Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 45

Jinsi ya Kuwasaidia Wengine Washike Amri za Kristo

Jinsi ya Kuwasaidia Wengine Washike Amri za Kristo

“Basi, nendeni mkafanye wanafunzi . . . , na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.”​—MT. 28:19, 20.

WIMBO 89 Sikiliza, Tii, Upate Baraka

MUHTASARI *

1. Yesu aliwaamuru wanafunzi wake wafanye nini kwenye Mathayo 28:18-20?

BAADA ya Yesu kufufuliwa kutoka kwa wafu aliwatokea, wanafunzi wake waliokuwa wamekusanyika huko Galilaya. Alikuwa na jambo fulani muhimu la kuwaambia. Jambo gani hilo? Maneno yake yanapatikana kwenye Mathayo 28:18-20.​—Soma.

2. Tutachunguza maswali gani?

2 Amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi inamhusu kila mtumishi wa Mungu leo. Hivyo, acheni tuchunguze maswali matatu yanayohusiana na mgawo ambao Yesu ametupatia. Kwanza, tunahitaji kufanya jambo gani lingine zaidi ya kuwafundisha wanafunzi wapya matakwa ya Mungu? Pili, wahubiri wote kutanikoni wanaweza kuchangiaje ukuzi wa kiroho wa mwanafunzi wa Biblia? Tatu, tunaweza kuwasaidiaje waamini wenzetu wasiotenda waanze tena kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi?

WAFUNDISHE KUSHIKA AMRI ZA KRISTO

3. Amri ya Yesu ilitia ndani maagizo gani hususa?

3 Maagizo ya Yesu yako wazi. Ni lazima tuwafundishe watu mambo ambayo aliamuru. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka jambo fulani muhimu. Yesu hakusema: ‘Wafundishe mambo yote niliyowaamuru.’ Badala yake, alisema: “Wafundishe kushika mambo yote niliyowaamuru.” Ili tufuate mwongozo huo hususa tunapomfundisha mwanafunzi wetu wa Biblia, hatutamfundisha tu, bali pia tutamwongoza. (Mdo. 8:31) Kwa nini tunahitaji kufanya hivyo?

4. Kushika amri fulani kunamaanisha nini? Toa mfano.

4 “Kushika” amri fulani kunamaanisha kuitii. Ili kufafanua jinsi tunavyoweza kumfundisha mtu kushika au kutii mambo ambayo Kristo aliamuru, fikiria mfano ufuatao. Mwalimu wa udereva anawafundishaje wanafunzi wake kushika sheria za barabarani? Kwanza, mwalimu anaweza kuanza kuwafundisha sheria za barabarani wakiwa darasani. Hata hivyo, ili kuwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kutii sheria hizo, anahitaji kuchukua hatua nyingine. Anahitaji kuwa pamoja na wanafunzi hao ili kuwaongoza wanapokuwa wakiendesha barabarani huku wakijaribu kufanyia kazi mambo waliyojifunza. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano huo?

5. (a) Kulingana na Yohana 14:15 na 1 Yohana 2:3, tunahitaji kuwafundisha nini wanafunzi wa Biblia? (b) Toa mifano ya jinsi tunavyoweza kuwapa mwongozo wanafunzi wetu.

5 Tunapojifunza Biblia na wengine, tunawafundisha mambo ambayo Mungu anataka tufanye. Hata hivyo, ni lazima tufanye mengi zaidi. Ni lazima tuwafundishe wanafunzi wetu wa Biblia kutumia maishani mwao mambo wanayojifunza. (Soma Yohana 14:15; 1 Yohana 2:3.) Kupitia mfano wetu, tunaweza kuwaonyesha wanafunzi wetu jinsi ya kutumia kweli wanazojifunza katika Biblia wanapokuwa shuleni, kazini, au wakati wa tafrija. Tunaweza kuwasimulia jambo fulani lililotukia maishani mwetu ili kuwaonyesha jinsi ambavyo kutumia mwongozo wa Biblia kulitulinda au jinsi kulivyotusaidia kufanya uamuzi fulani wa hekima. Tunapokuwa na wanafunzi wetu, tunaweza kusali kwa Yehova na kumwomba awaongoze kwa roho yake takatifu.—Yoh. 16:13.

