Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 43

Yehova Analiongoza Tengenezo Lake

Yehova Analiongoza Tengenezo Lake

“‘Si kwa jeshi, wala si kwa nguvu, bali kwa roho yangu,’ asema Yehova wa majeshi.”​—ZEK. 4:6.

WIMBO 40 Sisi Ni wa Nani?

MUHTASARI *

1. Ni lazima Wakristo waliobatizwa waendelee kufanya nini?

JE, UMEBATIZWA? Ikiwa ndivyo, umeonyesha imani yako kwa Yehova hadharani na utayari wako wa kumtumikia pamoja na tengenezo lake. * Bila shaka, imani yako kwa Yehova lazima iendelee kukua. Na unahitaji kuendelea kuimarisha uhakika wako kwamba Yehova analitumia tengenezo lake leo.

2-3. Yehova analiongozaje tengenezo lake leo? Toa mifano.

2 Leo, Yehova analiongoza tengenezo lake kwa njia inayofunua sifa zake, kusudi lake, na viwango vyake. Acheni tuchunguze sifa tatu za Yehova zinazoonyeshwa na tengenezo lake.

3 Kwanza, “Mungu hana ubaguzi.” (Mdo. 10:34) Upendo ulimchochea Yehova kumtoa mwana wake awe fidia “kwa ajili ya wote.” (1 Tim. 2:6; Yoh. 3:16) Yehova huwatumia watu wake kuwahubiria habari njema wote watakaosikiliza, na hivyo kuwasaidia wengi iwezekanavyo wafaidike kutokana na fidia. Pili, Yehova ni Mungu mwenye utaratibu na wa amani. (1 Kor. 14:33, 40) Hivyo, tunatarajia kwamba waabudu wake wanamtumikia wakiwa kikundi chenye utaratibu na amani. Tatu, Yehova ni ‘Mfundishaji Mkuu.’ (Isa. 30:20, 21) Hivyo, tengenezo lake linajitahidi sana kutumia Neno lake lililoongozwa na roho kufundisha kutanikoni na katika huduma ya hadharani. Wakristo wa kutaniko la mapema waliigaje sifa hizo tatu za utu wa Yehova? Watu wa Yehova wanaigaje sifa hizo katika nyakati zetu? Na roho takatifu inaweza kukusaidiaje unapomtumikia Yehova pamoja na tengenezo lake?

MUNGU HANA UBAGUZI

4. Kama inavyotajwa kwenye Matendo 1:8, Yesu aliwaamuru wafuasi wake wafanye nini, nao wangepokea msaada gani?

4 Katika karne ya kwanza. Ujumbe ambao Yesu alihubiri uliwapa wanadamu wote tumaini. (Luka 4:43) Aliwaamuru wafuasi wake waendeleze kazi aliyokuwa ameanzisha, yaani, kutoa ushahidi “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Soma Matendo 1:8.) Bila shaka, wasingeweza kufanya kazi hiyo kwa nguvu zao wenyewe. Wangehitaji roho takatifu, yaani, “msaidizi” ambaye Yesu alikuwa amewaahidi.—Yoh. 14:26; Zek. 4:6.

5-6. Roho takatifu iliwasaidia wafuasi wa Yesu kwa njia gani?

5 Wafuasi wa Yesu walipokea roho takatifu siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Kwa msaada wa roho hiyo mara moja walianza kuhubiri, na kwa muda mfupi, maelfu ya watu walikubali habari njema. (Mdo. 2:41; 4:4) Upinzani ulipotokea, wanafunzi hawakushindwa na woga bali walimwomba Mungu ili awasaidie. Walisali hivi: “[Wawezeshe] watumwa wako waendelee kutangaza neno lako kwa ujasiri wote.” Kisha walijazwa roho takatifu na kuendelea “kutangaza neno la Mungu kwa ujasiri.”—Mdo. 4:18-20, 29, 31.

6 Pia, wanafunzi wa Yesu walikabili changamoto nyingine. Kwa mfano, kulikuwa na nakala chache za Maandiko. Hawakuwa na machapisho ya kujifunzia kama tuliyo nayo leo. Na walihitaji kuwahubiria watu waliozungumza lugha nyingi tofauti. Licha ya changamoto hizo zote, wanafunzi hao wenye bidii walifanya jambo ambalo lilionekana kana kwamba haliwezekani—katika kipindi cha miaka thelathini hivi, walikuwa wamehubiri habari njema “katika uumbaji wote chini ya mbingu.”—Kol. 1:6, 23.

