Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 44

Je, Watamtumikia Yehova Watakapokuwa Watu Wazima?

Je, Watamtumikia Yehova Watakapokuwa Watu Wazima?

“Yesu akaendelea kukua na kupata hekima zaidi, pia akazidi kupata kibali cha Mungu na wanadamu.”—LUKA 2:52.

WIMBO 134 Watoto—Amana Kutoka kwa Mungu

MUHTASARI *

1. Ni uamuzi gani ulio bora zaidi ambao mtu anaweza kufanya?

MARA nyingi maamuzi ambayo wazazi hufanya huwaathiri watoto wao kwa miaka mingi. Ikiwa wazazi watafanya maamuzi mabaya, yanaweza kuwasababishia watoto wao matatizo. Lakini ikiwa watafanya maamuzi kwa hekima, watawapa watoto wao fursa nzuri zaidi ya kuwa na maisha yenye furaha. Bila shaka, ni lazima watoto pia wafanye maamuzi mazuri. Uamuzi bora zaidi ambao mtu anaweza kufanya ni kumtumikia Yehova, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo. —Zab. 73:28.

2. Yesu na wazazi wake walifanya maamuzi gani mazuri?

2 Wazazi wa Yesu walikuwa wameazimia kuwasaidia watoto wao wamtumikie Yehova, na maamuzi waliyofanya yalithibitisha kwamba kumtumikia Yehova kulikuwa jambo muhimu zaidi maishani mwao. (Luka 2:40, 41, 52) Kama wazazi wake, Yesu alifanya maamuzi mazuri ambayo yalimsaidia kutimiza jukumu lake katika kusudi la Yehova. (Mt. 4:1-10) Yesu alikuja kuwa mwanamume mwenye fadhili, mshikamanifu, na jasiri. Mzazi yeyote anayempenda Yehova angefurahia na kujivunia kuwa na mwana kama huyo.

3. Tutajibu maswali gani katika makala hii?

3 Katika makala hii, tutajibu maswali yafuatayo: Yehova alifanya maamuzi gani mazuri kwa ajili ya Yesu? Wazazi Wakristo wanaweza kujifunza mambo gani kutokana na maamuzi ambayo wazazi wa Yesu walifanya? Na vijana Wakristo wanaweza kujifunza nini kutokana na maamuzi ambayo Yesu alifanya?

JIFUNZE KUTOKA KWA YEHOVA

4. Yehova alifanya uamuzi gani muhimu kwa ajili ya Mwana wake?

4 Yehova alimchagulia Yesu wazazi bora. (Mt. 1:18-23; Luka 1:26-38) Maneno ya Maria ya kutoka moyoni yaliyoandikwa katika Biblia yanafunua upendo wake wenye kina kwa Yehova na Neno lake. (Luka 1:46-55) Na namna ambavyo Yosefu aliitikia mwongozo wa Yehova inaonyesha jinsi ambavyo alimwogopa Mungu na alitaka kumpendeza.—Mt. 1:24.

5-6. Yehova aliruhusu mwana wake apitie mambo gani?

5 Ona kwamba Yehova hakumchagulia Yesu wazazi waliokuwa matajiri. Dhabihu ambayo Yosefu na Maria walitoa inaonyesha kwamba walikuwa maskini. (Luka 2:24) Huenda Yosefu alikuwa na karakana ndogo kando ya nyumba yake huko Nazareti ambako alifanya kazi ya useremala. Ni wazi kwamba walikuwa na maisha rahisi, hasa kadiri familia ilivyoongezeka ukubwa na kufikia angalau watoto saba.—Mt. 13:55, 56.

6 Yehova alimlinda Yesu kutokana na hatari fulani, lakini hakumkinga Mwana Wake kutokana na matatizo yote. (Mt. 2:13-15) Kwa mfano, Yesu alihitaji kushughulika na watu wa ukoo ambao hawakumwamini. Wazia jinsi Yesu alivyovunjika moyo kuwa na watu wa familia yake ambao mwanzoni hawakukubali kwamba yeye ni Masihi. (Marko 3:21; Yoh. 7:5) Pia, kuna uwezekano mkubwa kwamba Yesu alihitaji kukabiliana na huzuni ya kifo cha Yosefu, baba yake wa kambo. Huenda kifo cha Yosefu kilimaanisha kwamba Yesu, akiwa mwana mkubwa, alihitaji kuchukua jukumu la kusimamia biashara ya familia. (Marko 6:3) Alipoendelea kukua, Yesu alijifunza jinsi ya kuhangaikia hali njema ya familia. Bila shaka, alihitaji kufanya kazi kwa bidii ili kuwategemeza. Hivyo, alielewa uchovu ambao mtu huhisi baada ya kufanya kazi siku nzima.