6. Kuwafundisha wengine kushika amri za Yesu kunahusisha nini?

6 Kuwafundisha wengine kushika amri za Yesu kunahusisha nini? Tunahitaji kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia wasitawishe tamaa ya kufanya wanafunzi. Huenda wazo la kushiriki katika kazi ya kuhubiri likawaogopesha baadhi ya wanafunzi. Hivyo, tunahitaji kuwa na subira tunapowapa mwongozo utakaowasaidia kuboresha uelewaji wao wa Biblia hatua kwa hatua, utakaogusa mioyo yao, na kuwachochea kutenda. Tunaweza kutumia mbinu gani ili kuwasaidia wanafunzi wetu wa Biblia wasitawishe tamaa ya kuwahubiria wengine habari njema?

7. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi asitawishe tamaa ya kuwahubiria wengine habari njema?

7 Tunaweza kumuuliza mwanafunzi wetu maswali kama haya: “Kukubali ujumbe wa Ufalme kumeyafanyaje maisha yako yawe bora zaidi? Je, unafikiri kwamba watu wengine wanahitaji kusikia ujumbe huo? Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia?” (Met. 3:27; Mt. 9:37, 38) Mwonyeshe mwanafunzi trakti ambazo ni sehemu ya Sanduku letu la Vifaa vya Kufundishia na umpe nafasi ya kuchagua zile anazofikiri kwamba zitawavutia ndugu, rafiki, na wafanyakazi wenzake. Mpe mwanafunzi wako idadi kadhaa ya trakti hizo. Fanya pamoja naye mazoezi ya jinsi ya kutoa trakti hizo kwa busara. Bila shaka, baada ya mwanafunzi wetu kukubaliwa kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, tutahitaji kuhubiri pamoja naye ili kumsaidia na kumwongoza.—Mhu. 4:9, 10; Luka 6:40.

JINSI KUTANIKO LINAVYOWASAIDIA WANAFUNZI WAFANYE MAENDELEO

8. Kwa nini ni muhimu wanafunzi wetu wasitawishe upendo wenye kina kwa Mungu na jirani? (Pia, tazama sanduku “ Jinsi ya Kuwasaidia Wanafunzi Wetu wa Biblia Waongeze Upendo Wao kwa Mungu.”)

8 Kumbuka kwamba Yesu alituagiza tuwafundishe wengine “kushika mambo yote” aliyoamuru. Bila shaka, mambo aliyoagiza yanatia ndani amri mbili zilizo kuu zaidi, yaani, kumpenda Mungu na kumpenda jirani; na zote kwa pamoja zinahusiana kwa ukaribu sana na kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mt. 22:37-39) Zinahusianaje na kazi ya kuhubiri? Sababu moja kuu inayotuchochea kushiriki katika kazi ya kuhubiri ni upendo​—upendo wetu kwa Mungu na jirani zetu. Inaeleweka kwamba huenda baadhi ya wanafunzi wa Biblia wakaogopa kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Lakini tunaweza kuwahakikishia wanafunzi hao kwamba kwa msaada wa Yehova hatua kwa hatua wanaweza kuacha kuwaogopa wanadamu. (Zab. 18:1-3; Met. 29:25) Sanduku linaloambatana na makala hii linafafanua hatua tunazoweza kuchukua ili kumsaidia mwanafunzi wetu akuze upendo wake kwa Mungu. Pia, kutaniko linaweza kufanya nini ili kuwasaidia wanafunzi wapya wampende zaidi Mungu na jirani zao?

