Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

C. Joseph F. Rutherford na wengine wakati wa safari yao huko Ulaya

1920—Miaka Mia Moja Iliyopita

1920—Miaka Mia Moja Iliyopita

KUANZIA mwanzoni mwa mwaka wa 1920, watu wa Yehova walikuwa na hamu kubwa ya kufanya kazi iliyokuwa mbele yao. Mwaka wa 1920, walichagua maneno haya kuwa andiko lao la mwaka, “BWANA ni nguvu zangu na wimbo.”—Zab. 118:14, Union Version.

Yehova aliwaimarisha wahubiri hao wenye bidii. Mwaka huo idadi ya makolpota, au mapainia, iliongezeka kutoka 225 hadi 350. Na kwa mara ya kwanza wafanyakazi wa darasa, au wahubiri zaidi ya 8,000 waliripoti utendaji wao makao makuu. Yehova aliwabariki kwa kuwa na ongezeko kubwa sana.

WAONYESHA BIDII YA PEKEE

Machi 21, 1920, Joseph F. Rutherford, ambaye alikuwa akiongoza miongoni mwa wanafunzi wa Biblia wakati huo alizungumzia kichwa, “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Wanafunzi wa Biblia walifanya juu chini ili kuwaalika watu kwenye tukio hilo. Walikodi ukumbi mkubwa jijini New York na kugawa mialiko 320,000 hivi.

Gazeti lililokuwa na tangazo la hotuba “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe”

Idadi ya watu waliohudhuria ilizidi matarajio ya wanafunzi hao. Wahudhuriaji zaidi ya 5,000 walijaza kabisa ukumbi huo, na watu wengine zaidi ya 7,000 walikosa nafasi na hivyo wakazuiwa kuingia. Gazeti la Mnara wa Mlinzi liliuita mkutano huo, “mojawapo ya mikutano iliyofanikiwa zaidi kuwahi kufanywa na Wanafunzi wa Biblia.”

Wanafunzi wa Biblia walikuja kujulikana sana kwa kutangaza kwamba “mamilioni wanaoishi sasa hawatakufa kamwe.” Wakati huo, hawakuelewa kwamba ujumbe wa Ufalme ulihitaji kutangazwa kwa kiwango kikubwa zaidi. Ingawa hivyo, bidii yao ilikuwa ya pekee. Ida Olmstead, ambaye alianza kuhudhuria mikutano mwaka wa 1902, anakumbuka hivi: “Tulijua kwamba wanadamu wote wangefurahia baraka kubwa wakati ujao, na hatungeacha kamwe kuwaambia habari hii njema watu tuliokutana nao katika huduma.”

WAANZA KAZI YA UCHAPISHAJI

Ili kuhakikisha kwamba chakula cha kiroho kinapatikana, akina ndugu katika Betheli walianza kuchapisha baadhi ya machapisho wao wenyewe. Walinunua mtambo na kuufunga katika jengo la kukodi lililokuwa huko 35 Myrtle Avenue, Brooklyn, New York, karibu na makao ya Betheli.

Leo Pelle na Walter Kessler walianza utumishi wa Betheli Januari 1920. Walter anakumbuka hivi: “Tulipowasili msimamizi wa kiwanda cha uchapishaji alituangalia na kusema hivi, ‘Mna saa moja na nusu kabla ya chakula cha mchana.’ Hivyo, akatupatia kazi ya kubeba makatoni ya vitabu kutoka chumba cha ardhini.”

Leo anakumbuka jambo lililotukia siku iliyofuata: “Kazi yetu ilikuwa kusafisha ukuta kwenye ghorofa ya chini. Ilikuwa kazi yenye kuchafua sana kuliko kazi zote nilizowahi kufanya. Lakini ilikuwa kazi ya Bwana na hilo lilifanya iwe kazi yenye kuridhisha.”

Mashine iliyotumiwa kuchapisha gazeti Mnara wa Mlinzi

Ndani ya majuma machache, Mnara wa Mlinzi ulikuwa ukichapishwa na wahudumu wenye bidii waliokuwa wamejitolea. Nakala 60,000 za toleo la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 1920 zilichapishwa katika mashine ya kuchapisha iliyokuwa kwenye ghorofa ya kwanza. Wakati huohuo kwenye chumba cha chini ya ardhi, akina ndugu walifunga mashine ya kuchapisha waliyoiita Meli ya Kivita. Kuanzia toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 14, 1920, walianza pia kuchapisha gazeti The Golden Age. Bila shaka, Yehova alibariki jitihada za wafanyakazi hao waliojitolea.