Wazazi, waandaeni watoto wenu ili waweze kukabiliana na hali halisi za maisha kwa kuwafundisha jinsi ya kutegemea ushauri wa Neno la Mungu (Tazama fungu la 7) *

7. (a) Ni maswali gani yatakayowasaidia wenzi wa ndoa kuwalea watoto wao vizuri? (b) Methali 2:1-6 inaweza kuwasaidiaje wazazi kuwazoeza watoto wao?

7 Ikiwa ninyi ni wenzi wa ndoa na mngependa kupata watoto, jiulizeni hivi: ‘Je, sisi ni watu wanyenyekevu na wa kiroho ambao Yehova angependa kuwakabidhi uhai mpya wenye thamani?’ (Zab. 127:3, 4) Ikiwa wewe ni mzazi, jiulize hivi: ‘Je, ninawafundisha watoto wangu umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii?’ (Mhu. 3:12, 13) ‘Je, ninafanya yote niwezayo kuwalinda watoto wangu dhidi ya hatari za kimwili na za kiadili, ambazo huenda wakakumbuna nazo katika ulimwengu wa Shetani?’ (Met. 22:3) Huwezi kuwakinga watoto wako kutokana na changamoto zote ambazo huenda wakakabili. Hilo ni jambo lisilowezekana. Lakini hatua kwa hatua na kwa upendo, unaweza kuwatayarisha ili waweze kukabiliana na hali halisi za maisha kwa kuwafundisha jinsi ya kutegemea ushauri wa Neno la Mungu. (Soma Methali 2:1-6.) Kwa mfano, ikiwa mtu wa ukoo ataacha kumtumikia Yehova, wasaidie watoto wako kujifunza kutoka katika Neno la Mungu kwa nini ni muhimu sana waendelea kubaki washikamanifu kwa Yehova. (Zab. 31:23) Au ikiwa mtafiwa na mpendwa wenu, waonyeshe watoto wako jinsi ya kutumia Neno la Mungu kukabiliana na huzuni na kupata amani ya akili.—2 Kor. 1:3, 4; 2 Tim. 3:16.

JIFUNZE KUTOKA KWA YOSEFU NA MARIA

8. Kulingana na Kumbukumbu la Torati 6:6, 7, Yosefu na Maria walihitaji kufanya nini?

8 Yosefu na Maria walimsaidia Yesu awe mtu mzima mwenye kibali cha Yehova; walifuata mwongozo ambao Yehova aliwapa wazazi. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.) Yosefu na Maria walimpenda sana Yehova, na lengo lao kuu lilikuwa kuwatia moyo watoto wao wasitawishe upendo wa aina hiyohiyo.

9. Yosefu na Maria walifanya maamuzi gani muhimu?

9 Yosefu na Maria walichagua kudumisha ratiba nzuri ya kiroho wakiwa familia. Hapana shaka, kwamba kila juma walihudhuria mikutano katika sinagogi huko Nazareti, na pia Pasaka ya kila mwaka huko Yerusalemu. (Luka 2:41; 4:16) Huenda walitumia pindi hizo walizosafiri kwenda Yerusalemu kumfundisha Yesu na watoto wao wengine kuhusu historia ya watu wa Yehova. Na huenda wakiwa njiani walitembelea maeneo yanayotajwa katika Maandiko. Kadiri familia ilivyoongezeka, ni wazi kwamba haikuwa rahisi kwa Yosefu na Maria kudumisha ratiba nzuri ya kiroho. Lakini kazi yao haikuwa ya bure! Kwa kuwa walitanguliza ibada ya Yehova maishani, familia yao ilikuwa na hali nzuri ya kiroho.

10. Wazazi Wakristo wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yosefu na Maria?

10 Wazazi wanaomwogopa Mungu wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Yosefu na Maria? Jambo muhimu zaidi, wafundishe watoto wako kwa maneno na kupitia matendo kwamba unampenda sana Yehova. Tambua kwamba zawadi kubwa zaidi unayoweza kuwapa ni kuwasaidia wampende Yehova. Mojawapo ya mambo yenye thamani unayoweza kuwafundisha ni jinsi ya kudumisha ratiba nzuri ya kiroho ya kujifunza, kusali, kuhudhuria mikutano, na kushiriki katika huduma. (1 Tim. 6:6) Bila shaka, ni lazima uwaandalie watoto wako vitu vya kimwili wanavyohitaji. (1 Tim. 5:8) Lakini kumbuka kwamba uhusiano wa karibu ambao watoto wako wanao pamoja na Yehova ndio utakaowasaidia kuokoka mwisho wa mfumo huu wa mambo na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu, na si vitu vya kimwili walivyo navyo. *Eze. 7:19; 1 Tim. 4:8.