9. Ni kwa njia gani nyingine mwanafunzi wa udereva anaweza kujifunza masomo muhimu?

9 Fikiria tena mfano wa mwanafunzi wa udereva. Mwanafunzi huyo anajifunza kwa njia gani anapokuwa anaendesha gari huku mwalimu wake akiwa kando yake? Ni kwa kumsikiliza mwalimu wake, na kwa kuwatazama madereva wengine walio makini. Kwa mfano, mwalimu anaweza kumwonyesha dereva mwingine ambaye kwa fadhili anasimama ili kuruhusu magari mengine yaingie kwenye barabara kuu. Au anaweza kumwonyesha dereva mwingine ambaye anapunguza mwangaza wa taa zake ili madereva wengine waweze kuona vizuri wanapopishana naye. Mifano kama hiyo inaweza kumfundisha mwanafunzi mambo muhimu anayoweza kutumia anapoendesha gari.

10. Ni jambo gani litakalomsaidia mwanafunzi wa Biblia kufanya maendeleo ya kiroho?

10 Vivyo hivyo, mwanafunzi wa Biblia anayeanza kutembea katika njia ya uzima hajifunzi tu kutoka kwa mwalimu wake, bali pia kutokana na mifano mizuri ya watumishi wengine wa Yehova. Hivyo basi, ni nini kitakachowasaidia sana wanafunzi wa Biblia wafanye maendeleo ya kiroho? Ni kuhudhuria mikutano yetu ya Kikristo. Kwa nini? Kwa sababu mwongozo wa Kimaandiko unaotolewa kwenye mikutano utaongeza ujuzi wao, utaimarisha imani yao, na kuwasaidia wakuze upendo wao kwa Mungu. (Mdo. 15:30-32) Zaidi ya hayo, kwenye mikutano mwalimu wa Biblia anaweza kumtambulisha mwanafunzi kwa ndugu na dada ambao huenda wana hali zinazofanana na zake. Wanafunzi wanaweza kuona mifano mizuri ya ndugu na dada wanaoonyesha upendo wa Kikristo. Fikiria hali zifuatazo.

11. Mwanafunzi anaweza kuona mifano gani kutanikoni, na mifano hiyo inaweza kuwa na matokeo gani kwake?

11 Mama anayejifunza Biblia na kulea watoto akiwa peke yake anamwona dada Mkristo anayepitia hali kama yake. Mwanafunzi huyo anaguswa sana moyo kuona jitihada za dada huyo za kuja na watoto wake wadogo kwenye Jumba la Ufalme. Mwanafunzi anayepambana ili aache kuvuta sigara anafahamiana na mhubiri aliyekuwa na tatizo kama lake lakini alifaulu kulishinda. Mhubiri anamwambia mwanafunzi huyo kwamba kadiri upendo wake kumwelekea Yehova ulivyokua, ndivyo alivyochochewa kutii amri za Mungu. (2 Kor. 7:1; Flp. 4:13) Baada ya kumsikiliza mhubiri huyo akieleza historia yake, mwanafunzi anapata uhakika zaidi ndugu huyo anapomhakikishia hivi: “Wewe pia unaweza kuacha.” Binti anayejifunza Biblia anamwona dada kijana ambaye ni wazi kwamba anafurahia maisha akiwa Shahidi. Mwanafunzi huyo anapomwona dada kijana akiwa na furaha sikuzote, anatamani kujua kwa nini dada huyo ni mwenye furaha hivyo.