“Ilikuwa kazi ya Bwana, na hilo lilifanya iwe kazi yenye kuridhisha”

“TUKAE PAMOJA KWA AMANI”

Watu washikamanifu wa Yehova walikuwa wakifurahia utendaji mpya na ushirika mzuri pamoja. Hata hivyo, baadhi ya Wanafunzi wa Biblia waliliacha tengenezo wakati wa kipindi kigumu kilichoanza mwaka wa 1917 hadi 1919. Wangeweza kusaidiwaje?

Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1920, lilikuwa na kichwa “Tukae Pamoja kwa Amani.” Liliwahimiza hivi kwa upendo: “Tuna hakika . . . kila mtu mwenye roho ya Bwana . . . yuko tayari kusahau mambo ya nyuma, . . . kukaa pamoja kwa umoja na kuendelea kama mwili mmoja uliounganishwa.”

Watu wengi waliitikia vizuri maneno hayo yenye fadhili. Wenzi fulani wa ndoa waliandika hivi: “Tulitambua kwamba lilikuwa jambo lisilofaa kutoshiriki katika kazi ya kuhubiri ambayo wengine walikuwa wakifanya kwa zaidi ya mwaka mmoja uliopita. . . . Tunatumaini kwamba hatutakengeushwa tena kamwe.” Wafanyakazi hao wote ambao walianza utendaji wao upya walikuwa na mengi ya kufanya mbele yao.

WASAMBAZA KITABU “ZG”

Juni 21, 1920, Wanafunzi wa Biblia walianza kusambaza kitabu “ZG,” ambacho ni toleo la kitabu The Finished Mystery * chenye jalada la karatasi. Nakala nyingi za kitabu hicho zilikuwa zimehifadhiwa kilipokuwa kimepigwa marufuku mwaka wa 1918.

Wafanyakazi wote wa darasa, si makolpota pekee, walialikwa kushiriki katika kazi hiyo ya usambazaji. Edmund Hooper anasema hivi: “Kila mtu aliyejitoa [aliyebatizwa] kutoka katika kila darasa na ambaye anaweza kushiriki anapaswa kufanya hivyo kwa hiari. Acheni hii iwe kauli mbiu ya kila mmoja wetu kwa sasa: ‘Jambo hili moja ndilo nitakalolifanya’, yaani, kutoa kitabu ZG.” Edmund Hooper anakumbuka kwamba kampeni hiyo iliwapatia wengi fursa ya kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa mara ya kwanza maishani. Aliongezea kusema hivi: “Tulianza kuelewa kikamili mambo yaliyohusika katika kazi ambayo ingefanywa kwa kiasi kikubwa kuliko matarajio yetu yote.”

KUPANGA UPYA KAZI BARANI ULAYA

Kwa kuwa ilikuwa vigumu kuwasiliana na Wanafunzi wa Biblia katika nchi nyingine wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, Ndugu Rutherford alitaka kuwatia moyo ndugu hao na kupanga upya kazi ya kuhubiri. Hivyo Agosti 12, 1920, yeye na ndugu wengine wanne walifanya ziara ndefu nchini Uingereza, Bara la Ulaya, na Mashariki ya Kati.

Ndugu Rutherford akiwa Misri

Rutherford alipotembelea Uingereza Wanafunzi wa Biblia walifanya makusanyiko matatu na mikutano 12 ya watu wote. Jumla ya watu waliohudhuria ilikadiriwa kuwa watu 50,000. Likielezea ziara hiyo, gazeti la Mnara wa Mlinzi lilisema: “Akina ndugu waliburudishwa na kutiwa moyo. Walikuwa wameunganishwa katika upendo na utumishi hata zaidi, na hilo liliwafanya wawe na furaha na mioyo mingi iliyokuwa na huzuni ilipata shangwe.” Akiwa Paris, kwa mara nyingine tena Ndugu Rutherford alizungumzia kichwa: “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Hotuba ilipoanza ukumbi ulikuwa umejaa kabisa. Watu 300 waliomba kupata habari zaidi.