7. Zaidi ya miaka 100 iliyopita, watumishi wa Yehova walijuaje kile ambacho Mungu alitaka wafanye, nao waliitikiaje?

7 Katika siku zetu. Yehova anaendelea kuwaongoza na kuwaimarisha watu wake. Bila shaka, kwa sehemu kubwa mwongozo unakuja kupitia Neno la Mungu lilioongozwa na roho. Katika Biblia tunasoma kuhusu huduma ya Yesu na amri yake kwamba wafuasi wake waendelee kufanya kazi aliyoianzisha. (Mt. 28:19, 20) Tangu Julai 1881, gazeti hili lilisema: “Sisi hatukuitwa wala kutiwa mafuta tupokee heshima na kukusanya mali, bali kutumika na kutumikishwa, na kuhubiri habari njema.” Kijitabu Kwa Wale Waliokabidhiwa Kazi (cha Kiingereza), kilichochapishwa mwaka wa 1919 kilisema hivi: “Kazi inaonekana kuwa nyingi sana, lakini ni kazi ya Bwana, na kwa nguvu zake tutaifanya.” Naam, kama Wakristo wa mapema, kwa ujasiri ndugu hao walijimimina wenyewe katika kazi wakiwa na uhakika kwamba roho takatifu ingewasaidia kuwahubiria watu wa namna zote. Tunaendelea kuwa na uhakika huohuo.

Tengenezo la Yehova limetumia vifaa bora vinavyopatikana ili kutangaza habari njema (Tazama fungu la 8 na 9)

8-9. Tengenezo la Yehova limetumia mbinu gani ili kuendeleza kazi ya kuhubiri?

8 Tengenezo la Yehova limetumia vifaa bora kabisa vinavyopatikana ili kueneza habari njema. Vifaa hivyo vinatia ndani machapisho, sinema ya “Photo-Drama of Creation,” gramafoni, magari yenye vipaza sauti, vipindi vya redio, na hivi karibuni, kompyuta na intaneti. Pia, tengenezo la Yehova linatafsiri habari katika lugha nyingi zaidi kuliko wakati mwingine wowote! Kwa nini? Ili watu wa namna zote waweze kusikia habari njema katika lugha zao wenyewe. Yehova hana ubaguzi; alitabiri kwamba habari njema zingehubiriwa “kwa kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6, 7) Anataka ujumbe wa Ufalme uwafikie watu wote.

9 Lakini vipi kuhusu watu ambao si rahisi kuwafikia kwa sababu labda wanaishi kwenye majengo yenye ulinzi mkali? Ili kuwafikia watu wengi zaidi kama hao, tengenezo la Yehova liliamua kuanzisha njia nyingine mbalimbali za kuhubiri hadharani. Kwa mfano, mwaka wa 2001, Baraza Linaloongoza liliidhinisha matumizi ya vigari na meza za machapisho nchini Ufaransa na baadaye katika maeneo mengine pia. Matokeo yalikuwa mazuri. Katika mwaka wa 2011, programu mpya ilianzishwa nchini Marekani kwenye mojawapo ya maeneo yenye shughuli nyingi sana jijini New York. Katika mwaka wa kwanza, vitabu 102,129 na magazeti 68,911 yaligawanywa. Na watu 4,701 waliomba kujifunza Biblia! Ni wazi kwamba roho takatifu ilikuwa ikitegemeza kazi hiyo. Hivyo, Baraza Linaloongoza liliidhinisha matumizi ya vigari ulimwenguni pote.

10. Tunaweza kufanya nini ili kuboresha huduma yetu?

10 Unachoweza kufanya. Tumia kikamili mazoezi ambayo Yehova anaandaa kupitia mikutano ya Kikristo. Hubiri kwa ukawaida na kikundi chako cha utumishi. Ukifanya hivyo, utaboresha njia yako ya kuhubiri na kufundisha na kutiwa moyo na mfano mzuri wa wengine. Endelea kuhubiri licha ya changamoto. Kama tu andiko letu la msingi linavyotukumbusha, hatutimizi mapenzi ya Mungu kwa nguvu zetu wenyewe, bali kupitia roho takatifu. (Zek. 4:6) Kwa maana, tunafanya kazi ya Mungu.

YEHOVA NI MUNGU MWENYE UTARATIBU NA WA AMANI

11. Baraza linaloongoza la karne ya kwanza lilifanyaje kazi kwa umoja ili kudumisha utaratibu na amani miongoni mwa watu wa Mungu?