Inatia moyo kuona wazazi Wakristo wakifanya maamuzi mazuri ya kiroho kwa ajili ya familia zao! (Tazama fungu la 11) *

11. (a) Shauri linalopatikana kwenye 1 Timotheo 6:17-19, linawasaidiaje wazazi kufanya maamuzi mazuri wanapowalea watoto wao? (b) Familia yako inaweza kufikiria kujiwekea malengo gani, na huenda mtapata baraka gani? (Tazama sanduku “ Mtajiwekea Malengo Gani?”)

11 Inatia moyo sana kuona wazazi wengi Wakristo ambao wamefanya maamuzi mazuri ya kiroho kwa ajili ya familia zao! Wanaabudu pamoja kwa ukawaida. Wanahudhuria mikutano ya kutaniko na makusanyiko. Na wanashiriki katika utumishi wa shambani. Baadhi ya familia hata zimeweza kwenda kuhubiri kwenye eneo lisilohubiriwa kwa ukawaida. Wengine hutembelea Betheli au kushiriki katika miradi ya ujenzi ya kitheokrasi. Ni lazima familia zinazoshiriki katika utendaji huo zijidhabihu kifedha, na huenda wakakabili changamoto mbalimbali. Lakini kwa kweli, faida wanazopata zinawatajirisha kiroho. (Soma 1 Timotheo 6:17-19.) Watoto wanaolelewa katika familia hizo mara nyingi huendelea kufuata ratiba nzuri waliyojifunza, nao hawana majuto yoyote! *Met. 10:22.

JIFUNZE KUTOKA KWA YESU

12. Yesu alihitaji kufanya nini alipokuwa akikua?

12 Baba wa kimbingu wa Yesu hufanya maamuzi mazuri sikuzote, na wazazi wake wa duniani walifanya maamuzi mazuri pia. Hata hivyo, kadiri Yesu alivyoendelea kukua alifanya maamuzi yake mwenyewe. (Gal. 6:5) Kama tu ilivyo kwetu, yeye pia alikuwa na zawadi ya uhuru wa kuchagua. Angeweza kuamua kuchagua mapendezi yake ya kibinafsi maishani. Badala ya kufanya hivyo, aliamua kudumisha uhusiano mzuri pamoja na Yehova. (Yoh. 8:29) Mfano wake mzuri unaweza kuwasaidiaje vijana leo?

Vijana msikatae kamwe mwongozo wa wazazi wenu (Tazama fungu la 13) *

13. Yesu alifanya uamuzi gani muhimu alipokuwa angali kijana?

13 Mwanzoni mwa maisha yake akiwa mwanadamu, Yesu alichagua kujitiisha kwa wazazi wake. Kamwe hakupinga mwongozo wa wazazi wake, akifikiri kwamba yeye alijua mambo mengi kuliko wao. Badala yake “aliendelea kuwatii.” (Luka 2:51) Bila shaka, Yesu alichukua jukumu lake akiwa mwana wa kwanza. Hapana shaka kwamba alijifunza kwa bidii kutoka kwa baba yake wa kambo jinsi ya kufanya kazi ambayo ingemsaidia kuitegemeza familia yao.

14. Tunajuaje kwamba Yesu alikuwa mwanafunzi mzuri wa Neno la Mungu?

14 Inaelekea wazazi wa Yesu walimweleza kuhusu alivyozaliwa kimuujiza na mambo ambayo wajumbe wa Mungu walisema kumhusu. (Luka 2:8-19, 25-38) Yesu hakuridhika tu na mambo aliyoelezwa; bali alijifunza pia Maandiko kibinafsi. Tunajuaje kwamba Yesu alikuwa mwanafunzi mzuri wa Neno la Mungu? Kwa sababu alipokuwa angali mvulana, walimu huko Yerusalemu ‘walishangazwa na majibu yake na uwezo wake wa kuelewa.’ (Luka 2:46, 47) Akiwa na umri wa miaka 12 tu, tayari Yesu alikuwa amejithibitishia kwamba Yehova alikuwa Baba yake.—Luka 2:42, 43, 49.

15. Yesu alionyeshaje kwamba alichagua kufanya mapenzi ya Yehova?

15 Yesu alipoelewa jukumu lake katika kusudi la Yehova, aliamua kukubali mgawo wake. (Yoh. 6:38) Alijua kwamba atachukiwa na watu wengi, na ni lazima alitafakari jambo hilo kwa uzito. Hata hivyo, alichagua kujitiisha kwa Yehova. Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., jambo kuu maishani mwake lilikuwa kufanya mambo ambayo Yehova alitaka afanye. (Ebr. 10:5-7) Hata alipokuwa anakufa kwenye mti wa mateso, Yesu hakukengeuka kamwe na kuacha kufanya mapenzi ya Baba yake.—Yoh. 19:30.