Bango lenye tangazo la hotuba iliyotolewa kwenye ukumbi wa Royal Albert Hall huko London

Katika majuma yaliyofuata, baadhi ya akina ndugu walitembelea miji ya Athens, Cairo, na Jerusalem. Ili kufuatia upendezi uliopatikana katika maeneo hayo, Ndugu Rutherford alianzisha depo ya machapisho katika mji wa Ramallah, karibu na Jerusalem. Kisha alirudi Ulaya na kuanzisha Ofisi ya Ulaya ya Kati na kufanya mipango ili machapisho yaanze kuchapishwa hapo.

WAFUNUA UKOSEFU WA HAKI

Septemba mwaka wa 1920, Wanafunzi wa Biblia walitoa toleo Na. 27 la The Golden Age, ambalo lilikuwa toleo la pekee lililofunua mateso ambayo Wanafunzi wa Biblia walipata mwaka wa 1918. Ile Meli ya Kivita iliyotajwa awali, ilifanya kazi usiku na mchana ili kuchapisha nakala zaidi ya milioni nne za gazeti hilo.

Picha ya Emma Martin akiwa polisi

Wasomaji wa gazeti hilo walijifunza kuhusu kisa cha pekee cha Emma Martin. Dada Martin alikuwa kolpota huko San Bernardino, California. Machi 17, 1918, yeye na ndugu watatu, E. Hamm, E. J. Sonnenburg, na E. A. Stevens, walihudhuria kikusanyiko kidogo cha Wanafunzi wa Biblia.

Mwanamume mmoja aliyehudhuria hakuwa hapo ili kujifunza Biblia. Baadaye alitoa ushahidi huu: “Nilienda kwenye mkutano huo . . . kwa mwongozo wa Mwendesha Mashtaka wa serikali. Nilihudhuria mkutano huo kwa lengo la kutafuta ushahidi.” Alipata “ushahidi” aliokuwa akitafuta, yaani, nakala ya kitabu The Finished Mystery. Siku chache baadaye Dada Martin na wale ndugu watatu walikamatwa. Walihukumiwa kuwa wamevunja sheria ya ujasusi kwa kusambaza nakala za kitabu kilichopigwa marufuku.

Emma na rafiki zake walikutwa na hatia, nao wakahukumiwa miaka mitatu gerezani. Mei 17, 1920, walianza kutumikia kifungo chao baada ya rufaa zao zote kukataliwa. Lakini baada ya muda mfupi mambo yalibadilika na kuwa mazuri zaidi.

Juni 20, 1920, Ndugu Rutherford alisimulia kisa chao katika kusanyiko huko San Francisco. Wahudhuriaji walichukizwa na jinsi Wakristo hao walivyotendewa, hivyo wakamtumia rais wa Marekani ujumbe wa telegramu. Waliandika hivi: “Tunaiona hukumu . . . ya Bi. Martin . . . chini ya sheria ya ujasusi kuwa si ya haki . . . Kitendo cha maofisa wa serikali kuu kutumia mamlaka za ofisi zao . . . kumtega . . . Bi. Martin . . . na kisha kuzusha kesi dhidi yake ili afungwe gerezani kuwa jambo lenye. . . kushtua sana.”

Mara moja siku iliyofuata, Rais Woodrow Wilson alibatilisha kifungo cha Dada Martin na Ndugu Hamm, Sonnenburg, na Stevens. Kifungo chao kisicho cha haki kilikuwa kimekwisha.

Mwaka wa 1920 ulipokaribia kwisha Wanafunzi wa Biblia walikuwa na mengi ya kufurahia. Kazi kwenye makao makuu iliendelea kupanuka, na kuliko wakati mwingine wowote walikuwa wakitangaza kwamba Ufalme wa Mungu ndio suluhisho la matatizo ya wanadamu. (Mt. 24:14) Mwaka uliofuata wa 1921, ungekuwa mwaka mzuri hata zaidi wa kutangaza kweli za Ufalme.

^ fu. 18 Kitabu The Finished Mystery kilikuwa buku la saba la mfululizo wa vitabu Studies in the Scriptures. Kitabu ZG kilikuwa toleo lenye jalada la karatasi kilichochapishwa kama toleo la Mnara wa Mlinzi la Machi 1, 1918. Herufi “Z” ilirejelea Zion’s Watch Tower na herufi “G,” ambayo ni herufi ya saba katika mpangilio wa alfabeti ilirejelea buku la saba.