11 Katika karne ya kwanza. Baraza linaloongoza huko Yerusalemu lilifanya kazi kwa umoja ili kudumisha utaratibu na amani miongoni mwa watu wa Mungu. (Mdo. 2:42) Kwa mfano, suala la tohara lilipojitokeza mwaka wa 49 W.K. hivi, Baraza linaloongoza chini ya mwongozo wa roho takatifu lilizungumzia jambo hilo. Ikiwa kutaniko lingeendelea kuwa na mgawanyiko kuhusu jambo hilo, kazi ya kuhubiri ingeathirika. Ingawa walikuwa Wayahudi, mitume na wanaume wazee hawakuathiriwa na utamaduni wa Kiyahudi wala na wale waliokuwa wakiushikilia sana utamaduni huo. Badala yake, walichunguza Neno la Mungu na kutafuta mwongozo wa roho takatifu. (Mdo. 15:1, 2, 5-20, 28) Matokeo yakawaje? Yehova alibariki uamuzi wao, amani na umoja vikatawala, na kazi ya kuhubiri ikasonga mbele.—Mdo. 15:30, 31; 16:4, 5.

12. Ni nini kinachoonyesha kwamba leo tengenezo la Yehova lina utaratibu na amani?

12 Katika siku zetu. Tengenezo la Yehova limewasaidia watu wake kudumisha utaratibu na amani miongoni mwao. Tangu mwaka wa 1895 gazeti Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence la Novemba 15, lilikuwa na makala yenye kichwa: “Kwa Uzuri na kwa Utaratibu,” kilichotegemea 1 Wakorintho 14:40. Makala hiyo ilisema: “Mitume walikuwa na mengi ya kusema kwa kanisa la mapema kuhusu utaratibu . . . Ni salama kuendelea kutii kwa uangalifu ‘mambo yaliyoandikwa zamani ili kutufundisha.’” (Rom. 15:4) Naam, tamaa ileile ya kuwa na utaratibu na amani iliyoonyeshwa na Wakristo wa mapema inaonekana katika tengenezo la Yehova leo. Kwa mfano, ikiwa utahudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi katika kutaniko lingine—hata katika nchi nyingine—unajua jinsi funzo hilo litakavyoongozwa na ni makala gani itakayozungumziwa. Mara moja utajihisi uko nyumbani! Ni roho ya Mungu pekee inayoweza kutokeza umoja huo wenye thamani.—Sef. 3:9, maelezo ya chini.

13. Tukiwa na andiko la Yakobo 3:17 akilini, tunapaswa kujiuliza maswali gani?

13 Unachoweza kufanya. Yehova anataka watu wake ‘wadumishe roho ya umoja katika kifungo cha muungano cha amani.’ (Efe. 4:1-3) Hivyo jiulize: ‘Je, ninachangia amani na umoja kutanikoni? Je, ninawatii wale wanaoongoza? Je, wengine wanaweza kunitegemea hasa ikiwa nina majukumu kutanikoni? Je, ninafanya mambo kwa wakati, niko tayari kusaidia, na nina tamaa ya kuwatumikia wengine?’ (Soma Yakobo 3:17.) Ikiwa unahisi unahitaji kuboresha lolote kati ya mambo hayo, mwombe Yehova akupe roho yake takatifu. Kadiri unavyoiruhusu ifinyange utu wako na iongoze matendo yako, ndivyo ndugu na dada zako watakavyokupenda na kukuthamini.

YEHOVA ANATUFUNDISHA NA KUTUPATIA VIFAA TUNAVYOHITAJI

14. Kulingana na Wakolosai 1:9, 10, Yehova aliwaelimishaje watu wake katika karne ya kwanza?

14 Katika karne ya kwanza. Yehova anapenda sana kuwaelimisha watu wake. (Zab. 32:8) Anataka wamjue, wampende, na waishi milele wakiwa watoto wake wapendwa. Mambo hayo yote hayangewezekana ikiwa tusingepata elimu anayotuandalia. (Yoh. 17:3) Yehova alilitumia kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza kuwaelimisha watu wake. (Soma Wakolosai 1:9, 10.) “Msaidizi” ambaye Yesu aliwaahidi, yaani, roho takatifu, iliwasaidia kwa njia kubwa. (Yoh. 14:16) Iliwasaidia wanafunzi kuelewa zaidi Neno la Mungu na kuwakumbusha mambo mengi ambayo Yesu alisema na kutenda, kama ambavyo baadaye yaliandikwa kwenye vitabu vya Injili. Ujuzi huo uliimarisha imani ya Wakristo wa mapema na pia upendo wao kwa Mungu, kwa Mwana wake, na kati yao wenyewe.