16. Watoto wanajifunza jambo gani kutoka kwa Yesu?

16 Tii wazazi wako. Kama ilivyokuwa kwa Yosefu na Maria, wazazi wako si wakamilifu. Hata hivyo, Yehova amewapa wazazi wako mgawo wa kukulinda, kukuzoeza, na kukuongoza. Ikiwa utathamini ushauri wao na kuheshimu mamlaka yao, ‘mambo yatakuendea vema.’—Efe. 6:1-4.

17. Kulingana na Yoshua 24:15, vijana wanahitaji kufanya uamuzi gani wa kibinafsi?

17 Chagua ni nani utakayemtumikia. Unahitaji kujithibitishia mwenyewe Yehova ni nani, kusudi lake linahusisha nini, na jinsi mapenzi yake yanavyohusiana na maisha yako. (Rom. 12:2) Kisha, utaweza kufanya uamuzi muhimu zaidi maishani mwako, yaani, uamuzi wa kumtumikia Yehova. (Soma Yoshua 24:15; Mhu. 12:1) Ikiwa utadumisha ratiba ya kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida, upendo wako kwa Yehova utaendelea kukua na imani yako kumwelekea itakuwa imara zaidi.

18. Ni lazima vijana wafanye uamuzi gani, na matokeo yatakuwa nini?

18 Chagua kutanguliza mapenzi ya Yehova maishani mwako. Ulimwengu wa Shetani unatuahidi kwamba ikiwa tutatumia vipawa vyetu kujinufaisha tutakuwa na furaha. Lakini ukweli ni kwamba, wale wanaokazia fikira malengo ya kimwili wanajichoma wenyewe “kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Tim. 6:9, 10) Kwa upande mwingine, ikiwa utamsikiliza Yehova na kuchagua kutanguliza mapenzi yake, utafanikiwa maishani ‘nawe utatenda kwa hekima.’—Yos. 1:8.

UTACHAGUA KUFANYA NINI?

19. Ni lazima wazazi wakumbuke nini?

19 Wazazi, fanyeni yote mnayoweza kuwasaidia watoto wenu wamtumikie Yehova. Mtegemeeni yeye, naye atawasaidia kufanya maamuzi mazuri. (Met. 3:5, 6) Kumbukeni kwamba watoto wenu watachochewa zaidi kupitia mambo mnayofanya kuliko mambo mnayosema. Hivyo, fanyeni maamuzi yatakayowapa watoto wenu fursa nzuri zaidi ya kupata kibali cha Yehova.

20. Vijana watapata baraka gani ikiwa watachagua kumtumikia Yehova?

20 Vijana, wazazi wenu wanaweza kuwasaidia mfanye maamuzi mazuri maishani mwenu. Lakini ni juu yenu kufanya maamuzi yatakayowasaidia kupata kibali cha Mungu. Hivyo, mwigeni Yesu na mchague kumtumikia Baba yenu wa mbinguni mwenye upendo. Mkifanya hivyo, maisha yenu yatakuwa yenye shughuli nyingi, yenye kuthawabisha, na yenye kusisimua. (1 Tim. 4:16) Na wakati ujao, mtakuwa na maisha bora kabisa ambayo hamjapata kuyaona!

WIMBO 133 Mwabudu Yehova Ujanani

^ fu. 5 Wazazi Wakristo wangependa watoto wao wawe na furaha na wamtumikie Yehova watakapokuwa watu wazima. Ni maamuzi gani ambayo wazazi wanaweza kufanya ili wawasaidie watoto wao kufikia lengo hilo? Vijana Wakristo wanahitaji kufanya maamuzi gani ili wapate mafanikio ya kweli maishani? Makala hii itajibu maswali hayo.

^ fu. 11 Tazama sanduku “Siwezi Kuwazia Kuwa na Wazazi Bora Kuliko Hawa” kwenye gazeti la Amkeni! la Oktoba 2011, ukurasa wa 20, na makala yenye kichwa “Barua ya Pekee kwa Wazazi Wao” kwenye gazeti la Amkeni!, Machi 8, 1999, ukurasa 25.

^ fu. 66 MAELEZO YA PICHA: Ni lazima Maria alimfundisha kijana Yesu kumpenda sana Yehova. Vivyo hivyo, leo akina mama wanaweza kuwafundisha watoto wao wampende Yehova.

^ fu. 68 MAELEZO YA PICHA: Lazima Yosefu alichukulia kwa uzito kwenda kwenye sinagogi pamoja familia yake. Leo, akina baba wanaweza kuchukulia kwa uzito kuhudhuria mikutano ya kutaniko pamoja na familia zao

^ fu. 70 MAELEZO YA PICHA: Yesu alijifunza stadi za kazi kutoka kwa baba yake. Leo, vijana wanaweza kujifunza stadi za kazi kutoka kwa baba zao.