12. Kwa nini tunaweza kusema kwamba kila mmoja kutanikoni ana jukumu fulani katika kuwasaidia wanafunzi wa Biblia?

12 Mwanafunzi wa Biblia anapowafahamu wahubiri waaminifu wenye hali mbalimbali, anajifunza kutokana na mfano wao mzuri maana ya kushika amri ya Yesu ya kumpenda Mungu na jirani. (Yoh. 13:35; 1 Tim. 4:12) Pia, kama ilivyotajwa mapema, mwanafunzi wa Biblia anaweza kujifunza kutoka kwa wahubiri ambao wanakabiliana na changamoto kama zile anazokabili. Mwanafunzi anajifunza kutokana na mifano hiyo kwamba mabadiliko anayohitaji kufanya ili kuwa mwanafunzi wa Kristo yanawezekana. (Kum. 30:11) Kila mtu kutanikoni anaweza kuchangia kwa njia mbalimbali maendeleo ya kiroho ya mwanafunzi wa Biblia. (Mt. 5:16) Wewe binafsi unafanya jitihada gani ili kuwatia moyo wanafunzi wa Biblia wanaokuja kwenye mikutano?

WASAIDIE WASIOTENDA WAANZE KUHUBIRI TENA

13-14. Yesu aliwatendeaje mitume wake waliokuwa wamevunjika moyo?

13 Tunataka kuwasaidia ndugu na dada zetu wasiotenda waanze tena kushiriki katika kutimiza amri ya Yesu ya kufanya wanafunzi. Namna ambavyo Yesu aliwatendea mitume wake waliovunjika moyo inaonyesha jinsi tunavyoweza kufanya vivyo hivyo leo.

14 Mwishoni mwa huduma ya Yesu hapa duniani, wakati kifo chake kilipokuwa kikikaribia, mitume wake ‘wote walimwacha na kukikimbia.’ (Marko 14:50; Yoh. 16:32) Yesu aliwatendeaje mitume wake pindi walipovunjika moyo? Muda mfupi baada ya kufufuliwa, Yesu aliwaambia hivi baadhi ya wafuasi wake: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu [kwamba nimefufuliwa].” (Mt. 28:10a) Yesu hakukatishwa tamaa na mitume wake. Ingawa walikuwa wamemwacha, bado aliendelea kuwaita “ndugu zangu.” Kama Yehova, Yesu alikuwa mwenye rehema na mwenye kusamehe.—2 Fal. 13:23.

15. Tunahisije kuhusu wale ambao wameacha kushiriki katika huduma?

15 Sisi pia tunawajali sana wale ambao wameacha kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Wao ni ndugu na dada zetu, na tunawapenda! Bado tunakumbuka kazi yenye upendo ambayo waamini wenzetu walifanya wakati uliopita na baadhi yao huenda walifanya hivyo kwa miaka mingi. (Ebr. 6:10) Tunawakosa sana! (Luka 15:4-7) Kama Yesu, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali sana?

16. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali ndugu na dada zetu wasiotenda?

16 Waalike kwenye mikutano kwa uchangamfu. Njia moja ambayo Yesu aliwatia moyo mitume waliovunjika moyo ni kwa kuwaalika kwenye mkutano. (Mt. 28:10b; 1 Kor. 15:6) Vivyo hivyo leo, tunaweza kuwatia moyo wahubiri wasiotenda wahudhurie mikutano, ikiwa hawafanyi hivyo. Tunatambua kwamba huenda tukawaalika mara kadhaa kabla hawajaanza kuhudhuria. Bila shaka, Yesu alifurahi sana wanafunzi wake walipokubali mwaliko wake.—Linganisha Mathayo 28:16 na Luka 15:6.

17. Tunapaswa kutendaje ndugu au dada asiyetenda anapohudhuria mkutano?

17 Wakaribishe kwa uchangamfu mikutanoni. Yesu aliwafanya wanafunzi wake wajihisi huru walipokutana naye; alichukua hatua ya kwanza kuzungumza nao. (Mt. 28:18) Tutatendaje ikiwa ndugu asiyetenda atafika kwenye Jumba la Ufalme? Tunapaswa kuchukua hatua ya kwanza kwa kumkaribisha kwa uchangamfu. Mwanzoni, huenda tukaogopa kwamba hatutajua cha kusema. Lakini tunaweza kumwambia jinsi tulivyofurahi kumwona bila kumwaibisha.