15. Umejionea Yehova akitimiza jinsi gani ahadi yake inayopatikana katika andiko la Isaya 2:2, 3?

15 Katika siku zetu. Yehova alitabiri kwamba “katika siku za mwisho,” watu wa mataifa yote wangemiminika kwenye mlima wake wa mfano ili wafundishwe njia zake. (Soma Isaya 2:2, 3.) Tunashuhudia unabii huo ukitimizwa. Ibada safi imeinuliwa juu zaidi kuliko ibada nyingine zote za uwongo. Na Yehova anaandaa karamu bora sana ya kiroho! (Isa. 25:6) Kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” Yehova hatuandalii tu chakula kingi bali pia anatuandalia chakula cha aina mbalimbali, kinachotia ndani makala, hotuba, vibonzo na video mbalimbali. (Mt. 24:45) Tunahisi kama alivyohisi Elihu rafiki ya Ayubu, aliyesema hivi kwa usahihi: “Ni nani aliye mfundishaji kama [Mungu]?”— Ayu. 36:22.

Acha kweli ikite mizizi moyoni mwako na uitumie maishani mwako (Tazama fungu la 16) *

16. Unaweza kufanya nini ili ukue kiroho?

16 Unachoweza kufanya. Roho takatifu itakusaidia utumie maishani mambo unayojifunza katika Neno la Mungu. Unaweza kusali hivi kama mtunga zaburi: “Nifundishe, Ee Yehova, kuhusu njia yako. Nitatembea katika kweli yako. Unganisha moyo wangu ili niliogope jina lako.” (Zab. 86:11) Endelea kujilisha chakula cha kiroho ambacho Yehova anaandaa kupitia Neno lake na tengenezo lake. Hapana shaka kwamba lengo lako si tu kupata ujuzi. Ungependa kweli ikite mizizi moyoni mwako, na uitumie maishani mwako. Roho ya Yehova inaweza kukusaidia ufanye hivyo. Pia, ungependa kuwatia moyo ndugu na dada zako. (Ebr. 10:24, 25) Kwa nini? Kwa sababu wao ni familia yako ya kiroho. Mwombe Yehova akupe roho yake ili ikusaidie kutoa maelezo ya kutoka moyoni na kufanya migawo yako kadiri uwezavyo kwenye mikutano ya Kikristo. Kwa njia hizo, unamwonyesha Yehova na Mwana wake kwamba unawapenda “kondoo” wao wenye thamani.—Yoh. 21:15-17.

17. Unaweza kuonyeshaje kwamba unaliunga mkono tengenezo la Yehova kwa uaminifu?

17 Hivi karibuni, tengenezo pekee litakalobaki duniani ni lile linaloongozwa na roho ya Mungu. Hivyo, shirikiana kwa bidii na tengenezo la Yehova. Waonyeshe watu upendo wa Mungu usio na ubaguzi kwa kuwahubiria wale wote unaokutana nao. Uwe mwenye amani kwa kuendeleza umoja kutanikoni. Na msikilize Mfundishaji wako Mkuu kwa kujilisha kikamili katika karamu yake ya kiroho anayoandaa. Kisha, wakati ulimwengu wa Shetani unapofikia mwisho wake, hutakuwa na hofu. Badala yake, utasimama imara kati ya wale wanaomtumikia Yehova kwa ushikamanifu pamoja na tengenezo lake.

WIMBO 3 Tumaini, Nguvu, na Uhakika Wetu

^ fu. 5 Je, unasadiki kwamba Yehova analiongoza tengenezo lake leo? Katika makala hii tutachunguza jinsi Yehova alivyoliongoza kutaniko la Kikristo la mapema na jinsi anavyoendelea kuwaongoza watu wake leo.

^ fu. 1 UFAFANUZI WA MANENO: Tengenezo la Yehova la ulimwengu mzima lina sehemu ya kimbingu na sehemu ya kidunia. Katika makala hii, neno “tengenezo” linarejelea sehemu ya kidunia.

^ fu. 52 MAELEZO YA PICHA: Baada ya kutazama video na kuwaona wengine wanaotumikia katika nchi zilizo na uhitaji mkubwa wa wahubiri, dada ambaye ni painia anachochewa kuiga mfano wao. Baada ya muda anafikia lengo lake la kutumikia katika nchi yenye uhitaji mkubwa wa wahubiri.