nyumba na kushirikiana na marafiki kutanikoni.” Sasa Danieli anatumikia akiwa painia na mzee wa kutaniko.

15. Kwa nini hadithi za uwongo ni hatari?

15 Kama Timotheo, ni lazima sisi pia tutambue hatari inayotokana na maneno ya uwongo yanayosambazwa na waasi-imani. (1 Tim. 4:1, 7; 2 Tim. 2:16) Kwa mfano, huenda wakajaribu kueneza hadithi za uwongo kuhusu ndugu zetu au kufanya tutilie shaka tengenezo la Yehova. Habari kama hizo zinaweza kudhoofisha imani yetu. Ni lazima tuepuke kupotoshwa na propaganda hizo. Kwa nini? Kwa sababu habari kama hizo zinaenezwa na “watu waliopotoka kiakili na wasiojua kweli.” Lengo lao ni kuanzisha ‘mabishano na kushindana.’ (1 Tim. 6:4, 5) Wanataka tuamini uchongezi wao na tusitawishe shaka zenye uovu kuhusu ndugu zetu.

16. Ni lazima tuepuke mambo gani yanayoweza kutukengeusha?

16 Epuka mambo yanayoweza kukukengeusha. Akiwa “mwanajeshi mwema wa Kristo Yesu,” Timotheo alihitaji kukazia fikira huduma badala ya kufuatia vitu vya kimwili na mambo mengine ambayo si ya kiroho. (2 Tim. 2:3, 4) Kama Timotheo, hatupaswi kuruhusu tukengeushwe na tamaa ya kujikusanyia vitu vingi zaidi vya kimwili. “Nguvu za udanganyifu za utajiri” zinaweza kusonga upendo wetu kwa Yehova, uthamini wetu kwa Neno la Mungu, na tamaa yetu ya kulishiriki pamoja na wengine. (Mt. 13:22) Ni lazima tuwe na maisha rahisi na tutumie wakati na nguvu zetu ‘kuendelea kuutafuta kwanza Ufalme.’—Mt. 6:22-25, 33.

17-18. Tunaweza kufanya nini ili kuepuka madhara ya kiroho?

17 Uwe tayari kuchukua hatua haraka. Mwanajeshi anahitaji kupanga mapema jinsi atakavyojilinda. Ili tulinde mambo ambayo Yehova ametukabidhi, tunahitaji kutenda haraka tunapoona hatari. Ni nini kitakachotusaidia kuchukua hatua haraka? Tunahitaji kupanga mapema jinsi tutakavyotenda hatari inapotokea.

18 Kwa mfano, kunapokuwa na tukio fulani, mara nyingi wahudhuriaji hujulishwa mlango wa kutokea ulio karibu nao kabla ya programu kuanza. Kwa nini? Ili waweze kutoka haraka dharura inapotokea. Vivyo hivyo, sisi pia tunaweza kujizoeza mapema “mlango wa kutokea” tutakaotumia ikiwa tutaona kwa ghafla picha chafu, ukatili, au habari za waasi-imani tunapokuwa tukitumia intaneti au kutazama sinema, au kipindi fulani cha televisheni. Ikiwa tutajitayarisha mapema kukabiliana na mambo ambayo huenda yakatokea, tutaweza kuchukua hatua haraka ili tuepuke madhara ya kiroho na tubaki tukiwa safi machoni pa Yehova.—Zab. 101:3; 1 Tim. 4:12.

19. Tutapata baraka gani ikiwa tutalinda vitu vyenye thamani ambavyo Yehova ametukabidhi?

19 Ni lazima tulinde vitu vyenye thamani ambavyo Yehova ametupatia, yaani, kweli zenye thamani za Biblia na pendeleo la kuwafundisha wengine kweli hizo. Tunapofanya hivyo, tutakuwa na dhamiri safi, tutakuwa na kusudi la kweli maishani, na shangwe ya kuwasaidia wengine wamjue Yehova. Na kwa msaada wake, tutaweza kulinda mambo yote ambayo tumekabidhiwa.—1 Tim. 6:12, 19.

WIMBO 127 Napaswa Kuwa Mtu wa Namna Gani?

^ fu. 5 Tuna pendeleo kubwa la kujua kweli na kuwafundisha wengine kweli hiyo. Makala hii itatusaidia kulilinda pendeleo hilo na kutoliachia kamwe.

^ fu. 8 Jina limebadilishwa.