18. Tunaweza kuwatiaje moyo wahubiri wasiotenda?

18 Watie moyo kwa unyoofu. Inaelekea wanafunzi wa Yesu walihisi hawangeweza kutimiza utume wa kuhubiri ulimwenguni pote. Yesu aliwatia moyo wafuasi wake kwa kusema: “Nipo pamoja nanyi sikuzote.” (Mt. 28:20) Je, maneno hayo yaliwasaidia wanafunzi wake? Ndiyo. Baada ya muda mfupi, walikuwa wakishiriki kwa bidii katika “kufundisha na kutangaza habari njema.” (Mdo. 5:42) Wahubiri wasiotenda pia wanahitaji kutiwa moyo. Huenda wakaogopa kuanza kuhubiri tena. Tunaweza kuwatia moyo kwamba hawahitaji kuanza kuhubiri wakiwa peke yao. Wakiwa tayari tunaweza kuandamana nao katika huduma. Bila shaka, watathamini msaada wetu wanapoanza tena kuhubiri habari njema. Tunapowaona na kuwatendea wahubiri wasiotenda kama ndugu na dada zetu, tutapata matokeo mazuri sana katika kutaniko letu.

TUNATAKA KUIMALIZA KAZI TULIYOKABIDHIWA

19. Tunatamani nini kutoka moyoni, na kwa nini?

19 Tunapaswa kuendelea kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi hadi lini? Hadi mwisho wa umalizio wa mfumo huu wa mambo. (Mt. 28:20; tazama Kamusi, “Umalizio wa Mfumo wa Mambo.”) Je, tutafaulu kuhubiri na kufanya wanafunzi hadi wakati huo ufike? Tumeazimia kufanya hivyo! Tunafurahi kutumia muda, nguvu, na mali zetu ili kuwatafuta wale walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.” (Mdo. 13:48) Tunapofanya hivyo tunafuata mfano wa Yesu. Alisema hivi: “Chakula changu ni kufanya mapenzi ya yule aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yoh. 4:34; 17:4) Hiyo pia ni tamaa yetu ya kutoka moyoni. Tunataka kukamilisha kazi tuliyokabidhiwa. (Yoh. 20:21) Na tunataka wengine, kutia ndani wahubiri wasiotenda, wavumilie pamoja nasi katika kufanya kazi hii.—Mt. 24:13.

20. Kulingana na Wafilipi 4:13, kwa nini tunaweza kutimiza kazi ambayo Yesu alituamuru tuifanye?

20 Ni wazi kwamba si rahisi kutimiza kazi ambayo Yesu alituamuru tufanye. Hata hivyo, hatufanyi kazi hiyo tukiwa peke yetu. Yesu aliahidi kwamba atakuwa pamoja nasi. Tunaufanya mgawo wa kufanya wanafunzi tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” na kwa “kushirikiana na Kristo.” (1 Kor. 3:9; 2 Kor. 2:17) Hivyo, tunaweza kuitimiza. Inafurahisha sana na ni pendeleo kubwa kufanya mgawo huo na kuwasaidia wengine wafanye hivyo pia!—Soma Wafilipi 4:13.

WIMBO 79 Wafundishe Kusimama Imara

^ fu. 5 Yesu aliwaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi na kuwafundisha kushika mambo yote aliyokuwa amewaamuru. Makala hii inazungumzia jinsi tunavyoweza kufuata maagizo ya Yesu. Habari tutakayozungumzia inategemea kwa kadiri fulani makala iliyochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2004, ukurasa wa 14-19.

^ fu. 66 MAELEZO YA PICHA: Dada anayeongoza funzo la Biblia anamweleza mwanafunzi wake hatua za kuchukua ili aongeze upendo wake kwa Mungu. Baadaye mwanafunzi anatumia mapendekezo matatu aliyopewa na mwalimu wake wa Biblia.